Thursday, October 31, 2019

KAIMU MENEJA MKUU NARCO KAGERA ATUHUMIWA KWA RUSHWA

Na Alodia Dominick, Bukoba.

Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) inatarajia kumfikisha mahakama ya hakimu mkazi Bukoba, Kaimu meneja mkuu wa Ranchi za Taifa (NARCO) Profesa Philemon Nyangi Wambura kwa tuhuma mbalimbali za rushwa ikiwemo kuomba shilingi milioni 12,000,000.

Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kagera John Joseph ameviambia vyombo vya habari kuwa, kaimu meneja mkuu wa NARCO anatarajia kufikishwa mahakamani kwa tuhuma za rushwa ikiwa ni pamoja na kuomba na kupokea rushwa, matumizi mabaya ya ofisi, ubadhilifu na uhujumu uchumi kinyume na sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa, sheria namba 11 ya mwaka 2007.

TAKUKURU Mkoa wa Kagera ikiwa katika utekelezaji wa majukumu yake ya kuzuia na kupambana na rushwa mnamo septemba 23 mwaka huu ilipata taarifa kutoka kwa vyanzo vyake ambavyo vilionyesha kuwa Profesa Wambura amekuwa akijihusisha na vitendo dhidi ya rushwa ikiwemo kuomba na kupokea rushwa kutoka kwa baadhi ya wafugaji wenye uhitaji wa vitalu vya kufugia Ng'ombe au wenye vitalu ambao wanahitaji kuhuisha mikataba yao ya awali.

Taarifa ya uchunguzi imeonyesha kwamba Januari 3 mwaka 2018 profesa Wambura alipokea shilingi milioni 12 kutoka kwa mtu mmoja ambaye jina limehifadhiwa kwa sababu za kiuchunguzi ili aweze kumpatia kitalu kwa ajili ya kufanyia shughuli za ufugaji huku akifahamu kuwa, jambo hilo ni kosa na kinyume cha sheria.

Aidha, watu wengine wanne Octoba 25 mwaka huu walifikishwa mahakamani kwa tuhuma mbalimbali ikiwemo kughushi na kutumia nyaraka kwa lengo la kumdanganya mwajiri.

Stanslaus Katto ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya ujenzi wa shule ya sekondari Kashenye aliyefikishwa katika mahakama ya Hakimu mkazi Bukoba na kufunguliwa shauri jinai namba 226/2019 kwa makosa ya kughushi, kujipatia mamlaka asiyokuwa nayo na kuwasilisha nyaraka zenye maelezo ya uongo kwa mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Misenyi kwa lengo la kujipatia fedha kiasi cha shilingi 5.7 milioni.

Uchunguzi uliweza kubaini kuwa, June 9 mwaka 2015 Kato alighushi sahihi ya mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Bukwali na kisha kughushi sahihi ya mkandarasi wa kampuni ambayo imehifadhiwa katika hati ya malipo iliyokuwa itumike kufanya malipo kwa mkandarasi na kuwasilisha hati hiyo ya malipo kwa mkurugenzi wa halmashauri ya Misenyi huku akifahamu kuwa jambo hilo ni kinyume cha sheria.

Watuhumiwa wengine ni Richardi Machumi Kavogoro mwenyekiti wa kijiji cha Mkalinzi, Josephati Desekahino Nzeye mtendaji wa kijiji cha Mkalinzi na Onesmo Mabadiliko Tiara ambaye alikuwa mwenyekiti wa kamati ya vocher za pembejeo wa kata ya Muganza kutoka halmashauri ya Ngara ambao walifunguliwa shauri la jinai namba 166/2019.

Wote wamefikishwa mahakama ya wilaya ya Ngara octoba 25 mwaka huu kujibu tuhuma zinazowakabili za kutumia nyaraka kwa lengo la kumdanganya mwajiri.

No comments:

Post a Comment