Tuesday, February 27, 2018

VIONGOZI WALIOKULA FEDHA ZA WAKULIMA WA KOROSHO WARUDISHE.



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema viongozi wa Vyama vya Ushirika waliokula fedha za wakulima wa korosho wilayani Masasi wazirudishe na wakishindwa mali zao zikiwemo nyumba zitauzwa ili kufidia.

Pia Waziri Mkuu amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Bw. Gelasius Byakanwa ahakikishe anawasaka viongozi wa chama Ushirika cha Msingi cha Nanyindwa wilayani Masasi ambao wamekula fedha za wakulima na kisha kutoroka.

Amesema viongozi wa vyama vya Ushirika katika wilaya hiyo si waaminifu, ambapo mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya sh. bilioni 2.3 za wakulima ziliibiwa na viongozi hao, ambapo mwaka 2017/2018 sh. bilioni 1.7 zimeibiwa.

Waziri Mkuu alitoa maagizo hayo jana (Jumatatu, Februari 2018) alipozungumza kwa nyakati tofauti na wananchi pamoja na watumishi wa wilaya akiwa kwenye ziara yake ya kikazi mkoani Mtwara.

Alisema viongozi wa Ushirika wa Nanyindwa ambao wametoroka ni Michael Mkali, Yusuph Mataula, ambapo alimuagiza Bw. Byakanwa kuwasaka na kuwafikisha kwenye vyombo vya dola ili waweze kuchukuliwa hatua zinazostahili.

Pia Waziri Mkuu aliwaagiza Wakuu wa wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri nchini kuvichunguza vyama vya Msingi katika maeneo na wakikuta kuna kiongozi amekula fedha za wakulima wamkamate na kumchukulia hatua za kisheria.

Alisema wakati wa watu kuomba kuchaguliwa kuongoza vyama vya Ushirika kwa lengo la kujitajirisha umepita na Serikali imedhamilia inawasimamia wakulima wa mazao mbalimbali nchini wakiwemo wa korosho ili kuhakikisha nao wananufaika.

Waziri Mkuu alisema vyama vya Ushirika wilaya hiyo vinaongoza kwa ubadhilifu wa fedha za wakulima ambapo wiki iliyopita Bw. Byakanwa aliwakamata viongozi 36 wa Vyama vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) wilayani Masasi.

Viongozi hao ambao ni wenyeviti na makatibu wanakabiliwa na tuhuma za ubadhirifu wa fedha za wakulima wa korosho ambazo ni zaidi ya sh bilioni 2.3, ambazo ni malipo ya zao hilo kwa msimu wa ununuzi 2016/2017 na 2017/18.

Alisema mbali na wafanyabiasharahao, pia Meneja wa benki ya NMB tawi la Masasi, Aidan Msuya anaye alikamatwa kwa tuhuma za kufanya muamala wa fedha za malipo ya wakulima sh milioni 45 kwa zaidi ya mara 11 kwa siku moja.

Waziri Mkuu alimpongeza  Bw. Byakanwa kwa hatua alizozichukua dhidi ya viongozi hao na kumuagiza ahakikishe viongozi wote waliosababisha ubadhirifu huo wakamatwe na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Monday, February 26, 2018

WATOTO 6 WAWASHIWA VIFAA VYA USIKIVU (COCHLEAR IMPLANT).



Mtaalam wa Huduma ya Usikivu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Mathayo Majogoro Alfred (katikati) akiunganisha kifaa cha usikivu cha nje na cha ndani ili mtoto Matilda Katobesi aweze kusikia kwa mara ya kwanza. Kulia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Pua, Koo na Masikio, Dkt. Edwin Liyombo akifuatilia na kushoto ni mama wa mtoto huyo, Angelina Cosmas.
................................

Watoto sita ambao wamewekewa vifaa vya usikivu Januari mwaka huu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) leo wameanza kusikia kwa mara ya kwanza baada ya kuwashiwa vifaa hivyo. 

Kuwashwa kwa vifaa hivyo kumeleta furaha kwa wazazi kwani wameshuhudia watoto wao wakisikia sauti kwa mara ya kwanza na hivyo kuwajengea matumaini ya watoto hao kuanza maisha mapya.

Zoezi la kuwawashia vifaa hivyo (Switch On) limefanyika leo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili  kwa kushirikiana na wataalaam kutoka Medel Austria ambao ndio wasambazaji wa vifaa hivyo.

Akizungumza na waandishi wa habari , Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Pua,  Koo na Masikio Dkt. Edwin Liyombo amesema watoto hao walifanyiwa upasuaji wa upandikizaji kifaa cha usikivu Januari mwaka huu ambapo zaidi ya asilimia 80 ya upasuaji huo ulifanywa na watalaam wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili .

 ‘’Watoto hawa wataanza maisha mapya ya kusikia sauti mbalimbali katika mazingira yanayowazunguka baada ya kuunganisha vifaa hivi na kuviwasha’’. Amesema Dkt. Liyombo.

Akifafanua amesema mbali na watoto hao sita lakini pia watoto wengine watano ambao walifanyiwa upasuaji huo mwaka jana  na  wengine sita  ambao walifanyiwa upasuaji huo nchini India nao wamekuja kufuatiliwa maendeleo yao ili kubaini changamoto zinazowakabili  na kupewa ushauri wa kitaalam.  

Akielezea ukubwa tatizo  Dkt. Liyombo amesema takwimu za Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) zinaonesha kuwa katika watoto 1,000 wanaozaliwa,  inakadiriwa kuwa watoto watano wanazaliwa na tatizo kubwa la usikivu .
Pia amesema MNH ipo kwenye mchakato wa kuanzisha utaratibu wa kuwachunguza watoto wachanga ili kubaini mapema wenye matatizo yakutosikia. 

Kwa upande wake Muwakilishi kutoka Medel Fayaz Jafar amesema upasuji huo umekua na mafanikio makubwa kwakua  katika awamu hiyo kumekua na mabadiliko  kwani asilimia kubwa  ya upasuaji umefanywa na watalaam wa MNH  na kwamba hatua hiyo ni ya kuridhisha.

Huduma ya Upandikizaji wa kifaa cha usikivu (Cochlear Implant) ilizinduliwa Juni 7 , 2017 na  Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii , Jinsia , Wazee na Watoto Mheshimiwa Ummy Mwalimu hivyo Tanzania imekuwa nchi ya pili kutoa huduma hiyo katika nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki baada ya Kenya. Aidha Tanzania imekuwa nchi ya kwanza kutoa huduma hiyo  kupitia Hospitali ya Umma ambayo ni Muhimbili yenye hadhi ya ubingwa wa hali ya juu.

Mtoto Matilda kwa mara ya kwanza tarehe 24, Januari, 2018 akianza kutamka baadhi ya maneno baada ya kufundishwa na mtaalamu wa sauti kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Wazazi wa watoto wenye matatizo ya kusikia wakiwa kweny mkutano huo.

Sunday, February 25, 2018

NAIBU WAZIRI ANGELINA MABULA ASHUHUDIA UZINDUZI WA HUDUMA ZA KISASA KITUO CHA AFYA NYAMWAGA TARIME


Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Angelina Mabula akiangalia vifaa vilivyopo katika kituo cha afya cha Nyamwaga kilichopo wilaya ya Tarime mkoa wa Mara. 
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Angelina Mabula akitoa nasaha wakati alipokwenda kushuhudia uzinduzi wa huduma za kisasa katika kituo cha Afya cha Nyamwaga kilichopo Wilaya ya Tarime mkoa wa Mara.
Baadhi ya wananchi wakisikiliza nasaha zilizokuwa zikitolewa na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Angelina Mabula wakati wa uzinduzi wa kituo cha afya cha Nyamwaga kilichopo Tarime mkoa wa Mara.
Sehemu ya majengo ya kituo cha Afya cha Nyamwaga kilichopo Tarime mkoa wa Mara .

PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI-WANMM

NMB YASAIDIA VIFAATIBA VYA MIL. 5, HOSPITALI YA BAGAMOYO.


Meneja wa NMB kanda ya Mashariki, Aikasia Muro (wa nne kulia) akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga (mwenye suti) moja ya vifaatiba walivyotoa msaada kwa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo, wanaoshuhudia wa pili kushoto ni mwenyekiti wa halmashauri ya bagamoyo, Ally Ally Issa na wa tatu kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Afya Hospitali ya Wilaya Bagamoyo, Mwajuma Saidi Masaiganah.
...............................................
Benki ya NMB imesaidia vifaa tiba katika Hospitali ya wilaya ya Bagamoyo vyenye thamani ya shilingi milioni tano.

Akizungumza katika kukabidhi vifa hivyo, Meneja wa NMB kanda ya Mashariki, Aikasia Muro alisema Benki hiyo imefikia hatua hiyo ikiwa ni katika mipango yake ya kurudisha faida inayopata kwenye jamii.

Alisema NMB katika mipango yake imekuwa ikishiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii kama vile kusaidia katika sekta ya Elimu, kusaidia vifaa vya ujenzi, sekta ya Afya na kusaidia watu katika kipindi cha majanga kama ya mafuriko na ajali mbalimbali.

Alisema Hospitali ni sehemu ambayo kila mwana jamii anafika kupata huduma za matibabu na hivyo kupeleka msada katika hospitali ni sawa na kusaidia jamii nzima.

Aliongeza kwa kusema kuwa, Benki ya NMB ni Benki pekee yenye matawi mengi nchini na hivyo kuwa na wateja wengi hali inayopelekea kufikiria kuridisha fadhila kwa jamii ikiwa ni pamoja na kutoa misaada mbalimbali.

Akipokea msaada huo, mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Majid mwanga ameishukuru Benki hiyo kwa msaada huo na kusema kuwa ni kuonyesha mahusiano mema baina ya Benki hiyo na Serikali.

Alisema vifa hivyo vitasaidia kwa Hospitali ya Bagamoyo kwakuwa Hospitali hiyo inahudumia watu kutoka sehemu mbalimbali ndani na nje ya wilaya ya Bagamoyo.

Wakati huohuo, Mkuu  huyo wa wilaya huyo amewataka madiwani katika halmashauri ya Bagamoyo kuandaa maeneo kwenye kata zao ya kujenga zahanati ili kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya wilaya.

Alisema kuwepo kwa Zahanati kwenye kata kutasaidia wagonjwa kutibiwa kwenye kata zao na kwamba watakaokwenda Hospitali ya wilaya ni wale ambao wameshindikana kutibiwa kwenye zahanati.

Nae Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya Dkt. Salvio Wikesi alisema anatoa shukrani kwa Benki ya NMB kwa kuwapatia vifaa hivyo ambavyo vitasaidi katika kuwahudumia wagonjwa wanaofika katika Hospitali hiyo.

Alisema katika vifaa vilivyotolewa ni pamoja Delivery kit moja ambapo alisema kwenye muongozo wa wizara ya afya Hospitali ya Bagamoyo inatakiwa kuwa na Delivery kit 10 na kwamba hospitali hiyo sasa ina Delivery kit tano baada ya kupokea moja kutoka NMB.

Vifaa hivyo vyenye thamani ya shilingi milioni tano vilivyotolewa na benki ya NMB ni pamoja na Mashuka 35,  Vitanda 6 pamoa na magodoro yake, Kitanda cha kuifungulia 1, Seti 1 ya vifaa vya kujifungulia (Delivery kit) na Mashine ya kupimia BP 1.
 Meneja wa NMB kanda ya Mashariki, Aikasia Muro (wa tano kulia) akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga (wa tatu kushoto) moja ya vifaatiba walivyotoa msaada kwa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo.
 Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga, (wa pili kushoto) Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bagamoyo, Ally Ally (wa kwanza kushoto) na Mwenyekiti wa Bodi ya Afya Hospitali ya wilaya ya Bagamoyo, Mwajuma Saidi Masiganah ( wa tatu kushoto, kwa pamoja wakimkabidhi kaimu Mganga Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Dkt. Salvio Wikesi (katikati) wa tatu kulia ni Meneja wa NMB kanda ya Mashariki, Aikasia Muro, Meneja wa NMB tawi la Bagamoyo wakishuhudia baada ya wao kukabidhi kwa Mkuu wa wilaya.
 Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga, akitoa neno la shukrani kwa NMB mara baada ya kupokea msaada wa vifaatiba.
 Meneja wa NMB kanda ya Mashariki, Aikasia Muro, akizungumza wakati wa kukabidhi vifaatiba hivyo katika ukumbi wa Halmashauri Bagamoyo.

Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya Dkt. Salvio Wikesi, akitoa neno la shukrani kwa Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo kwa kutafuta wafadhili pamoja NMB kukubali kusaidia vifaatiba katika Hospitali ya wilaya ya Bagamoyo.

Timu ya wasimamizi wa Afya Halmashauri ya Bagamoyo (CHMT) wakifuatilia kwa karibu makabidhiano ya vifaatiba kutoka kwa Benki ya NMB yayofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri ya Bagamoyo.
Meneja wa NMB tawi la Bagamoyo (kulia) akifuatilia makabidhiano ya vifaatiba vyenye thamani ya shilingi milioni 5, vilivyotolewa na Benki hiyo kwa hospitali ya wilaya ya Bagamoyo.

Timu ya kutoka NMB tawi la Bagamoyo wakiongozwa na Meneja wa kanda ya Mashariki, Aikasia Muro, (wa pili kulia) wakipiga picha ya pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Majid Mwanga, (wa pili kushoto) wa kwanza kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Afya, Mwajuma Saidi Masaigana, na wa kwanza kushoto ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bagamoyo, Ally Ally.
 Timu ya wasimamizi wa Afya Halmashauri ya Bagamoyo (CHMT) wakipiga picha ya pamoja na meza kuu.

Saturday, February 24, 2018

DC BAGAMOYO ATOA SIKU 3 WINDE (RAZABA)

Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga,kihutubia wakuu wa idara katika Ukumbi wa Halmashauri ya Bagamoyo Tarehe 23 February 2018.

Na Athumani Shomari 
.....................................
Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga, ametoa siku tatu kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bagamoyo, kufuatilia taarifa za watu wanaogawana viwanja katika shamba linalomilikiwa na Ranchi ya Zanzibar Bagamoyo (RAZABA) lililopo kijiji cha Winde kata ya Makulunge.

Mkuu huyo wa wilaya alitoa agizo hilo Tarehe 22 Februry 2018 katika Ukumbi wa Halmashauri ya Bagamoyo, kufuatia taarifa za kuwepo watu wanaogawana viwanja ndani ya shamba hilo bila ya kujali mipaka na umiliki halali walionao RAZABA.

Alimtaka mkurugenzi kumpa taarifa za kitaalamu kuhusu mipaka ya RAZABA ili kubaini ukubwa wa eneo lililovamiwa na kuangalia hatua za kuchukua ili kunusuru eneo hilo ambalo lipo chini ya umiliki wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar .

Alisema hatua za haraka zichukuliwe ili kusitisha zoezi linaloendelea katika eneo la RAZABA na kuwaepusha watu wasie kutapeliwa kwa kuuziwa au kugaiwa eneo linalomilikiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Aidha, Mkuu  huyo wa wilaaya aliwataka wataalamu wa Ardhi Halmashauri ya Bagamoyo kufanya kazi zao kwa weledi ikiwa ni pamoja na kuzingatia maadili ya kazi zao.

Kufuatia hali hiyo, Mkuu huyo wa wilaya alitoa wito kwa wananchi wanaotaka Viwanja wilayani Bagamoyo kufika ofisi za Ardhi ili kupewa maelekezo yaliyokuwa sahihi juu ya wapi hakuna mgogoro wa kiumiliki ili kuondoa usumbufu unaoweza kujitokeza kwa kupewa eneo ambalo tayari lina umiliki wa mtu mwingine.

Mkuu huyo wa wilaya alisema wananchi wa kijiji cha Winde waliwasilisha malalamiko yao mbele ya Waziri wa Ardhi, nyumba na Maendeleo ya Makazi Wiliam Lukuvi ambapo walitaka mipaka ya RAZABA iwekwe wazi ili kutenganisha kati ya eneo la wananchi na RAZABA jambo ambalo tayari limeshafanyika.

KAULI YA CCM WILAYA YA BAGAMOYO NOVEMBA 18, 2017

Tarehe 18 Novemba 2017, Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Bagamoyo Abduli Rashidi Sharifu alisema Chama Cha Mapinduzi wilaya ya Bagamoyo kinatambua uwepo wa kjiji cha Winde na kwamba hakijawahi kuvunjwa wala kuondolewa kwenye ramani ya Bagamoyo.

akizungumza katika Mkutano ulioitishwa katika kijiji cha Winde kata ya Makurunge wilayani Bagamoyo, Sharifu alisema Ranchi ya Zanzibar Bagamoyo (RAZABA) ina mipaka yake na wananchi wa winde wana mipaka yao hivyo kila mmoja anapaswa kuheshimu mipaka yake.

KAULI YA HALMASHAURI YA BAGAMOYO JUNI 22, 2016.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bagamoyo Aliy Aliy alipiga marufuku utoaji wa hati za ardhi ikiwemo hati za kimila, katika maeneo yanayopakana na ardhi iliyohifadhiwa kama vile Ranchi ya Zanzibar Bagamoyo (RAZABA) inayomilikiwa na wizara kilimo na maliasili Zanziba, na Ranchi ya ruvu iliyopo wilayani Bagamoyo ambayo iko chini ya umiliki wa Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO).

Mwenyekiti huyo wa Halmashauri alitoa kauli hiyo Juni 22, 2016. katika Mkutano Mkuu Maalum wa kijiji cha Kidomole kata ya Fukayosi Halmashauri ya Bagamoyo na kuongeza kuwa Afisa aridhi atakaebainika kutoa hati ndani ya maeneo hayo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake ikiwemo kusimamishwa kazi.

Kauli hiyo ya Mwenyekiti huyo ilikuja kufuatia taarifa za kuuzwa kwa baadhi ya maeneo ndani ya Ranchi hizo jambo ambalo ni kinyume na sheria kwakuwa kampuni zinazomiliki maeneo hayo bado hazijavuliwa umiliki wake.

MSIMAMO WA WANANCHI WA WINDE.
  Wananchi wa kitongoji cha RAZABA Kata ya Makurunge Halmashauri ya Bagamoyo wilaya ya Bagamoyo,wakionyesha mabango yao kudai Ardhi yao ambayo kwa sasa inamilikiwa na Ranchi ya Zanzibar Bagamoyo (RAZABA) kwenye mkutano uliofanyika Tarehe 18 Novemba 2017, kitongoji cha RAZABA. ambapo mgeni rasmi alikuwa Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Abdul Rashid Sharifu.

HISTORIA YA MGOGORO KWA UFUPI
Mgogoro  wa watu wa kijiji cha Winde na Ranchi ya Zanzibar Bagamoyo (RAZABA) umedumu kwa zaidi ya miaka 40 sasa huku RAZABA ikidai kuchukua eneo hilo kwa kuwalipa fidia wananchi hao toka mwaka 1977 na wananchi wa kijiji cha Winde wakidai hawajawahi kulipwa fidia.

MSIMAMO WA RAZABA.
Ranchi ya Zanzibar Bagamoyo (RAZABA) inasema RAZABA imeanzishwa rasmi mwaka 1977 mwezi wa kumi na kwa makubaliano kati ya serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo jumla ya  heka 77,663 zilikabidhiwa kwa serikali ya mapinduzi Zanzibar chini ya wizara ya kilimo na maliasili kwa lengo la ufugaji wa Ng'ombe na kwamba wananchi wote walilipwa fidia toka wakati huo. 
Bango linaloonyesha kwamba eneo hilo linamilikiwa na Ranchi ya Zanzibar Bagamoyo (RAZABA) chini ya wizara ya kilimo na maliasili ya serikali ya mapinduzi ya Zanzibar.
Ramani ya eneo la Ranchi ya Zanzibar Bagamoyo (RAZABA).

DAWASA KUONDOA TATIZO LA MAJI BAGAMOYO.


Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Majid Mwanga, (katikati) akiongoza Mkutano wa kujadili upatikanaji wa maji Bagamoyo pamoja na kuanzisha mfumo wa kusafirisha maji taka.
........................................................... 
Wadau wa maji wilayani Bagamoyo wamekutana kujadili namna ya kuboresha miundombinu ya maji safi pamoja na kuandaa mpango mkakati wa kuanzisha namna kusafirisha maji taka ili mji wa Bagamoyo ubaki safi na salama.

Mwenyekiti wa Mkutano huo, Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Majid Mwanga alisema kufuatia kukua kwa mji wa Bagamoyo ipo haja ya kujadili namna bora ya kusafirisha maji taka badala ya kuwa na maeneo yasiyo rasmi kwa utupaji wa taka.

Alisema lengo la mkutano huo ni kuwa na uelewa wa pamoja kuhusu mradi wa maji taka ambao DAWASA tayari wameshafanyia upembezi yakinifu juu ya utekelezaji wa mradi huo.

Akizungumza katika Mkutano huo, Mhandisi wa Miradi Chrisitian Gava alisema katika kipindi cha mwaka 2014 mpaka 2016 Mamlaka ya maji safi na maji taka Dar es Salaam (DAWASA) imeongeza uzalishaji kutoka mita za ujazo milioni 262 mpaka mita za ujazo milioni 466 kwa siku  ambazo zinazalishwa katika mitambo ya Ruvu juu na Ruvu chini iliyoko Bagamoyo.

Alisema uzalishaji huo umekuwa hadi kufikia kiwango hicho baada ya kuzinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli Mwezi Juni 2017.

Aliongeza kwa kusema kuwa,  kufuatia hali hiyo uzalishai wa maji kwa ujumla katika maeneo yanayohudumiwa na DAWASA ikiwemo wilaya ya Bagamoyo umeongezeka kutoka mita za ujazo milioni 300 mpaka mita za ujazo milioni 544,000 kwa siku.

Aidha,  alisema uzalishaji wa maji kutoka Ruvu juu, Ruvu chini, mtoni, na Visima vidogo umeongezeka kutoka lita milioni 300 mpaka lita milioni 502 kwa siku.

Alifafanua kuwa, katika kuhakikisha adha ya maji inaondoka katika wilaya ya  Bagamoyo DAWASA inaendelea na mradi wa ujenzi wa tenki la kuhifadhia na kusambaza maji katika maeneo ya mji wa Bagamoyo lenye ukubwa wa mita za ujazo 6000, ambalo lina uwezo wa kuhifadhi maji lita milioni sita.

Alisema Tenki hilo litakapokamilika litahudumia wananchi wa maeneo ya Mpii, Zinga, Kiromo, Kitopeni, Ukuni, Kerege, Buma, Mataya, Bagamoyo mjini na ukanda maalum wa ewekezaji EPZA.

Akizungumzia Mradi wa usanifu wa mpango wa muda mrefu na muda mfupi wa kujenga mfumo wa kutibu majitaka, Mhandisi Christian Gava alisema tayari muandaaji wa mpango mkakati ambae ni Mhandisi mshauri (Consultant) ameshaanza kazi  kwaajili ya kupembua na kuandaa mpango mkakati wa muda mrefu pamoja na kupendekeza  mfumo nafuu wa kutibu majitaka katika wilaya za Kibaha, Bagamoyo na eneo  maalum la uwekezaji wilayani Bagamoyo  (BSEZ).

Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Dkt. Shukuru Kawambwa amesema mji wa Bagamoyo unakuwa kwa kasi hivyo ni vyema mikakati ya kukabiliana na majitaka iwepo ili kwenda sambamba na ukuaji wa mji.

Alisema katika kkufanya mji kuwa wa kisasa usiokuwa na taka kila mahali, ni vyema maandalizi ya kitaalamu yakafanyika mapema ili kila mwananchi ajue namna ya kusafirisha majitaka badala ya kuacha kila mtu atupe taka kwa namna anayoitaka yeye.

Akizungumza wakati wa kufunga mkutano huo, Mwenyekiti wa mkutano huo ambae  ni Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga alisema anamshukuru Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya maji safi na maji taka (DAWASA) kwa kushirikiana na serikali ya wilaya ya Bagamoyo katika kuboresha miundombinu ya maji safi na maji taka ndani ya Wilaya ya Bagamoyo. 
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bagamoyo, Fatuma Latu akiwatambulisha washiriki wa mkutano huo mbele ya Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo ambae ndiye Mwenyekiti wa Mkutano huo. 
Mhandisi wa Miradi kutoka mamlaka ya maji safi na maji taka (DAWASA) Christian Gava akiwasilisha Taarifa ya Miradi ya kusambaza maji safi pamoja na kutibu maji taka katika wilaya ya Bagamoyo.
Wahandisi kutoka DAWASA wakisikiliza kwa makini mapendekezo kutoka kwa washiriki wa mkutano huo uliofanyika ukumbi wa Halmashari ya Bagamoyo.
Madiwani wa Halmashauri ya Bagamoyo pamoa na watalamu wa Halmashauri hiyo wakisikiliza Taarifa ya wataalamu wa DAWASA. 
Mwenyekiti wa mkutano huo ambae ni Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Majid Mwanga (katikati) kulia ni Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Dkt. Shukuru Kawambwa, Kushoto ni Makamo Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bagamoyo,  Saidi Ngatipula.

Thursday, February 22, 2018

NAIBU WAZIRI WA NISHATI AWASHA KITUO CHA UMEME MBAGALA.



Naibu waziri wa nishati awasha umeme kituo cha Mbagala baada ya mradi huo kukamilika.

Kufuatia kuwashwa kwa kituo hicho, Wananchi wa Mbagala ,Kigamboni ,Tandika na Mkuranga na Wenye Viwanda watapata Umeme wenye Nguvu na wenye uhakika ambao hautokatika.

Naibu waziri wa Nishati, amewapongeza wananchi wakazi wa maeneo hayo Kwa kuwa na subira huku akiwapa pole kwa kero ya umeme ya muda Mrefu.

Aidha, alisema amewashukuru Waheshimiwa Wabunge wa Majimbo ya Kigamboni Dk Ndungulile na Mhe Mangungu na Wakuu wa Wilaya Kwa kufuatilia Jitahada za kuondosha Kero hiyo ya Upatikanaji wa Nishati ya Uhakika katika Maeneo hayo.

Alisema Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk John Pombe Magufuli imefanya juhudi kubwa kutekeleza mradi huo ili wananchi waondokane na kero hiyo.

Alisema kufuatia ushirikiano alionao yeye pamoja na Waziri wa nishati Dk Medard Kalemani wameweza kufanikisha Miradi mbalimbali ya Nishati ya umeme hapa nchini hali inayopelekea wananchi kujenga imani na serikali yao ya awamu ya tano katika utekelezaji wa miradi.

Aliongeza kwa kusema kuwa, kufuatia ushirikiano na Waziri wa nishati, imepelekea kuwa karibu na Wataalam wote wa TANESCO pamoja na Wakandarasi na hatimae kufanikisha mradi huo na miradi mingine iliyo chini ya wizara hiyo.

MAKAMU WA RAIS AHUDHURIA MAHAFALI YA 34 YA CHUO KIKUU HURIA


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akishiriki matembezi ya mahafali ya 34 ya Chuko Kikuu Huria pamoja na Mkuu wa chuo hicho Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda (kulia) kuelekea kwenye uwanja wa Halmashauri ya  Bariadi kwenye sherehe za mahafali ya 34 ya Chuo Kikuu Huria Tanzania.
..............................................................

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amewakumbusha wahitimu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kuwa Vyeti walivyotunukiwa  ni tuzo halali kwa juhudi na jitihada walizoonesha darasani.

Makamu wa Rais aliyasema hayo wakati wa sherehe za mahafali ya 34 ya Chuo Kikuu Huria yaliyofanyika kwenye uwanja wa Halmashauri Bariadi mkoani Simiyu.

Makamu wa Rais alisema “ Jamii inategemea mtaipatia tuzo ya utendaji bora na ufanisi katika fani zenu utakao akisi viwango vilivyoainishwa kwenye vyeti vyenu”.

Makamu wa Rais aliupongeza uongozi wa chuo kwa jitihada zake katika kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais hasa katika sula la Uchumi wa Viwanda ambapo chuo hicho kimefanya Kongamano kubwa la Elimu ya Juu na Uchumi wa Viwanda mjini Bariadi lakini pia chuo hicho kipo kwenye mchakato wa Kigoda cha kiprofesa cha Viwanda na Maendeleo.

Makamu wa Rais aliwakumbusha uongozi wa chuo katika jitihada zake za kutekeleza majukumu ya chuo , uendelee kujikita kwenye kauli mbiu yake Elimu Bora na Nafuu kwa Wote .

Katika Mahafali hayo ambayo zaidi ya wanafunzi 941 wamehitimu kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar pamoja na nchi za jirani ambapo wanafunzi saba (7) walihitimu Shahada ya Uzamivu ya Udaktari wa Falsafa ya Chuo Kikuu Huria.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu Huria Tanzania Profesa Rwekaza Mukandala wakati wa mahafali ya 34 ya chuo hicho yaliyofanyika kwenye uwanja wa Halmashauri ya Bariadi mkoani Simiyu.



Sehemu ya Wanafunzi waliohitimu katika Chuo Kikuu Huria wakiwa kwenye sherehe za mahafali ya 34 ya chuo hicho.
Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais