Friday, February 20, 2026
Thursday, February 12, 2026
SERIKALI YASHUSHA ADA KWA WANABLOGU.
SERIKALI YASHUSHA ADA KWA WANABLOGU.
TCRA Yazindua Redio ya Kisasa 'DSB'
SERIKALI imetangaza neema ya kihistoria kwa wanablogu, vijana wabunifu, na watoa maudhui mtandaoni nchini kwa kupunguza ada za leseni kwa kiwango kikubwa, hatua inayolenga kuchochea ukuaji wa uchumi wa kidijitali na kurasimisha shughuli za wahabarishaji wa mitandao.
Hatua hiyo imekuja kufuatia utafiti wa kina na mikutano ya kimkakati ya takribani mwaka mzima kati ya mtandao wa Tanzania Bloggers Network (TBN) na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ikielezea vikwazo vya gharama vilivyokuwa vikikwaza uandishi wa habari za kidijitali nchini.
Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Watoa Huduma za Utangazaji (ABC 2026) jijini Dodoma leo, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamisi Mwinjuma, amesema ada ya leseni kwa watoa maudhui mtandaoni imeshushwa kutoka Sh500,000 hadi Sh50,000 tu, huku ada ya maombi ikiwa ni Sh10,000 pekee.
Mageuzi hayo pia yamegusa kundi la wakusanyaji wa maudhui (Online Content Aggregators), ambao ada yao imeshushwa kutoka Sh1,000,000 hadi Sh100,000 pekee. Aidha, kundi la "Amateteur" limeanzishwa kwa ajili ya vijana wanaochipukia ili waweze kujitambulisha rasmi na kukuza vipaji vyao bila vikwazo vya kifedha.
Mapinduzi ya Teknolojia ya DSB
Wakati neema hiyo ikitangazwa, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabiri Bakari, ametangaza kuanza kwa teknolojia mpya ya utangazaji wa redio ya kidijitali nchini inayojulikana kama Digital Sound Broadcasting (DSB).
Teknolojia hiyo itaanza kufanya kazi katika mikoa mitano ya majaribio ya Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Arusha, na Mbeya, lengo likiwa ni kuongeza ubora wa sauti na huduma za utangazaji nchini.
"Tumekamilisha maandalizi yote ya kiudhibiti na watoa huduma wa miundombinu wameshapatikana. Hii ni hatua kubwa ya kuendana na mabadiliko ya teknolojia duniani na kuimarisha utangazaji, hususan maeneo ya vijijini," alisema Dkt. Bakari.
Utafiti: Redio Bado ni Kinara
Katika mkutano huo, Injinia Andrew Kisaka wa TCRA amewasilisha matokeo ya utafiti wa hali ya utangazaji kwa mwaka 2025/2026, ukionyesha kuwa redio inaendelea kuwa chanzo kikuu cha habari kwa asilimia 85 ya Watanzania. Hata hivyo, utafiti huo umebaini ukuaji mkubwa wa matumizi ya intaneti miongoni mwa vijana, ambapo asilimia 45 hupata habari kupitia mitandao ya kijamii kabla ya kusikiliza redio au kutazama televisheni.
Upande wa televisheni, utafiti unaonyesha asilimia 65 ya watazamaji wanatumia ving'amuzi, huku maudhui ya ndani yakipendwa zaidi kwa asilimia 70. Serikali imewahimiza watoa huduma za kienyeji kuwekeza zaidi kwenye majukwaa ya kidijitali (OTT) ili kukidhi mahitaji ya soko la sasa.
Ulinzi wa Hakimiliki na Mikopo
Ili kuhakikisha wanahabari wa kidijitali wanufaika na kazi zao, Serikali imezielekeza taasisi za COSOTA na TCRA kuandaa mpango wa kulinda hakimiliki na kudhibiti uharamia mtandaoni. Aidha, Serikali imeanza kutoa mikopo ya masharti nafuu kwa watengeneza maudhui kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kisasa vya kufanyia kazi.
Hadi kufikia Desemba 2025, TCRA imetoa jumla ya leseni 707 za utangazaji, zikiwemo 318 za maudhui mtandaoni, jambo linaloashiria kukua kwa uhuru wa habari na demokrasia nchini chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.
Friday, December 19, 2025
ITHIBATI YA WAANDISHI WA HABARI NI NGAO YA TAIFA KATIKA VITA.
SERIKALI YAAHIDI ULINZI NA USHIRIKIANO KWA WAANDISHI WA MTANDAONI.
Thursday, December 18, 2025
HALMASHAURI YA MJI BAGAMOYO YAKABIDHI VIFAA VYA TEHAMA KWA WALIMU WAKUU.
Halmashauri ya mji wa Bagamoyo, imekabidhi vifaa vya TEHAMA kwa walimu wakuu wa shule za kata za Zinga, Dunda na Kata ya Yombo.
Makabidhiano hayo yameongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo Mhe Mohamedi Usinga Desemba 17,2025.
Katika makabidhiano hayo Mhe Mwenyekiti amekabidhi jumla ya komputa (Desktop)44 katika Shule ya Msingi Yombo wamepata Komputa 20,shule ya Msingi Kizuiani 12 na Shule ya Zinga 12 pamoja na Komputa Mpakato moja kwa kila shule na vifaa vyake kwa ujumla.
Mhe Usinga ametoa wito kwa walimu hao kuhakikisha wanavitunza na kuvilinda vifaaa hivyo kwa ajili ya kujifunzia kwa wanafunzi mashuleni ili kuendana na kasi ya teknologia.
Vilevile Mhe Mwenyekiti ametoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha anawezesha upatikanaji wa vifaa vya Tehama mashuleni lakini pia na kuwezesha miundombinu bora mashuleni.
Nae Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo Ndg Shauri Selenda amewasisitiza walimu hao kuhakikisha wanavitunza vifaa hivyo Pamoja na kuhakikisha wanatoa elimu iliyobora kwa wanafunzi ili kujenga msingi bora wa elimu katika Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo.
Aidha Ndg Selenda ametoa shukrani kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais Samia Suluhu Hassani kwa kuhakikisha kila shule inakuwa na miundombinu bora lakini pia inapata vifaa vya kujifunzia mashuleni.
Kadhalika Afisa Elimu awali na Msingi Bi Wema Kajigili akitoa shukrani kwa niaba ya Walimu hao wote amesema kuwa “naendelea kutoa shukrani kwa Rais Samia Suluhu Hassani Pamoja na wadau wote wa elimu nchini vifaa hivi tutahakikisha tunavitunza na kuvilinda na kuhakikisha mwanafunzi ananufaika na vifaa hivi kwa kuwapatia elimu bora”.Bi Wema Kajigili.

















































