Tuesday, June 23, 2026

TANROADS YATANGA BARABARA SITA ZA PPP KUUNGANISHA MIKOA YA DAR, PWANI, DODOMA, SINGIDA NA TANGA KM 969

 

Katika hatua nyingine kubwa ya kuharakisha maendeleo ya miundombinu na kuimarisha ukuaji wa uchumi wa Taifa, Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) umetangaza fursa za uwekezaji katika miradi sita mikubwa ya barabara yenye urefu wa kilomita 969 kupitia mfumo wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP).

 

Tangazo hilo la kimataifa la kutafuta wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kubuni, kujenga, kugharamia, kuendesha, kutunza na hatimaye kukabidhi miradi hiyo kwa Serikali kupitia mfumo wa Design, Build, Finance, Operate, Maintain and Transfer (DBFOMT), linaendelea kudhihirisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutumia nguvu ya sekta binafsi kuharakisha utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo.

 

Hatua hiyo pia inaakisi mafanikio ya mageuzi makubwa yanayosimamiwa na Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC) chini ya Mkurugenzi Mtendaji David Kafulila, ambaye amekuwa mstari wa mbele kuhamasisha ushiriki wa sekta binafsi katika uwekezaji wa miundombinu na huduma za kijamii nchini.

 

Miradi iliyowekwa mezani kwa wawekezaji ni pamoja na upanuzi wa Barabara ya Morogoro–Dodoma yenye urefu wa kilomita 260 kuwa njia nne, Barabara ya Handeni–Kiberashi–Chemba–Kwamtoro–Singida yenye kilomita 384, upanuzi wa Barabara ya Chalinze–Segera–Tanga yenye kilomita 246 kuwa njia nne pamoja na ujenzi wa Kitonga Escarpment Bypass yenye kilomita 27.

 

Miradi mingine ni Dar es Salaam Port–Kibaha Expressway yenye kilomita 42 na Dar es Salaam CBD–Julius Nyerere International Airport Expressway yenye kilomita 10.

 

Kwa mujibu wa TANROADS, miradi hiyo inalenga kupunguza msongamano wa magari, kuboresha usafirishaji wa watu na mizigo, kuongeza ushindani wa uchumi wa Tanzania na kuimarisha nafasi ya nchi kama kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

 

Kwa ujumla, miradi hiyo ina urefu wa kilomita 969. Kwa makadirio ya wastani ambapo kilomita moja ya barabara inaweza kugharimu takribani Dola za Marekani milioni moja sawa na karibu tsh trilioni tatu za Kitanzania kwa zote.


TWPF YAKAGUA ENEO LAKE LA KIMKAKATI DODOMA

 

 

Na Oscar Mbuza, MNRT

 

BODI ya Mfuko wa Kuhifadhi Wanyawapori (TWPF) imetembelea kiwanja kinachomilikiwa na Mfuko huo  eneo la Njedengwa katika Manispaa ya Dodoma ambacho kitapangiwa matumizi yake hivi karibuni.

 

Msafara wa Bodi hiyo umeongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya TWPF Profesa Jafari Kideghesho akiambatana na  Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Alexander Lobora na baadhi ya wajumbe wa Bodi.

 

Wajumbe wengine ambao wameshiriki  ziara hiyo ni Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) Dkt. Eblate Mjingo na  Kamishna wa Uhifadhi kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Mlage Kabange.

 

Aidha ujumbe huo pia ulimjumuisha  Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCCA), Victoria Shayo aliyemwakilisha Kamisha wa Uhifadhi wa NCCA.

 

Akizungumza baada ya kukagua eneo hilo lililopo Kitalu Namba 16, lenye ukubwa wa mita za mraba 39,700, Profesa Kideghesho amesema ameridhishwa na usimamizi na uhifadhi wa kiwanja hicho ambacho kitapangiwa matumizi yake hususani kwenye maendeleo ya uhifadhi wa wanyamapori hivi karibuni.

 

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Wanyamapori, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Lobora amesema wizara italitumia eneo hilo kama eneo la mkakati la uendeshaji wa shughuli za uhifadhi wa wanyamapori nchini.

 

Mfuko wa Hifadhi ya Wanyamapori Tanzania ni wa kudumu maalum kwa ajili ya kusaidia kutatua baadhi ya changamoto zinazohitaji fedha kwenye uhifadhi.

 

Madhumuni ya Mfuko ni kurahisisha na kusaidia uhifadhi wa wanyamapori, ndani na nje ya maeneo yaliyohifadhiwa. Bodi ya TWPF ina wajumbe tisa.

                


Monday, June 22, 2026

KATAMBI AWAONYA WAHALIFU NA MAANDAMANO HARAMU YA TAREHE 07

 


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi amewaasa watu wanaotoa kauli za kichochezi katika mitandao ya kijamii, majukwaa ya kisiasa na maeneo mbalimbali ambapo kauli hizo za kibaguzi na kichochezi zinahusu Muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Viongozi mbalimbali wa serikali au wa dini.

 

Waziri Katambi ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na waumini wa Msikiti wa Mukadam uliopo Kata ya Chang’ombe iliyopo wilaya ya Dodoma Mjini ambapo kumefanyika Mashindano ya Quran na Harambee ya Ujenzi wa Msikiti huo.

 

“Taifa hili limejengwa kwa maumivu makubwa ya waasisi, limejengwa kwa jasho na hata damu ilipobidi ili Taifa Tanzania liwepo, nitumie fursa hii kuwaomba sana na kuwaasa wale wote ambao wanatumia majukwaa ya kisiasa kuchonganisha wananchi, kuwajaza chuki, kuchochea lakini pia kuhamasisha kufanya uhalifu na wanaounda magenge ya uhalifu yanayolenga kuharibu taifa letu, niwasihi na kuwaomba waache mara moja kwasababu kufanya hivyo hakuna ambae atabaki salama tutaathirika sisi Watanzania wote na athari hii italiathiri taifa kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni.” amesema Waziri Katambi.

 

“Tutarudi nyuma kimaendeleo,tutashindwa kuswali, tutashindwa kwenda kanisani, tutashindwa kufanya kazi za kiuchumi, tutashindwa kujenga nchi yetu, tutashindwa kujenga uchumi wa mtu mmoja mmoja, tuwakanye na kuwaelekeza vijana wetu wakaishi mwenendo mwema na uzalendo kwa taifa lao na pale yanapotolewa maonyo na maelekezo ya vyombo vya ulinzi na usalama wasikaidi kwani kwenda kinyume ni kuvunja sheria, katiba na taratibu.” aliongeza Waziri Katambi.







VIONGOZI WA REA ZAMBIA, WAWASILI TANZANIA KWA ZIARA YA KIKAZI

 


Viongozi wa Mamlaka ya Nishati Vijijini (REA) kutoka nchini Zambia wamewasili nchini kwa ajili ya ziara ya kujifunza na kubadilishana ujuzi na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

 

REA Zambia ambao wameongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati Zambia anayeshughulikia Umeme, Mhandisi Arnold Simwaba wamewasili Tanzania Juni 21, 2026 katika Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere na kupokelewa na Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati Tanzania, Wilson Nyamanga pamoja na Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA Tanzania, Mhandisi Jones Olotu, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala wa REA Tanzania, Renatus Msangira.

 

Uongozi wa REA Zambia utakuwa nchini kwa ziara ya kikazi ya Siku 7 ambapo pamoja na vikao vya kubadilishana ujuzi, wajumbe hao wanatarajiwa kutembelea miradi mbalimbali ya umeme vijijini inayotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini.






Saturday, June 20, 2026

SERIKALI YAAHIDI KUSIMAMIA HAKI ZA WAKIMBIZI

 


 

Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM

 

Serikali ya Tanzania imeahidi kuendelea kulinda, kusimamia na kutekeleza haki za binadamu ikiwemo haki za raia wa Tanzania na Wakimbizi kutoka nchi mbalimbali wanaohifadhiwa hapa nchini ambapo pia imesema itaendelea kusimamia Amani na Usalama ili madhila yanayotokea katika nchi nyingine yasitokee hapa nchini.

 

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Mheshimiwa Patrobas Katambi (MB) wakati akizungumza katika Maadhimisho ya Siku ya Wakimbizi Duniani ambayo huadhimishwa kila ifikapo Tarehe 20 ya mwezi Juni, kila mwaka, huku kauli mbiu ya mwaka huu ikisema “Hadi Kila Mtu awe Salama”

 

Waziri Katambi akizungumza mbele ya Wakimbizi wanaoishi jijini Dar es Salaam ambao waliwawakilisha wakimbizi wanaoishi katika maeneo mbalimbali nchini amesema nchi ya Tanzania inajifunza kwa yaliyotokea nchi jirani huku akitoa ahadi ya serikali ya kuwahudumia Wakimbizi.

 

“Ni agizo la Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia, watu wote ambao ni ndugu zetu Wakimbizi waliohifadhiwa hapa tutawahudumia hata pale itakapohitajika rasilimali za nchi yetu tutazitumia, Rais wetu amekua anafanya hivyo wakati wote hata pale tulipokosa ufadhili na fedha za wadhamini, UNHCR aliendelea kutushika mkono lakini wapo wengine ambao hawakupata tuliwaombea kwa Mwenyezi Mungu ili wapate waongeze nguvu lakini zilipokosekana kabisa Rais wetu hakusita kuweka mkono wake ili Wakimbizi muendelee kuishi kwa amani na utulivu, tunawapenda ndugu zetu, mmetupa uzoefu mmetupa mifano na uhalisia na sisi tunajifunza kutoka kwenu” amesema Waziri Katambi

 

“Mmeeleza sababu zilizopelekea kukosekana kwa Amani katika nchi zenu, zipo sababu ambazo pengine zinafanana na zenu ikiwemo rushwa, kujipatia fedha kwa manufaa binafsi, utakatishaji fedha, ukwepaji kodi na magendo yanayonufaisha wachache na kuumiza walio wengi, ubadhilifu, wizi wa mali za umma, kughushi na kufanya udanganyifu, uhalifu wa kiuchumi, makosa yanayoweza kuhatarisha amani ya nchi, uhaini, uchochezi wa vurugu, vurugu za kisiasa, vyeo na mali, ubaguzi wa kidini, kikabila na ukanda, utapeli na dhulma kwa wananchi, unyanyasaji wa kijinsia.” aliongeza Waziri Katambi

 

Waziri Katambi amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Katiba ya Mwaka 1977 na marekebisho yake chini ya Uongozi wa Dkt.Samia Suluhu Hassan ambae ni Rais na Amiri Jeshi Mkuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Bunge na Mahakama wataendelea kusimamia haki za binadamu, utii wa sheria, maslahi ya wananchi wote wakiwepo Wakimbizi.


Monday, March 23, 2026

SERIKALI YAHIMIZA MELI YA NEW MV MWANZA KUKUZA UCHUMI, UTALII KANDA YA ZIWA.

 



Serikali imetoa wito kwa wafanyabiashara, wasafirishaji na wawekezaji mbalimbali kutumia fursa ya meli mpya ya MV New Mwanza kibiashara na kiutalii ili kukuza uchumi wa Kanda ya Ziwa.

Itakumbukwa meli hiyo imejengwa kwa zaidi ya Tsh. Bilioni 120, ikiwa na uwezo wa kubeba abiria 1,200, tani 400 za mizigo, magari makubwa matatu na madogo, ambapo itafanya safari zake katika bandari zote zinazozunguka Ziwa Victoria ikiwemo Kisumu (Kenya), Port Bay (Uganda) na Kemondo (Bukoba).

‎Akizungumza Jumapili Machi 22, 2026 na waandishi wa habari katika bandari ya Mwanza Kusini jijini Mwanza ilipoegeshwa meli hiyo, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema kutokana na uwekezaji huo wakazi wa Kanda ya Ziwa, wawekezaji na wafanyabiashara wakubwa na wadogo wanapaswa kuitumia kwenye shughuli zao na kuleta tija ya uwekezaji huo mkubwa.

‎Amesema Serikali imetimiza jukumu lake la kutekeleza wajibu wa kujenga mazingira mazuri ya biashara, uwekezaji na ustawi wa jamii, hivyo mpira sasa unahamia kwa wananchi kuitumia ili kulinufaisha taifa na malengo yaliyokusudiwa yafikiwe.

‎"Nawaombeni mkiiona New MV Mwanza, oneni suluhuhisho la uhakika la usafiri na usafirishaji wa abiria na mizigo, oneni fursa muhimu na adhimu ya utalii" amesema Msigwa na kuongeza;

‎"Serikali inategemea kuona utalii unakua kwa kasi hapa Mwanza, Bukoba na kwingine, watalii waje hapa Mwanza kisha waingie Serengeti, waende Rubondo, Burigi- Chato na kwingineko" amesema.

‎Ameongeza kuwa, wafanyabiashara na wawekezaji wanapaswa kuiona meli hiyo kama suluhisho la uhakika la kukua kwa biashara mbalimbali za madini, samaki, pamba, nyama na maziwa.

‎"Katika kanda ya Ziwa, amkeni mkamate biashara za maeneo yote ambayo yanazungukwa na Ziwa Victoria - Tanzania, Kenya, Uganda na kote ambako uwepo wa meli unarahishisha mambo, pia fursa zilizopo DRC, Sudan Kusini, Rwanda, Burundi" amesisitiza Msigwa.

‎Kwa mujibu wa Msigwa, mafanikio ya ujenzi wa meli hiyo ni moja ya mambo makubwa ya kujivunia kwa watanzania wakiwa na kila sababu ya kutembea kifua mbele kwa kuwa na serikali yenye maono na dhamira ya kuwekeza katika mambo makubwa ambayo yatatoa mchango mkubwa katika mageuzi ya kiuchumi.   

‎"Hii inafanya meli hii sio tu kuwa kubwa kuliko zote katika ziwa Victoria na maziwa makuu bali pia hii ndiyo meli kubwa kuliko zote katika maji baridi barani Afrika" amesema



MAKAMU WA RAIS AONGOZA MAADHIMISHO YA KILELE CHA WIKI YA MAJI 2026

 











Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa Mamlaka zinazohusika pamoja na Watanzania kwa ujumla kuweka kipaumbele katika utunzaji na ulinzi wa vya vyanzo vya maji ili kuweza kurithisha kizazi kijacho nchi inayofaa kuishi.
 
Makamu wa Rais ametoa wito huo alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Maadhimisho ya Kilele cha Wiki ya Maji kwa Mwaka 2026 na Siku ya Maji Duniani iliyofanyika katika Viwanja vya Mkwawa mkoani Morogoro leo tarehe 22 Machi 2026. Amesema ni lazima kuangalia sana umuhimu wa kulinda vyanzo vya maji kwa kufanya uwekezaji wa kimkakati ambao unaangalia kuvitunza na kuongeza vyanzo vya maji.
 
Halikadhalika, Makamu wa Rais ametoa rai kwa Wizara na Taasisi zote za Umma nchini kujenga mtandao wa ushirikiano katika kuzikabili kuzitatua na kurekebisha changamoto za maji ili dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwa na Taifa lilioondokana na changamoto za maji safi na salama iweze kufanikiwa.
 
Pia amesema, ni vema kwa Mamlaka za Maji nchini kuendelea kubuni vyanzo vipya vya mapato ili kukuza sekta ya maji. Ameipongeza Mamlaka ya Maji Tanga kwa kutumia mfumo wa Hati fungani katika kugharamia miradi ya maji inayotekelezwa mkoani humo. Makamu wa Rais amesema kila mtanzania anapaswa kuona wajibu wa utunzaji wa mazingira.
 
Vilevile, Makamu wa Rais amesema, Sekta binafsi ni mdau muhimu katika kufanikisha miradi ya maji kwa maendeleo ya sekta hiyo. Ametoa wito kwa wadau wote wa sekta ya maji kutambua kwamba maji ni muhimu na hitaji la kila mwanadamu hivyo ni vema kuendelea kushirikiana.
 
Makamu wa Rais, amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha mpango wa Gridi ya Taifa ya Maji unafanikiwa kikamilifu kwani kufanikiwa kwake ndio kuondokana na tatizo la maji nchini. Amewasihi Wizara ya Maji kuhakikisha wanafanikisha ufungaji wa mita katika maeneo ya matumizi ya maji ili kuepusha upotevu wa maji lakini pia kufanya watu wanaotumia maji kuwajibika.
 
Vilevile, Makamu wa Rais amesema Dira ya Maendeleo 2050 imelenga kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii, ambapo matarajio ni kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye uchumi wa kipato cha kati ngazi ya juu. Wakati idadi ya watu nchini ikitarajiwa kuongezeka hadi kufikia takriban watu milioni 118, inatarajiwa pia kuwa zaidi ya nusu yao watakuwa wanaishi maeneo ya mijini. Ongezeko hilo la watu linahitaji kujipanga ili kuwa na uhakika wa upatikanaji wa chakula, fursa za ajira na huduma za kijamii kama afya na elimu na maji.
 
Moja ya malengo makuu ya Sera ya Taifa ya Maji ya Mwaka 2002, Toleo la 2025 ni kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi, hususan wanaoishi vijijini. Katika utekelezaji wa Sera hii na Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, miradi mbalimbali ya maji nchini imetekelezwa na kuwezesha kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi, ambapo kwa sasa vijijini huduma hiyo imefikia wastani wa 85.2%, na mjini wastani wa 92.5%. Jumla ya Vijiji 10,758 vimefikiwa na huduma ya maji, vikisalia Vijiji 1,575 ambavyo Wizara ya Maji imezindua kampeni maalum ya kuhakikisha inafikisha huduma hiyo.
 
Kwa upande wake, Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha vema Wizara ya Maji kutekeleza miradi kwa ufanisi. Ameongeza kwamba, Wizara hiyo haitokuwa kikwazo katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.
 
Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais amezindua Mfumo wa Utabiri wa Kiasi cha Maji kwenye mito nchini Tanzania. Uzinduzi huo umefanyika katika la Bwawa la Mindu Mjini Morogoro. Mfumo huo ni moja ya jitihada za Wizara ya Maji kuhakikishia inaondoa changamoto za Sekta kwa kuwezesha upatikanani wa taarifa sahihi za kiwango cha Maji katika mito yote nchini.
 
Pamoja na uzinduzi huo, Makamu wa Rais amepanda miti rafiki wa maji kwenye chanzo hicho ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Maji Duniani na kilele cha Wiki ya Maji Tanzania.
 
Maadhimisho hayo yana kaulimbiu isemayo “Maji na Usawa wa Kijinsia” (Water and Gender) yikilenga kutafakari kwa kina uhusiano uliopo kati ya upatikanaji wa maji safi na usawa wa kijinsia katika jamii. Ripoti ya Umoja wa Afrika kwenye Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu Maji (mwaka 2023) inaonesha kuwa Afrika, kusini mwa Jangwa la Sahara inapoteza 5% ya Pato lake la Taifa kwa mwaka (takriban Dola za Marekani Bilioni 170) kutokana na ukosefu wa maji, matumizi ya maji yasiyo salama na ukosefu wa huduma bora za usafi wa mazingira.
 
Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
22 Machi 2026
Morogoro.