Monday, March 23, 2026

SERIKALI YAHIMIZA MELI YA NEW MV MWANZA KUKUZA UCHUMI, UTALII KANDA YA ZIWA.

 



Serikali imetoa wito kwa wafanyabiashara, wasafirishaji na wawekezaji mbalimbali kutumia fursa ya meli mpya ya MV New Mwanza kibiashara na kiutalii ili kukuza uchumi wa Kanda ya Ziwa.

Itakumbukwa meli hiyo imejengwa kwa zaidi ya Tsh. Bilioni 120, ikiwa na uwezo wa kubeba abiria 1,200, tani 400 za mizigo, magari makubwa matatu na madogo, ambapo itafanya safari zake katika bandari zote zinazozunguka Ziwa Victoria ikiwemo Kisumu (Kenya), Port Bay (Uganda) na Kemondo (Bukoba).

‎Akizungumza Jumapili Machi 22, 2026 na waandishi wa habari katika bandari ya Mwanza Kusini jijini Mwanza ilipoegeshwa meli hiyo, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema kutokana na uwekezaji huo wakazi wa Kanda ya Ziwa, wawekezaji na wafanyabiashara wakubwa na wadogo wanapaswa kuitumia kwenye shughuli zao na kuleta tija ya uwekezaji huo mkubwa.

‎Amesema Serikali imetimiza jukumu lake la kutekeleza wajibu wa kujenga mazingira mazuri ya biashara, uwekezaji na ustawi wa jamii, hivyo mpira sasa unahamia kwa wananchi kuitumia ili kulinufaisha taifa na malengo yaliyokusudiwa yafikiwe.

‎"Nawaombeni mkiiona New MV Mwanza, oneni suluhuhisho la uhakika la usafiri na usafirishaji wa abiria na mizigo, oneni fursa muhimu na adhimu ya utalii" amesema Msigwa na kuongeza;

‎"Serikali inategemea kuona utalii unakua kwa kasi hapa Mwanza, Bukoba na kwingine, watalii waje hapa Mwanza kisha waingie Serengeti, waende Rubondo, Burigi- Chato na kwingineko" amesema.

‎Ameongeza kuwa, wafanyabiashara na wawekezaji wanapaswa kuiona meli hiyo kama suluhisho la uhakika la kukua kwa biashara mbalimbali za madini, samaki, pamba, nyama na maziwa.

‎"Katika kanda ya Ziwa, amkeni mkamate biashara za maeneo yote ambayo yanazungukwa na Ziwa Victoria - Tanzania, Kenya, Uganda na kote ambako uwepo wa meli unarahishisha mambo, pia fursa zilizopo DRC, Sudan Kusini, Rwanda, Burundi" amesisitiza Msigwa.

‎Kwa mujibu wa Msigwa, mafanikio ya ujenzi wa meli hiyo ni moja ya mambo makubwa ya kujivunia kwa watanzania wakiwa na kila sababu ya kutembea kifua mbele kwa kuwa na serikali yenye maono na dhamira ya kuwekeza katika mambo makubwa ambayo yatatoa mchango mkubwa katika mageuzi ya kiuchumi.   

‎"Hii inafanya meli hii sio tu kuwa kubwa kuliko zote katika ziwa Victoria na maziwa makuu bali pia hii ndiyo meli kubwa kuliko zote katika maji baridi barani Afrika" amesema



MAKAMU WA RAIS AONGOZA MAADHIMISHO YA KILELE CHA WIKI YA MAJI 2026

 











Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa Mamlaka zinazohusika pamoja na Watanzania kwa ujumla kuweka kipaumbele katika utunzaji na ulinzi wa vya vyanzo vya maji ili kuweza kurithisha kizazi kijacho nchi inayofaa kuishi.
 
Makamu wa Rais ametoa wito huo alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Maadhimisho ya Kilele cha Wiki ya Maji kwa Mwaka 2026 na Siku ya Maji Duniani iliyofanyika katika Viwanja vya Mkwawa mkoani Morogoro leo tarehe 22 Machi 2026. Amesema ni lazima kuangalia sana umuhimu wa kulinda vyanzo vya maji kwa kufanya uwekezaji wa kimkakati ambao unaangalia kuvitunza na kuongeza vyanzo vya maji.
 
Halikadhalika, Makamu wa Rais ametoa rai kwa Wizara na Taasisi zote za Umma nchini kujenga mtandao wa ushirikiano katika kuzikabili kuzitatua na kurekebisha changamoto za maji ili dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwa na Taifa lilioondokana na changamoto za maji safi na salama iweze kufanikiwa.
 
Pia amesema, ni vema kwa Mamlaka za Maji nchini kuendelea kubuni vyanzo vipya vya mapato ili kukuza sekta ya maji. Ameipongeza Mamlaka ya Maji Tanga kwa kutumia mfumo wa Hati fungani katika kugharamia miradi ya maji inayotekelezwa mkoani humo. Makamu wa Rais amesema kila mtanzania anapaswa kuona wajibu wa utunzaji wa mazingira.
 
Vilevile, Makamu wa Rais amesema, Sekta binafsi ni mdau muhimu katika kufanikisha miradi ya maji kwa maendeleo ya sekta hiyo. Ametoa wito kwa wadau wote wa sekta ya maji kutambua kwamba maji ni muhimu na hitaji la kila mwanadamu hivyo ni vema kuendelea kushirikiana.
 
Makamu wa Rais, amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha mpango wa Gridi ya Taifa ya Maji unafanikiwa kikamilifu kwani kufanikiwa kwake ndio kuondokana na tatizo la maji nchini. Amewasihi Wizara ya Maji kuhakikisha wanafanikisha ufungaji wa mita katika maeneo ya matumizi ya maji ili kuepusha upotevu wa maji lakini pia kufanya watu wanaotumia maji kuwajibika.
 
Vilevile, Makamu wa Rais amesema Dira ya Maendeleo 2050 imelenga kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii, ambapo matarajio ni kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye uchumi wa kipato cha kati ngazi ya juu. Wakati idadi ya watu nchini ikitarajiwa kuongezeka hadi kufikia takriban watu milioni 118, inatarajiwa pia kuwa zaidi ya nusu yao watakuwa wanaishi maeneo ya mijini. Ongezeko hilo la watu linahitaji kujipanga ili kuwa na uhakika wa upatikanaji wa chakula, fursa za ajira na huduma za kijamii kama afya na elimu na maji.
 
Moja ya malengo makuu ya Sera ya Taifa ya Maji ya Mwaka 2002, Toleo la 2025 ni kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi, hususan wanaoishi vijijini. Katika utekelezaji wa Sera hii na Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, miradi mbalimbali ya maji nchini imetekelezwa na kuwezesha kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi, ambapo kwa sasa vijijini huduma hiyo imefikia wastani wa 85.2%, na mjini wastani wa 92.5%. Jumla ya Vijiji 10,758 vimefikiwa na huduma ya maji, vikisalia Vijiji 1,575 ambavyo Wizara ya Maji imezindua kampeni maalum ya kuhakikisha inafikisha huduma hiyo.
 
Kwa upande wake, Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha vema Wizara ya Maji kutekeleza miradi kwa ufanisi. Ameongeza kwamba, Wizara hiyo haitokuwa kikwazo katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.
 
Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais amezindua Mfumo wa Utabiri wa Kiasi cha Maji kwenye mito nchini Tanzania. Uzinduzi huo umefanyika katika la Bwawa la Mindu Mjini Morogoro. Mfumo huo ni moja ya jitihada za Wizara ya Maji kuhakikishia inaondoa changamoto za Sekta kwa kuwezesha upatikanani wa taarifa sahihi za kiwango cha Maji katika mito yote nchini.
 
Pamoja na uzinduzi huo, Makamu wa Rais amepanda miti rafiki wa maji kwenye chanzo hicho ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Maji Duniani na kilele cha Wiki ya Maji Tanzania.
 
Maadhimisho hayo yana kaulimbiu isemayo “Maji na Usawa wa Kijinsia” (Water and Gender) yikilenga kutafakari kwa kina uhusiano uliopo kati ya upatikanaji wa maji safi na usawa wa kijinsia katika jamii. Ripoti ya Umoja wa Afrika kwenye Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu Maji (mwaka 2023) inaonesha kuwa Afrika, kusini mwa Jangwa la Sahara inapoteza 5% ya Pato lake la Taifa kwa mwaka (takriban Dola za Marekani Bilioni 170) kutokana na ukosefu wa maji, matumizi ya maji yasiyo salama na ukosefu wa huduma bora za usafi wa mazingira.
 
Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
22 Machi 2026
Morogoro.

Friday, March 20, 2026

MFALME WA SWEDEN AMUAGA BALOZI MATINYI

 

Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, akiwa katika picha ya pamoja na Mfalme wa Sweden, Carl XVI Gustaf, wakati alipokwenda kumuaga katika Jumba la Kifalme jijini Stockholm, tarehe 19 Machi, 2026 (Picha kwa hisani ya Jumba la Kifalme).

.......................................................


Mfalme Carl XVI Gustaf wa Sweden, amemuaga aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, katika hafla fupi iliyofanyika kwenye Jumba la Kifalme jijini Stockholm, jana tarehe 19 Machi, 2026.

 

Katika mazungumzo yao mafupi, viongozi hao walijadiliana namna ya kuendelea kuimarisha ushirikiano baina ya nchi hizi mbili katika sekta za nishati, mazingira, kilimo, utalii, miundombinu, madini na teknolojia.

 

Mfalme Gustaf aliipongeza Tanzania kwa kuweka utulivu nchini na kubuni mipango thabiti ya kutafuta maendeleo na kukuza uchumi wake licha ya changamoto nyingi zinazoikabili dunia nzima hivi sasa.

 

Balozi Matinyi alimshukuru Mfalme Gustaf kwa ushirikiano mzuri alioupata katika kipindi alichohudumu nchini Sweden ambapo Tanzania imefaidika katika sekta za nishati, kilimo, miundombinu, teknolojia na elimu ya juu.

 

Hii ilikuwa mara ya tatu kwa Balozi Matinyi kukutana na Mfalme Gustaf tangu awasili nchini Sweden mwezi Mei 2025. Mara ya kwanza ilikuwa wakati wa kukabidhi hati zake za utambulisho tarehe 12 Juni, 2025, na tarehe 9 Desemba, 2025, kwenye mazungumzo ya kibalozi ya mwisho wa mwaka.

 

Imetolewa na Ubalozi wa Tanzania, Stockholm, Sweden,

19 Machi, 2026.


Sunday, March 8, 2026

JET YAPONGEZA JUHUDI ZA WANAWAKE KATIKA KUTUNZA MAZINGIRA.

 


Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET) kinawatakia heri wanawake wote nchini na duniani katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani leo Machi 8,2026.


JET inatambua mchango mkubwa wa mwanamke katika kulinda na kuhifadhi mazingira. 


Kwa muda mrefu wanawake wamekuwa mstari wa mbele katika matumizi ya rasilimali asilia ndani ya familia na jamii, hivyo kuwa na nafasi muhimu katika kuhakikisha mazingira yanatunzwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.


 Mwanamke ndiye mlezi wa familia na mara nyingi ndiye anayehusika moja kwa moja na matumizi ya nishati ya kupikia, maji, na rasilimali nyingine muhimu za mazingira.



Kupitia nafasi hiyo, wanawake wameendelea kuwa kichocheo muhimu cha utunzaji wa mazingira, kwa kuhamasisha matumizi bora ya rasilimali, kupunguza uharibifu wa misitu, na kuhimiza mbinu rafiki kwa mazingira katika shughuli za kila siku za kijamii na kiuchumi.


Katika maadhimisho haya, JET pia inatoa pongezi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake thabiti katika kulinda mazingira, hususan kupitia ajenda ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini. 


Hatua hii ni muhimu katika kupunguza ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa, kuboresha afya za wananchi, na kuchangia juhudi za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.


JET inaamini kuwa juhudi hizi zina mchango mkubwa katika kuimarisha maendeleo endelevu na kulinda mifumo ya ikolojia ambayo ndiyo msingi wa ustawi wa jamii na uchumi wa Taifa.


Aidha, JET inatoa wito kwa wadau wote—serikali, sekta binafsi, asasi za kiraia na jamii kwa ujumla—kuendelea kuwawezesha wanawake kwa elimu, teknolojia na rasilimali zitakazowawezesha kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wa mazingira. 


Uwezeshaji wa wanawake katika masuala ya mazingira ni uwekezaji wa moja kwa moja katika mustakabali wa Taifa na dunia kwa ujumla.


Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania kitaendelea kutumia taaluma ya uandishi wa habari kuelimisha umma, kuhamasisha uwajibikaji, na kukuza uelewa kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira kwa maendeleo endelevu.


Imetolewa na:

John Chikomo

Kwa niaba ya

Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET)

Thursday, February 12, 2026

SERIKALI YASHUSHA ADA KWA WANABLOGU.


SERIKALI YASHUSHA ADA KWA WANABLOGU.


TCRA Yazindua Redio ya Kisasa 'DSB'


SERIKALI imetangaza neema ya kihistoria kwa wanablogu, vijana wabunifu, na watoa maudhui mtandaoni nchini kwa kupunguza ada za leseni kwa kiwango kikubwa, hatua inayolenga kuchochea ukuaji wa uchumi wa kidijitali na kurasimisha shughuli za wahabarishaji wa mitandao.


Hatua hiyo imekuja kufuatia utafiti wa kina na mikutano ya kimkakati ya takribani mwaka mzima kati ya mtandao wa Tanzania Bloggers Network (TBN) na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ikielezea vikwazo vya gharama vilivyokuwa vikikwaza uandishi wa habari za kidijitali nchini.


Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Watoa Huduma za Utangazaji (ABC 2026) jijini Dodoma leo, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamisi Mwinjuma, amesema ada ya leseni kwa watoa maudhui mtandaoni imeshushwa kutoka Sh500,000 hadi Sh50,000 tu, huku ada ya maombi ikiwa ni Sh10,000 pekee.


Mageuzi hayo pia yamegusa kundi la wakusanyaji wa maudhui (Online Content Aggregators), ambao ada yao imeshushwa kutoka Sh1,000,000 hadi Sh100,000 pekee. Aidha, kundi la "Amateteur" limeanzishwa kwa ajili ya vijana wanaochipukia ili waweze kujitambulisha rasmi na kukuza vipaji vyao bila vikwazo vya kifedha.


Mapinduzi ya Teknolojia ya DSB

Wakati neema hiyo ikitangazwa, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabiri Bakari, ametangaza kuanza kwa teknolojia mpya ya utangazaji wa redio ya kidijitali nchini inayojulikana kama Digital Sound Broadcasting (DSB).


Teknolojia hiyo itaanza kufanya kazi katika mikoa mitano ya majaribio ya Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Arusha, na Mbeya, lengo likiwa ni kuongeza ubora wa sauti na huduma za utangazaji nchini.


"Tumekamilisha maandalizi yote ya kiudhibiti na watoa huduma wa miundombinu wameshapatikana. Hii ni hatua kubwa ya kuendana na mabadiliko ya teknolojia duniani na kuimarisha utangazaji, hususan maeneo ya vijijini," alisema Dkt. Bakari.


Utafiti: Redio Bado ni Kinara

Katika mkutano huo, Injinia Andrew Kisaka wa TCRA amewasilisha matokeo ya utafiti wa hali ya utangazaji kwa mwaka 2025/2026, ukionyesha kuwa redio inaendelea kuwa chanzo kikuu cha habari kwa asilimia 85 ya Watanzania. Hata hivyo, utafiti huo umebaini ukuaji mkubwa wa matumizi ya intaneti miongoni mwa vijana, ambapo asilimia 45 hupata habari kupitia mitandao ya kijamii kabla ya kusikiliza redio au kutazama televisheni.


Upande wa televisheni, utafiti unaonyesha asilimia 65 ya watazamaji wanatumia ving'amuzi, huku maudhui ya ndani yakipendwa zaidi kwa asilimia 70. Serikali imewahimiza watoa huduma za kienyeji kuwekeza zaidi kwenye majukwaa ya kidijitali (OTT) ili kukidhi mahitaji ya soko la sasa.


Ulinzi wa Hakimiliki na Mikopo

Ili kuhakikisha wanahabari wa kidijitali wanufaika na kazi zao, Serikali imezielekeza taasisi za COSOTA na TCRA kuandaa mpango wa kulinda hakimiliki na kudhibiti uharamia mtandaoni. Aidha, Serikali imeanza kutoa mikopo ya masharti nafuu kwa watengeneza maudhui kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kisasa vya kufanyia kazi.


Hadi kufikia Desemba 2025, TCRA imetoa jumla ya leseni 707 za utangazaji, zikiwemo 318 za maudhui mtandaoni, jambo linaloashiria kukua kwa uhuru wa habari na demokrasia nchini chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.