Thursday, February 12, 2026

SERIKALI YASHUSHA ADA KWA WANABLOGU.


SERIKALI YASHUSHA ADA KWA WANABLOGU.


TCRA Yazindua Redio ya Kisasa 'DSB'


SERIKALI imetangaza neema ya kihistoria kwa wanablogu, vijana wabunifu, na watoa maudhui mtandaoni nchini kwa kupunguza ada za leseni kwa kiwango kikubwa, hatua inayolenga kuchochea ukuaji wa uchumi wa kidijitali na kurasimisha shughuli za wahabarishaji wa mitandao.


Hatua hiyo imekuja kufuatia utafiti wa kina na mikutano ya kimkakati ya takribani mwaka mzima kati ya mtandao wa Tanzania Bloggers Network (TBN) na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ikielezea vikwazo vya gharama vilivyokuwa vikikwaza uandishi wa habari za kidijitali nchini.


Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Watoa Huduma za Utangazaji (ABC 2026) jijini Dodoma leo, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamisi Mwinjuma, amesema ada ya leseni kwa watoa maudhui mtandaoni imeshushwa kutoka Sh500,000 hadi Sh50,000 tu, huku ada ya maombi ikiwa ni Sh10,000 pekee.


Mageuzi hayo pia yamegusa kundi la wakusanyaji wa maudhui (Online Content Aggregators), ambao ada yao imeshushwa kutoka Sh1,000,000 hadi Sh100,000 pekee. Aidha, kundi la "Amateteur" limeanzishwa kwa ajili ya vijana wanaochipukia ili waweze kujitambulisha rasmi na kukuza vipaji vyao bila vikwazo vya kifedha.


Mapinduzi ya Teknolojia ya DSB

Wakati neema hiyo ikitangazwa, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabiri Bakari, ametangaza kuanza kwa teknolojia mpya ya utangazaji wa redio ya kidijitali nchini inayojulikana kama Digital Sound Broadcasting (DSB).


Teknolojia hiyo itaanza kufanya kazi katika mikoa mitano ya majaribio ya Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Arusha, na Mbeya, lengo likiwa ni kuongeza ubora wa sauti na huduma za utangazaji nchini.


"Tumekamilisha maandalizi yote ya kiudhibiti na watoa huduma wa miundombinu wameshapatikana. Hii ni hatua kubwa ya kuendana na mabadiliko ya teknolojia duniani na kuimarisha utangazaji, hususan maeneo ya vijijini," alisema Dkt. Bakari.


Utafiti: Redio Bado ni Kinara

Katika mkutano huo, Injinia Andrew Kisaka wa TCRA amewasilisha matokeo ya utafiti wa hali ya utangazaji kwa mwaka 2025/2026, ukionyesha kuwa redio inaendelea kuwa chanzo kikuu cha habari kwa asilimia 85 ya Watanzania. Hata hivyo, utafiti huo umebaini ukuaji mkubwa wa matumizi ya intaneti miongoni mwa vijana, ambapo asilimia 45 hupata habari kupitia mitandao ya kijamii kabla ya kusikiliza redio au kutazama televisheni.


Upande wa televisheni, utafiti unaonyesha asilimia 65 ya watazamaji wanatumia ving'amuzi, huku maudhui ya ndani yakipendwa zaidi kwa asilimia 70. Serikali imewahimiza watoa huduma za kienyeji kuwekeza zaidi kwenye majukwaa ya kidijitali (OTT) ili kukidhi mahitaji ya soko la sasa.


Ulinzi wa Hakimiliki na Mikopo

Ili kuhakikisha wanahabari wa kidijitali wanufaika na kazi zao, Serikali imezielekeza taasisi za COSOTA na TCRA kuandaa mpango wa kulinda hakimiliki na kudhibiti uharamia mtandaoni. Aidha, Serikali imeanza kutoa mikopo ya masharti nafuu kwa watengeneza maudhui kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kisasa vya kufanyia kazi.


Hadi kufikia Desemba 2025, TCRA imetoa jumla ya leseni 707 za utangazaji, zikiwemo 318 za maudhui mtandaoni, jambo linaloashiria kukua kwa uhuru wa habari na demokrasia nchini chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.











Friday, December 19, 2025

ITHIBATI YA WAANDISHI WA HABARI NI NGAO YA TAIFA KATIKA VITA.

 


Ithibati ya waandishi wa habari imeendelea kujidhihirisha kama nguzo muhimu ya ulinzi wa Taifa katika dunia ya sasa inayotawaliwa na vita ya taarifa.
 

Kupitia Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), inayotoa ithibati na vitambulisho vya uandishi wa habari kwa waandishi wenye vigezo kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Taifa linapata waandishi wanaotambulika, wanaowajibika na wanaofanya kazi kwa kufuata misingi ya taaluma, weledi na maadili. 


Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Greyson Msigwa, wakati akizungumza katika kikao kazi na waandishi wa habari kilichoratibiwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) tarehe 18 Desemba 2025 jijini Dar es Salaam. 


Amesema kuwa hatua hiyo inasaidia kudhibiti upotoshaji wa taarifa na kulinda taswira ya nchi ndani na nje ya mipaka yake kwani dunia ya sasa haipigani tena vita kwa silaha za kijeshi pekee, bali kwa taarifa zinazozalishwa na kusambazwa kupitia mitandao ya kijamii.


Amesisitiza kuwa katika mazingira hayo, waandishi waliothibitishwa wanakuwa mstari wa mbele kulinda usalama wa Taifa kupitia taarifa sahihi, zenye weledi na uzalendo. 


Bw. Msigwa ameongeza kuwa kipindi kigumu kilichopita kimeonesha wazi jinsi taarifa potofu zinavyoweza kuchochea taharuki na kuathiri mshikamano wa kijamii.


Hata hivyo, amepongeza waandishi wa habari wa Tanzania, hususan wazalishaji wa maudhui mtandaoni, kwa kuonesha uzalendo na nidhamu ya taaluma kwa kutokutumia kalamu zao vibaya, licha ya shinikizo kubwa la mitandao na madai ya nje kwamba waandishi wa Tanzania ni dhaifu.


Kwa mujibu wa Msemaji Mkuu wa Serikali, ithibati si kikwazo cha uhuru wa habari bali ni nyenzo ya kulinda taaluma na waandishi wenyewe. Waandishi waliothibitishwa wanatambulika rasmi kama wadau wa ulinzi wa Taifa na taarifa wanazozalisha zinakuwa silaha ya kulinda amani, umoja na uthabiti wa nchi badala ya kuchochea migawanyiko.







SERIKALI YAAHIDI ULINZI NA USHIRIKIANO KWA WAANDISHI WA MTANDAONI.

 


Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kulea na kuwawezesha waandishi wa habari wa mitandaoni na mabloga, badala ya kuwashughulikia kwa mtazamo wa adhabu, ili kujenga tasnia imara na yenye tija ya habari nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, na Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, aliipongeza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa mwelekeo wake wa kulea wadau wa sekta ya habari badala ya kuchukua hatua kali za kinidhamu.

Msigwa alisema mwelekeo huo unaendana na falsafa ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambayo inalenga kushirikiana na wadau mbalimbali kwa manufaa ya taifa.

Aliitaja Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jukwaa la Mitandao Tanzania (JUMIKITA) kuwa ni wadau wakubwa wa serikali katika tasnia ya habari, akisisitiza kuwa mchango wao ni muhimu katika kusambaza taarifa na kujenga mawasiliano kati ya serikali na wananchi.

“Serikali imewaamini waandishi wa mitandaoni, sasa nanyi muendelee kuonesha imani kwa serikali. Ushirikiano wetu umeendelea kuimarika na changamoto zinazojitokeza tunazitatua kwa pamoja,” alisema Msigwa.

Akikanusha madai kuwa waandishi wa habari wa mitandaoni ni dhaifu, Msigwa alisema wanatekeleza wajibu wao ipasavyo na wana nafasi kubwa ya kutumia kalamu zao kujenga taifa.

“Nimekuwa nikisisitiza waandishi tutumie kalamu zetu kujenga nchi. Mnafanya kazi sahihi na mnalinda maslahi ya taifa,” aliongeza.

Msigwa aliwahakikishia waandishi ulinzi wa serikali, akisema endapo sheria, kanuni au sera zitabainika kuwa kikwazo katika utendaji wao, zitafanyiwa marekebisho kwa maslahi mapana ya taifa.

Alitangaza pia kuanza kwa maandalizi ya mafunzo kwa waandishi wa habari kwa kushirikiana na TCRA, akiwataka kuyapokea kwa mtazamo chanya kama sehemu ya kuongeza weledi na taaluma.

Kuhusu masuala ya kodi, Msigwa alisema serikali itaendelea kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili kutatua changamoto zinazowakabili waandishi wa mitandaoni, akitambua mchango wao katika kuitangaza nchi na kuvutia uwekezaji.

Aidha, alieleza kuwa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo ipo katika mchakato wa kuanzisha mfuko maalum kwa ajili ya kuwawezesha waandishi wa habari, hususan wa mitandaoni.

Akizungumzia mazingira ya sasa ya kimataifa, Msigwa alisema vita vya dunia ya sasa vimehama kutoka silaha za kijeshi kwenda kwenye taarifa, akisisitiza kuwa vyombo vya habari vina jukumu kubwa la kulinda na kuipromote nchi.

Aliwahimiza waandishi kuhakikisha majukwaa yao yanatumika kulinda maslahi ya taifa na kuonya dhidi ya matumizi mabaya ya mitandao yanayoweza kuharibu taswira ya Tanzania.

Hata hivyo, Msigwa alionesha kusikitishwa na tabia ya baadhi ya waandishi kunyamaza wanapodhalilishwa, akiwataka kusimama na kulinda hadhi ya taaluma yao.




Thursday, December 18, 2025

HALMASHAURI YA MJI BAGAMOYO YAKABIDHI VIFAA VYA TEHAMA KWA WALIMU WAKUU.

 


Halmashauri ya mji wa Bagamoyo, imekabidhi vifaa vya TEHAMA kwa walimu wakuu wa shule za kata za Zinga, Dunda na Kata ya Yombo.



Makabidhiano hayo yameongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo Mhe Mohamedi Usinga  Desemba 17,2025.


Katika makabidhiano hayo Mhe Mwenyekiti amekabidhi jumla ya komputa (Desktop)44 katika Shule ya Msingi Yombo wamepata Komputa 20,shule ya Msingi Kizuiani 12 na Shule ya Zinga 12 pamoja na Komputa Mpakato moja kwa kila shule na vifaa vyake kwa ujumla.


Mhe Usinga ametoa wito kwa walimu hao kuhakikisha wanavitunza na kuvilinda vifaaa hivyo kwa ajili ya kujifunzia kwa wanafunzi mashuleni ili kuendana na kasi ya teknologia.


Vilevile Mhe Mwenyekiti ametoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha anawezesha upatikanaji wa vifaa vya Tehama mashuleni lakini pia na kuwezesha miundombinu bora mashuleni.


Nae Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo Ndg Shauri Selenda amewasisitiza walimu hao kuhakikisha wanavitunza vifaa hivyo Pamoja na kuhakikisha wanatoa elimu iliyobora kwa wanafunzi ili kujenga msingi bora wa elimu katika Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo.


Aidha Ndg Selenda ametoa shukrani kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais Samia Suluhu Hassani kwa kuhakikisha kila shule inakuwa na miundombinu bora lakini pia inapata vifaa vya kujifunzia mashuleni.


Kadhalika Afisa Elimu awali na Msingi Bi Wema Kajigili akitoa shukrani kwa niaba ya Walimu hao wote amesema kuwa “naendelea kutoa shukrani kwa Rais Samia Suluhu Hassani Pamoja na wadau wote wa elimu nchini vifaa hivi tutahakikisha tunavitunza na kuvilinda na kuhakikisha mwanafunzi ananufaika na vifaa hivi kwa kuwapatia elimu bora”.Bi  Wema Kajigili.