Na Albert Kawogo, BAGAMOYO: Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amezitaka shule kutumia ipasavyo karakana zinazojengwa katika utekelezaji wa mtaala ulioboreshwa ili kuwawezesha vijana kupata ujuzi, kukuza vipaji na kujenga uwezo wa kujiajiri. Kikwete amesema karakana hizo hazipaswi kufunguliwa au kutumika wakati wa ziara za viongozi pekee, bali zinapaswa kuwa sehemu muhimu ya mazingira ya kujifunzia na kuwaandaa vijana kwa maisha ya baadaye. Amesema Taifa haliwezi kujengwa kwa kutegemea vyeti pekee, bali linahitaji watu wenye uwezo wa kutumia maarifa yao kutatua changamoto na kubadilisha changamoto hizo kuwa fursa za kiuchumi. “Endapo karakana hizi zitatumika vizuri, zitaibua fani na vipaji vya watoto na kuwafanya kuwa wabunifu, jambo ambalo litawasaidia kujiajiri na kuajirika katika maeneo mbalimbali hapa nchini,” amesema Kikwete. Waziri huyo ameyasema hayo Agosti 15 alipokuwa akizungumza katika sherehe za maadhimish...