JITIHADA ZA RAIS SAMIA KUIWEKA TANZANIA KAMA KITOVU CHA UCHUMI WA NCHI ZA MAZIWA MAKUU KUPITIA BANDARI YA DAR ES SALAAM
Na Albert Kawogo Tanzania inaendelea kujijengea nafasi muhimu katika uchumi wa Afrika Mashariki na Kati, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan za kuifanya nchi kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji kwa nchi za ukanda wa Maziwa Makuu. Miongoni mwa nguzo muhimu katika kufanikisha azma hiyo ni Bandari ya Dar es Salaam, ambayo imekuwa lango kuu la biashara kwa Tanzania na nchi jirani zisizo na bandari, hususan Burundi, Rwanda, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Zambia na Malawi. Uwekezaji katika kuboresha miundombinu ya bandari, kuongeza ufanisi wa upakuaji na upakiaji wa mizigo, kupunguza muda wa meli kukaa bandarini na kurahisisha taratibu za forodha ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kuongeza ushindani wa Bandari ya Dar es Salaam. Rais Samia amekuwa akisisitiza umuhimu wa Tanzania kutumia nafasi yake ya kijiografia na miundombinu yake kuimarisha biashara ya kikanda. Kwa kuwa Tanzania ina mwambao mrefu...