Tuesday, March 24, 2026
Monday, March 23, 2026
SERIKALI YAHIMIZA MELI YA NEW MV MWANZA KUKUZA UCHUMI, UTALII KANDA YA ZIWA.
Serikali imetoa wito kwa wafanyabiashara, wasafirishaji na wawekezaji mbalimbali kutumia fursa ya meli mpya ya MV New Mwanza kibiashara na kiutalii ili kukuza uchumi wa Kanda ya Ziwa.
Itakumbukwa meli hiyo imejengwa kwa zaidi ya Tsh. Bilioni 120, ikiwa na uwezo wa kubeba abiria 1,200, tani 400 za mizigo, magari makubwa matatu na madogo, ambapo itafanya safari zake katika bandari zote zinazozunguka Ziwa Victoria ikiwemo Kisumu (Kenya), Port Bay (Uganda) na Kemondo (Bukoba).
Akizungumza Jumapili Machi 22, 2026 na waandishi wa habari katika bandari ya Mwanza Kusini jijini Mwanza ilipoegeshwa meli hiyo, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema kutokana na uwekezaji huo wakazi wa Kanda ya Ziwa, wawekezaji na wafanyabiashara wakubwa na wadogo wanapaswa kuitumia kwenye shughuli zao na kuleta tija ya uwekezaji huo mkubwa.
Amesema Serikali imetimiza jukumu lake la kutekeleza wajibu wa kujenga mazingira mazuri ya biashara, uwekezaji na ustawi wa jamii, hivyo mpira sasa unahamia kwa wananchi kuitumia ili kulinufaisha taifa na malengo yaliyokusudiwa yafikiwe.
"Nawaombeni mkiiona New MV Mwanza, oneni suluhuhisho la uhakika la usafiri na usafirishaji wa abiria na mizigo, oneni fursa muhimu na adhimu ya utalii" amesema Msigwa na kuongeza;
"Serikali inategemea kuona utalii unakua kwa kasi hapa Mwanza, Bukoba na kwingine, watalii waje hapa Mwanza kisha waingie Serengeti, waende Rubondo, Burigi- Chato na kwingineko" amesema.
Ameongeza kuwa, wafanyabiashara na wawekezaji wanapaswa kuiona meli hiyo kama suluhisho la uhakika la kukua kwa biashara mbalimbali za madini, samaki, pamba, nyama na maziwa.
"Katika kanda ya Ziwa, amkeni mkamate biashara za maeneo yote ambayo yanazungukwa na Ziwa Victoria - Tanzania, Kenya, Uganda na kote ambako uwepo wa meli unarahishisha mambo, pia fursa zilizopo DRC, Sudan Kusini, Rwanda, Burundi" amesisitiza Msigwa.
Kwa mujibu wa Msigwa, mafanikio ya ujenzi wa meli hiyo ni moja ya mambo makubwa ya kujivunia kwa watanzania wakiwa na kila sababu ya kutembea kifua mbele kwa kuwa na serikali yenye maono na dhamira ya kuwekeza katika mambo makubwa ambayo yatatoa mchango mkubwa katika mageuzi ya kiuchumi.
"Hii inafanya meli hii sio tu kuwa kubwa kuliko zote katika ziwa Victoria na maziwa makuu bali pia hii ndiyo meli kubwa kuliko zote katika maji baridi barani Afrika" amesema
MAKAMU WA RAIS AONGOZA MAADHIMISHO YA KILELE CHA WIKI YA MAJI 2026
Friday, March 20, 2026
MFALME WA SWEDEN AMUAGA BALOZI MATINYI
Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare
Matinyi, akiwa katika picha ya pamoja na Mfalme wa Sweden, Carl XVI Gustaf,
wakati alipokwenda kumuaga katika Jumba la Kifalme jijini Stockholm, tarehe 19
Machi, 2026 (Picha kwa hisani ya Jumba la Kifalme).
.......................................................
Mfalme Carl XVI Gustaf wa Sweden, amemuaga aliyekuwa Balozi
wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, katika hafla fupi iliyofanyika
kwenye Jumba la Kifalme jijini Stockholm, jana tarehe 19 Machi, 2026.
Katika mazungumzo yao mafupi, viongozi hao walijadiliana
namna ya kuendelea kuimarisha ushirikiano baina ya nchi hizi mbili katika sekta
za nishati, mazingira, kilimo, utalii, miundombinu, madini na teknolojia.
Mfalme Gustaf aliipongeza Tanzania kwa kuweka utulivu nchini
na kubuni mipango thabiti ya kutafuta maendeleo na kukuza uchumi wake licha ya
changamoto nyingi zinazoikabili dunia nzima hivi sasa.
Balozi Matinyi alimshukuru Mfalme Gustaf kwa ushirikiano
mzuri alioupata katika kipindi alichohudumu nchini Sweden ambapo Tanzania
imefaidika katika sekta za nishati, kilimo, miundombinu, teknolojia na elimu ya
juu.
Hii ilikuwa mara ya tatu kwa Balozi Matinyi kukutana na
Mfalme Gustaf tangu awasili nchini Sweden mwezi Mei 2025. Mara ya kwanza
ilikuwa wakati wa kukabidhi hati zake za utambulisho tarehe 12 Juni, 2025, na
tarehe 9 Desemba, 2025, kwenye mazungumzo ya kibalozi ya mwisho wa mwaka.
Imetolewa na Ubalozi wa Tanzania, Stockholm, Sweden,
19 Machi, 2026.
Sunday, March 8, 2026
JET YAPONGEZA JUHUDI ZA WANAWAKE KATIKA KUTUNZA MAZINGIRA.
Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET) kinawatakia heri wanawake wote nchini na duniani katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani leo Machi 8,2026.
JET inatambua mchango mkubwa wa mwanamke katika kulinda na kuhifadhi mazingira.
Kwa muda mrefu wanawake wamekuwa mstari wa mbele katika matumizi ya rasilimali asilia ndani ya familia na jamii, hivyo kuwa na nafasi muhimu katika kuhakikisha mazingira yanatunzwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Mwanamke ndiye mlezi wa familia na mara nyingi ndiye anayehusika moja kwa moja na matumizi ya nishati ya kupikia, maji, na rasilimali nyingine muhimu za mazingira.
Kupitia nafasi hiyo, wanawake wameendelea kuwa kichocheo muhimu cha utunzaji wa mazingira, kwa kuhamasisha matumizi bora ya rasilimali, kupunguza uharibifu wa misitu, na kuhimiza mbinu rafiki kwa mazingira katika shughuli za kila siku za kijamii na kiuchumi.
Katika maadhimisho haya, JET pia inatoa pongezi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake thabiti katika kulinda mazingira, hususan kupitia ajenda ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.
Hatua hii ni muhimu katika kupunguza ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa, kuboresha afya za wananchi, na kuchangia juhudi za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
JET inaamini kuwa juhudi hizi zina mchango mkubwa katika kuimarisha maendeleo endelevu na kulinda mifumo ya ikolojia ambayo ndiyo msingi wa ustawi wa jamii na uchumi wa Taifa.
Aidha, JET inatoa wito kwa wadau wote—serikali, sekta binafsi, asasi za kiraia na jamii kwa ujumla—kuendelea kuwawezesha wanawake kwa elimu, teknolojia na rasilimali zitakazowawezesha kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wa mazingira.
Uwezeshaji wa wanawake katika masuala ya mazingira ni uwekezaji wa moja kwa moja katika mustakabali wa Taifa na dunia kwa ujumla.
Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania kitaendelea kutumia taaluma ya uandishi wa habari kuelimisha umma, kuhamasisha uwajibikaji, na kukuza uelewa kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira kwa maendeleo endelevu.
Imetolewa na:
John Chikomo
Kwa niaba ya
Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET)








































































