Na Allan Kitwe, Tabora JESHI la Polisi Mkoani Tabora limekamata jumla ya watuhumiwa 128 na kuwafikisha mahakamani kwa makosa mbalimbali ikiwemo wizi, ubakaji, mauaji, kujeruhi na kuharibu mali, ambapo 16 kati yao wamehukumiwa kifungo. Kamanda wa Polisi Mkoani hapa Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Twaha Lulengelule amethibitisha kukamatwa watuhumiwa hao na kufikishwa mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake. Amefafanua kuwa watuhumiwa hao wamekamatwa katika oparesheni maalumu iliyofanywa na askari polisi kuanzia Julai 1 mwaka huu hadi sasa katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo kwa lengo la kuimarisha amani na usalama. Kamanda Lulengelule, amebainisha kuwa miongoni mwa watuhumiwa hao, 16 walioswekwa jela wapo waliohusika na makosa ya mauaji, ubakaji, wizi wa mali za watu, kujeruhi, kuharibu mali, kutishia kuua kwa silaha, shambulio la mwili na kutelekeza mtoto. Ametaja aliyehukumiwa kwa kosa la kubaka kuwa ni Shaban Haruna Kilingo ambaye amefungwa miaka 30 jela huku Isack Ma...