Monday, December 31, 2018

RAIS WA ZANZIBAR DKT. SHEIN ATOA SALAMU ZA MWAKA MPYA 2019

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akitoa salamu za Mwaka Mpya wa 2019, Ikulu Zanzibar.(Picha na Ikulu)

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wananchi  wa Zanzibar kuendelea kuidumisha hali ya amani na utulivu ambayo ndio msingi wa mafanikio yanayoendelea kupatikana hivi sasa na yatakayopatikana hapo baadae.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika risala yake ya kuukaribisha mwaka mpya wa 2019 aliyoitoa kupitia vyombo vya habari, Ikulu mjini Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisema kuwa katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya mwaka 2018 mafanikio makubwa yamepatikana ambayo yamechangiwa na kuwepo kwa amani, mshikamano, umoja na mapenzi yaliopo.

Katika risala yake hiyo Rais Dk. Shein alieleza kuwa hali ya amani, umoja na mshikamano uliopo nchini ni jambo muhimu linalowavutia Washirika wa maendeleo ambao wanaridhika na jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na ndio maana wanaiunga mkono katika mipango yake ya maendeleo.

Alisema kuwa hapana shaka kwamba iwapo amani, usalama na utulivu vitadumishwa na kufanya kazi kwa bidii Washirika wa Maendeleo watakuwa pamoja na Zanzibar katika kuisaidia ili kuweza kutekeleza malengo yaliyopangwa.

Rais Dk. Shein alitoa shukurani kwa wananchi wote kwa kuunga mkono juhudiza serikali za kuiletea maendeleo Zanzibar na kueleza kuwa moyo wao huo wa umoja na mshikamano umewezesha kuimarisha vizuri hali ya uchumi wa Zanzibar.

Hata hivyo, Dk. Shein alitoa shukurani nyingi kwa wananchi wote kwa kuunga mkono juhudi za Serikali za kuiletea maendeleo Zanzibar ambapo moyo wao huo wa umoja na mshikamano umewezesha kuimarisha vizuri hali ya uchumi wa Zanzibar.

“Tukiwa tunaukaribisha mwaka mpya wa 2019, nachukua fursa hii kwa niaba ya wananchi wote  wa Zanzibar kuwashukuru kwa dhati  Washirika wetu wa Maendeleo kwa kuendelea kutuunga mkono, tunathamini mikopo, misaada na ushauri tulioupata kutoka kwao”, alisema Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa wakati unakaribishwa mwaka 2019 ni wajibu wa kila Taasisi ya Serikali ikajipima namna inavyoendelea kutekeleza mambo yaliyoagizwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015-2020.

“Nawakumbusha viongozi wenzangu viongozi wenzangu wote wa CCM tuliochaguliwa na wananchi katika Uchaguzi Mkuu wa 2015, uliorudiwa mwezi Machi, 2016. Kadhalika jukumu hili wanapaswa walizingatie na wale wote niliowateua katika nyadhifa mbali mbali”,alisema Dk. Shein katika risala yake hiyo.

Katika risala yake hiyo Rais Dk. Shein alizitaja kumbukumbu za matukio yalitokea katika mwaka 2018 ikiwa ni pamoja na utiaji wa saini wa Mkataba wa Mgawanyo wa Uzalishaji wa Mafuta na Gesi Asilia (PSA), baina ya Kampuni ya Maendeleo ya Mafuta na Gesi Asilia na kampuni ya RAK GAS ya Ras Al Khaimah.

Aliongeza kuwa tukio jengine la kihistoria ni kufanyika kwa Tamasha la Utalii la Kimataifa ambalo lilihudhuriwa na Makampuni 150 ya Utalii ya ndani na nje ya nchi ambalo lilileta mafanikio katika kuwaunganisha wafanyabiashara wa utalii wa Zanzibar na wale wa Kimataifa na kuitangaza Zanzibar katika masoko ya Kimataifa.

Alieleza kuwa mwaka 2018 umefungua milango katika utekelezaji wa dhamira ya kuendeleza kilimo cha mpunga kwa njia ya umwagiliaji maji na utumiaji wa zana za kisasa ambapo tarehe 6 Disemba, 2018 Serikali ilitiliana saini Mkataba wa Ujenzi wa Miundombinu ya Kilino cha Umwagiliaji maji na Kampuni ya Kokon Hansol JV ya Jamhuri ya Korea kupitia Shirika la Maendeleo la nchi hiyo.

Pia, Rais Dk. Shein alieleza kuwa katika lengo la kuungana na nchi nyengine katika kuendeleza uchumi wa Bahari tarehe 26 hadi 28 aliongoza Ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mkutano wa Kimataifa uliofanyika Nairobi nchini Kenya.

Alisisitiza kuwa kwa upande wa Zanzibar inauanza mwaka 2019 ikiwa imejipanga kwa kutafuta njia bora za kutumia rasilimali za bahari kwa kuitumia vizuri bahari ya Hindi iliyoizunguka kwani hili ni eneo muhimu kwa uchumi wa Zanzibar.

Akieleza jambo jengine muhimu ambalo limefanyika katika mwaka 2018, Rais Dk. Shein alisema kuwa tukio linalohusu jitihada za Serikali za kuwakinga wanawake wa Zanzibar na janga la saratani ya shingo ya kizazi ambapo mnamo April 10 Mama Mwanamwema Shein alizindua rasmi Mpango wa Chanjo dhidi ya Ugonjwa wa Saratani ya Shingo wa Kizazi.

Vile vile, tarehe 5 Disemba 2018 alizindua Mpango wa Miaka Minne wa Uchunguzi wa Saratani ya Shingo ya Kizazi ambao unawajumuisha wanawake wenye umri wa miaka 21 hadi 65 kazi ambayo itafanywa kwa kushirikiana na Wataalamu kutoka Jamhuri ya Watu wa China ambapo huduma zote pamoja na matibabu zitatolewa bure.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Zanzibar inasifika kwa uzuri wake, historia yake na khulka nzuri za watu wake na hali ya usalama iliyopo ambapo Serikali nayo inafanya jitihada za kuhakikisha kwamba sifa njema ya Zanzibar ya kuwa ni sehemu salama yenye utulivu inaendelea kwua ni kichocheo cha kuwavutia wageni, watalii na wawekezaji sambamba na kurahisiha utekelezaji wa mipango ya kamedneleo.

Hivyo, mnamo tarehe 3 Novemba 2018 ulizinduliwa rasmi  Mradi wa Ulinzi wa Mji Salama ambao lengo lake ni kuhakikisha hali ya usalama kwa kutumia CCTV na vyombo vyengine vya kisasa ambapo dhamira ni kuendeleza mradi huu katika Mikoa mengine ya Unguja na Pemba hatua kwa hatua.

Licha ya mafanikio hayo yaliopatikana mwaka 2018, Rais Dk. Shein alieleza kuwa bado kunahitajika kuzidisha mapambano dhidi ya udhalilishaji wa wanwake na watoto na unyanyasaji wa kijinsia kwa vile kesi za vitendo hivyo bado zinaendelea kuripotiwa kwenye maeneo mbali mbali.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwaahidi wananchi wote kwamba wale wote watakaobainika kwamba wamehusika kwenye tukio la uvujaji wa mitihani ya kidato cha Pili kwenye sekta ya elimu watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Aliongeza kuwa tukio hilo ni la kusikitisha, linalokwenda kinyume na mipango ya maendeleo ya elimu ambalo halijengi mustakbali mwema wa elimu kwa watoto na kuwataka wananchi kujifunza athari za tukio hilo kwa Serikali, Wizara, Walimu, Wazazi, Wanafunzi na nchi kwa jumla.

Akimalizia risala yake hiyo, Rais Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi wote kushiriki kwa wingi katika shughuli mbali mbali za kuadhimisha miaka 55 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964 zitakazofanyika katika maeneo yao kwani hizo ni sherehe zao kila mmoja ahakikishe anashiriki ipasavyo katika hatua zote.

IGP SIRRO AZINDUA RASMI CHAMA CHA WASTAAFU WA JESHI LA POLISI (TARPOA)

Mwenyekiti wa Chama cha Wastaafu wa Jeshi la Polisi (TARPOA) Kamishna Mstaafu CP Suleiman Kova (Kushoto), akimkabidhi zawadi Kamishna wa Kamisheni ya Ushirikishwaji wa Jamii Mussa Ali Mussa kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini, katika sherehe za Uzinduzi Rasmi wa chama hicho zilizofanyika mwishoni mwa juma katika bwalo la maafisa wa Polisi Oysterbay jijini Dar es salaam. Picha na Jeshi la Polisi.

Mgeni Rasmi Kamishna wa Kamisheni ya Ushirikishwaji wa Jamii CP Mussa Ali Mussa kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini, akiwaongoza aliyekuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi Mstaafu IGP Said A. Mwema (kulia) na kamishna mstaafu suleiman Kova ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Wastaafu wa Jeshi la Polisi (TARPOA) katika zoezi la kukata utepe wakati wa sherehe za Uzinduzi Rasmi wa Chama hicho zilizofanyika mwishoni mwa juma katika bwalo la maafisa wa Polisi Oysterbay jijini Dar es salaam. Picha na Jeshi la Polisi.
Baadhi ya Wastaafu wa Jeshi la Polisi ambao pia ni Wanachama wa Chama cha Wastaafu wa Jeshi hilo TARPOA wakifuatilia matukio mbalimbali yaliyokuwa yakiendelea wakati wa sherehe za Uzinduzi Rasmi wa Chama hicho kilichoanzishwa mwaka 2006 na aliyekuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi IGP Mstaafu Said Mwema. Picha na Jeshi la Polisi.

SHARIFU AWATAKA VIONGOZI WA CCM BAGAMOYO WASHIRIKIANE

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Bagamoyo Abduli Sharifu akizungumza katika semina ya siku mbili iliyoandaliwa na Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo ambayo imelenga kuwajengea uwezo watendaji wa CCM kata na makatibu wa Elima na Malezi.
...................................

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Bagamoyo Abduli Sharifu amewataka wanachama wa CCM wilayani humo kuwa na ushirikiano katika kutekeleza majukumu yao ili kukiletea maendeleo chama hicho.

Akizungumza katika semina ya siku mbili iliyoandaliwa na Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo ambayo imelenga kuwajengea uwezo watendaji wa CCM kata na makatibu wa Elimu na Malezi, Mwenyekiti Sharifu amesema siri pekee ya mafanikio ndani ya Chama ni ushirikiano katika kutekeleza majukumu.

Sharifu ameongeza kwa kusema kuwa,  Mwenyekiti wa CCM Taifa Dkt. John Magufuli anahimiza viongozi kujituma na kuzingatia maadili ya uongozi hivyo ni vyema kila kiongozi atekeleze wajibu wake katika nafasi yake aliyo nayo.

Aliwataka wanajumiya hao ambao wamepata semina ya uongozi na maadili kuyafanyia kazi yale waliyofundishwa katika semina hiyo ili kuleta maendeleo ndani ya jumuiya ya wazazi na chama kwa ujumla.

Alisisitiza kuwa, CCM wilaya ya Bagamoyo haitamvumilia kiongozi yeyote mzembe asietimiza wajibu na kwamba hatua zitachukuliwa dhidi ya viongozi wenye kuzembea kwenye nafasi zao.

Mwenyekiti huyo wa CCM wilaya ambe awali aliwahi kuwa Mwenyekiti wa jumuiya ya wazazi wilaya, amempongeza Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo Aboubakari Mlawa kwa kusimamia vizuri jumuiya hiyo na kuleta mabadiliko mbalimbali ya kimaendeleo.

Aidha, ametoa wito kwa jumuiya zote ndani ya chama kuhakikisha kuwa wanashirikiana na kuacha makundi katika kipindi cha utendaji kazi.

Alisema imezoeleka kuwa na makundi katika vipindi vya uchaaguzi lakini mara chaguzi zinapoisha ni vyema wanachama wote wakawa kitu kimoja ili kushirikiana kukijenga chama.

Alitumia nafasi hiyo kumtambulisha rasmi Katibu mpya wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Salum Mtelela ambae anachukua nafasi ya Kombo Kamote aliyestaafu kwa mujibu wa sheria.

Mwenyekiti huyo wa CCM wilaya, alimtaka Katibu anaeanza kazi katika wilaya hiyo kufanya kazi zake kwaa kuzingatia katiba ya CCM, Kanuni, Busara na miongozo mbalimbali iliyotolewa kwa mujibu wa sheria bila ya kumuogopa mtu yeyote.

Alisema Chama Cha Mapinduzi kina Dira inayowaongoza watendaji wote katika kutekeleza majukumu yao hivyo atakaekwenda kinyume katibu ya chama itamuhukumu.

Kwa upande wake Katibu wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Salum  Mtelela amesema anashukuru kwa mapokezi aliyoyapata na kwamba ameahidi kushirikiana na viongozi mbalimbali kwa lengo la kuimarisha chama ndani ya wilaya.

Amewataka viongozi na wanachama kwa ujumla kumpa ushirikiano ili CCM iendelee kuchukua ushindi katika chaguzi mbalimbali zinazokuja.
 
Katibu wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Salum Khalfani Mtelela akizungumza katika semina hiyo.

Kutoka kulia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aboubakari Mlawa, Katibu wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani, Juma Gama, Mwenyekiti wa CCM tawi la Tandika Bagamoyo, Katibu Mwenezi wilaya ya Bagamoyo, Francis Bolizozo, Mjumbe wa kamati ya utekelezaji jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo, Mariamu Hassan.  


MKURUGENZI WA TIBA ATOA TAARIFA KWENDA KWA WAMILIKI WA MAABARA BINAFSI ZA AFYA KUHUSU UTEKELEZAJI WA SHERIA YA UMILIKI WA MAABARA BINAFSI ZA AFYA.

Mkurugenzi wa Tiba, Wizara ya Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima akisisitiza jambo katika mkutano na Waandishi wa Habari kuhusu utekelezaji wa sheria ya umiliki wa maabara binafsi za Afya.
.................................................


Dkt. Dorothy Gwajima, Mkurugenzi wa Tiba wa WAMJW ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Maabara Binafsi za Afya (Private Health Laboratory Board) (PHLB). amewatakia heri ya mwaka mpya 2019 na hongera wamiliki wa maabara binafsi za afya kwa kazi kubwa waliyofanya mwaka 2018 ya kushirikiana bega kwa bega na sekta ya afya katika kuhakikisha taarifa sahihi zinawafikia wananchi na wadau wote kokote waliko.

Katika kufikisha salaam zangu kwa wamiliki wa maabara binafsi, amewashukuru wamiliki hawa kwa kuchagua kuwekeza katika sekta ya afya nchini Tanzania, na kuwapongeza wale wote waliowekeza huku wakihakikisha wanafuata taratibu zote za kisheria za uwekezaji huo.

Aidha, amewakumbusha wamiliki wa maabara binafsi kuwa, umiliki huu unasimamiwa na sheria namba 10 ya mwaka 1997 inayowataka wamiliki wote kusajiliwa na kutambuliwa na PHLB kisheria. Hii ni hata kama maabara husika inajitegemea au iko ndani ya kituo cha kutolea huduma za tiba cha aina yoyote cha ngazi yoyote ile, maabara husika inatakiwa itimize matakwa ya kisheria.

Amesema  kufikia Septemba, 2018 PHLB ilikuwa inazitambua jumla maabara 641 zinazojitegemea na 719 zilizoshikizwa kwenye vituo vya tiba vya watu binafsi vya ngazi mbalimbali.

Katika utekelezaji wa majukumu yake, Bodi imeendelea kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa shughuli za maabara binafsi kama sheria inavyotaka, na kupitia utekelezaji huo imebaini wako baadhi ya wamiliki ambao, hawatimizi matakwa ya kisheria.


Kutotekeleza matakwa ya kisheria siyo tu kunaifanya maabara husika kuwa mbali na macho ya Bodi katika kuhakikisha usimamizi wa ubora wa huduma, bali kunamfanya mmiliki husika kukwepa wajibu wake wa msingi kwa serikali ikiwemo kulipa tozo na ada stahiki zitokanazo na biashara anayofanya na hii ni kukwamisha juhudi za Serikali katika kuwaletea wananchi maendeleo kulingana na mipango yake. Hili halikubaliki hata kidogo.

 Kanuni za kumiliki maabara binafsi zinataka mmiliki kutekeleza mambo makubwa yafuatayo;-

1. Kufuata utaratibu wa kusajiliwa (kwa maabara zinazojitegemea) na kufuata utaratibu wa kujiandikisha na kutambuliwa na Bodi husika kwa maabara ambazo zimesajiliwa pamoja na vituo vya tiba (zilizoshikizwa).
2. Kulipa ada stahiki kila mwaka ambazo ni ada ya uhakiki wa ubora wa huduma na ingine ni ada ya ukaguzi.


Kutokana na baadhi ya wamiliki wa maabara binafsi hususan zilizoshikizwa kutofuata maadili ya uwajibikaji kisheria, bodi imebaini kuwa, kufikia Septemba 2018, kati ya vituo vya tiba 1731 vya watu binafsi vyenye maabara ndani ni maabara 1012 (58%) tu ndiyo zilikuwa zimetimiza wajibu wake wa kujiandikisha kwenye Bodi ya Usimamizi wa Maabara Binafsi na kutekeleza matakwa yote ya kisheria kama nilivyoeleza hapo awali.

Ni kweli kwamba, vituo hivi vya maabara binafsi viko ndani ya vituo vya tiba ambavyo, vinasimamiwa na Sheria ya Usajili wa Vituo Binafsi (PHAB) lakini, hili haliondoi utekelezaji wa sheria ya PHLB yenye dhamana ya kusimamia maabara binafsi. Wizara inakubalina na hoja kuwa, vema sheria hizi zikajumuishwa, na tayari imeanza kufanyia kazi na wadau wote wanafahamu na wameshiriki hivyo, hii haiwezi ikawa ndiyo sababu ya kutowajibika kutekeleza sheria halali ambazo bado ziko hai.

Wizara kupitia Bodi husika imeendelea kuelimisha na kufafanua juu ya mamlaka tofauti za sheria hizi mbili, lakini bado baadhi ya wamiliki wa maabara binafsi wamekuwa wakikwepa tu kuwajibika kwa makusudi.

Aidha, leo hii, watendaji wa sekretarieti ya bodi ya PHLB kwa kushirikiana na sekretarieti ya PHAB na viongozi wa sekta ya afya ngazi zote wakiwemo OR TAMISEMI, Ofisi za Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya mbalimbali, tumehitimisha ziara ya kufuatilia utekelezaji wa shughuli za maabara binafsi za afya katika mikoa mbalimbali ukiwemo mkoa wa Dar es Salaam.

Kupitia ziara hii, tumechambua na kubaini kuwa, wamiliki wengi wasiotekeleza sheria ya umiliki wa maabara binafsi wanatokea miongoni mwa wanaomiliki maabara zilizoshikizwa yaani, zilizomo ndani ya vituo vya tiba ngazi mbalimbali. Aidha, katika kundi hili, wapo watu ambao, kimsingi huwezi kuwatarajia kutokana na elimu zao, kazi zao na Imani zao kwa jamii inayowazunguka (wao wanajijua). Hii haivumiliki kabisa.

Kwa kuwa nilikuwa mstari wa mbele kuwafikia wale wamiliki wa maabara binafsi walioripotiwa kuwa eti wameshindikana, nimewafikia baadhi yao na kusikiliza hoja zao na kubaini kuwa, hazina mashiko kabisa. Eti, hoja yao ya msingi ni kuwa, wanapolipa kusajili kituo cha tiba huwa wanadhani kuwa, tayari na maabara imejumuishwa humo.

 Utetezi huu siyo wa kweli kwa kuwa, sheria ya kusimamia umiliki wa vituo binafsi vya tiba iko wazi na ina bodi yake na hii ya kusimamia umiliki wa maabara binafsi nayo iko wazi na ina bodi yake na siku zote wamekuwa wakielimishwa na mimi nimeshiriki mara nyingi kutoa elimu hiyo.

Nimeona leo nirudie tena kufafanua kuwa, bodi ya usajili wa vituo vya Tiba inajukumu lake na haiingiliani kabisa na sheria ya bodi ya usimamizi wa kumiliki maabara binafsi.

Kwa kuwa wako wamiliki wa maabara binafsi ambao, wameamua kuamini kwenye kufuatiliwa kila siku, sasa ufuatiliaji na uelimishaji uliokwisha fanyika awali unatosha, wakati wa kuelewa somo umepita sasa ni saa ya KAZI TU !. Imefika zamu ya wamiliki wa maabara binafsi waliokuwa hawajatekeleza wajibu wao wa kumiliki maabara hizo kisheria kuchukua hatua mara moja za kwenda kutimiza wajibu wao bila shurti tena pasipo kuendelea kuisababishia Serikali gharama za ziada za kuwafuatilia. 


Hivyo, ifikapo tarehe 15/1/2019 ambaye hajatimiza wajibu wake ni kwamba, atafungiwa bila taarifa ya ziada na kushtakiwa. Iwapo kuna ambaye anayejiandaa kutotimiza matakwa hayo, bora atumie muda huu kufunga ofisi yake kabisa ili kuepuka usumbufu usio wa lazima. Hata hivyo, kufunga ofisi hakutamuepusha mvunja sheria yeyote yule kuwajibika kwa uvunjifu wa sheria alioufanya awali.

Naomba ifahamike kuwa, kutimiza wajibu wa matakwa ya kisheria kwa wamiliki husika wa mabaara binafsi ni pamoja na;-

1. Kila mmiliki kuhakikisha amekidhi vigezo vyote vya kumiliki maabara binafsi kama ambavyo amekuwa akielekezwa na wataalamu walioko kila halmashauri na mikoa husika, pamoja na

 
2. Kuhakikisha amelipa ada na tozo stahiki zikiwemo malimbikizo ya nyuma na faini zote stahiki.

 
3. Amepata risiti halali za malipo hayo

 
4. Anaendelea kulipa tozo stahiki kila mwaka ili, kuwezesha bodi husika kutimiza wajibu wake wa kufanya uhakiki wa ubora wa huduma kwa kila kituo kila mwaka na kufanya ukaguzi maalumu wa vituo husika kama vinaendelea kuwa katika viwango stahiki kama siku vilipopewa kibali cha kutoa huduma husika.


Kwa kuwa tumebaini kuwa, wasiofuata sheria wanatoa huduma bubu mita chache tu toka serikali za mitaa, Bodi imeendelea kuimarisha ushirikiano wake na vyombo vyote vya Serikali ngazi zote kuanzia OR TAMISEMI na ngazi zake zote za Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na sasa, Bodi inaandaa orodha ya maabara binafsi nchi nzima na itaweka katika gazeti la Serikali na vyombo vya habari na itasambaza kwa wadau wote.

Hivyo, yeyote ambaye hayumo katika orodha hiyo asithubutu kutoa huduma hizo maana, mamlaka za Serikali za mitaa zitambaini na taarifa zitafika mahali sahihi mara moja na hatua kali zitachukuliwa.
Aidha, natoa wito kwa mamlaka zote za Serikali ngazi zote tuendelee kupeana taarifa kwa haraka zaidi na kujipanga vema zaidi katika kuhakikisha hakuna mvunja sheria anathubutu kutoa huduma za kijamii bila kibali.


Ni matumaini yangu kuwa mtatumia umahiri wenu katika kuhakikisha ujumbe huu unawafikia wadau wote kwa usahihi. Aidha, nina Imani kuwa, wadau husika sasa wataacha utetezi dhaifu na watatimiza wajibu wao mara moja.

Mwisho, naomba kuwakumbusha wadau wote sekta ya afya kuwa, katika kujenga taifa letu, ni budi kila mmoja atimize wajibu wake ili, tuongeze kasi, kwa kuwa hakuna mtazamaji bali wote tuna majukumu na wajibu kamili.

Kaimu Msajili wa Bodi ya Maabara Binafsi za Afya akijibu maswali ya Waandishi wa habari wakati wa mkutano na Waandishi wa Habari uliohusu utekelezaji wa sheria ya umiliki wa maabara binafsi za Afya.

Wajumbe wa Sekretariet ya Maabara binafsi pamoja na kamati ya Afya ya msingi za manispaa za jiji la Dar es salaam wakifuatilia maelekezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Tiba, Wizara ya Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima kuhusu utekelezaji wa sheria ya umiliki wa maabara binafsi za Afya katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es salaam.

ASKOFU KANISA KATOLIKI ZANZIBAR AITAKA JAMII KUWALEA WATOTO KATIKA MAADILI MEMA

Na Masanja Mabula -PEMBA

 ASKOFU wa kanisa katoliki Zanzibar Agustino Shao ameitaka jamii kuwalea watoto katika maadili mema , na kuhakikisha wanawalinda na vikundi viovu ili kuwafanya wawe nashuhuda wa ukweli.

Amesema ni jukumu la kila mzazi na mlezi kuhakikisha mtoto wake anaishi kwa hofu ya mungu kwa kufuata mafundisho ya dini.

 Askofu shao, ameyasema hayo wakati akizungumza na watoto wa haki na amani katika maadhimisho ya kumbukumbu ya watoto mashahidi iliyofanyika kitaifa  katika kanisa kuu wete pemba.

Amesema wazazi wanajukumu la kumtayarisha mtoto kuweza kutambua leo yake paamoja na kesho yake, pamoja na kuwapatia elimu ambayo ndio mkombozi wao.

“Kila mzazi analojukumu la kuhakikisha mtoto wake anapata malezi bora ambayo yatamsaidia kuishi kwa hofu ya Mungu na kujiepusha na makundi maovu ”alifahamisha.

 Aidha amelaani tabia ya baadhi ya wazazi ya kuwakosesha haki ya elimu watoto wa kike , na kusema wote wanahaki ya kupata elimu.
Amesema mipango ya Mungu iko juu kuliko ya mwanadamu , na kuitaka jamii kumtegemea Mungu katika kazi zao za kila siku.

Kwa upande wao walezi wa watoto wa haki na amani akiwemo Frola Vicent John kutoka Pemba na Jenister Mvula kutoka Unguja wamesema changamoto kubwa inayowakabili ni wazazi kutokuwa na mwamko wa kuwaruhusu watoto kushiriki utume.

Wamesema pamoja na juhudi wanazochukuwa kuwafuatilia watoto, lakini bado baadhi ya wazazi wanaonekana kuwa ni kikwazo katika kuwahimiza watoto kushiriki mafundisho.

“Tunapa changamoto kutoka kwa wazazi kwani baadhi yao wanakwamisha  mipango yetu kwa kutowahimiza watoto wao kushiriki mafundisho “alisema Frola.

Watoto wa haki na amani Judith Damian Modest na Mikael Costa Gerevas wameitaka kuwalinda watoto dhidi ya matendo ya udhalilishaji ili waishi kwa amani na upendo.

Mikael ameiomba serikali kuwachukulia hatua wanahusika na vitendo vya kuwabaka watoto wadogo, ili kuwalinda na kuwafaanya watoto waishi kwa amani na upendo kutoka kwa wazazi wao.

Maadhimisho hayo ya kumbukumbu ya watoto mashahidi , zaidi ya watoto mia moja na ishirini kutoka Unguja na Pemba wameshiriki.

MAGAZETI YA LEO DESEMBA 31, 2018.

TFS YATOA UFAFANUZI WA UKAMATAJI WA MAZAO YA MISITU

Sunday, December 30, 2018

MLAWA ATOA WITO KWA WAZAZI BAGAMOYO.

  Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aboubakari Mlawa, akizungumza wakati wa kufunga semina ya siku mbili ya watendaji wajumuiya hiyo na makatibu Elimu, Malezi na Mazingira wa kata iliyofanyika Nianjema Bagamoyo, kulia ni Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Abduli Sharifu na kushoto ni Katibu wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani, Juma Gama.
..............................

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aboubakari Mlawa amewataka wazazi na walezi kuhakikisha wanawaandikisha watoto wenye umri wa kuanza shule ya msingi ili wapate haki yao ya kupata elimu huku wale wanaotakiwa kujiunga na kidato cha kwanza wapelekwe kwenye shule walizopangiwa haraka iwezekanvyo.

Mlawa ameyasema hayo leo Desemba 30, 2018 wakati wa kufunga semina elekezi ya siku mbili kwa watendaji wa Jumuiya ya wazazi, kata pamoja na makatibu Elimu na Malezi wa kata iliyofanyika kata ya Nianjema Halmashauri ya Bagamoyo.

Alisema Jumuiya ya wazazi pamoja na majukumu mengine ni pamoja na kusimamia Mazingira na Malezi pamoja na maadili kwa watoto hivyo ni lazima jumuiya ihakikisha inasimamia vyema majukumu hayo na kuwahimiza wazazi na walezi kutekeleza hilo.

Aliongeza kwa kusema kuwa licha ya kuwa wilaya ya Bagamoyo ni wilaya inayoongoza kitaaluma katika mkoa wa Pwani, lakini pia ndio wilaya ambayo watoto wengi hawaandikshwi kuanza darasa la kwanza na kuendelea na kidato cha kwanza.

Aidha, ametumia fursa hiyo kusisitiza umoja na mshikamano ndani ya jumuiya kuanzia ngazi ya kata mpaka wilaya kwani hiyo ndio siri ya mafanikio yanayopatikana ndani ya jumuiya ya wazazi.

Alisema jumuiya hiyo wilaya iko imara na kwamba haiwezi kutetereka kwakuwa inafanya kazi kama timu moja na hivyo inaweza kupambana na changamoto mbalimbali zinazoweza kujitokeza kwaajili ya kukwamisha maendeleo.

Mwenyekiti huyo wa jumuia ya wazazi aliwaataka washiriki wa semina hiyo kutumia mafunzo hayo kama njia ya kuongeza uwajibikaji kwa ufanisi zaidi na kuongeza wigo wa wanachama ndani ya jumuia na chama kwa ujumla.

Alisema jumuiya ya wazazi ikitekeleza majukumu yake ipasavyo ndio njia pekee ya kuipatia ushindi CCM katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka 2019 na hata ule wa Rais, madiwani na wabunge 2020.

Aliendelea kusema kuwa,  jumuiya hiyo inatekeleza majukumu yake kwa weledi katika kusimamia maadili kila mmoja kwenye eneo lake anapaswa kuhakikisha anapinga vitendo vya rushwa ili kila hatua inayofikiwa katika chaguzi mbalimbali ifikiwe kwa haki na uadilifu.

Kwa upande wake Katibu wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani Juma Gama ametoa wito kwa wana jumuiya kuinua uchumi wa mmoja mmoja, na jumuiya kwa ujumla kwa kuanzisha miradi mbalimbali ikiwemo ya ufugaji wa nyuki ili kujiletea maendeleo.

Alisema kiongozi atakapojiimarisha kiuchumi ataweza kutekeleza majukumu yake ipasavyo na kujenga uaminifu katika jamii kwakuwa hatapita kuomba omba.

Alisema kama jumuiya ya wazazi inapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika kujiinua kiuchumi ili utekelezaji wa majukumu ya jumuiya na chama uende kwa ufanisi na sio kwa utapeli.

Aidha, aliwaonya wale wote waliochaguliwa ndani ya jumuiya na wanashindwa kutekeleza majukumu yao ni vyema sasa sheria ikachukua mkondo wake kwa kumsimamisha ili nafasi yake izibwe na mtu mwingine.

Alisema uongozi ni uwajibikaji hivyo yule ambae hawezi kuwajibika anastahili kuwekwa pembeni ili watu wenye nia ya dhati na jumuiya hiyo waweze kusonga mbele.

Washiriki wa semina hiyo wamesema wamefaidika na kile walichofundishwa na kwamba wataleta mabadiliko kwenye maeneo yao.

Katika semina hiyo ambayo imeandaliwa na Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo na kukusanya washiriki kutoka kata zote za wilaya hiyo wamejifunza mipaka ya uongozi, uandaaji wa mihutasari, Barua, Taarifa na kazi pamoja na mambo mbalimbali yanayohusu itifaki ndani ya Chama Cha Mapinduzi.
 
Muwezeshaji Hassan Tambaza akitoa mafunzo kwa washiriki
 
Muwezeshaji Mwinyi Sangaraza akitoa mafunzo kwa washiriki

 Katibu wa Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aeshi akizungumza na washiriki katika semina hiyo.

Washiriki wakifuatilia mada zilizowasilishwa katika semina hiyo
 
Washiriki wakifuatilia mada zilizowasilishwa katika semina hiyo
   Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aboubakari Mlawa, (kulia) na Katibu wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani, Juma Gama (kushoto) wakifuatilia semina hiyo.

WAZIRI HASUNGA AZIAGIZA BODI ZA MAZAO NCHINI KUWASAJILI WAKULIMA WOTE.

Waziri wa Kilimo, Mhe. Japhet Hasunga (Mb) akisisitiza jambo wakati akizungumza na Wenyeviti wa Bodi za Mazao pamoja na Wakurugenzi wa Bodi hizo za Mazao, kwenye ukumbi wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Jijini Dodoma jana tarehe 29 Disemba 2018
.......................................................


Waziriwa Kilimo, Mhe. Japhet Hasunga (Mb)  amewaagiza Wakurugenzi wa Bodi za Mazao kuanza mara moja zoezi la kuwatambua na kuwasajili wakulima wa mazao yote nchini lengo likiwa kuwatambua ili kupanga mipango sahihi yenye kuongeza tija na uzalishaji katika mazao yote.


Ametoa agizo hilo jana tarehe 29 Disemba 2018 wakati akizungumza na Wenyeviti wa Bodi za Mazao pamoja na Wakurugenzi wa Bodi hizo za Mazao, kwenye ukumbi wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Jijini Dodoma.


Mhe. Hasunga amesema ili kuongeza tija na uzalishaji katika Sekta ya kilimo na kuandaa mipango madhubuti ya kuendeleza mazao yote ni vyema kuwatambua Wakulima wote nchini na kuongeza kuwa Wakulima wa zao la korosho wametoa funzo kubwa kwa Wizara yake kufanya jambo kama hili katika mazao mengine hapa nchini.


Itakumbukwa kuwa wiki tatu zilizopita, Waziri Hasunga alitoa agizo kwa Bodi ya Korosho agizo kuandaa daftali maalumu la kuwatambua Wakulima wa korosho kote nchi ambapo moja ya taarifa ambazo zitajumuishwa katika daftali hilo ni pamoja na

Jina Kamili la Mkulima,  Mkoa, Wilaya, Kata na Tarafa anayotoka.


Mambo mengine ni pamoja na Kitongoji, Mtaa au Jina la Kijijini anapotoka, mahali lilipo shamba pamoja na ukubwa wa shamba lake.


Waziri Hasunga ameongeza kuwa mipango sahihi ya kuwaendeleza Wakulima kuanzia kwenye kilimo chenyewe hadi kufikia katika hatua ya kuvuna, kuhifadhi na kulifikia soko ni vyema kuwa na mfumo maalumu wa kanzi data (Database) ya kuwafahamu ili kushughulikia mahitaji yao kisasa na kwa haraka zaidi.


Waziri Hasunga alienda mbali na kushauri matumizi ya TEHAMA na ya Mfumo wa GPS ili kuboresha daftari hilo kwa lengo la kuboresha uwekaji wa taarifa za Wakulima na

maeneo wanayotoka Wakulima kwa usahihi zaidi.


“Tumepata changamoto kadhaa wakati wa kuwahakiki Wakulima wa korosho katika mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na Ruvuma na kama Bodi ya Korosho ingekuwa makini kuandaa daftari la Wakulima zoezi la uhakiki lingekuwa rahisi, kwa ajili hiyo niliwaagiza Bodi ya Korosho kukamilisha zoezi hili mpaka Mwezi Machi, 2019 na Bodi za Mazao zilizobaki ukiacha Bodi ya Tumbaku ambao wao tayari walishafanya hivyo, kukamilisha Mwezi June, 2019”. Amekaririwa Mhe. Hasunga.


Waziri ameitisha kikao maalumu na Viongozi wa Bodi za Mazao, Wakala na Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Kilimo kwa lengo la kuboresha mikakati na kuongeza ufanisi katika utendaji wa Wizara pamoja na kujitathmini kabla ya kufikia nusu mwaka wa utekelezaji wa vipaumbele vya bajeti ya Wizara ya mwaka 2018/2019 ili kujipanga kwa ajili ya utekelezaji wa bajeti ya Wizara ya kilimo ya mwaka ujao wa 2019/2020.


Bodi za Mazao zilizoshiriki mkutano huo ni pamoja na Bodi ya Korosho, Bodi ya Pamba, Bodi ya Mkonge, Bodi ya Pareto, Bodi ya Chai, Bodi ya Kahawa, Bodi ya Tumbaku, Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko na Bodi ya Sukari.


Wakala zilizoshiriki ni pamoja na  Wakala wa Taifa wa Mbolea (ASA) Wakala wa Wakulima Wadogo wa Chai (TSHTDA).


Taasisi nyengine za Wizara ya Kilimo zilizoshiriki ni pamoja na Taasisi ya Udhibiti wa Mbegu (TOSCI), Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO), Taasisi ya Utafiti wa Viuatilifu vya Ukanda wa Kitropiki (TPRI), Mfuko wa Pembejeo za Kilimo (AGITF), Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA),


Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea (TFRA), Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI), Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Kampuni ya Taifa ya Mbolea (TFC) na Bodi ya Leseni za Maghala.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe akifatilia mkutano wa Wenyeviti wa Bodi za Mazao pamoja na Wakurugenzi wa Bodi hizo za Mazao,  uliongozwa na Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) kwenye ukumbi wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Jijini Dodoma jana tarehe 29 Disemba 2018.
 
Wenyeviti wa Bodi za Mazao pamoja na Wakurugenzi wa Bodi hizo za Mazao,  wakifatilia mkutano wa kazi ulioongozwa na Waziri wa Kilimo, Mhe. Japhet Hasunga (Mb) kwenye ukumbi wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Jijini Dodoma jana tarehe 29 Disemba 2018.


(Picha Zote Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo)