Sunday, October 27, 2019

JULIANA SHONZA AFUNGA TAMASHA BAGAMOYO

 
Naibu waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza, akizungumza na waandishi wa Habari wakati wa kufunga Tamasha la 38 la kimataifa la sanaa na utamaduni lililofanyika TaSUBa mjini Bagamoyo.
.....................................

Wasanii nchini wametakiwa kuboresha kazi zao ili ziingie kwenye ushindani wa soko ndani na nje ya nchi.

Wito huo umetolewa na Naibu waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza alipokuwa akizungumza wakati wa kufunga Tamasha la 38 la kimataifa la sanaa na utamaduni lililofanyika TaSUBa mjini Bagamoyo.


Alisema kazi za sanaa na utamaduni ni miongoni mwa vitu vinavyokuza utalii hapa nchini hivyo kazi hizo zinatakiwa kufanywa kwa umakini, ubunifu na utaalamu wa hali ya juu ili kwenda sambamba na mahitaji ya soko.


Aliongeza kwa kusema kuwa, Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo, (TaSUBa) ni chuo chenye uzoefu wa kufundisha kazi za sanaa na uandaaji wa matamasha hivyo wasanii watumie Tamasha hilo la mwaka huu kurekebisha kasoro zao walizoziona.


Alisema wizara ya habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo itaendelea kusimamia ubora wa sanaa na utamaduni ili kwa kushirikiana na wizara ya maliasili na utalii, sana iwe kivutio cha utalii hapa nchini.


Aidha, Naibu waziri huyo alitumia nafasi hiyo kuupongeza uongozi wa TaSUBa kwa kuimarisha mahusiano mema kati ya Tanzania na nchi za nje kupitia sanaa na utamaduni vinavyofundishwa chuoni hapo.


Alisema kutokana na mafunzo yanayotolewa chuoni hapo, wapo wanafunzi kutoka nchi mbalimbali wanaokuja kusoma na pia wapo watanzania kupitia TaSUBa wanaenda kusoma nchi za nje jambo ambalo linasaidia kukuza taaluma ya sanaa na kuitangaza Tanzania kimataifa.


Alitoa wito kwa uongozi wa TaSUBa mara tu baada ya kukamilika kwa tamasha hilo la 38 kukaa chini na kamati mbalimbali kutathmini namna lilivyofanikiwa tamasha la mwaka huu ili kuboresha zaidi katika Tamasha la 39 litakalofanyika mwaka 2020.


Alisema Tamasha la sanaa na utamaduni linatoa fursa kwa watanzania kufahamu kuwa kuna watu wengi wenye vipaji na kwamba kupitia ubunifu mbalimbali unaofanywa na wasanii, sanaa haiwezi kufa hapa nchini.


Aliongeza kuwa, nje ya Tamasha huwezi kujua uwezo vipaji wa wasanii tofauti tofauti lakini kupitia tamasha hilo vikundi mbalimbali vya sanaa na utamaduni vinaweza kuwasilisha kazi zao na watanzania wakajionea wenyewe kwa muda wote wa siku nane.


Awali akizungumza mbele ya mgeni rasmi, Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo, (TaSUBa) Dkt. Herbert Makoye alisema anaishukuru Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuendelea kushirikiana na Taasisi hiyo ili kufanikisha matamasha yanayofanyika kila mwaka.


Alisema Tamasha hilo ni muhimu sana ndani na nje ya nchini na kuiomba wizara hiyo, iendelee kuliona tamasha hilo kama tukio muhimu kwa wizara katika kukuza na kuendeleza vipaji vya wasanii hapa nchini.


Kwa upande wake Katibu Tawala wilaya ya Bagamoyo, Kasilda Mgeni, akizungumza wakati wa kumkaribisha mgeni rasmi, alisema wilaya ya Bagamoyo inajivunia kuwepo kwa Tamasha hilo licha ya kutangaza vipaji vya wasanii, pia linaitangaza wilaya ya hiyo, Mkoa wa Pwani na Taifa kwa ujumla kwani linakuza mahusiano ya nchi mbalimbali kutokana na wageni wanaofika kwenye tamasha hilo.


Alisema miongoni mwa faida zinazopatikana katika tamasha hilo ni pamoja na kutoa ajira kwa vijana na wajasiriamali.


Alimueleza mgeni rasmi kuwa, kutokana na faida hizo zinazopatikana kwenye tamasha hilo, wilaya ya Bagamoyo imehakikisha inaimarisha hali ya ulinzi na usalama ili wageni wote waliofika wakae katika hali ya usalama.



 Naibu waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza, (katikati) akiwa katika sherehe za kufunga Tamasha la 38 la kimataifa la sanaa na utamaduni lililofanyika TaSUBa mjini Bagamoyo, jana Oktoba 26, 2019, kutoka kulia ni Kaimu Mkurugenzi, Idara ya mambo ya kale, Dkt. Fabian Kigadye kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, wa pili ni Kaimu Mkurugenzi, Maendeleo ya sanaa, kutoka wizara ya habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Joyce Fissoo na watatu ni Katibu Tawala Wilaya ya Bagamoyo, Kasilda Mgeni, kutoka kushoto ni Mjumbe wa bodi ya ushauri TaSUBa, Lilian Godfrey Kihiyo, wapili ni
Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo, (TaSUBa) Dkt. Herbert Makoye
Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo, (TaSUBa) Dkt. Herbert Makoye, akizungumza wakati wa kufunga Tamasha la 38 la kimataifa la sanaa na utamaduni lililofanyika TaSUBa mjini Bagamoyo, jana Oktoba 26, 2019.

   


No comments:

Post a Comment