Friday, December 15, 2023

RMO KAGERA ATENGULIWA KWA KUZUILIWA MWILI WA MTOTO MCHANGA KWA MADAI YA DENI LA MATIBABU HOSPITALINI.

 


Na Alodia Babara

Bukoba.

Waziri wa nchi ofisi ya Rais TAMISEMI Mohamed Mchengerwa amemwagiza katibu mkuu wa TAMISEMI nchini kutengua nafasi ya mganga mkuu wa mkoa wa Kagera Issesanda Kaniki baada ya hospitali ya rufaa ya Bukoba ya mkoa huo kuzuia mwili wa mtoto mchanga kwa muda wa siku mbili kutoruhusiwa kwenda kuzikwa wakati wakijua watoto wanatibiwa bure.


Maagizo mengine ameyatoa kwa viongozi wa serikali, siasa na watumishi mbalimbali nchini.


Waziri Mchengerwa ametoa maagizo hayo  Desemba 15, mwaka huu wa 2023, wakati akizungumza na wananchi wa mkoa wa Kagera katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kituo cha mabasi yaendayo mikoani kinachokarabatiwa ambapo pia alishuhudia utiaji wa saini ya mikataba ya usanifu miradi ya uboreshaji wa miundomninu ya miji Tanzania (TACTIC) kwa miji 15 ya kundi la pili.


Ameagiza katibu mkuu TAMISEMI kwa kushirikiana na sekta ya afya kufanyika mapitio ya menejimenti nzima ya hospitali hiyo na kutoa maamuzi kwani alipata malalamiko kuwa wapo baadhi ya watumishi wamekuwa wakitoa lugha chafu kwa wagonjwa.


Amesema,  muda wa kubembelezana haupo tena kwa nyakati hizi watu wamekuwa wakifanya kazi kwa mazoea sasa hatuwezi kuendelea na watumishi wa namna hiyo kwa sababu wananchi wana imani na serikali yao.


Wakati huo huo waziri Mchengerwa alisema mtu yoyote au kiongozi yoyote awe wa kisiasa au mtendaji yeyote wa serikali atakaye jaribu kufanya ubadhilifu au kukwamisha miradi inayotarajiwa kutekelezwa katika manispaa ya Bukoba ikiwemo stend kuu, soko kuu, barabara ya kilomita saba na kingo za mto Kanoni na kufunga taa za barabani
hatofumbiwa macho atachukulia hatua kali za kisheria.


"Tunataka  tubadilishe muonekano wa Kagera mhe. Rais alizitafuta fedha hizi maeneo mbalimbali anataka kuibadilisha Kagera hivyo, kiongozi yoyote awe wa kisiasa au serikali atakayejaribu kuingiza mkono bila kujali nafasi yake nitashugulika naye ikiwemo kumfukuza kazi, hatutaki ubabaishaji katika miradi hii"amesema Mchengerwa.


Aidha amesema, kama kuna viongozi wa siasa ndani ya manispaa ya Bukoba au mkoa wa Kagera wanaokwamisha miradi ya maendeleo ambayo imekuwa ni kiu ya wanakagera kwa muda mrefu atasimamisha baraza la madiwani mpaka miradi hiyo ikamilike.


"Maagizo yangu ujenzi wa soko uzingatie wale wafanyabiashara  wa zamani waliondolewa kinyume na taratibu wapate vibanda ndipo wapya wapewe mabanda na wale waliko nje ya soko wote wapate nafasi hii pia tukikamilisha hatutaki kuona wafanyabiasha wakiendesha shughuli zao nje ya soko hili ambalo Dk.Samia anakwenda kulijenga katika maeneo haya kiongozi yoyote atakaye kaidi maagizo, ujeuri na kiburi aliyeko kwenye mamlaka yangu nitamfukuza kazi na walioko kwenye mamlaka za juu nitawafikisha kwa Rais awafukuze kazi”alisema.


Pia waziri aliwaagiza  wakurugenzi wote nchini kuendana na kasi ya Ras Samia ambapo kila mkurugenzi anatakiwa kuanzisha vyanzo viwili vya kuingiza mapato atakayeshindwa kufanya hivyo atahovumiliwa.


Mratibu wa miradi ya ushirikiano na benki ya dunia TACTIC  mhandisi Humphrey  Kanyenye alisema miradi hiyo inatakiwa kutekelezwa kwa miezi nane ikiwezekana mwezi Machi mwakani ujenzi uanze mara moja.


Ujenzi wa kituo cha mabasi Bukoba na soko kuu kimekuwa kitendawili cha muda mrefu baada ya kukwama kujengwa takribani miaka 15 iliyopita baada ya kutokea mgongano wa masrahi ya kisiasa.


Miradi hii ya uboreshaji wa miundombinu ya miji Tanzania TACTIC  kwa miji 15 ya kundi la pili (Tier) ambapo Manispaa ya Bukoba ni miongoni mwa miji itakayonufaika na miradi hiyo zilitengwa fedha kiasi cha shilingi bilioni 23 kwa ajili ya ujenzi huo kati ya sh moja trilioni ya miradi yote.


Thursday, December 14, 2023

POLISI KAGERA WAKAMATA SILAHA 11. NA RISASI 115.

 

Na Alodia Babara

Bukoba.

Jeshi la polisi mkoani Kagera limekamata silaha 11 zikiwemo bunduki 2 aina ya AK 47 zikiwa na magazine tatu, risasi 115, bastola aina ya glock 17 na bunduki aina ya gobore.


Kamanda wa polisi mkoani Kagera, Kamishna Msaidizi wa Polisi, ACP. Blasius Chatanda, akizungumza na waandishi wa habari leo Desemba 14, 2023, amesema kuwa, jeshi hilo  linaendelea kufanya oparasheni mbalimbali na kuimarisha ulinzi na usalama wa wananchi katika mkoa huo ambapo katika oparasheni iliyofanyika kuanzia Septemba, 2023 hadi sasa silaha 11 zilikamatwa.


“Katika kudhibiti matukio ya utekaji  nyara hasa kwa wafugaji katika mkoa wetu wa Kagera tumefanikiwa kukamata watuhumiwa 14 wa utekaji, tumekamata silaha mbili aina ya AK 47 zikiwa na magazine tatu pamoja na risasi 115 na bastola aina ya grock 17” amesema Chatanda.


Aidha amesema katika kudhibiti matukio ya unyang’anyi wa kutumia silaha na ujagili jumla ya bunduki nane aina ya gobore zimekamatwa na kati ya hizo nne zilisalimishwa na watuhumiwa watano kufikishwa mahakamani kwa hatua za kisheria.


Amesema jeshi hilo limeendelea kudhibiti wimbi la wizi wa watoto na kufanikiwa kukamata watu wanne ambao walihusika na wizi wa watoto na watoto wanne walikamatwa wakiwa hai.


Ameongeza kuwa, watuhumiwa hao walifikishwa mahakamani kwa hatua mbalimbali ili kujibu tuhuma zinazowakabili.


Wakati huo huo, amesems pikipiki za wizi ambazo hazikuwa na nyaraka zozote zipatazo 157 zimekamatwa mkoani Kagera pamoja na nchi jirani ya Burundi baada ya kufanyika oparashen.


Amesema pikipiki 157 zilizokamatwa kati ya hizo 92 zilikamatwa nchini Burundi zikiwa na usajili wa namba za Tanzania zikiwa zinatumika nchini humo, huku pikipiki 65 zikikamatwa mkoani Kagera.


“Kwa sasa pikipiki hizo bado ziko Burundi baada ya kukamilisha taratibu zote za kuzirejesha hapa nchini tutawatangazia wananchi ili waje kuzitambua, na pikipiki zilizopo mkoani hapa watu waje kuzitambua” amesema Chatanda.


Mmoja wa waendesha pikipiki maarufu boda boda manispaa ya Bukoba, Enock Novath, ameliomba jeshi la polisi kuimarisha ulinzi ili kudhibiti matukio ya wizi wa pikipiki ambayo yameshamiri katika mkoa wa Kagera.


Joanes Festo mkazi wa manispaa ya Bukoba amedai kuwa mwaka huu ameibiwa pikipiki mbili na kutoa taarifa kituo cha polisi na kuwa hakuna pikipiki yake ambayo imeishapatikana.


Ameliomba jeshi la polisi kuwa zinapotolewa taarifa za wizi wa pikipiki msako uanze mara moja na siyo kusubili oparasheni kwani kufanya hivyo zitakamatwa pikipiki kabla hazijasafirishwa kwenda nje ya mkoa






Tuesday, December 5, 2023

WAHITIMU ADEM WAPEWA SOMO NA PROF. MKENDA.

 

Wahitimu katika chuo cha Wakala wa Maendeleo ya uongozi wa elimu
­(ADEM) wametakiwa kwenda kusimamia vyema taaluma ya uongozi na utawala katika maeneo yao ili kutimiza malengo ya serikali katika
maboresho ya elimu hapa nchini.

Katika Mahafali ya 31 ya waahitimu hao yaliyofanyika tarehe 01 Desemba
2023, mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia,
Prof. Adolf Mkenda, amesema katika kipindi hiki cha mageuzi ya elimu,
serikali inawategemea sana walimu hasa waliosomea uongozi na utawala
katika kuhakikisha yale yote yanayotakiwa kuboreshwa yanasimamiwa ipasavyo.

Amesema tayari serikali inaendelea na mchakato wa maboresho ya elimu
nchini kwa kuangazia mambo saba muhimu ambayo ni sera ya elimu,
mabadiliko ya sheria ya elimu ya mwaka 1978 ambapo sasa elimu ya
lazima ni miaka 10 kwa kila Mtanzania.

Prof. Mkenda ameongeza kwa kusema kuwa, katika maboresho hayo , kuna
marekebisho ya mitaala, kuwa na walimu, wakufunzi na wahadhiri kwa
mgawanyo uliokuwa sawa, Ubora wa walimu, wakufunzi na wahadhiri,
vitendea kazi pamoja na miundombinu.

Alisisitiza kuwa ili kuweza kupata matokeo mazuri ya utekelezaji wa
maboresho hayo viongozi wa elimu wa ngazi mbalimbali wana mchango
mkubwa katika kufikia malengo hayo.

Alisema walimu ni walezi kama walivyo wazazi, mwalimu anapokuwa na mtoto shuleni anapaswa kujiona yeye ni mzazi ambae atamuangalia mtoto sio tu kwa kumfundisha bali pia ni kwa kumpa ulinzi anaostahiki ili
asidhurike kimaadili na na kimwili kwakuwa mzazi anatarajia pia
usimamizi mahiri wa mwalimu.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Siston Masanja, amesema
malengo ya ADEM ni kutekeleza azma ya serikali ya kuboresha Uongozi,
Usimamizi, na Uendeshaji wa Elimu nchini katika shule za Msingi,
Sekondari Vyuo vya ualimu na kwa maafisa elimu wote, ambapo mafunzo
yanayotolewa yanawawezesha kuimarisha utendaji katika ngazi zote za elimu.

Dkt. Masanja ameipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa
kuendelea na maboresho ya elimu hapa nchini kwa kuhuisha sera ya elimu
na mafunzo na kusema kuwa ADEM ipo tayari kutoa mafunzo ya Uongozi,
Usimamizi na uendeshaji wa Elimu pamoja na kufanya tafiti zitakazosaidia kutoa majibu mafanikio na changamoto zinazojitokeza katika elimu.

Awali wakisoma risala mbele ya mgeni rasmi, wahitimu hao walisema wamejifunza namna Uongozi bora unavyoweza kuwa chachu ya maendeleo katika sekta ya Elimu na kuleta tija na matokeo chanya katika ukuaji wa Taifa kwa ujumla.

Waliongeza kwa kusema kuwa wamejifunza jinsi ya kutoa elimu kwa watu wazima pamoja na kutambua mazingira rafiki kwao katika kujifunza. Hali hiyo  itasaidia uendelezaji wa vituo vya Elimu ya watu wazima katika vituo
vyetu vya kazi.

Mahafali hayo yalikuwa ya whitimu wa stashahada ya uongozi na usimamizi wa elimu, (DEMA), Stashahada ya uthibiti ubora wa shule (DSQA) na Astashahada ya uongozi, usimamizi na utawala katika elimu (CELMA)









Thursday, November 30, 2023

MAAMBUKIZI YA MALARIA KAGERA YAFIKIA ASILIMIA 18.

 

Na Alodia Babara 

Bukoba. 

Misimu miwili ya mvua ya vuli na masika inayonyesha mkoani Kagera imetajwa kama sababu ya mbu kuzaliana na hivyo kusababisha kiwango cha maambukizi ya malaria kufikia asilimia 18,  mkoani humo huku kiwango cha taifa kikitajwa kuwa ni asilimia 8.

Kufuatia kiwango hicho kuwa juu, wilaya mbili za Karagwe na Kyerwa ambazo ziko pembezoni na vijiji viko umbali wa kuanzia kilomita tano kufika katika vituo vya afya wahudumu wa afya ngazi ya jamii wapatao 38 wamepewa vifaa tiba.

Akizungumza leo Novemba 30,2023 katika hafla fupi ya kukabidhi vifaa mbalimbali vya kutolea huduma za tiba katika ofisi ya mkuu wa mkoa huo mkurugenzi wa mradi wa Shinda malaria Dk Dunstan Bishanga amesema wahudumu hao walipewa mafunzo ya awali jinsi ya kupima joto na kuwaelimisha wanachi juu ya matumizi sahihi ya vyandarua.

“Mkoa wa Kagera ni miongoni mwa mikoa mitatu hapa nchini yenye maambukizi ya juu ya malaria ambapo watu 18 kati ya watu 100 wameathirika na vimelia vya ugonjwa huo, pamoja na jitihada zote tunashukuru kuna upungufu wa visa hivyo, kwani mwaka 2019 Kagera ilikuwa na visa vya malaria 580,000 na mwaka 2022 visa hivyo vimepungua hadi 250,000”amesema Dk Bishanga

Dk Bishanga ameongeza kuwa, kiwango cha malaria mkoani hapa kimekuwa kikipanda juu zaidi katika vipindi viwili vya msimu wa mvua ambavyo ni vuli kuanzia Oktoba hadi Desemba na msimu wa masika kuanzia Machi hadi Mei.

 Kwa upande wake mkurugenzi wa IHI taasisi ya afya ya Ifakara Honorath Masanja amesema kuwa, vifaa tiba vyenye thamani ya Shilingi milioni 60, vimegaiwa kwa wahudumu hao na vifaa hivyo ni vipima joto, buti, baiskeli, makoti ya mvua, mizani na kifaa cha kubebea vifaa (kit).

Katibu tawala mkoa wa Kagera Toba Nguvila akiwa amemwakilisha mkuu wa mkoa huo amesisitiza viongozi wa ngazi zote kuwa wanapaswa kushirikiana kupiga vita ugonjwa wa maralia kwani yeye kama kiongozi wa mkoa hajisikii vizuri kuona watu wake wanaugua maralia na kuwa jamii ielimishwe maatumizi ya vyandarua na mazalia ya mbu yateketezwe.

Jastini Jakson kutoka wilaya ya Kyerwa ni mmoja wa wahudumu ngazi ya jamii waliopokea vifaa hivyo amesema kuwa, walipatiwa mafunzo jinsi ya kumtambua mgonjwa wa maralia kwa kumhoji kwanza na baadaye kumpima joto la mwili.

Amesema kuwa, kutokana na mafunzo waliyopewa walifundishwa kuwa, baada ya kuona mgonjwa ana homa kali, anawangwa kichwa na anatapika wanapaswa kuchukua jukumu la kumpa rufaa kwenda kituo cha afya na wamejifunza utunzaji wa kumbukumbu na kutunza siri za mgonjwa. 

Wednesday, November 15, 2023

EDU KWANZA WATOA FURSA YA MASOMO KWA VYUO VIKUU VYA CANADA & USA KWA WANAFUNZI WA TANZANIA

 

Na Andrew Chale, Dar es Salaam.


EDUKWANZA Consultants Limited ambao ni Mawakala wa Vyuo vya nje ya Nchi kwa kushirikiana na Taasisi ya Kimataifa ya ushauri huduma za Wanafunzi ya ILLUME imeendesha zoezi kwa Wanafunzi wa Tanzania kupata fursa za masomo katika Vyuo vya nchi za Canada na Marekani (USA) tukio lililofanyika Jijini Dar es Salaam mapema leo Novemba 15,2023.


Akizungumza katika tukio hilo lililowakutanisha wanafunzi mbalimbali waliofika kupata muongozo sahihi wa Vyuo vya nje, Mkurugenzi wa Edukwanza, Bw. Sarfraz Kassam amesema taasisi yao hiyo ina ushirikiano na Vyuo zaidi ya 500 Duniani ikiwemo Vyuo hivyo vya Canada na Marekani.


"Edukwanza Consultants Limited leo Novemba 15,2023 tumefanya maonesho ya kuvinadi Vyuo vya Canada na Marekani katika mpango wa ‘Study in Canada & USA Fair 2023 ambao unasaidia kutoa fursa kwa in wanafunzi kusoma nje.


Wanafunzi mbalimbali wa Tanzania wamefika na kupata ushauri kutoka kwa Wawakilishi wa vyuo hivyo vya nje, wakipata ushauri wa kujiunga na vyuo hivyo, namna ya kupata visa za masomo, ama namna ya masomo ya kuchagua na muongozo mwingine kwa ajili ya taaluma yao." Amesema Sarfraz Kassam

 





Aidha, amesema kuwa, Vyuo hivyo vya Canada na Marekani ni miongoni mwa vyuo bora na wanafunzi wamepata namna bora ya kupata ushauri wa jinsi ya kuomba kusoma kwenye vyuo hivyo.


Lakini pia amewataka wanafunzi hao kuweza kupitia mitandao ya kijamii ya Edukwanza kupata muongozo sahihi kwa ajili ya hatma yao ya kuchagua Vyuo bora nje ya Nchi.


Edukwanza ni miongoni mwa Mawakala wa Vyuo vya nje ya Nchi iliyosajiliwa na Tume ya vyuo vikuu nchini (TCU) imekuwa kinara katika kunadi na kuongoza kushauri wanafunzi kwenda kusoma nje.


UNESCO, WADAU WAKUTANA DAR KUJADILI UKATILI NA UNYANYASAJI KWA WENYEULEMAVU VYUO VYA UFUNDI NCHINI

 

Na Andrew Chale, Dar es Salaam.


SHIRIKA la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO) limekutana na Wadau Wataalam kutoka mashirika yasiyo ya Kiserikali, Serikali na Mashirika ya watu wenye Ulemavu kupitia na kutolea maoni nyenzo za kukabiliana na vitendo vya kikatili na kinyanyasaji kwa wanafunzi walemavu wanaosoma Vyuo vya ufundi hapa nchini.


Mkutano huo wa siku mbili yaani Novemba 14- 15,2023 mbali ya Tanzania, pia unafanyika sambamba katika nchi zingine tatu za Namibia, Msumbiji na Zimbabwe kwa pamoja wakijadiliana kupitia video kwa mtandao wa ZOOM.

 

Mkutano huo ni mpango unaotekelezwa na UNESCO na Shirika la Kazi Duniani (ILO)kupitia mradi unaofadhiliwa na United Nations Partnership on the Rights of Persons with Disabilities (UNPRPD) wenye lengo la kukomesha unyanyapaa na ubaguzi wa watu wenye ulemavu katika vyuo vya ufundi na kazini. 


Katika majadiliano hayo, Wadau wameweza kutoa maoni yao na namna bora ya hatua za kuchukuliwa ilikufikiwa malengo, huku pia wakijifunza kutoka kwa wenzao wanchi za Msumbiji, Zimbabwe na Namibia.


Katika mazungumzo ambayo mengine yamefanyika kwa njia ya video.


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Elimu maalumu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Magreth Matonya ameyashukuru Shirika la Kimataifa la UNESCO na ILO kwa mkutano huo wa wadau namna bora ya kukabiliana na vitendo vya kikatili ambavyo vinaendelea katika Vyuo vya Ufundi vya Tanzania.


Ambapo amesema mkutano huo ni muhimu kwani tayari kuna nyenzo zimeandaliwa ambazo zitasaidia kupata taarifa mbalimbali za vitendo vya kikatili na kinyanyasi kwa watoto walemavu ambavyo vinafanyika kwenye vyuo hivyo.


“Nyenzo hii imetumika kupata taarifa mbalimbali kwenye Vyuo vya ufundi nchini. Tumeijadili na tumeona ni muhimu kwani imeandaliwa vizuri.


Lakini pia italeta chachu namna bora ya kubaini ni aina gani ya vitendo vya kikatili ambavyo vinafanyika, lakini ni nani ambaye ni msababishi mkuu wa hivyo vitendo vya kikatili katika vyuo vya ufundi vya Tanzania.’’ Amesema Dk. Magreth Matonya.


Ameongeza kuwa kama Serikali itaendelea kuwasaidia vijana wote wenye Ulemavu Vyuo vya ufundi ambao wanatakiwa kusoma na kuepuka changamoto za ukatili.


‘’Vijana wenye ulemavu wanahitaji kusoma,wanapokutana na changamoto ya vitendo vya kikatili wanapata msongo wa mawazo kiasi kwamba hawawezi kusoma na wakafanikiwa na kutimiza ndoto zao. 


Lakini pia wanapata msongo wa mawazo kutoka kwenye jamii, kutoka kwenye familia, lakini upande wa mfumo wa vyuoni, wanapata msongo wa mawazo kutoka kwa Wanafunzi pamoja na Walimu kwani mpaka sasa wapo baadhi yao bado hawajawatambua wenye ulemavu, hivyo nyenzo hii inakuja kusaidia na muhimu zaidi.’’ Amesema Dk. Magreth Matonya 


Kwa Upande wake, Mshiriki kutoka (NACTVET) Taasisi ambayo inasimamia Vyuo hapa nchini, Bw. Eligius Bwalya, ambaye ana ulemavu wa aina mbili unaohusisha viungo na macho, amesema kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwani wameweza kubainisha vitu mbalimbali ilikuweza kuchukuliwa hatua za haraka katika kumsaidia Kijana mwenye ulemavu yakiwemo masuala ya kuomba usajili wa vyuo ama kazi pamoja na matangazo mengi yanawabagua walemavu.


‘’Kuna shida katika masuala ya matangazo ama katika masuala ya kutuma maombi yawe ya kazi ama kujiunga na vyuo ama shule.


Matangazo haya yanawatenga walemavu ikiwemo mfano kujiunga na vyuo muombaji anawez kushindwa kufanya vizuri katika kujaza maoni yake mtandaoni ipo mifumo ambayo sio rafiki hali ambayo inaweza muombaji kujaziwa uongo,

 

Lakini pia Mfano unakuta matangazo haya yanaweka masharti fulani fulani ambayo yanawatenga walemavu, ama unakuta baadhi ya matangazo hasa ya kwenye televisheni mwanzo limeanza vizuri muombaji awe na sifa hii na zile, lakini kule mwishoni linamalizia kwa maoni zaidi wasiliana na mawasiliano yanayopita chini’’ hii inatenga walemavu hasa wasioona nchini hivyo, ameomba namna ya kuona hatua za kuchukuliwa ilikuwa katika usawa pande zote.’’ Amesema Eligius Bwalya. 


Aidha, Wadau hao kwa pamoja na wenzao kutoka nchi za Zimbabwe, Msumbiji, Namibia wameweza kutoa maoni yao kwa kila nchi kuona jinsi ya kupata hatua sahihi za kuwasaidia walemavu katika vyuo vya ufundi.






TMDA YANG'ARA MASHINDANO YA SHIMMUTA, YAICHAPA LGTI MABAO 4 KWA 2.

 

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.


TIMU ya soka ya Mamlaka ya Dawa na Vifaa tiba (TMDA) maarufu kama TMDA FC imeicharaza timu yaChuo cha Serikali za Mitaa-Hombolo ya LGTI FC kwa jumla ya mabao 4 dhidi ya 2 katika mashindano ya SHIMMUTA yanayoendelea Jijini Dodoma.


Mchezo huo umechezwa leo saa 2:00 asubuhi katika uwanja wa Humanity-1 uliopo Chuo Kikuu cha Dodoma.


Akizungumza mara baada ya mchezo huo kocha wa TMDA Bw. Brian Kyando ameeleza kuwa timu yake ilijiandaa vyema kupata matokeo katika mchezo huo.


"Tunamshukuru Mungu kwa kupata matokeo mechi ya leo. 

Tulijipanga kushambulia kuanzia dakika ya kwanza ili tuweze kupata magoli mengi lakini wapinzani wetu nao walijitahidi kutuzuia tukaishia magoli hayo manne. Mchezo huo umeshapita na sasa tunaangalia michezo iliyo mbele yetu ili nayo tufanye vizuri.


Mashindano ya SHIMMUTA yameanza kuanzia tarehe 12 Novemba, 2023 na yanatarajiwa kuendelea hadi tarehe 25 Novemba, 2023.