Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
Serikali ya Tanzania imeahidi
kuendelea kulinda, kusimamia na kutekeleza haki za binadamu ikiwemo haki za
raia wa Tanzania na Wakimbizi kutoka nchi mbalimbali wanaohifadhiwa hapa nchini
ambapo pia imesema itaendelea kusimamia Amani na Usalama ili madhila
yanayotokea katika nchi nyingine yasitokee hapa nchini.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es
Salaam na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Mheshimiwa Patrobas Katambi (MB)
wakati akizungumza katika Maadhimisho ya Siku ya Wakimbizi Duniani ambayo
huadhimishwa kila ifikapo Tarehe 20 ya mwezi Juni, kila mwaka, huku kauli mbiu
ya mwaka huu ikisema “Hadi Kila Mtu awe Salama”
Waziri Katambi akizungumza mbele ya
Wakimbizi wanaoishi jijini Dar es Salaam ambao waliwawakilisha wakimbizi
wanaoishi katika maeneo mbalimbali nchini amesema nchi ya Tanzania inajifunza
kwa yaliyotokea nchi jirani huku akitoa ahadi ya serikali ya kuwahudumia
Wakimbizi.
“Ni agizo la Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia,
watu wote ambao ni ndugu zetu Wakimbizi waliohifadhiwa hapa tutawahudumia hata
pale itakapohitajika rasilimali za nchi yetu tutazitumia, Rais wetu amekua
anafanya hivyo wakati wote hata pale tulipokosa ufadhili na fedha za wadhamini,
UNHCR aliendelea kutushika mkono lakini wapo wengine ambao hawakupata
tuliwaombea kwa Mwenyezi Mungu ili wapate waongeze nguvu lakini zilipokosekana
kabisa Rais wetu hakusita kuweka mkono wake ili Wakimbizi muendelee kuishi kwa
amani na utulivu, tunawapenda ndugu zetu, mmetupa uzoefu mmetupa mifano na
uhalisia na sisi tunajifunza kutoka kwenu” amesema Waziri Katambi
“Mmeeleza sababu zilizopelekea
kukosekana kwa Amani katika nchi zenu, zipo sababu ambazo pengine zinafanana na
zenu ikiwemo rushwa, kujipatia fedha kwa manufaa binafsi, utakatishaji fedha, ukwepaji
kodi na magendo yanayonufaisha wachache na kuumiza walio wengi, ubadhilifu, wizi
wa mali za umma, kughushi na kufanya udanganyifu, uhalifu wa kiuchumi, makosa
yanayoweza kuhatarisha amani ya nchi, uhaini, uchochezi wa vurugu, vurugu za
kisiasa, vyeo na mali, ubaguzi wa kidini, kikabila na ukanda, utapeli na dhulma
kwa wananchi, unyanyasaji wa kijinsia.” aliongeza Waziri Katambi
Waziri Katambi amesema Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Katiba ya Mwaka 1977 na marekebisho
yake chini ya Uongozi wa Dkt.Samia Suluhu Hassan ambae ni Rais na Amiri Jeshi
Mkuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Bunge na Mahakama wataendelea kusimamia
haki za binadamu, utii wa sheria, maslahi ya wananchi wote wakiwepo Wakimbizi.
