Friday, December 21, 2018

NAIBU WAZIRI WA NISHATI ATAKA WAKANDARASI WASICHELESHE KAZI.

Asema Hali ya hewa isiwe kisingizio cha kuchelewesha miradi ya umeme vijijini.

Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu amewataka wakandarasi wanaosambaza umeme vijijini kutochelewesha utekelezaji wa miradi hiyo kwa kisingizo cha mabadiliko ya hali ya hewa kama vile uwepo wa mvua. 

Aliyasema hayo wilayani Makete mkoani Njombe wakati alipokuwa akikagua kazi ya usambazaji umeme vijijini inayotekelezwa kupitia mradi wa usambazaji umeme vijijini wa Awamu ya Tatu (REA III) mzunguko wa kwanza.

“ Kabla ya Serikali kuwakabidhi kazi hii ya usambazaji umeme vijijini, mlishafanya upembuzi wa maeneo mnayoenda kufanyia kazi na mnayafahamu vizuri, hivyo basi, iwe Jua au mvua, tunataka kuona kazi hii inaendelea kutekelezwa ili wananchi wengi wapate huduma ya umeme,” alisema Mgalu

Aliongeza kuwa, wakandarasi hao wanapaswa kuwa na mipango mbalimbali ya utekelezaji wa kazi kulingana na hali ya hewa ya maeneo wanayofanyia kazi ili kuweza kusambaza umeme katika vijiji vyote walivyopangiwa na Serikali ifikapo Juni 2019.

Awali, Mkuu Wilaya ya Makete, Veronica Kessy, alimweleza Naibu Waziri kuwa, jumla ya vijiji 29 vimepangwa kuunganishiwa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa kwanza ambapo mkandarasi anaendelea na kazi ya usambazaji umeme vijijini, ingawa uongozi wa Wilaya hiyo umekuwa na wasiwasi na kasi yake katika usambazaji umeme.

Kuhusu hali ya upatikanaji umeme, alisema kuwa Wilaya hiyo inapata umeme kutokea mkoani Mbeya lakini laini hiyo ni ndefu na inapelekea changamoto ya kukatika kwa umeme mara kwa mara hivyo aliomba Wilaya hiyo ipate laini nyingine ya umeme kutokea mkoani Njombe.

Kuhusu suala hilo, Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, alisema kuwa, Serikali ilishaona changamoto hiyo ya umeme wilayani Makete na kueleza kuwa Wilaya hiyo ipo katika mpango wa kupelekewa umeme kupitia mradi wa Makambako- Songea ambao umekamilika.

Akiwa wilayani humo, NaibuWaziri aliwasha umeme katika kijiji cha Bulongwa na kukagua miundombinu ya umeme katika Kijiji cha Usagatikwa na Usungilo ambapo alimsisittiza mkandarasi kuongeza kasi ya kusambaza umeme.

Wilaya ya Makete ina Vijiji 96 ambapo vijiji 29 tayari vimeshasambaziwa umeme, vijiji 29 vinasambaziwa umeme kupitia REA III mzunguko wa kwanza na Vijiji 38 vinavyosalia vitasambaziwa umeme kupitia mradi wa usambazaji umeme vijijini wa Awamu ya Tatu unaotarajiwa kuanza Julai mwakani.



No comments:

Post a Comment