Friday, December 21, 2018

VULLU ATOA MSAADA KATIKA WODI YA UZAZI KISARAWE NA SARUJI MIFUKO 80 KWA AJILI YA UKARABATI WA ZAHANATI NA SHULE


NA MWAMVUA MWINYI, KISARAWE 

MBUNGE wa viti maalum mkoani Pwani, Zainab Vullu ametoa msaada wa mapazia mazito yanayotumika kusaidia kuweka usiri kwa akinamama wanaokwenda kujifungua katika wodi ya uzazi hospital ya wilaya ya Kisarawe. 

Msaada huo unaelezwa kuwaondolea kero waliyokuwa wakiipata akinamama hao kipindi cha nyuma ambapo walikuwa wakikataa kujifungua hospitalini hapo kwa kuhofia kukosa faragha wakati wa kujifungua. 

Mbali ya msaada huo pia ametoa mifuko 80 ya saruji kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa vituo vya afya ,zahanati na shule vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya sh.milioni mbili.

Akitoa msaada huo ,Zainab alieleza kipindi cha nyuma akinamama wanaojifungua walikuwa wanakaa sehemu ambayo haijazibwa  jambo ambalo limemsukuma kujitolea mapazia hayo.

“Faragha inaanza tangu pale anapoanza kutafutwa mtoto hadi anapozaliwa lazima usiri uwepo,” alifafanua Zainab.

Nae mkuu wa wilaya ya Kisarawe ,Jokate Mwegelo alimshukuru mbunge huyo na kudai suala la ukosefu wa mapazia hayo ilikuwa ni changamoto kwa akinamama wanaojifungua.

Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Hamis Dikupatile alisema, serikali imekuwa ikijitahidi kuboresha mazingira ya kutolea huduma lakini bado jitihada zinapaswa kufanywa na kila mmoja.

Mganga mkuu wa halmashauri ya Kisarawe, Jonathan Budenu alibainisha kutokana na changamoto hiyo baadhi ya akinamama walikuwa wakikataa kujifungulia hapo kutokana na hali hiyo.

No comments:

Post a Comment