Thursday, December 6, 2018

WATENDAJI KATIKA SEKTA YA UMMA WATAKIWA KUJIEPUSHA NA MGONGANO WA MASLAHI ILI KUJENGA UCHUMI IMARA WA TAIFA

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb), akizungumza na washiriki wa mjadala kwenye maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu Kitaifa, kabla ya kumkaribisha Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Mhe. Mohamed Chande Othman kufungua rasmi mjadala huo jijini Dodoma.
....................................

Viongozi, watumishi na wataalam mbalimbali nchini, wametakiwa kujiepusha na mgongano wa maslahi kwa kutotumia nyadhifa zao au ofisi zao kujinufaisha wao wenyewe, kuwanufaisha ndugu zao au jamaa zao na watu wengine ili waweze kutekeleza wajibu wao ipasavyo katika ujenzi wa uchumi imara wa taifa.

Wito huo umetolewa na Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Mhe. Mohamed Chande Othman wakati akifungua mjadala kwenye maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu Kitaifa, jijini Dodoma.

Mhe. Othman amesema, mgongano ya maslahi ni lazima udhibitiwe kwa nguvu zote kwani unailetea sifa mbaya serikali, taasisi, idara na sekta binafsi ambazo mgongano wa maslahi unajitokeza, na kuongeza kuwa unamletea pia sifa mbaya ya kiutendaji kiongozi au mtumishi kwenye fani au taaluma aliyobobea.

Mhe. Othman ameainisha njia za kuweza kuepukana na mgongano wa maslahi, njia hizo ni kujiuzulu au kujitoa endapo kiongozi anaona kuna maslahi binafsi kwenye jambo atakalolitolea maamuzi kwa ajili ya kulinda maslahi ya umma.

Mhe. Othman amesisitiza kuwa, ni jukumu la mtendaji mwenyewe kutamka mapema, kukiri kwa hiari na kwa uwazi kwamba ana mgongano wa maslahi kwenye suala atakaloenda kulitolea maamuzi badala ya kungoja kuambiwa ajiuzulu na kushutumiwa kuwa na mgongano wa maslahi kwenye suala aliloshiriki kutoa maamuzi.

Naye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika amesema, moja kati ya mambo ambayo ofisi yake inapambana nayo ni kuhakikisha inaondoa uwezekano wa kuwepo kwa mgongano wa maslahi katika taasisi za umma.

Mhe. Mkuchika amefafanua kuwa, kiongozi au mtumishi yeyote katika sekta ya umma hatakiwi kufanya biashara na taasisi yake kwasababu kuna uwezekano mkubwa wa kupendelea kampuni yake kuipatia zabuni na kuiongezea malipo ili aweze kujinufaisha na hatimaye kuitia hasara serikali.

Aidha, Mhe. Mkuchika ametoa wito kwa washiriki wa mjadala kuhakikisha wanatoa maoni na mapendekezo ambayo yataondoa changamoto ya mgongano wa maslahi katika sekta ya umma.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) amesema, viongozi na watumishi ambao wanasimamia maadili wanapaswa kuyaisha yale wanayoyasema, na ni muhimu pia ni wajibu wao kuonyesha njia katika uzingatiaji wa maadili ili wanapohubiri maadili mema wawe na ushawishi kwa umma.

Mhe. Dkt. Mwanjelwa ameongeza kuwa, vitendo vya mmomonyoko wa maadili vinatakiwa kukemewa bila kusita wala kuonewa haya kuanzia kwenye ngazi ya familia ili kujenga taifa lenye uadilifu.

Mada zilizojadiliwa katika mjadala huo ni pamoja na, Mgongano wa masilahi katika utumishi wa umma, Ulinzi wa haki za binadamu na mgongano wa maslahi na matumizi mabaya ya madaraka yanayopelekea mgongano wa maslahi na uwepo wa rushwa nchini.

No comments:

Post a Comment