Tuesday, December 11, 2018

RAIS DKT. MAGUFULI ATOA VITAMBULISHO KWA WAJASIRIAMALI NCHI NZIMA

Na. Immaculate  Makilika – MAELEZO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amegawa vitambulisho kwa wajasiriamali nchi nzima wenye mitaji isiyozidi shilingi milioni nne kwa lengo la kuwasaidia kufanya biashara zao kwa uhakika sambamba na kutambulika katika Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Akizungumza mapema leo jijini Dar es salaam, katika  kikao kazi na viongozi wa TRA, Rais Magufuli aligawa jumla ya vitambulisho 25,000 kwa kila Mkuu wa Mkoa, na kusema kuwa vitambulisho hivyo vimelengwa kutolewa kwa wajasiriamali wote nchi nzima wenye mitaji isiyozidi shilingi milioni nne ili viwasaidie kufanya shughuli zao mahali popote nchini, ikiwa ni pamoja na kutambulika TRA.

Ambapo Rais Magufuli alisema kuwa vitambulisho hivyo vinagawiwa bure, isipokuwa  kila mjasiriamali atatozwa gharama ya shilingi 20,000/= ikiwa ni sehemu ya gharama ya uandaaji wa kitambulisho husika.

“Kitambulisho hiki nimetoa mimi bure, sioni kama kuna mtu atakayekuja kuwasumbua, na kila Mkuu wa Mkoa atapata vitambulisho 25,000, ambapo atashirikiana na Wakuu wa wilaya ili kugawa vitambulisho hivyo kwa wajasiriamali walioko katika mkoa wake”

Halikadhalika, Rais Magufuli aliwataka wajasiriamali hao kuwa waaminifu, na kutokubali kufanya biashara za wafanyabiashara wakubwa wenye mitaji yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni nne.

Sambamba na hilo, Rais Magufuli alisisitiza watanzania kulipa kodi kwa kuwa kodi ndio msingi wa maendeleo kwa taifa lolote lile duniani, huku akiwataka TRA kupunguza viwango vikubwa vya kodi ambavyo wananchi wamekuwa wakivilalamikia.

Kwa upande wake, Gavana wa Benki Kuu, Profesa Florence Luoga alisema kuwa Benki hiyo imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali ikiwemo kudhibiti matumizi haramu ya fedha,  kuhakikisha kuwa thamani ya fedha haiyumbi na kudhibiti matumizi ya dola kwa kufungia maduka ya kubadilishia fedha ambayo hayakuwa na leseni.

Profesa Luoga alisema  kuwa BOT iligunduwa kuwepo kwa maduka ya kubadilishia fedha 1,000 badala ya maduka 300 yaliyokuwepo awali na ambayo hayakuwa na leseni.

“Tunajadiliana na Waziri wa Fedha ili kuwezesha wananchi au wafanyabiashara kulipia bidhaa  kwa kutumia benki” alisema Profesa Luoga

Profesa Luoga  aliongeza kuwa kwa sasa hivi hali ya fedha ni nzuri na hivyo Serikali ina fedha za kutosha kufanya matumizi mbalimbali kwa kipindi cha miezi mitano ijayo na kuwataka wananchi wasiwe na hofu.

Aidha, aliongeza kuwa kabla ya mwezi Desemba kuisha , BOT itakuwa imeshatengeneza kanuni za kuwalinda watumiaji wa mabenki.

Naye, Kamishna wa Mamlaka ya Mapato (TRA), Charles Kichere, alisema kuwa katika kipindi cha miaka ya Serikali ya Awamu ya Tano, TRA imefanikiwa kukusanya mapato ya jumla ya shilingi trilioni 42.9
Ambapo, katika kipindi cha robo mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali kupitia TRA imekusanya kodi jumla ya shilingi trilioni 3.8.

Aidha, Kichere alisema kuwa licha ya changamoto mbalimbali zinazoikabili Mamlaka hiyo, wameweza kusajili jumla ya wafanyabiashara wadogo yaani wamachinga 97,256 huku takribani  asilimia 80 ya wafanyabiashara wanatumia mashine za EFD

No comments:

Post a Comment