Saturday, December 8, 2018

JIJI LA DAR KUONGOZWA NA CCM, UKAWA

UCHAGUZI wa Naibu Meya wa jiji la Dar es Salaam, umefanyika Desemba 07, 2018 ambapo wajumbe wa Baraza hilo wamekubaliana kwa kauli moja kuwa na Manaibu wawili kutoka Chama Cha Wananchi CUF  na mwingine  Chama Cha Chamapinduzi CCM.

Hatua hiyo imetokana na kuwepo kwa idadi sawa ya wajumbe kwa pande zote mbili ambapo Ukawa ulikuwa na wajumbe 12 huku CCM ikiwa na wajumbe 12.

Akizungumza wakati wakutangaza uamuzi huo ulioafikiwa   na wajumbe wa Baraza hilo, Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita alisema kuwa kutokana na hali hiyo kila mmoja ataongoza kwa kipindi cha miezi mitatu hadi Juni 30 mwaka 2019.

Meya Mwita alieleza wajumbe wa baraza hilo kuwa, wamefikia uamuzi huo kwani viongozi wamechaguliwa kwa ajili ya kuleta maendeleo ya waanchi bila kujali vyama vyao.

Alisema kuwepo kwa viongozi wa vyama viwili tofauti haita  wakosesha wananchi maendeleo kwakuwa wote wamechaguliwa kwa lengo la kuwatumikia wakazi wa jijini hapa.

 Meya Mwita alitumia nafai hiyo  kuwasihi manaibu hao walioteuliwa kuonyesha ushirikiano mkubwa kwa ajili ya kuleta maendeleo jijini hapa kwakuweka itikadi ya vyama vyao pembeni.

“ Ndani ya ofisi hii kupata wasaidizi kutoka vyama tofauti sio dhambi, lengo langu ni kulifikisha jiji sehemu ambayo inatakiwa, ninaimani kuwa walioteuliwa leo tutasaidiana bila kujali itikadi za vyama vyetu” alisema Meya Mwita.

 Kabla ya kufanyika kwa maamuzi hayo, Meya wa Manispaa ya Kinondoni Benjamini Sita alitoa hoja baada ya kuwepo kwa mvutano mkali kuwa baraza lijigeuze kamati ili kufanya maamuzi ambayo yatakuwa na maslahi kwa wananchi kuliko kuendelea na mabishano.

“ Ndugu mwenyekiti hakuna haja ya kuendelea kubishana ,wote hapa tunafanya kazi kwa ajili ya wanachi wa jiji hili hapa, ningeshauri tujigeuze kamati ili kufikia muafa wa jambo hili.

 Baada ya hoja hiyo kutolewa, wajumbe wa baraza hilo walikubaliana kuwa kamati ambapo baada ya nusu saa, walirudi kuwa baraza na hivyo  Meya Mwita kutoa maamuzi ya uchaguzi huo.

Uchaguzi huo umefanyika ikiwa ni baada ya aliyekuwa Naibu Meya Mussa Kafana kujiuzulu nafasi yake na kujiunga na CCM Septemba mwaka huu.

No comments:

Post a Comment