Sunday, July 7, 2019

VETA WAJA NA MASHINE YA KUBANGUA KOROSHO





Na Selemani Magali; Daresalaam


ADHA ya kubangua korosho kwa kukoka moto sasa huenda ikabaki historia baada ya mamlaka  ya Ufundi  Stadi (VETA) Songea  kubuni  mashine  ndogo  ya kubangulia  korosho  yenye uwezo wa kubangua debe tatu kwa siku, huku ikiwa na uwezo wa kutenganisha ubora wa bidhaa hiyo. 

Mwalimu kutoka VETA Songea,  Susack Mbulu, amesema hayo katika banda la VETA, lililopo katika  maonesho  ya 43 ya biashara ya Kimataifa (DITF),  yanayoendelea katika viwanja  vya Mwalimu Nyerere barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam. 

Amesema mashine  hiyo inatumia nguvu  za binadamu  na itawasaidia  wazalishaji  wadogo  kuondokana na mfumo  wa  kukoka  moto  na kukaanga korosho  na kisha kuanza  kuzipasua kwa  mkono, badala yake sasa watatumia  mashine  hiyo. 

"Ukitumia mashine hii, unaweza kutenganisha korosho  kwa ubora, yaani kama ni daraja la kwanza hadi la tatu. Na  iwapo mtumiaji wa  mashine  hii ataanza  kubangua bila kukausha  korosho hizo vyema  zitavunjika na iwapo zitakauka  hazitovunjika bali  zitatoka  sawa," amesema.

Ameongeza kuwa mashine hiyo inauwezo wa kuanza kubangua  korosho  ndogondogo  ama zilizo kubwa kwa kuwa ina meno ya aina mbili ambayo kwa pamoja yanaweza kubangua zao  hilo na kumrahisishia mkulima mdogo. 

Hata hivyo, Mbulu ameushukuru  uongozi wa VETA makao  makuu  kwa ushirikiano  wao  na kuwezesha  kutekeleza  wazo  hilo, ambalo  linaunga  mkono  dhana ya  serikali  ya kufikia  uchumi  wa  kati  ambao  ni  wa  viwanda. 

Amesema katika  kufikia uchumi  wa  viwanda  VETA inaunga mkono  jitihada  hizo ambapo  wataweza  kuwafikia na  kuwasaidia wajasiriamali  wadogo. Lakini pia kusaidia korosho  kuingia  sokoni  katika  hali  ya  ubora.

"Lengo  letu ni kuhakikisha mashine hii inafikia kiwango  cha kutumia umeme au mota ambayo itafikisha hatua ya  kubangua  hata gunia moja  kwa  siku  la  korosho," amesema.

Aidha amewashauri  wafanyabiashara  wa  korosho kuwasiliana na VETA ili kuweza  kupata  mashine  hiyo na kuahidi kuwa  wanaweza  kuifikisha  serikali  katika  uchumi  wa viwanda.

No comments:

Post a Comment