Saturday, July 27, 2019

WALIOSAMBAZA PICHA ZA WANAWAKE MTANDAONI KUSHTAKIWA


Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu LHRC Anna Henga

Mtandao wa kupinga Ukatili wa Kijinsia (MKUKI) umesikitishwa na vitendo vya kusambazwa kwa picha zinazoonesha wanawake wanne, katika mitandao ya kijamii waliokuwa wakituhumiwa na kushikiliwa katika kituo cha polisi cha Mburahati Jijini Dar es Salaama kwa makosa ya jinai.

Akitoa tamko kwa niaba ya mtandao huo, Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu LHRC Anna Henga, amesema vitendo hivyo ni vya udhalilishaji wa utu wa mwanamke, ukiukwaji wa haki za binadamu pamoja na kuingilia uhuru wa faragha.

"Katika hali isiyokuwa ya kawaida picha za wanawake hao zilisambaa mitandaoni na imethibitika kwamba zilipigwa na maofisa wa polisi wa kituo cha Mburahati na tuliongea na Mkuu wa kituo hicho na akathibitisha kwa kusema zilipigwa kwa manufaa ya kikazi lakini tukaziona kwenye mitandao'' Amesema Anna Henga.

Aidha mtandao huo umetoa wito kwa Jeshi la polisi, kuwachukulia hatua za kinidhamu wahusika wa kitendo hicho ili kulinda utu wa mwanamke na watuhumiwa wa makosa ya jinai.

Ameongeza kwamba mtandao huo hautosita kuchukua sheria, ikiwemo kufungua mashtaka kwa wahusika wa tukio hilo.

No comments:

Post a Comment