Friday, July 5, 2019

OLENASHA ATAKA COSTECH KUSIMAMIA HAKI MILIKI ZA KAZI ZA WABUNIFU

Image may contain: 2 people, people smiling
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha ameitaka Tume ya Sayansi na Teknolojia nchini kusimamia wabunifu kupata haki ya umiliki wa bunifu zao.


Naibu Waziri Ole Nasha ametoa agizo hilo jijini Dar es Salaam, wakati alipotembelea mabanda ya Taasisi za Elimu zilizo chini ya Wizara hiyo ambazo zimeshiriki maonesho ya 43 ya biashara ya kimataifa maarufu kwa jina la Sabasaba na kukutana na mmoja wa wabunifu aliyeomba serikali imtambue kwa kuwa amebuni nyenzo ya kufundishia mfumo wa sayari shuleni.


Alisema ni vizuri wabunifu wanapoandaa kazi zao zikatambuliwa na kupatiwa haki miliki ya bunifu au ugunduzi walioufanya lakini pia kuendelea kuwafadhili ili waweze kukuza bunifu zao.


“Ninyi COSTECH hakikisheni bunifu mbalimbali nilizoziona hapa sabasaba katika mabanda yetu haziishii katika maonesho tu, bali zikuzwe na tumieni nafasi hii ya maonesho kuwakutanisha wabunifu na wafanya biashara kwa ajili ya uzalishaji,” alisema Naibu Waziri Ole Nasha.


Katika hatua nyingine Waziri Ole Nasha ameipongeza Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya ya kukuza ubunifu na ujuzi na kuwataka kuendelea kusimamia bunifu mbalimbali za wanafunzi ili ziingie katika soko na kutatua changamoto mbalimbali za kijamii.


Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia zilizoshiriki maonesho ya Sabasaba kwa mwaka 2019 ni pamoja na Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE), Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu Mzumbe, Tume ya Nguvu za Atomiki nchini (TAEC), Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Taasisi ya Elimu Tanzania (TIE) na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST)


No comments:

Post a Comment