Saturday, July 13, 2019

CHALIWASA YAWAPIGA MSASA WATUMISHI WAKE

Na Omary Mngindo, Chalinze.

WATUMISHI wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Chalinze (CHALIWASA) wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani, wametakiwa kuwatuliza wateja na kuwapa lugha nzuri, hasa pale wanapokuja kwenye ofisi wakiwa na jazba.


Kauli ya Mhandisi Raymond imefuatia malalamiko kutoka kwa Abdallah Kipolelo, aliyelalamikia kuwepo kwa baadhi ya viongozi wa CHALIWASA kutokuwa na lugha nzuri, mara baada ya kupokea taarifa za utendaji wa kazi kutoka kwa wateja.


Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka hiyo Mhandisi Honest Raymond, alipozungumza na watumishi katika kikao cha kukumbushana majukimu ya kazi, huku suala la nidhamu likisisitizwa katika kikao hicho.


"Sisi tunafundishwa namna ya kuwahudumia wateja, wao hawana somo kama hilo hivyo unapokutana na mteja anakuwa mkali, wewe jukumu lako ni kumtuliza, kwani wakati mwingine anaweza kufikia hatua ya kukupiga ngumi," alisema Mhandisi Raymond.


Kwa upande wake Kipolelo alisema kuwa kuna wakati mtumishi anapokea simu ya upole kutoka kwa mteja akimjulisha kuwepo kwa uvujaji maji eneo alilopo, lakini utakuta kiongozi anapiga simu kwa ukali, hatua aliyodai kama ya udhalilishaji.


"Mteja anakupigia simu kwa upole akikuelezea kuwepo kwa tatizo eneo moja, wakati huohuo unapigiwa simu kwa lugha ya ukali kutoka kwa kiongozi, wee Kipolelo uko wapi, nenda eneo fulani kuna tatizo, lugha ambayo ni ya udhalilishaji," alisema Kipolelo.


Akitoa mada katika kikao hicho, Elizabeth Eusebius ambaye ni Ofisa Maendeleo ya Jamii aliwaambia watumishi hao kuwa wameamua kutoa mafunzo hayo kwa lengo la kuongeza ufanisi wa utendaji kazi wa taasisi.


"Tumekuwa tukijikita katika utoaji wa elimu kwa watumiaji wa maji, kwetu tumejisahau warsha tunayopeana leo inalenga kufahamishana masuala mbalimbali ili wote tukafanyekazi za Mamlaka," alisema Elizabeth.

No comments:

Post a Comment