Wednesday, July 31, 2019

WANACHAMA WA YANGA BAGAMOYO WAFANYA USAFI WA MAZINGIRA.

Na Selestian James.

Wanachama wa klabu ya yanga wilayani Bagamoyo wameadhimisha wiki ya wananchi kwa kufanya usafi maeneo mbalimbali ya mji wa Bagamoyo.

Shughuli hiyo ya usafi imewajumuisha watu wa kada mbalimbali ambao ni wanachama wa yanga wakiongozwa na Diwani wa kata ya Nianjema  iliyopo katika halmashauri ya wilaya Bagamoyo, Abdul Mzee Pyallah ambaye pia ni katibu wa hamasa ya kuchangia Yanga Bagamoyo.

Miongoni mwa sehemu walizofika kufanya usafi ni pamoja na Hospitali ya wilaya ya Bagamoyo.

Shughuli hiyo yenye kauli mbiu "funga kazi kusanya kijiji" ni miongoni mwa hatua muhimu za maadhimisho ya  wiki ya wananchi ambayo ilizinduliwa  visiwani Zanzibar na itafikia kilele mwanzoni mwa mwezi ujao katika uwanja wa taifa jijini Dar es salaam.

Sambamba na hilo Diwani Pyallah pia amezungumzia uwepo wao tena hospitalini hapo siku ya tarehe tatu  ni kwa ajili ya kutembelea wodi ya watoto na kutoa zawadi mbalimbali kwa wagonjwa.

Aidha, alisema watatembelea kituo cha  watoto waishio katika mazingira magumu kilichopo katika kata ya Nianjema, na ziara hiyo itamalizikia katika gereza la Kigongoni kwa ajili ya kuwaona wafungwa gerezani humo.

Miongoni mwa shughuli walizoweza kufanya ni pamoja na kuchangia damu kwa wagonjwa pamoja na kushiriki na wananchi katika shughuli za kijamii ikiwa vitendo vinavyoakisi makusudio ya wiki ya wananchi.


Kwa upande wao madaktari waliokuwepo katika tukio hilo wameeleza kufurahishwa na hatua hiyo na kuwapongeza huku wakiwaomba kuendeleza utamaduni huo.

Aidha, waliowaomba pia kusaidia kifaa maalum cha kupimia upumuaji wa watoto kwani ni moja ya vifaa vinavyohitajika sana katika utendaji kazi wa hospitalini hapo.
 Wanachama wa Yanga Bagamoyo wakishiriki katika usafi wa mazingira katika hospitali ya wilaya Bagamoyo, ikiwa ni katika kuadhimisha wiki ya wananchi.
Diwani wa kata ya Nianjema  iliyopo katika halmashauri ya wilaya Bagamoyo, Abdul Mzee, akishiriki usafi wa mazingira pamoja na wananchama wengine wa Yanga ikiwa ni maadhimisho ya wiki ya wananchi.

PICHA ZOTE NA SELESTIAN JAMES. 

No comments:

Post a Comment