Thursday, July 25, 2019

SERIKALI YATUMIA ZAIDI YA BILIONI 19 KUKARABATI SHULE KONGWE 17 NCHINI

Image may contain: 3 people, people standing and beard
Serikali imetumia zaidi ya shilingi bilioni 19 kukarabati shule kongwe 17 nchini lengo likiwa ni kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia katika shule hizo za kitaifa ambapo jukumu la uratibu wa ukarabati wa shule hizo 17 ilipewa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA).


Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako wakati wa makabidhiano ya Miradi ya ukarabati wa shule hizo 17 yaliyofanyika katika shule ya sekondari ya wavulana Sengerema, wilayani Sengerema Mkoani Mwanza ambapo amesema ukarabati huo umefanywa kwa kutumia fedha za Serikali.


Prof. Ndalichako amesema ukarabati wa shule hizo 17 zilizosimamiwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania ni utekelezaji wa mpango kabambe wa serikali wa kukarabati shule zote 89 kongwe za serikali ambapo amesema mpaka sasa tayari shule kongwe 46 zimeshakamilika.


Alisema serikali inaendelea na utekelezaji awamu ya tatu ya mpango huu ambapo shule nyingine 17 zitakarabatiwa mwaka huu wa fedha.


Akizungumzia ukarabati huo Waziri Ndalichako alisema kama uamuzi wa uboreshaji wa mazingira ya kufundishia na kujifunzia katika shule kongwe usingefanyika mapema kungeweza kutokea majanga kwani hali ya miundombinu ilikuwa katika hali mbaya hasa katika mifumo ya umeme, maji safi na taka na mapaa mengi yalikuwa yameoza kabisa.


Nawaambia watanzania kwamba tulikuwa na hatari ya kupata majanga makubwa kama shule hizi zisingefanyiwa ukarabati huu mkubwa kwani sehemu nyingine hali ilikuwa mbaya zingeweza kudondoka na katika baadhi ya shule mabati ambayo yalikuwa yameezekwa ni yale ambayo kiafya hayaruhusiwi amesema Waziri Ndalichako.


Alisema ukarabati huo mkubwa katika shule kongwe umewezekana kufanyika kutokana na mwelekeo wa Serikali wa Awamu ya Tano ya kuhakikisha kwamba huduma kwa wananachi zinaboresha na dhamira ya serikali ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ya kuhakikisha kwamba fedha za umma zinaelekezwa kwa ajili ya maendeleo.


'Fedha zilizotumika katika uboreshaji huu ni matunda ya kodi za watanzania, narudia tena ni fedha za umma ambazo zimetolewa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba watoto wa kitanzania ambao wana safari ya kupata elimu wanapata katika mazingira bora" alisisitiza Ndalichako.


Ndalichako amepongeza Uongozi wa Wilaya, shule na mshauri muelekezi ambao ni Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya kwa usimamizi mzuri wa mradi huo pamoja na kusimamia vizuri matumizi ya fedha za mradi huo ambapo alisema hali na ubora wa majengo inavyoonekana inaakisi thamani ya fedha zilizotolewa.


Hata hivyo amewaasa wanafunzi kujenga utamaduni wa kutunza majengo na vifaa na viongozi wa shule hizo kuhakikisha pia pamoja na kutunza wanajenga utamaduni wa kufanya ukarabati mdogondogo kila wakati.


Prof. Ndalichako alisema serikali inaendelea kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji ambapo alitolea mfano katika mwaka wa fedha ulioisha wa 2018/19 serikali kupitia Mradi wa Lipa kulingana na Matokeo EP4R ilitenga na kutoa fedha ambazo ziliwezesha kujengwa kwa madarasa 1,208, mabweni 222, matundu ya vyuo 2,141 na nyumba za walimu 99 pamoja na kutatua changamoto ya huduma ya maji safi ambapo katika baadhi ya shule visima vilichimbwa.


Mkuu wa Wilaya ya Sengerema Emanueli Kipole amemshukuru waziri kwa uboreshaji wa sekta ya elimu katika wilaya hiyo kwani mambo makubwa yanafanyika katika kuhakikisha utoaji wa elimu unaboreshwa ukiondoa ukarabati wa shule sekondari ya wavulana Sengerema.


Ameeleza baadhi ya miradi ambayo tayari imeshapatiwa fedha ikiwemo ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya shule kiasi cha milioni 254, milion 410 kwa ajili ya ukarabati wa chuo cha wananchi ambacho kilikuwa kimechakaa na sasa inajengwa ofisi ya uthibiti ubora wa shule kwa zaidi ya shilingi milioni 152 ambazo zimetolewa na wizara.


Mwenyeiki wa Bodi ya Mamlaka ya Elimu Tanzania Prof. Maurice Mbago amemshukuru waziri na serikali kwa kuiamini Bodi ya Mamlaka hiyo kwa kuwapa kazi yakusimamia ukarabati wa shule kongwe 17 kati ya 89 na kutoa ufadhili wa asilimia 100 jambo ambalo linaonyesha ilivyodhamiria kuboresha elimu hususan mazaingira ya kufundishia na kujifunzia.


Awali Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania(TEA) Bahati Geuzye alimweleza waziri kuwa TEA iliingilia makubaliana ya kiutendaji na Halmashauri za maeneo husika juu ya usimamizi wa kazi kwa kusaidiaana na wataalam elekezi katika kusimamia ili matokeo ya kazi yaweze kutokea kwa wakati.


Waziri ndalichako katika kukabidhiwa mradi huo pia alitembelea Shulle ya Sekondari ya Wasichana Bwiru iliyoko katika Wilaya ya Ilemela Mkoani Mwanza ambayo imekarabatiwa katika mradi huo ambapo ametumia nafasi hiyo kuiagiza Mamlaka ya Elimu Tanzania kuwajengea Bweni moja katika shule. 


Mbunge wa Jimbo hilo Mh. Angelina Mabula alimpongeza na Kumshukuru Waziri wa Elimu kwa jitihada kubwa zinazoedelea katika kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji katika Wilaya hiyo na kuahidi kushirikiana kuhahakikisha shule hiyo inafanya vizuri zaidi katika mitihani ya kitaifa.


Shule 17 zilizokarabatiwa kwa uratibu wa TEA ni pamoja na Shule ya sekondari ya Dodoma, Mwenge sekondari singida, Sekondari ya Wasichana Ruvu, Kilakala Sekondari na Shule ya Sekondari Ilboru.
Image may contain: sky, tree and outdoorImage may contain: sky, tree and outdoor

No comments:

Post a Comment