Saturday, July 13, 2019

KAMISHNA MHIFADHI WA MISITU PROF. DOS SANTOS SILAYO AWASILI MAKAO MAKUU YA TFS JIJINI DAR ES SALAAM

Image may contain: 1 person, standing and outdoor
Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Tehama, Harold Chipanha akimpigia saluti Kamishna Mhifadhi wa Misitu Prof. Dos Santos Silayo mara baada ya kuwasili makao makuu ya Ofisi za Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania jijini Dar es Salaam kwa mara ya kwanza tangu kuvishwa cheo hiko cha kijeshi Julai 9,2019 wilayani Chato mkoani Geita
......................................... 


Kwa mara ya kwanza tangu avishwe cheo cha Kamishna Mhifadhi wa Misitu na Mhe. Dkt Hamisi Kigwangalla, Waziri wa Maliasili na Utalii na hatimaye kula Kiapo cha Utii na uadilifu mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Julai 9, 2019, Kamishna Prof. Dos Santos Silayo amewasili makao Makuu ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), jana, Julai 12 jijini Dar es salaam na kupokelewa na Viongozi Waandamizi na watumishi wa TFS.


Akizungumza na watumishi wake mara baada ya kuwasili ofisini hapo, Kamishna Prof. Silayo alisema mabadiliko yanayotokea katika sekta ya maliasili yamepelekea pia kubadili mfumo wa usimamizi na utendaji wetu toka ule wa Kiraia kwenda Jeshi Usu.


Hatua hiyo ikapelekea kuvishwa cheo cha Kamishna Mhifadhi wa Misitu na Mhe Dkt. Hamisi Kigwangalla, Waziri wa Maliasili na Utalii na kula Kiapo cha Utii mbele ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama Dkt. John Pombe Magufuli siku ya tarehe 9 Julai 2019.


“Mabadiliko hayo yanalenga kujenga uwezo wa taasisi, uwezo wa watumishi ikiwa ni pamoja na kuwajengea ari, uzalendo, weledi na ujasiri katika kusimamia rasilimali za misitu na nyuki,” alisema Kamishna Prof. Silayo.


Kamishna Prof. Silayo alisema uwezo wa watumishi wa TFS utaenda sambamba na weledi katika matumizi ya mbinu na vifaa vya kisasa vinavyoweza kumudu mabadiliko ya changamoto za uhifadhi kuanzia usalama wao pamoja na usalama wa mali zenyewe unaotokana na kuongezeka kwa mbinu za kihalifu kila wakati.


Aidha Prof. Silayo alitoa shukurani kwa Mheshimiwa Rais na viongozi wote wa wizara ya Maliasili na Utalii kwa hatua hiyo waliyofikia ambayo anaamini itasaidia kukuwa kwa sekta ya misitu nchini na kuongeza ushirikiano na wadau wengine hususani wananchi katika kusimamia misitu yetu.


Akiongea kwa njia ya simu Naibu Kamishna wa Huduma Saidizi, Emmanuel Wilfred alisema mabadiliko hayo yamepelekea kubadili mfumo wa usimamizi na utendaji wa TFS toka ule wa Kiraia kwenda Jeshi Usu na hivyo kulazimu watumishi wote kwenda kwenye mafunzo.


“Tunaendelea kutoa mafunzo kwa watumishi wachache waliobaki na kwa wale waliokwishakwenda kwenye mafunzo tunakamilisha taratibu ili Kamishna aweze kuwatunuku vyeo vyao, lakini niwatake wafanyakazi wote kuenda sambamba na mabadiliko kwa kasi hitajika,” alisema Kamishna Msaidizi huyo.


Rosemary Sabida mmoja wa watumishi wa TFS anasema mabadiliko hayo yataisaidia TFS kukabiliana na changamoto mbalimbali za uhifadhi nchini.


Jumla ya Makamishna wanne, Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) Dkt Allan Kijazi, Kamishna wa Uhifadhi wa Misitu toka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Prof Dos Santos Silayo na Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Dkt. James V. Wakibara pamoja na Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), Freddy Manongi walivishwa vyeo vya kijeshi Julai 9, 2019 katika sherehe za Uzinduzi wa Hifadhi ya Taifa ya Burigi – Chato zilizofanyika wilayani Chato mkoani Geita.
 Image may contain: 10 people, people standing, tree and outdoor

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Tehama, Harold Chipanha akimuongozo Kamishna Mhifadhi wa Misitu Prof. Dos Santos Silayo kwenda kwenye ukumbi wa mikutano wa Ngorongoro uliopo makuu ya Ofisi za Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuzungumza na watumish.
Image may contain: 18 people, people smiling, people standing 
Kamishna Mhifadhi wa Misitu Prof. Dos Santos Silayo akiwa katika picha ya pamoja na maofisa wa jeshi usu.


No comments:

Post a Comment