Saturday, August 20, 2016

WAAJIRI 264 SERIKALINI WAWASILISHA TAARIFA ZA WATUMISHI HEWA.

kai3
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.  Angellah J.  Kairuki (Mb) akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawako pichani) kuhusu utekelezaji wa agizo la kuondoa watumishi hewa katika orodha ya malipo ya mishahara Serikalini ofisini kwake mapema leo.
..............................................................................................


Waajiri 264 kati ya waajiri wote 409 Serikalini wamewasilisha taarifa zao kuhusu kuwepo kwa watumishi hewa ambapo kati ya waajiri hao waajiri 63 wamethibitisha kwamba hawana watumishi hewa katika Taasisi zao.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi Wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Angellah Kairuki (MB), amebainisha hayo wakati alipozungumzia na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa waajiri 201 wana watumishi hewa kuanzia mmoja na kuendelea.

“Waajiri 264 kati ya waajiri wote 409 wamewasilisha taarifa zao kuhusu uwepo wa watumishi hewa. Kati ya waajiri 264 waliowasilisha taarifa zao, waajiri 63 wamethibitisha kwamba hawana watumishi hewa katika Taasisi zao na waajiri 201 wana watumishi hewa mmoja (1) na kuendelea.” Alisema Waziri Kairuki.

Hata hivyo, alisema zipo taasisi 145 ambazo hazijawasilisha taarifa iwapo zina watumishi hewa au la ikiwemo Mabaraza 11, Bodi 10, Vyuo Vikuu 25, Hospitali 3 na Ofisi za Makatibu Tawala wa Mikoa  12.

Alizitaja taasisi nyingine kuwa ni Mamlaka 6, Tume 10, Mamlaka za Serikali za Mitaa 38, Taasisi za Umma na Wakala 30 ambapo aliziagiza Taasisi zote ambazo hazijawasilisha taarifa za watumishi hewa kufanya hivyo kabla au ifikapo tarehe 26 Agosti mwaka huu.

Waziri Kairuki alieleza kuwa kuanzia Agosti 15 mwaka huu, ofisi yake ilianza zoezi la uhakiki wa kushtukiza katika taasisi sabini za Serikali zikiwepo Wizara, Idara za Serikali Zinazojitegemea na kwamba zoezi hilo linaendelea.

Aliongeza kuwa uhakiki wa kustukiza utafanyika pia kwenye Sekretarieti za Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa na Taasisi za Umma kwa madhumuni ya kujiridhisha kwamba taarifa za watumishi hewa zilizowasilishwa na waajiri ni sahihi.

Alibainisha kuwa katika kufanikisha uhakiki huo, Ofisi yake imechukua hatua kadhaa ikiwemo kuendelea kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa Maafisa Utumishi wenye dhamana ya kutumia mfumo wa malipo ya mshahara kukuza uwajibikaji kwa maafisa wanaosimamia malipo ya mishahara kwa kuwachukulia hatua za kinidhamu au kisheria wanaobainika kusababisha watumishi hewa.

“Aidha ofisi yangu pia inafanya uhakiki wa kushtukiza na kuanza safari ya kuunganisha Mfumo wa Malipo ya Mishahara na mifumo mingine mikubwa kama ya NIDA, RITA na Baraza la Mitihani la Taifa, na kuwezesha mfumo kuwaondoa moja kwa moja (automatically) watumishi waliofikisha umri wa kustaafu kwa lazima.” alisema.

Waziri Kairuki atatoa taarifa kamili ya watumishi hewa baada ya kupata taarifa hizo kutoka kwa waajiri ambao hawajawasilisha taarifa hizo na kukamilika kwa zoezi la uhakiki wa Taasisi sabini (70) linaloendelea sasa.

“Hivyo naagiza Taasisi zote ambazo hazijawasilisha Taarifa za Watumishi Hewa kufanya hivyo kabla au ifikapo tarehe 26 Agosti, 2016.” Alisema Waziri Kairuki.

Alisema kuwa ofisi yake itawasilisha taarifa rasmi ya watumishi hewa kwa Mheshimiwa Rais ikiwa na orodha na majina ya Taasisi ambazo zimewasilisha taarifa ya watumishi hewa na na zile ambazo hazijawasilisha taarifa hizo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli mnamo Machi 15 mwaka huu aliwaagiza Wakuu wa Mikoa na Waajiri wote kwa ujumla kuchukua hatua ya kuhakikisha katika Mikoa au Taasisi zao hakuna watumishi hewa ifikapo tarehe 30 Machi, 2016.

Katika kutekeleza agizo hilo Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imekuwa ikifuatilia utekelezaji wa agizo hilo na mnamo  Mei 26 mwaka huu waajiri wote waliagizwa kuwasilisha taarifa za mwisho za zoezi la kuwabaini na kuwaondoa watumishi hewa katika orodha za malipo ya mshahara (payroll) ifikapo mwisho wa Mwezi Juni, 2016.

Waajiri walitakiwa kutuma jina la Taasisi, Fungu la Taasisi (Vote), namba ya Utambulisho ya Mtumishi wa Umma (Cheki Namba), jina kamili la mtumishi; cheo cha mtumishi, jina la tawi la Benki ambalo mshahara wa mtumishi umekuwa ukipitishwa au ukilipwa.

Taarifa nyingine zinazotakiwa kutumwa ni hatua zilizochukuliwa na mwajiri dhidi ya watumishi hewa waliobainika kama kurejesha fedha, na Maafisa wengine wa Taasisi husika waliosababisha uwepo wa Watumishi hao kuwachukulia wahusika hatua za kinidhamu au kisheria.

Nyingine ni namba ya akaunti ya Benki ya mtumishi, tarehe ambayo mtumishi aliondolewa kwenye mfumo wa taarifa ya Kiutumishi na Mshahara, kiasi cha fedha zilizolipwa kwa mtumishi husika tangu alipotakiwa kuondolewa hadi tarehe aliyoondolewa kwenye mfumo na sababu ya kuondolewa kama utoro, kufariki dunia, kuacha kazi, kustaafu na sababu nyingine.

No comments:

Post a Comment