Saturday, August 20, 2016

BASATA YATOA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KUFUATIA KIFO CHA MSANII SHAKILA

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limepokea kwa masikitiko na majonzi makubwa kifo cha Msanii wa muziki wa taarab Bi. Shakila Said kilichotokea ghafla nyumbani kwao Mbagala jijini Dar es Salaam jana Ijumaa ya tarehe 19/08/2016.

Shakila ni msanii na mdau wa muda mrefu wa sekta ya Sanaa nchini. Amekuwa na mchango mkubwa katika kukuza muziki wa taarab nchini hasa katika kubuni kazi za Sanaa za muziki mbalimbali ambazo zilikuja kupata umaarufu mkubwa. Moja ya kazi alizobuni na kupata umaarufu mkubwa ni pamoja na 'Macho yanacheka' na 'kifo cha mahaba'.

Mchango wake katika muziki wa taarab hasa katika kubuni na kutunga nyimbo zenye ubora, ujumbe na maadili kwa jamii hautasahaulika kamwe. Ni mwanamuziki aliyeacha misingi katika sekta ya muziki na alijitolea kwa kiasi kikubwa katika kuufikisha muziki wa taarab mahali ulipo leo.

Baraza, wasanii na wadau wote wa Sanaa hatuna budi kuendelea kuenzi mema yote aliyotuachia marehemu Shakila hasa katika kupenda kujitolea muda mwingi katika kukuza muziki wa taarab na sekta ya muziki kwa ujumla.

Baraza linatoa pole kwa ndugu wa marehemu, shirikisho la muziki, wasanii na wadau wote wa Sanaa katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na mpendwa wetu.

No comments:

Post a Comment