Thursday, August 15, 2019

WAKAZI KONGO WALILIA DARAJA MTO RUVU

Na Omary Mngindo,  

WAKAZI wa Kitongoji cha Umakondeni Kijiji cha Kongo Kata ya Yombo, wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani, wameomba wapelekewe Mhandisi wa ujenzi kuangalia uwezekano wa kujenga daraja katika mto Ruvu unaopita eneo lao.


Wakazi hao wametoa kilio hicho mbele ya mbunge Dkt. Shukuru Kawambwa, kwenye ziara ya kikazi jimboni humo, ambapo akiwa kijijini hapo wakazi hao walisema kuwa wanaliwa na mamba kutokana na kuvuka ng'ambo ya pili kwa ajili ya kilimo.


Aidha wamelalamikia gharama za kuunganishiwa maji, ambapo walisema kwamba pamoja na kuishi ndani ya eneo la mradi ulioko kijijini hapo, lakini gharama ya huduma hiyo kwa bomba yenye urefu wa mita 50 wanatakiwa walipie shilingi laki mbili.


Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Ally Jasilii alisema kuwa wanalima ng'ambo ya mto Ruvu chini ambapo kila siku wanavuka kwemda na kurudi, hali inayowaweka katika wakati mgumu huku akieleza kwamba kuna wenzao wameliwa au kujeruhiwa na mamba.


"Mheshimiwa Mbunge tunakuomba utuletee Mhandisi aangalie uwezekano wa kujenga daraja katika mto Ruvu chini, sisi tegemeo letu ni kilimo ng'ambo ya mto, wenzetu wameliwa na kujeruhiwa na mamba, tuletee Mhandisi," alisema Jasilii.


Kwa upande wake Ibrahimu Issa alisema kuwa wanakabiliwa na hatari ya mamba kutokana na kutegemea maji ya mto huo, pamoja na wao kuishi ndani ya mradi wa mradi lakini hawana huduma hiyo.


"Tunaambiwa kuunganishiwa bomba yenye urefu wa mita 50 shilingi laki mbili, mimi nina ardhi eka 3 sasa hizo mita zao 50 si zitaishia shamba la jirani yangu, tunakuomba na hili ukalifanyiekazi," alisema mkazi huyo.


Akijibia malalamiko hayo, Dkt. Kawambwa alisema kuwa amepokea malalamiko hayo na kuahidi kuyafanyiakazi, huku akisema kuwa ujenzi wa daraja mto huo unawezekana, huku akisema lakini kazi yake ni kubwa.


"Pamoja na kwamba ujenzi wa daraja mto Ruvu kazi yake ni kubwa, lakini hakuna lisilowezekana, nitakwenda kuzungumza na Wahandisi tutakuja kuangalia uwezekano wake," alisema Dkt. Kawambwa.


Akizungumzia kilio cha gharama ya kuunganishiwa maji, Dkt. Kawawambwa alisema kuwa kimsingi wakazi wanaoishi ndani ya eneo la mradi kungekuwa na unafuu wa bei, na kwamba kwa namna moja au nyingine wanasaidia kulinda miundombinu ya mradi.


"Haya yote nimeyapokea nitakwenda kukutana na viongozi husika kuzungumza nao hatimae kuwapatia mrejesho baada ya mazungumzo yetu, kuhusu mhandisi nitakuja nae kuona namna itakavyowezekana," alimalizia Dkt. Kawambwa.

No comments:

Post a Comment