Monday, September 26, 2016

PROF. LIPUMBA BADO MWENYEKITI HALALI WA CUF- MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA.

index 
 
Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inatumia fursa hii kufafanua kwamba, msimamo alioutoa Msajili wa Vyama vya Siasa kuhusu mgogoro wa uongozi katika chama cha CUF una maana kwamba, kwa mujibu wa taarifa zilizowasilishwa kwake  na pande mbili zinazosigana na kwa mujibu wa Katiba ya CUF toleo la 2014, Msajili alijiridhisha kwamba, Profesa Lipumba bado ni Mwenyekiti halali wa Taifa wa chama cha CUF, kwa sababu alitengua barua yake ya kujiuzulu kabla haijakubaliwa na mamlaka yake ya uteuzi, kama inavyoelekeza ibara ya 117(2).

Aidha, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inaviasa vyombo vya habari kufanya jitihada za kuelewa msimamo wa Msajili wa Vyama vya Siasa, badala ya kuandika habari au makala zinazopotosha umma.

Hivyo, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inatumia fursa hii pia, kukanusha taarifa zinazoenezwa katika vyombo vya habari ikiwamo mitandao ya kijamii kwamba, Msajili wa Vyama vya Siasa amesema kuwa, hakumrudishia Profesa Lipumba Uenyekiti wa Taifa wa CUF, bali Profesa Lipumba kajirudisha mwenyewe kinyemela. Habari hiyo siyo ya kweli, imepotoshwa kwa makusudi, Watanzania wanapaswa kuipuuza.

Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inawaasa viongozi wa kitaifa wa chama cha CUF, kusoma kwa makini msimamo uliotolewa na Msajili wa Vyama vya Siasa na kuuheshimu, kwani kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Siasa Sura ya 258, Msajili wa Vyama vya Siasa anao wajibu wa kujiridhisha kwamba, mabadiliko yoyote yaliyofanywa katika uongozi wa taifa wa chama cha siasa, ni halali na yamefanywa na mamlaka halali kwa mujibu wa Katiba na Kanuni za chama husika.

                            Sisty L. Nyahoza                          
         Kny: MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA    

No comments:

Post a Comment