Saturday, October 22, 2016

MANJI AWATAKA WANACHAMA YANGA KUWA WATULIVU BAADA YA MAHAKAMA KUZUIA MKUTANO WAO WA DHARULA ULIOKUWA UFANYIKE KESHO.

index
Mwenyekiti wa klabu ya Yanga, Yusuf Manji amewaomba wanachama wa timu hiyo kuwa watulivu mara baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Kisutu, kuzuia mkutano wa dharura uliopangwa kufanyika kesho kwenye makao makuu ya klabu hiyo.

Akizungumza na waandishi Leo Manji alisema kuwa ni kweli jana jioni walipata barua kutoka mahakama hiyo ya kuzuia mkutano ambao ulikuwa halali kikatba ya Yanga.

“ Tuwaombe radhi kwa wanachama wote kutoka sehemu mbalimbali kwa gharama zenu hata kama waliozuia mkutano wetu si wanachama na tunaamini itafikia siku, tutakutana kwa kuwa mkutano ni haki yetu ya msingi”alisema Manji.

Aidha amesema kuwa utulivu ni jambo jema, lazima tuonyeshe ukweli kuwa sisi ni watulivu, waelewa lakini tutekeleze uamuzi huo wa mahakama huku tukisubiri siku yetu itafikia na kila kitu kitafanyika kwa utaratibu.

Hata hivyo, Manji alisema waliopeleka zuio hilo la mkutano si wanachama kwa kuwa Frank Chacha hajalipia ada yake kwa zaidi ya miezi sita na mwingine Juma Magoma pia si mwanachama wa Yanga kwa kitambo sasa.

Aidha, alisisitiza hata hao waliokwenda mahakamani kama wangekuwa wanachama hai, basi wangekuwa wameishajifuta rasmi baada ya kwenda mahakamani kwa kuwa katiba ya Yanga inakataza kwenda mahakamani kama ilivyo kwa Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).

Klabu ya Yanga ilitarajia kufanya Mkutano Mkuu wa dharura wa kujadili mabadiliko yanayotaka kufanyika kwa mwenyekiti huyu kukodishiwa nembo ya klabu hiyo kwa miaka 10 jambo ambalo limeanza kugawa wanachama ambao wengine wanataka akodishiwe na wengine wanapinga.

No comments:

Post a Comment