Friday, July 8, 2016

CLOUDS TV YAKEMEWA KWA KUTANGAZA USHOGA.

Makamu Mwenyekiti wa kamati ya Maudhui, Joseph Method Mapunda.


Kamati ya maudhui ya Mamlaka ya mawasiliano nchini TCRA, imekionya kituo cha utangazaji cha Clouds Television kufuatia kuzungumzia ushoga katika kipindi chake cha TAKE ONE, kilichorushwa tarehe 28/06/2016 ambapo mwendeshaji wa kipindi hicho alimualika mtu aliyejitambulisha kwamba yeye ni shoga.

Akisoma maelezo ya hukumu yaliyochukua dakika 27, katika ofisi za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Makamu Mwenyekiti wa kamati ya maudhui ya TCRA, Joseph Method Mapunda alisema kituo hicho cha Television kilikiuka kanuni na maadili ya utangazaji kutokana na mambo yafuatayo

1.   Kipindi kimeonyesha waziwazi jinsi ushoga unavyofanyika pamoja na mbinu zinazotumika.
2.   Shoga aliyehojiwa hajuti kujiingiza katika katika tabia hii mbaya hasa pale anaposema kuwa, ataendelea kufanya ushoga hadi mwisho wa maisha yake.

3.   Lugha iliyotumika katika mahojiano haina staha.
4.   Tabia ya ushoga inaanzia shuleni.

5.    Mtangazaji alikuwa anauliza maswali yanayoashiria kushabikia ushoga.
Aidha, Mapunda aliongeza kuwa, kamati hiyo ya maudhui ya TCRA ilibaini kuwa, kipindi kilikuwa hakina ubora kwakuwa maswali mengi aliyokuwa anauliza mtangazaji yalilenga kuhamasisha ushoga ikiwa ni pamoja na matumizi ya lugha isiyo na staha.

Aliongeza kuwa, kila mwenye leseni ya utoaji huduma za utangazaji lazima ahakikishe kuwa, vipindi vyake vinaepuka kufuru katika jamii na vizingatie unyeti wa imani za kidini na utamaduni katika jamii.
Alisema watanzania kwa kuzingatia imani zao za kidini na utamaduni hawakubaliani na ushoga.

Katika utetezi wake Clouds Television walisema kuwa jamii imebadilika kwa kiasi kikubwa na kwamba ukubwa tatizo la ushoga lipo kwenye mitandao ya kijamii hadi kufikia matangazo kutolewa katika mitandao hiyo.

Aidha, Clouds Television walikiri kuwa, ushoga ni kitu kibaya na kuongeza kuwa ifike wakati mtu akifanya kitendo cha ushoga aogopwe.

Makamu mwenyekiti huyo wa kamati ya maudhui ya TCRA alisema kuwa baada ya kusikiliza na kutafakari kwa kina maelezo ya utetezi yaliyotlewa na uongozi wa Clouds Television, kamati ya maudhui imeridhika kuwa mada ya ushoga kupitia kipindi cha TAKE ONE kilichorushwa hewani tarehe 28/06/2016 kilikiuka baadhi ya kanuni za huduma za utangazaji (Maudhui) 2005, ambazo ni 5(b), 5(c), 5(d), 15(c) na 16(2).

Mapunda aliongeza kuwa hukumu iliyotolewa kwa Clouds Television ni kuwa
1.   inatakiwa kuwaomba radhi watazamaji wake na watanzania kwa ujumla kutokana na kuwakwaza pamoja na kuwasababishia usumbufu kwa kurusha mada inayoongelea ushoga kwa namna upotoshaji kupitia kupitia kipindi cha TAKE ONE kilichorushwa tarehe 28/06/2016.

Aidha, Taarifa ya kuomba radhi itoke siku tano mfululizo kwenye Taarifa za habari za saa 1:30 usiku na saa 5:00 usiku kuanzia siku ya kusomwa hukumu na uthibitisho wa taarifa hizo uwasilishwe Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania siku ya jumatano ya tarehe 13/07/2016 kabla ya saa 10:00 jioni.

2.   Clouds Television inatakiwa kurekebisha mapungufu yaliyojitokeza na kuhakikisha inazingatia kanuni zote za utangazaji nchini katika kutekeleza majukumu yake ya utangazaji.

3.   Kamati ya Maudhui, inawaonya vikali Clouds Television kwa kukiuka kanuni za utangazaji (Maudhui), 2005 na 5(b), 5(c), 5(d), 15(c), na 16(2).

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Clouds Television Ruge Mutahaba alisema wamepokea kwa masikitiko hukumu hiyo kwakuwa lengo la kipindi hicho ni kuielimsha jamii madhara ya ushoga na si vinginevyo.

No comments:

Post a Comment