Sunday, June 16, 2019

MKANDARASI WA MRADI WA UMEME WA RUFIJI KUANZA UJENZI RASMI.

Image may contain: 6 people, people smiling, people standing, outdoor and nature
Imeelezwa kuwa, Mkandarasi wa mradi wa umeme wa Rufiji, kampuni ya JV Arab Contractors na Elsewedy Electric ameanza rasmi kazi za ujenzi wa mradi huo hapo jana tarehe 15/6/2019.


Hayo yalisemwa na Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani tarehe mara baada ya kukagua kazi za maandalizi ya awali ya ujenzi wa mradi huo akiwa ameambatana na Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Regina Chonjo, Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, Mkurugenzi wa TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka na watendaji wengine kutoka kampuni ya mkandarasi, Wizara ya Nishati na TANESCO.


Mkandarasi huyo anaanza ujenzi ikiwa ni baada ya kufanya matayarisho mbalimbali ikiwemo upelekaji wa vifaa vitakavyotumika ktk shughuli za ujenzi, uwepo wa kambi za wafanyakazi, Ofisi na kukamilisha kazi nyingine za awali ambapo kwa mujibu wa mkataba, alipewa miezi Sita ya kufanya kazi hizo ambayo ukomo wake ulikuwa ni tarehe 14/6/2019.


Dkt Kalemani alisema kuwa, kazi anazoanza nazo ni upasuaji wa miamba ili kuruhusu maji kupita kwenda kwenye mitambo ya kufua umeme.


Alisema kazi nyingine za awali zitakazofanywa ni kujenga daraja la muda litakaloruhusu upitishaji wa vifaa kwenda kwenye eneo jingine la kazi pamoja na ujenzi wa daraja la kudumu.


Dkt Kalemani alieleza kuwa, Mkandarasi ameahidi kukamilisha mradi huo ifikapo mwezi Juni, mwaka 2022 na mradi utatekelezwa kwa kasi na ikiwezekana, megawati zote 2115 zitapatikana kwa wakati mmoja.


Kuhusu vifaa vitakavyotumika kwenye mradi huo, Dkt Kalemani aliwataka kutumia vifaa vinavyopatikana nchini na kwa vifaa visivyopatikana nchini, vitanunuliwa baada ya kupata kibali maalum.


Pia aliagiza Wataalam wa ndani kupewa kipaumbele katika ujenzi wa mradi huo, ili waweze kusimamia mradi huo mara baada ya mkandarasi kukamilisha kazi.


Aidha, aliwapongeza TANESCO na TANROADS kwa kusimamia mradi huo ipasavyo, na kuwaagiza kuendelea kuwasimamia wakandarasi usiku na mchana.
Image may contain: 8 people, people standing and outdoor

No comments:

Post a Comment