Monday, June 3, 2019

SERIKALI HAINA MPANGO WA KUVIBADILI VYUO VYA MAENDELEO YA WANANCHI KUWA VETA- OLE NASHA.

Image may contain: 1 person, smiling
Serikali imesema haina mpango wa kuvibadili Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi kuwa VETA na badala yake imejikita katika kuviboresha Vyuo hivyo kwa kuvikarabati na kuviongezea vifaa vya kujifunzia na kufundishia ili viweze kutoa mafunzo bora zaidi.


Kauli hiyo imetolewa Bungeni leo Juni 03, 2019 na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha, wakati akijibu swali la Mhe. Mohamed Omary Mchengerwa (Rufiji), aliyetaka kujua kama serikali haioni umuhimu wa kukibadili chuo cha Maendeleo ya Wananchi Ikwiriri FDC kuwa VETA ili kubadili fikra za wananchi wa Rufiji, Kibiti na Ikwiriri na hatimaye kuleta mwamko wa elimu.


Ole Nasha amesema serikali inaendelea kuvikarabati vyuo hivyo ambapo awamu ya kwanza ya ukarabati unaohusisha vyuo 20 upo katika hatua za mwisho za ukamilishaji na kwamba awamu ya pili inatarajiwa kuanza mapema mwezi Juni, 2019.


Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Ikwiriri kilikuwa katika Awamu ya kwanza na ukarabati umekamilika.


Aidha katika mwaka wa fedha 2019/20 Rufiji ni miongoni mwa wilaya zilizotengewa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) cha Wilaya.


"Kwa sasa, Serikali haina mpango wa kuvibadili Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi kuwa VETA na badala yake, imejikita katika kuviboresha Vyuo hivyo kwa kuvikarabati na kuviongezea vifaa vya kujifunzia na kufundishia viweze kutoa mafunzo bora" alisema Ole Nasha


Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi vilianzishwa kwa lengo la kumsaidia mwananchi kukabiliana na changamoto za kimaendeleo katika mazingira yake kwa kumpatia Maarifa na Stadi anuwai ambapo vyuo hivi hutoa Elimu ya Ufundi Stadi katika hatua ya Kwanza hadi ya Tatu.


Mafunzo yanayotolewa katika vyuo hivyo ni pamoja Ujasiriamali, Kilimo, Uvuvi, ufugaji na mengine kulingana na mahitaji ya eneo husika na kwamba hivi sasa nchini kuna vyuo vya maendeleo ya wananchi 55.

No comments:

Post a Comment