Monday, June 24, 2019

DED-BAGAMOYO ATAKA WATUMISHI KUFANYA KAZI KWA KUZINGATIA SHERIA.

Image may contain: 3 people, people sitting
Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Bi. Fatuma Latu amewaasa watumishi wa Halmashauri hiyo kufanya kazi kwa kuzingatia Sheria, Taratibu na Kanuni (STK) za utumishi wa Umma ili kuleta matokeo chanya kwenye utumishi.


Bi. Fatuma Latu, ameyasema hayo mapema wakati alipokuwa akifungua mkutano maalum wa watumishi takribani 200 wa Halmashauri hiyo, uliofanyika katika ukumbi wa Halmashauri, katika kilele cha maadhimisho ya juma la utumishi wa Umma.


“Kila mtumishi ahakikishe anafanya kazi kwa kuzingatia Sheria, taratibu na kanuni za utumishi wa Umma, hizi ziwe dira wakati tukitimiza majukumu yetu ya kila siku ili kuleta matokeo chanya ya utekelezaji wa shughuli za Serikali katika Halmashauri yetu” Alisema Bi. Fatuma Latu.


Bi. Fatuma Latu pia ametumia fursa hiyo kuwaasa Watumishi kuhakikisha wanajiepusha na vitendo vya rushwa, matumizi ya lugha chafu, na kuhimiza ushirikiano baina ya watumishi katika ngazi zote, huku akitanabaisha kwamba hatamvumilia mtumishi yeyote ambaye atapatikana na makosa ya kuomba ama kupokea rushwa.


Akaongeza, Suala la kutunza siri pia ni muhimu sana wakati wa utekelezaji wa Shughuli za Serikali kila mmoja katika nafasi yake, utunzaji wa Siri unatufanya kufanya kazi kwa kuaminiana na kwa usalama wakati wote hivyo kuongeza ari ya kutumikia Wananchi.


Vilevile, Mkurugenzi Mtendaji, Bi. Fatuma Latu, amewakumbusha watumishi kuhakikisha wanapata chakula bora na kujipa muda wa kupumzika baada ya kumaliza kutimiza majukumu yao ya kila siku ili mwili uwe na Afya wakati wote na kuongeza uwezo wa kufanya kazi.


Nae, Mkuu wa Idara ya Utumishi na Utawala Ndg. George Mwalukasa akizungumza na watumishi katika Mkutano huo amewahimiza watumishi kuwa makini pale wanapotakiwa kuhuisha taarifa zao za kiutumishi, kwani wengi wao wamekuwa na hulka ya kupuuzia maagizo ya usafishaji taarifa za kiutumishi yanapotolewa, kwani kupuuzia usafishaji wa taarifa za mtumishi kunaweza kupelekea mtumishi kuondolewa katika orodha ya malipo ya mshahara.


Aliongeza kwa kusema  “Mtumishi ambaye hatajaza fomu za OPRAS kuaniza tarehe 01 Julai, 2019, ambapo OPRAS zitaanza kujazwa kwa njia ya kielektroniki, hatapata mshahara hadi hapo atakapokuwa amejaza fomu hiyo ya upimaji wa utendaji kazi wa Mtumishi, yaani OPRAS”.


Wakati huo huo, watumishi wamepata darasa maalum la madhara ya kujihususha na vitendo vya rushwa ambapo Afisa TAKUKURU – Elimu kwa Umma, Bi. Jane Mgaya amezungumzia mada maalum ya madhara ya vitendo vya Rushwa katika utendaji kazi wa kila mtumishi anapokuwa akitekeleza majukumu yake ya kila siku.


“Tuepuke mambo yanayopelekea uwepo wa mazingira ya vitendo vya rushwa kutengenezwa, tunapokuwa tukitekeleza majukumu yetu ya kila siku, mambo hayo ni pamoja na ukosekanaji wa uwazi katika uwajibikaji, urasimu katika utoaji huduma na tamaa ya kujipatia mafanikio kwa haraka” Alisema Bi. Jane Mgaya


Aliongeza, athari za rushwa ni kubwa kwani rushwa huondoa utu na thamani ya mtu, hudhoofisha utoaji huduma bora, kukosekana kwa uwazi na uwajibikaji katika utumishi wa umma na hupelekea mtumishi kufanya maamuzi yenye upendeleo, hivyo akasisitiza kila mmoja kushiriki katika vita dhidi ya rushwa ili kuiletea jamii yetu maendeleo kwani vita dhidi ya rushwa si ya TAKUKURU peke yake bali ni ya jamii nzima ili kuiletea jamii yetu maendeleo.


Wiki ya utumishi wa umma huadhimishwa mara moja kila Mwaka kila ifikapo Mwezi Juni, ambapo shughuli mbalimbali za kiutumishi huambatana na maadhimisho hayo, ikiwa na pamoja kusikiliza kero na malalamiko toka kwa Watumishi na kuzipatia ufumbuzi,


Aidha, katika maadhimisho hayo kunakuwa na semina mbalimbali zinazohamasisha weledi na utawala bora katika utumishi wa umma, pamoja na mkutano maalum wa watumishi ambao hufanyika siku ya kilele cha Wiki ya Utumishi wa Umma ambao huhudhuriwa pia na wadau mbali mbali toka sekta binafsi zikiwemo taasisi za kifedha na mashirika binafsi Wilayani hapa.
Image may contain: 2 people, people sitting, table and indoor

No comments:

Post a Comment