MWENGE WA UHURU KUWASILI KAGERA AGOSTI 30, 2026
Mkuu wa mkoa wa Kagera Kanali Yahya Kido akizungumza na waandishi wa habari mkoani humo
...................
MWENGE WA UHURU KUWASILI KAGERA AGOSTI 30, 2026
Na Alodia Dominick
Bukoba
Miradi ya maendeleo ipatayo 54 yenye thamani ya sh bilioni 23 inatarajiwa, kuwekewa mawe ya msingi, kuzinduliwa, kukaguliwa na kufunguliwa na mbio za mwenge wa uhuru mwaka huu mkoani Kagera.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Augosti 26, 2026 Mkuu wa Mkoa wa Kagera Kanali Yahya Kido amesema, mwenge wa uhuru utapokelewa wilaya ya Muleba kutokea mkoa wa Geita Agosti 30,2026 na kukimbizwa katika halmadhauri nane za mkoa huo kwa umbali wa kilomita 1,230 ambapo miradi 54 yenye thamani ya sh bilioni 23 itafikiwa na mwenge huo.
Kanali Kido amesema, miradi 25 itawekewa mawe ya msingi, miradi mitano itafunguliwa, miradi 11 itazinduliwa na miradi 13 itakaguliwa na miradi hiyo inajikita katika sekta ya maji, afya, elimu, miundombinu, nishati, uwezeshaji vijana kiuchumi na mazingira wezeshi kwa uwekezaji.
"Ujumbe mkuu wa mwenge wa uhuru unahusu amani, umoja na mshikamano wa kitaifa chini ya kauli mbiu isemayo Tanzania ni yetu sote tushikamane kwa pamoja kuleta maendeleo" amesema Kanali Kido
Ameeleza kuwa, Mwenge wa uhuru utaendelea kuhamasisha na kuelimisha wananchi juu ya mapambano ya rushwa, maralia,vvu ukimwi, dawa za kulevya na uzingatiaji wa lishe bora.
"Niwaalike wanaanchi wote kujitokeza kwa wingi kuupokea mwenge wa uhuru mkoani Kagera tuupokee kwa bashasha na shangwe utakapowasili katika maeneo yetu ili kuonyesha ishara ya umoja, amani na mshikamano sisi wana Kagera".
Amewaomba wananchi kujitokeza kwa wingi katika maeneo yote ya mapokezi, barabarani, katika miradi na maeneo ya mikesha katika wilaya zote
Mwenge wa uhuru unatarajia kukamilisha mbio zake mkoani Kagera Septemba 6,2026 na kukabidhiwa mkoa wa Kigoma Septemba 7, 2026.




Comments
Post a Comment