HALMASHAURI YA BAGAMOYO YATENGA SHILINGI BILIONI 2, KWA MWAKA 2026/2027.
Na Mwandishi
wetu, Bagamoyo
Halmashauri ya
mji wa Bagamoyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 imetenga kiasi cha shilingi
Bilioni 2 ili kutekeleza miradi ya maendeleo kwa fedha za mapato ya ndani.
Akizungumza
na waandishi wa Habari, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Bagamoyo, Shauri
Selenda, amesema pia inatarajia kupokea fedha kiasi cha shilingi Bilioni 7
kutoka Serikali kuu, huku zaidi ya milioni 474 kutoka kwa wafadhili kwaajili ya
miradi mbalimbali.
Amesema
fedha hizo za mapato ya ndani zitatumika kutekeleza miradi mbalimbali kwa mwaka
wa 2026/2027 huku miongoni mwa miradi hiyo ikienda kuunga juhudi za kutekeleza
Dira ya Taifa ya mwaka 2050.
Alifafanua
kuwa, miradi yote hiyo inalenga Kwenda kuwakwamua wananchi wakazi wa Bagamoyo
katika kuboresha huduma mbalimbali na miundombinu ya mji wa Bagamoyo.
Selenda
alisema mwaka 2021/2022 Halmashauri ya Bagamoyo ilikuwa inatenga fedha kiasi
cha shilingi Milioni mia nane 800 lakini kwa sasa wameweza kufikia kiwango cha
shilingi Bilioni 2 ambazo zitapelekwa katika Kata 11 za Halmashauri ya mji wa
Bagamoyo.
Miongoni mwa
miradi itakayotekelezwa ni upande wa Afya, Elimu na masoko pamoja na
kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Akielezea
matumizi ya Bilioni mbili za mapato ya ndani ni pamoja na ujenzi wa madarasa manane
ya shule ya Sekondari ya Shushila Ladwa, iliyopo kata ya Mapinga ambapo kwa
mara ya kwanza unakwenda kutekelezwa
Mradi wa ujenzi wa madarasa ya kisasa ya ghorofa yaliyotengewa bajeti ya
shilingi milioni 250.
Amesema
ujenzi wa madarasa ya ghorofa utasaidia kubana matumizi ya Ardhi kwani mji wa
Bagamoyo unakuwa na uhitaji wa Ardhi ni mkubwa ukilinganisha na ukubwa wa Ardhi
iliyopo.
Alieleza
kuwa katika mabadiliko ya mfumo wa elimu nchini ifikapo mwaka 2028 kutakuwa na
mapokezi ya makundi mawili yanayoingia kidato cha kwanza, kwa wale
watakaomaliza darasa la saba na wale watakaoishia darasa la sita ambao wote wanatakiwa wapate vyumba vya
kusomea.
Kutokana na
hali hiyo, Selenda amesema Halmashauri ya mji Bagamoyo imejipanga ili
kuhakikisha katika kipindi hicho hakuna mwanafunzi atakaeshindwa kusoma
kwasababu ya upungufu wa vyumba vya madarasa au vitendea kazi.
Mkurugenzi
huyo wa Halmashauri yam ji Bagamoyo, amesema katika fedha hizo milioni mia moja
zimetengwa kwaajili ya ujenzi wa Barabara za mitaa ili kila mtaa uweze kufikiwa
kwa urahisi.

Comments
Post a Comment