SAMIA AKUTANA NA MAASKOFU WA KATOLIKI, WAZUNGUMZA AMANI NA MUSTAKABALI WA TAIFA

 

Na Albert Kawogo


RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekutana na kufanya mazungumzo na Maaskofu wa Kanisa Katoliki nchini kupitia Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), katika hatua inayolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na viongozi wa dini.


Mazungumzo hayo yamefanyika leo, Agosti 10, 2026, katika Ikulu ya Chamwino, mkoani Dodoma, ambapo viongozi hao wamejadili masuala mbalimbali ya kitaifa, yakiwemo siasa, imani, amani, mshikamano na maendeleo ya jamii.


Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari Machumu, mkutano huo umeangazia pia umuhimu wa kuendelea kuimarisha amani na mshikamano wa Taifa, pamoja na kujenga mustakabali wenye ustawi kwa Watanzania.


Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamejadili nafasi ya madhehebu ya dini na viongozi wake katika kujenga jamii yenye maadili mema, uwajibikaji na mshikamano, sambamba na kuchangia juhudi za maendeleo endelevu ya Taifa.


Rais Samia amewashukuru Maaskofu hao kwa kuona umuhimu wa kukutana naye na kujadili masuala yenye tija kwa Taifa, akisisitiza umuhimu wa mazungumzo na mashauriano katika kujenga uelewano na mshikamano miongoni mwa Watanzania.


Aidha, Rais Samia amewahakikishia viongozi hao dhamira yake ya kuendeleza utamaduni wa kushauriana na kushirikisha viongozi wa dini pamoja na makundi mbalimbali ya kijamii katika kujadili na kutafuta suluhisho la masuala muhimu yanayolihusu Taifa.


Mkutano huo unakuja wakati ambapo ushirikiano kati ya Serikali na taasisi za dini unaendelea kuwa sehemu muhimu katika juhudi za kuimarisha amani, maadili, mshikamano na maendeleo ya Tanzania.


Comments

Popular posts from this blog

TANZANIA KUPATA DOLA MILIONI 41 ZA KUHIMILI MABADILIKO YA TABIANCHI

BAGAMOYO: MJI WA KIHISTORIA UNAONGOJEA MAPINDUZI MAKUBWA YA KIUCHUMI KUPITIA BANDARI MPYA

KIKWETE ATEMBELEA BANDA LA HALMASHAURI YA MJI BAGAMOYO NANENANE

SAMIA URGES FASTER INFRASTRUCTURE DELIVERY ACROSS AFRICA.

WANAFUNZI WA SHULE YA VIPAJI YA KIBAHA SEKONDARI KUONDOKANA NA CHANGAMOTO YA UCHAKAVU WA MADARASA