Tuesday, December 6, 2016

MIKOA NA HALMASHAURI ZATAKIWA KUWEKA TAHADHARI JUU YA KIPINDUPINDU.


ummi1
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu kushoto akipokea vifaa mbalimbali vya matibabu ya mabadiliko ya awali ya Saratani ya mlango wa kizazi vyenye thamani takribani milioni 100 za kitanzania kutoka kwa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Pink Ribbon Red Ribbon  Bi. Celina Schocken jijini Dar es salaam.
..........................
 
MIKOA na halmashauri nchini zimetakiwa kuweka tahadhari juu ya ugonjwa wa kipindupindu kwa kuzingatia usafi binafsi na usafi wa mazingira hasa wakati wa mvua za vuli na msimu wa sikukuu za mwisho wa mwaka ili kuweza kuepuka ugonjwa huo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu mwenendo wa ugonjwa wa kipindupindu kwa mwezi Novemba 2016 uliofanyika jijini Dar es salaam.

“Mikoa na Halmashauri zote nchini ziwe katika hali ya tahadhari juu ya ugonjwa wa kipindupindu kwa kuzingatia usafi binafsi na usafi wa mazingira hasa wakati wa mvua za vuli na msimu wa sikukuu za mwisho wa mwaka ili kuweza kuepuka ugonjwa huo” alisema Waziri Ummy.

Aidha Waziri Ummy amesema kuwa Mikakati ya kudhibiti ugonjwa wa Kipindupindu ishirikishe sekta mbalimbali za afya nchini bila kusahau jamii husika na kuhakikisha kila Halmashauri inaunda na kuimarisha Kamati ya Afya ya Kata.

Aidha Waziri Ummy ameiagiza Mikoa na Halmashauri zote nchini kutoa taarifa ya wagonjwa wapya wa Kipindupindu ili jitihada za makusudi za kupambana na ugonjwa huo zifanyike mapema ili kujenga taifa lisilo na magonjwa ya mlipuko.

Mbali na hayo Waziri Ummy amesema kuwa takwimu zinaonesha katika mwezi Novemba 2016 jumla ya mikoa sita ikiwemo Morogoro yenye wagonjwa 282, Dodoma 96 na vifo 2, Mara 31, Kigoma 30 na vifo 4, Arusha 11 na Dar Es Salaam 8 kutoka wagonjwa  250 na vifo 4 kwa mwezi Oktoba mwaka huu.

Kwa wakati huohuo Waziri Ummy amepokea vifaa vya matibabu ya mabadiliko ya awali ya Saratani ya mlango wa kizazi vyenye thamani takribani milioni 100 za kitanzania kutoka Shirika la Kimataifa la Pink Ribbon Red Ribbon ili kupambana na ugonjwa huo nchini.

Akikabidhi msaada huo Mtendaji Mkuu wa Shirikahilo Bi. Celina Schocken amesema kuwa wametoa vifaa hivyo ili kuisaidia nchi kwa juhudi za kimakusudi katika kupambana na ugonjwa wa saratani ili kuokoa maisha ya wanawake wa Tanzania.

“Tumeamua kutoa vifaa hivi ili kuisaidia nchi kwa juhudi za kimakusudi katika kupambana na ugonjwa wa saratani ili kuokoa maisha ya wanawake wa Tanzania ”alisema Bi. Schocken.

No comments:

Post a Comment