Monday, September 25, 2023

WAANDISHI WA HABARI WAPATA ELIMU YA MATOKEO YA SENSA YA WATU NA MAKAZI YA 2022.

 

Kamisaa wa sensa ya watu na makazi 2022 Anna Makinda akizungumza na waandishi wa habari katika mikoa ya Mwanza, Kagera na Mara katika mafunzo ya matokeo ya sensa ya mwaka 2022 yaliyofanyika jijini Mwanza ukumbi wa mamlaka ya chakula na dawa TMDA
...............................
Alodia Dominick, Mwanza.

Waandishi wa habari katika mikoa ya Mwanza, Kagera na Mara wameanza mafunzo ya siku mbili yatakayowajengea uwezo wa kuandika habari kuhusu usambazaji na matumizi ya matokeo ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022.

Mafunzo hayo ya siku mbili yameanza leo Septemba 25, 2023 katika ukumbi wa mamlaka ya chakula na dawa (TMDA) jiji Mwanza na yatahitimishwa Septemba 26,2023.

Kamisaa wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 Anna Makinda akizungumza na waandishi wa habari amesema kuwa, wametoa mafunzo hayo ili kuwawezesha kupata uelewa jinsi ya kuandika habari za matokeo ya sensa ya 2022 ambayo ilikuwa na mazoezi mengine mawili ya kuhesabu majengo na anuani za makazi.


"Niombe muwe watulivu na wasikivu katika mafunzo haya ili mada zitakazofundishwa mzielewe na mnaporudi kwenye mikoa yenu muweze kuandika habari za takwimu kwa usahihi" amesema Makinda

Makinda amevipongeza vyombo vya habari hususani redio za kijamii kwa kufanikisha sensa ya watu na makazi ya 2022 kwani watumia redio hizo kuliendesha vipindi vya kuelimisha jamii na watu walikuwa wakiwauliza maswali ya uelewa katika vipindi hivyo.

Amesema, kuwa baada ya kupata takwimu na kujua idadi ya watu wote nchini sasa wanaenda kurudisha fadhira kwa wananchi kwani kipindi cha uhamasishaji waliomba wananchi wajiandikishe na sasa wanaenda kuwaletea maendeleo kwa kujenga miradi mbalimbali ya maendeleo inayogusa maisha yao.

Akifungua mafunzo hayo mgeni rasmi mkuu wa wilaya ya Nyamagana Amina Mwakilagi kwa niaba ya mkuu wa mkoa huo Amos Makala ametaja lengo la mafunzo kuwa ni kuwajengea uwezo waandishi wa habari jinsi ya kuandika habari za matokeo ya sensa ya watu na makazi iliyofanyika mwaka 2022.

Amesema mkoa Mwanza kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2022 ina watu 3.7 milioni huku 2012 ilikuwa na watu 2.7 milioni na kuwa ni miongoni mwa mikoa yenye watu wengi ambayo ni Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma, Tabora na Geita.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kagera press club Mbeki Mbeki amesema waandishi wayachukue yatakayofundishwa katika mafunzo ili yawawezeshe kuwaelimisha wananchi. 

Mgeni rasmi mkuu wa wilaya ya Nyamagana Amina Mwakilagi katika mafunzo ya siku mbili kwa waandishi wa habari juu ya matokeo ya sensa ya mwaka 2022

No comments:

Post a Comment