Friday, May 24, 2024

MWENGE WA UHURU WATUA LINDI, KUTEMBELEA MIRADI 53

 

Mkuu wa Mkoa wa Lindi Mhe. Zainab Telack leo, Mei 24, 2024 amepokea Mwenge wa Uhuru kutoka kwa  mkuu wa Mkoa wa kusini Unguja Mhe. Ayoub Mohammed Mahmoud, ambapo unatarajiwa kuwekwa mawe ya msingi, na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo yenye thamani ya shilingi bilioni 45.9


Makabidhiano ya Mwenge huo  yamefanyika katika viwanja vya Ndege Wilayani Kilwa Mkoani Lindi na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa chama na serikali sambamba na wananchi wa maeneo hayo.


Akitoa taarifa ya Mkoa wakati wa Makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru, Mhe Telack amesema kuwa katika Mkoa wa Lindi Mwenge wa Uhuru unatarajiwa kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo yenye thamani ya shilingi bilioni 45.9


Akipokea Mwenge huo Telack amesema Mwenge huo wa uhuru ukiwa Mkoani Lindi unatarajiwa kukimbizwa kwa umbali wa kilometa 1128.7 katika Wilaya 5 na halmashauri 6 za Mkoa huo ambapo jumla ya miradi 15 itawekwa mawe ya msingi, miradi 13 itazinduliwa na miradi 25 itatembelewa.


Telack amesema kwa kuzingatia Kauli mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2024 unaolenga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu "Uhifadhi wa mazingira na Uchaguzi wa serikali za Mitaa", Mhe. Telack ameeleza kuwa Mkoa wa Lindi umeweza kuongeza kasi ya upandaji miti ambapo hadi kufikia April mwaka huu, jumla ya miti 6,544,230 imepandwa.


Pia, Mkoa huo umeendelea kushirikiana na OR- TAMISEMI katika kuhakikisha maandalizi ya awali ikiwemo uhakiki wa vituo vya uchaguzi pamoja na kutoa hamasa na elimu kwa wananchi kushiriki uchaguzi wa serikali za mitaa katika mikutano mbalimbali vinafanyika.

Kwa upande wake kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa, Godfrey Eliakim Mzava , amewatahadharisha viongozi wa mkoa na wilaya kuwa na nyaraka zote muhimu katika miradi husika ambayo itatembelewa na Mwenge huo ili waweze kuzipitia kwa kina na kujiridhisha.


“Naomba niwakumbushe viongozi wangu wa Mkoa wa Lindi katika miradi yote tutakayotembelea huko wilayani kwenu naomba nyaraka zote zinazohusika ziwepo na tuzipate asubuhi mapema kabla hatujaanza kutembelea miradi yenyewe hii itatupa sisi urahisi wa kuzipitia taarifa mapema,” amesema Mzava






No comments:

Post a Comment