Saturday, August 8, 2026

MAKAMU WA RAIS ASHIRIKI IBADA YA MISA TAKATIFU YA JUMUIYA YA URU SEMINARI

 


MAKAMU WA RAIS ASHIRIKI IBADA YA MISA TAKATIFU YA JUMUIYA YA URU SEMINARI.


ASISITIZA SERIKALI INATHAMINI MCHANGO WA TAASISI ZA DINI KATIKA MAENDELEO YA TAIFA HUSUSANI SEKTA YA AFYA NA ELIMU



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema Serikali itaendelea kuthamini mchango wa Taasisi za Dini ambazo kwa namna ya pekee zimekuwa zikishiriki katika kutoa mchango kwenye sekta za Afya na Elimu hapa nchini.

 



Makamu wa Rais amesema hayo mara baada ya kushiriki Ibada ya Misa Takatifu Maalum ya Wanajumuiya wa Uru Seminari, iliyofanyika katika Kanisa Katoliki Parokia ya Kristo Mchungaji Mwema – Tabata Kimanga Jijini Dar es Salaam. 



Amesema kwa miaka mingi na kwa asilimia kubwa Taasisi za dini zimechangia katika utoaji wa huduma za elimu na afya, hivyo Serikali itaendelea kushirikiana na Taasisi hizo ili kufanikiwa zaidi katika kulijenga Taifa.



 

Makamu wa Rais amesema Malezi yanayotolewa katika Taasisi za elimu za dini ikiwemo Shule ya Uru Seminari ambayo husisitiza Sala, Kazi na Masomo yanapaswa kutiliwa mkazo katika malezi ya vijana wa sasa. 



Amesema vijana watakavyoweza kumjua Mungu, kufanya kazi kwa bidii pamoja na kupata elimu wataweza kulijenga vema Taifa kupitia ujuzi na hivyo kuepusha tabia za kupata kipato kupitia njia zisizo sahihi.



 

Makamu wa Rais amewashukuru, walimu, walezi na wanafunzi waliopata elimu Uru Seminari kwa ushirikiano na malezi mazuri ambayo yalifundisha kumtumikia Mungu pamoja na Wanadamu.

 



Amewasihi Wanajumuiya ya Uru Seminari kuendeleza umoja na kuhakikisha unakuwa wenye tija kwa Taifa, pamoja na kuendelea kuiombea nchi na Viongozi wake.

 



Ibada ya Misa Takatifu ya Wanajumuiya wa Uru Seminari, imeongozwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Kigoma, Mhashamu Joseph Mlola.

 



Akitoa mahubiri kwa Wanajumuiya wa Uru Seminari , Askofu Mlola amewasihi kukumbuka wito muhimu walionao wa kupeleka tunu njema ya Maisha ya kiimani kuishi kwa kumpendeza Mungu pamoja na wanadamu. 



Amesema ni muhimu kuwa mstari wa mbele kupeleka matumaini, ukweli, amani na haki.

 



Pia, Askofu Mlola amewasihi kuhakikisha uwepo wa kila mwanajumuiya wa Uru Seminari analeta upendo na matumaini, kwa kutambua huo ni wito kwao waliolelewa na kufundishwa katika malezi na maadili mema.

 

Uru Seminari ni Shule inayomilikiwa na Shirika la Mitume wa Yesu chini ya Kanisa Katoliki  Jimbo Moshi Mkoani Kilimanjaro.

 

Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais

08 Agosti 2026

Dar es Salaam.








SERIKALI YAELEKEZA SHILINGI BILIONI 300 KUCHOCHEA TIJA YA KILIMO NCHINI.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye Trekta baada ya uzinduzi wa magari kwa ajili ya Wakala ya Taifa ya Huduma za Ugani (NAESA) na Matrekta ya vyama vya Ushirika kwenye Maonesho ya Kilimo ya Nanenane, Kitaifa katika viwanja vya Maonesho vya Dkt. John Samuel Malecela, Jijini Dodoma, tarehe 08 Agosti, 2026.

....................................


Serikali imeongeza uwekezaji katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi kwa kupanua upatikanaji wa mikopo kwa vijana, wanawake na wajasiriamali, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza tija katika minyororo ya thamani ya sekta hizo.




Hatua hiyo imebainishwa leo katika Kilele cha Maonesho na Sherehe za Wakulima, Wafugaji na Wavuvi (Nanenane) mkoani Dodoma, ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amekabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya shilingi bilioni 300 kwa benki saba zitakazotekeleza mpango huo.



Benki zitakazoshiriki ni CRDB, Stanbic, Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Tanzania Commercial Bank (TCB), Azania Bank, Benki ya Ushirika, na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB).




Mpango huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuongeza rasilimali katika sekta hizo, sambamba na ongezeko la bajeti za kisekta na kuimarisha mtaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania katika kutoa mikopo ya kutekeleza shughuli za kilimo.




Rais Dkt. Samia amesema Serikali imeongeza mtaji wa benki hiyo kwa shughuli za kilimo, akisisitiza uwekezaji huo uonekane katika tija, uzalishaji, masoko na kipato cha wananchi.




“Tunataka kuona ufanisi huu ukitoa matokeo ya moja kwa moja; tuone mkulima, mvuvi na mfugaji ananufaika kule alipo na anaongeza kipato chake,” amesema Rais Dkt. Samia,

akiongeza kuwa Serikali itaendelea kutafuta masoko ya ndani na nje, huku ikipanua

ushiriki wa sekta binafsi katika uzalishaji, uwekezaji na kuongeza thamani.




Katika hatua nyingne, Rais Dkt. Samia ameagiza Wakala wa Taifa wa Huduma za Ugani Kilimo (NAESA) kuimarisha utoaji wa huduma kwa wazalishaji na kukamilisha mifumo ya kidijitali ya kusimamia huduma za ugani nchini.




Vilevile, ameeleza umuhimu wa uzalishaji kuongozwa na taarifa za soko, akitaja tumbaku, kahawa na mazao ya baharini kama mifano ya bidhaa ambazo uzalishaji wake umechochewa na upatikanaji wa taarifa za masoko duniani.




Kwa upande wake, Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo, amesema Serikali imeanza maandalizi ya vituo vya kimkakati vya biashara ya mahindi na mpunga katika maeneo manne nchini, ili kuimarisha masoko, uhifadhi na kupunguza upotevu baada ya mavuno.




Ameongeza kuwa Serikali imefikia makubaliano ya kibiashara na Jamhuri ya Sudan Kusini, yatakayowezesha mazao ya kilimo ya Tanzania kuuzwa moja kwa moja nchini humo.




Waziri Chongolo amesema hatua hiyo imefuatia ushiriki wa ujumbe wa Sudan Kusini katika Maonesho ya Nanenane mwaka huu, huku wafanyabiashara zaidi kutoka nchi hiyo wakitarajiwa kushiriki katika maonesho hayo mwaka 2027.




Naye, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, amesema Wizara hiyo

tayari imepokea shilingi bilioni 30 kati ya shilingi bilioni 200 zilizotengwa na Serikali kwa ajili ya uwezeshaji wa vijana, wanawake na makundi maalum.




Amesema shilingi bilioni saba tayari zimetolewa kwa walengwa, huku shilingi bilioni 23 zikitarajiwa kutolewa kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania kwa shughuli za mifugo na uvuvi.




Akiwasilisha salamu za sekta binafsi, Rais wa Shirikisho la Wakulima Tanzania, Bw. Jitu

Vrajlal Son, amesema ushirikiano wa Serikali na sekta binafsi utaongeza ufanisi katika kupanga vipaumbele vya kilimo na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.




Amesema ushirikiano huo unaweza pia kuharakisha uwekezaji katika uzalishaji wa mbolea nchini kwa kutumia malighafi zinazopatikana Tanzania, ikiwemo gesi asilia.




Mwenyekiti wa Wabia wa Maendeleo katika Kilimo, Dkt. Nyabenyi Tito Tipo, amesema Maonesho ya Nanenane yameonesha uwezo wa Tanzania kujenga sekta ya kilimo yenye tija, ushindani na ustahimilivu kupitia uwekezaji, sera wezeshi na ushirikiano.




Amesema Wabia wa Maendeleo wataendelea kushirikiana na Serikali kuimarisha uwekezaji katika minyororo ya thamani, teknolojia za kidijitali, kilimo himilivu kwa tabianchi, upatikanaji wa fedha na masoko.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo Maalum kutoka kwa Waziri wa Kilimo Mhe. Daniel Chongolo, kwa niaba ya Kamati ya Maandalizi ya Nanenane Kitaifa, 2026 katika viwanja vya Maonesho vya Dkt. John Samuel Malecela, Jijini Dodoma, tarehe 08 Agosti, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitembelea banda la Kampuni ya pembejeo za kilimo ya Betaren ya Urusi katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane yanayofanyika Kitaifa katika viwanja vya Maonesho vya Dkt. John Samuel Malecela, Jijini Dodoma, tarehe 08 Agosti, 2026.

VERONICA MREMA WA TANZANIA AINGIA SITA BORA TUZO ZA ISU ELIHLE 2026 AFRIKA

 

Na Mwandishi Wetu


Mtanzania Veronica Mrema , mwanachama wa Mtandao wa Mabloga Tanzania , TBN, anayeendesha jukwaa la kidijiti la  M24 TANZANIA MEDIA ni miongoni mwa waandishi wa  habari sita  waliochaguliwa kuendelea na mchakato wa tuzo za ISU Elihle kwa mwaka 2026 Barani Afrika.




Veronica ametajwa katika orodha hiyo baada ya wazo lake la habari kuhusu watoto wanaoishi na ugonjwa wa Siko Seli kupitiwa, na kuonekana ni bora.




Jopo la majaji wa tuzo hizo limesema kulikuwa na mawazo 155 ambayo walipokea kutoka nchi mbalimbali za Afrika.

Hatua ya Veronica kutajwa kwenye tuzo hiyo inaongeza rekodi nzuri katika uandishi wa habari za afya na maendeleo na kuiweka Tanzania katika nafasi ya kuendelea kutoa waandishi wa habari wanaotumia kalamu zao kuibua changamoto za watoto na kuchochea mabadiliko yenye manufaa kwa jamii.




Kupitia wazo lake lililochaguliwa Veronica atafanya uchunguzi na kuibua simulizi kuhusu mzigo unaoongezeka wa ugonjwa wa Siko Seli miongoni mwa watoto nchini Tanzania, akiangazia kwa kina namna ugonjwa huo unavyoathiri maisha ya watoto, kuanzia afya zao, lishe, elimu, ukuaji wa kimwili, pamoja na ustawi wao wa kihisia na kisaikolojia.




Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Afya, idadi ya watoto wanaozaliwa na ugonjwa wa Siko Seli nchini imeongezeka kutoka takribani watoto 8,000 hadi 14,000 kila mwaka, hali inayoifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye mzigo mkubwa wa ugonjwa huo Afrika na duniani. 




Tanzania inatajwa kuwa miongoni mwa nchi tatu zenye idadi kubwa ya watoto wanaozaliwa na ugonjwa huo Barani Afrika kila mwaka huku ikishika nafasi ya nne duniani.




Pamoja na ukubwa wa tatizo hilo, bado kuna watoto  hukumbana na changamoto za kuchelewa kugundulika, ukosefu wa huduma maalum za matibabu na uelewa mdogo wa jamii kuhusu ugonjwa huo.




Veronica atakusanya simulizi za watoto wanaoishi na Siko Seli, wazazi na walezi wao, wataalamu wa afya, wataalamu wa lishe pamoja na watunga sera, kwa lengo la kuonesha hali halisi ya maisha yao na kuibua suluhisho zinazoweza kuboresha afya na ustawi wa watoto hao.




Akizungumza baada ya kutangazwa kuwa mmoja wa washindi, Veronica amesema amepokea kwa heshima kubwa kutajwa katika orodha hiyo ya ISU Elihle.




"Ni fursa ya kuendelea kutumia uandishi wa habari kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

"Kuchaguliwa miongoni mwa waandishi sita kutoka kazi 155 zilizowasilishwa ni heshima kubwa kwangu na kwa Tanzania. 




Lakini zaidi ya yote, ni nafasi ya kuhakikisha sauti za watoto wanaoishi na Siko Seli zinasikika.




"Ninaamini simulizi hizi zitasaidia kuongeza uelewa wa jamii na kuhimiza uwekezaji zaidi katika uchunguzi wa mapema, huduma za afya na lishe kwa watoto hawa," amesema.




Ameongeza atatumia uandishi wa habari unaozingatia ushahidi, takwimu na simulizi za wahusika ili kuonesha changamoto halisi zinazowakabili watoto wenye Siko Seli na kuibua mijadala itakayochochea maboresho ya sera na huduma za afya.




ISU Elihle Award inalenga kuhamasisha uandishi wa habari unaoweka watoto katikati ya simulizi na unaochochea mijadala yenye kuleta mabadiliko ya sera, uwajibikaji na hatua za kuboresha ustawi wa watoto barani Afrika.




Pamoja na Veronica Mrema wa Tanzania, washindi wengine wa ISU Elihle Award 2026 ni David Arome wa The Development Report [Nigeria] na Hind Fawzi wa Medina FM [Morocco], Rakiya Mohamed wa Blueprint [Nigeria], Wezzie Joy Gausi wa Times Group [Malawi] na Kelvin Tambo wa Capital Radio [Malawi].




Kupitia tuzo hiyo, washindi watapata fursa ya kutekeleza miradi yao ya uandishi kwa msaada wa wahariri na wataalamu wa uandishi wa habari, pamoja na ushauri wa kitaalamu [mentorship] ili kuhakikisha simulizi hizo zinafikia viwango vya juu vya ubora na kuleta athari chanya kwa jamii.




Katika hatua hii, pia watapewa kiasi cha R.10,000 ili kwenda kutekeleza miradi ya uandishi wa makala kulingana na mawazo yao ya habari ambayo waliyawasilisha katika mchakato huo wa kwanza.




Baadae kazi zao zitapitia mchakato wa awamu ya pili ambapo zitashindanishwa ili kupata washindi watatu bora, miongoni mwao.


KIKWETE ATEMBELEA BANDA LA HALMASHAURI YA MJI BAGAMOYO NANENANE

 

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete ametembelea Banda la Halmashauri ya Mji Bagamoyo katika maonesho ya Nanenane kanda ya mashariki Mkoani Morogoro.


Dkt Jakaya amewasalimu Wajasiliamali wote waliokuwa katika Banda na watumushi wote  pamoja na kuona bidhaa walizonazo katika maonesho hayo huku akipendezwa na ubunifu wao katika bidhaa zao.


Halmashauri ya Mji Bagamoyo imeendelea kuwa washiriki wazuri katika maonesho ya Kilimo,Mifugo na Uvuvi Nanenane kwa kuendelea kuwa wabunifu wa utengenezaji wa Bidhaa mbalimbali kwa kila Mwaka.












Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete ametembelea Banda la Halmashauri ya Mji Bagamoyo katika maonesho ya Nanenane kanda ya mashariki Mkoani Morogoro.


Dkt Jakaya amewasalimu Wajasiliamali wote waliokuwa katika Banda na watumushi wote  pamoja na kuona bidhaa walizonazo katika maonesho hayo huku akipendezwa na ubunifu wao katika bidhaa zao.


Halmashauri ya Mji Bagamoyo imeendelea kuwa washiriki wazuri katika maonesho ya Kilimo,Mifugo na Uvuvi Nanenane kwa kuendelea kuwa wabunifu wa utengenezaji wa Bidhaa mbalimbali kwa kila Mwaka.