CCM YAPONGEZA MAFANIKIO MANISPAA TABORA
CCM YAPONGEZA MAFANIKIO MANISPAA TABORA
Na Allan Kitwe, Tabora
HALMASHAURI ya Manispaa Tabora imepongezwa kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana hadi sasa ambayo yamekuwa kichocheo kikubwa cha kuboreshwa huduma za kijamii katika kata zote 29.
Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Tabora Mjini Komredi Mohamed Katete alipokuwa akitoa salamu za chama kwenye kikao cha baraza la madiwani kilichoketi leo katika ukumbi mpya wa manispaa hiyo.
Katete ameeleza bayana kuwa manispaa hiyo imepiga hatua kubwa kimaendeleo kutokana na kazi nzuri iliyofanyika kwenye miradi ya maendeleo, hali ambayo imepelekea kutatuliwa changamoto za wananchi.
‘Nakupongeza sana Mstahiki Meya, ndugu yangu Gullam-Hussein Dewj, Mkurugenzi wa Manispaa Dkt John Pima, Mkuu wa Wilaya Upendo Wella, Waheshimiwa Madiwani na Wataalamu wote, kwa kazi yenu njema’, amesema.
Amebainisha wazi kuwa sasa hivi wananchi wanapata huduma bora za kijamii katika kata zote tofauti na hali ilivyokuwa huko nyuma, malalamiko yalikuwa mengi lakini sasa hali ni shwari.
Mkurugenzi umekuwa kiungo cha mafanikio haya kutokana na utendaji wako mzuri, rai yangu kwenu; endeleeni kudumisha mshikamano wenu, chapeni kazi kwa bidii, sikilizeni na kutatua kero za wananchi zinapojitokeza.
Katete amesisitiza kuwa CCM imeridhishwa na kazi nzuri ya utekelezaji ilani katika manispaa hiyo, menejimenti imekiheshimisha chama na kufanya wananchi waendelea kuipenda serikali yao na Chama chao cha Mapinduzi.
Akiongea katika kikao hicho Mstahiki Meya Ghullam-Hussein Dewj amepongeza kazi nzuri inayofanywa na Menejimenti, Watendaji na Madiwani kwani imepelekea halmashauri hiyo kuendelea kupata mafanikio makubwa.
Ameelekeza madiwani na watendaji kuendelea kufanya kazi kwa ukaribu zaidi katika kata zao ili kusaidia wananchi na kuhakikisha kero zote zinazojitokeza zinatatuliwa kwa wakati.




Comments
Post a Comment