TAASISI ZA UMMA ZAAGIZWA KUJENGA VICHOMEA TAKA
TAASISI ZA UMMA ZAAGIZWA KUJENGA VICHOMEA TAKA
Na Allan Kitwe, Tabora
TAASISI za umma na binafsi Mkoani Tabora zimetakiwa kutumia vichomea taka katika maeneo yao ili kuteketeza taka za kibaiolojia na kikemea na nyinginezo ili kulinda afya ya binadamu na mazingira yanayowazunguka.
Wito huo umetolewa juzi na Meneja wa Wakala wa Maabara ya Mifugo Tanzania (TVLA) Kanda ya Magharibi, Dkt. Qwari Bura, kwenye uzinduzi wa mtambo wa kisasa wa kuchomea taka uliojengwa kwenye Ofisi za Maabara ya Mifugo.
Alisema kuwa mtambo huo ni maalumu kwa ajili ya kuchomea taka hatarishi hivyo taasisi zote zinapaswa kuiga mfano huo, badala ya kuteketeza taka kwa njia za kawaida ambazo ni hatarishi kwa afya ya jamii na mazingira.
Dkt. Qwari alibainisha kuwa mtambo huo una uwezo wa kuchoma hadi kilo 30 za taka ngumu na hatarishi kwa wakati mmoja.
Dkt Bura alidokeza kuwa TVLA itatoa huduma hiyo bure kwa wananchi wote wanaohitaji kuchoma taka za kibaiolojia, ila taasisi za Serikali zitatakiwa kuchangia kiasi kidogo cha fedha kwa ajili ya huduma hiyo.
Kwa upande wake, Mtafiti wa Mifugo Daraja la Pili kutoka TVLA, Dikson Anjelo, alisema faida ya mtambo huo hauzalishi moshi mzito unaoweza kuathiri afya za watu wanaozunguka eneo la uchomaji taka.
Naye Daktari Mtafiti wa Mifupa kutoka TVLA, Denis Luumba, alisema uchomaji taka kwa njia za kawaida unaweza kuathiri mfumo wa upumuaji wa watu wanaohusika na zoezi hilo kutokana na moshi unaozalishwa.
Baadhi ya wananchi pia walieleza namna walivyokuwa wakikabiliwa na changamoto za kiafya na kimazingira kutokana na uchomaji wa taka kwa kutumia njia za kawaida.


Comments
Post a Comment