Friday, September 22, 2017

KAMATI YA AMANI BAGAMOYO YATEMBELEA HOSPITALI.



Wadau mbalimbali pamoja na wananchi wilayani Bagamoyo wametakiwa kujitokeza kuchangia damu salama katika Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo, ili kukabiliana na upungufu wa damu hospitalini hapo.

Wito huo umetolewa na Kamiu Muuguzi Mfawidhi Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo, Saufa Khalifa, alipokuwa akizungumza mara baada ya kamati ya Amanai wilayani Bagamoyo kutembelea Hospitalini hapo.

Saufa alisema kwa sasa Hospitali hiyo inakabiliwa na upungufu wa damu, hivyo ni vyema wananchi wakajitokeza kuchangia damu ili kuiwezesha Hospitali hiyo kutoa huduma stahiki kwa wagonjwa wanaofika hospitali hapo.

Alisema wanamshukuru Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Alhaji, Majid mwanga kwa kutafuta wafadhili ambao ni Taasisi ya Kiislamu ya  Dhi Nureyn  inayojenga jengo la wodi ya wazazi na jengo la wagonjwa wa dharula na kuongeza kuwa, jengo la huduma ya dharula linahitaji uwepo wa damu kwa wingi ili hata kama wanaletwa wagonjwa wa ajali ambao wametokwa na damu nyingi waweze kuwekewa damu haraka iwezekanavyo.

Kwa upande wao viongozi wa kamati ya Amani wilayani Bagamoyo, ambao wamefika Hospitalini hapo wamesema watashirikiana na serikali katika kuhamasisha wananchi kuchangia damu salama.

Walisema kazi ya kamati ya amani ambayo inaundwa na dini zote ni kuwajenga waumini wao kiroho na kuweza kujitolea katika shughuli za kijamii na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuwaletea maendeleo wananchi wake.

Kamati ya Amani wilayani Bagamoyo imefanya ziara katika Hospitali ya Bagamoyo kwa lengo la kuangalia wagonjwa na kuwaombea duwa pamoja na kukagua majengo yanayoendelea kujengwa Hospitali yanayojengwa na Taasisi ya Kiislamu ya Dhi Nureyn ya Mjini Iringa.
 Kamiu Muuguzi Mfawidhi Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo, Saufa Khalifa,akitoa maelezo kwa kamati ya Amani ya wilaya ya Bagamoyo iliyofika Hospitalini hapo.

No comments:

Post a Comment