Tuesday, November 21, 2017

AMANA BANK YAADHIMISHA MIAKA 6 YA KUTOA HUDUMA.



Mkurugenzi wa Amana Bank Dkt. Muhsin Masoud akizungumza na waandishi wa Habari.

Amana Bank imefanikiwa kupata wateja wapya elfu ishirini katika kipindi cha mwaka 2017 ikiwa ni asilimia 25 ya wateja wote toka kuanzishwa kwake mwaka 2011.

Akizungumza na waandishi wa Habari katika kuadhimisha miaka sita toka Benki hiyo ilipoanza kutoa huduma, Mkurugenzi wa Amana Bank Dkt. 
 Muhsin Masoud alisema Benki hiyo kwa sasa imeongeza wateja wake na kuongeza huduma mbalimbali katika matawi yake.

Maadhimisho hayo ya miaka sita yamekwenda sambamba na wiki ya huduma kwa wateja iliyoanza leo Tarehe 20 mwezi wa 11 mpaka 25 kwa mwaka huu 2017.

Dkt. Muhsin alisema uboreshaji wa huduma pamoja na kuongeza huduma ambazo hazikuwepo zimewavutia wateja na kuahidi kuboresha zaidi utoaji wa huduma katika matawi yake yote.

Akielezea mafanikio yaliyopatikana katika kipindi hiki cha miaka sita ni pamoja na kuwa na bidhaa mbalimbali ambazo zinakidhi mahitaji wa wateja, ikiwemo kuanzisha mikopo kwa wafanyabiashara wadogowadogo ambayo inaanzia milioni moja hadi milioni kumi.

Alisema katika kuhakikisha Benki hiyo inakuza mitaji kwa wateja wake kupitia mikopo isiyokuwa na riba kwa wafanyabiashara wadogo wadogo, tayari mpaka sasa Benki hiyo imeshatoa shilingi za kitanzania Bilioni moja na nusu.

Alisema miongoni mwa mafanikio ni kuanzishwa kwa kadi za Master Card ambayo itamuwezesha mteja kupata huduma kwenye ATM yoyote inayotumia mfumo wa Master Card na kupata huduma za kibenki hata akiwa nje ya nchi.

Alisema kwa sasa Benki hiyo ina matawi saba nchi nzima na kwamba hivi karibuni inatarajia kufungua tawi lingine mkoa  wa Tanga huku mawili mengine yakitarajiwa kujengwa katika mikoa ambayo bado haijawekwa wazi ikiwa lengo ni kufikisha matawi kumi kwa mwaka 2018.

Aliongeza kwa kusema kuwa katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma za Benki hiyo hata katika maeneo ambayo Amana Bank haina matawi, imesajili mawakala zaidi ya 300 ambao wanatoa huduma za kibenki kupitia huduma ya Amana Bank Mtaani.

Aidha, alisema licha ya kuwepo matawi saba kwa sasa, huduma ya Amana Bank Mtaani pia wateja wanaweza kupata huduma za kibenki kupitia mtandao ikiwemo huduma kwa njia ya simu (Mobile Internet) pamoja na Internet Banking.

Dkt. Muhsin alisema licha ya kuwa Benki hiyo inafanya shughuli zake kwa kufuata misingi ya sheria za kiislamu haina maana wanaohudumiwa ni waislamu pekee.

Alisema toka kuanzishwa kwake watu wa dini zote wanahudumiwa kama kawaida na kwamba wengi wasiokuwa waislamu wamenufaika na mfumo huo wa kiislamu ambao hauna riba ndani yake.

Aliongeza kuwa, katika uislamu imeharamishwa riba na imeruhusiwa biashara, hivyo Benki hiyo ya Amana inafanya biashara na wateja wake na ndio msingi wa kuendesha Benki hiyo.

Akifafanua zaidi alisema Benki hiyo haikopesha pesa taslimu na kwamba mteja atapewa kitu au huduma ambayo alipaswa kuipata kwa pesa taslimu na kupewa muda wa kulipa kitu hicho au huduma hiyo kwa bei ambayo watakuwa wamekubaliana kama ilivyo biashara yoyote ile.

Alisema mfumo huo umewanufaisha wengi kwani mtu anapata kitu alichotaka na kuepuka kutumia pesa nje ya malengo hali iliyowavutia hata wasiokuwa waislamu kufungua Akaunti katika Benki hiyo.

Dkt. Muhsin Alisema nchi za ulaya zinaendesha mfumo huo wa Benki za kiislamu na kwamba wamenufaika kwa kuinua hata uchumi wa nchi.

Akizungumzia taarifa zilizosambazwa kwenye mitandao zikisema Benki ya Amana imefungwa, Dkt. Muhsin alisema taarifa sio za kweli na kwamba tayari juhudi za kuwatafuta walihusika na kusambaza taarifa hizo zinafanywa na mamlaka zinazohusika ili kuwachukulia hatua za kisheria.

Alisema Benki hiyo haijafungwa na inaendelea na shughuli zake kama kawaida katika matawi yake yote hapa nchini.

Kufuatia uzushi huo wa kufungwa kwa Benki ya Amana, Benki kuu ya Tanzania (BoT) Novemba 17 mwaka huu imewataka wananchi kupuuza taarifa hizo na kuziita ni za uzushi na zimetolewa kinyume cha sheria. 

Mtaalamu wa Mfumo Benki za Kiislamu wa Amana Bank, Jamali Issa amewataka wananchi kutumia fursa hiyo ya wiki ya huduma kwa wateja ili kujua na kupata huduma zinazotolewa na Benki hiyo pekee inayofuata misingi ya sheria ya kiislamu hapa nchini.

Alisema wananchi wanaweza kufika tawi lolote la Amana Bank na kupata huduma mbalimbali ikiwemo jinsi ya kufungua Akaunti, kujua taratibu za mikopo na Aina mbalimbali za Akaunti zinazoweza kufunguliwa ndani ya benki ya Amana.

Jamali alisema wiki ya huduma kwa wateja imeanza leo Tarehe 20 Novemba na kufikia kilele chake Tarehe 25 mwezi huu wa Novemba 2017. 
Mkurugenzi wa Amana Bank Dkt. Muhsin Masoud akiwa na mteja wa kwanza katika Benki hiyo Dawson Ishengomawakikata utepe kuashiria uzinduzi wa wiki ya huduma kwa wateja na maadhimisho ya miaka sita toka kuanza kutoa huduma kwa Banki hiyo.
Mkurugenzi wa Amana Bank Dkt. Muhsin Masoud akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani).
Mtaalamu wa Mfumo Benki za Kiislamu wa Amana Bank, Jamali Issa akizungumza na waandishi wa Habari.
Mkurugenzi wa Amana Bank Dkt. Muhsin Masoud akiwa katika picha ya pamoja na watendaji wa Benki hiyo.

No comments:

Post a Comment