Sunday, August 27, 2017

WAVAMIZI MSITU WA ZIGUA WAONDOLEWA.


Kutoka kushoto ni Mkuu wa Plisi wilaya ya Kipolisi Chalinze, Mrakibu Mandamizi wa Polisi, SSP. Janet Magomi, katikati ni Mkuu wa Polisi wilaya ya Handeni, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, SSP. William Alloyce Nyello, wa kwanza kulia ni Mkuu wa Polisi wilaya ya Kilindi, Mrakibu wa Polisi, SP. Richard Nyansamdo, ambao kwa pamoja walishirikiana kuwaondoa wavamizi ndani ya Hifadhi ya Msitu wa Zigua. 
Mwenyekiti wa kamati ya kuondoa wavamizi katika msitu wa Zigua iliyoundwa na wilaya tatu za Kilindi, Handeni na Bagamoyo, Alhaji majid Mwanga, akizungumza wakati wa kufunga  oparesheni maalum ya kuondoa wavamizi ndani ya msitu wa Zigua.
.............................................

Watendaji wa vijiji na Kata, Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji Pamoja na Maafisa Tarafa wa Wiaya za Kilindi, Handeni na Bagamoyo wametakiwa kuitisha mikutano ya Vijiji ili kutoa Elimu ya Kuhifadhi Msitu wa Zigua ambao kwa muda mrefu umekuwa ukivamiwa.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa kamati ya kuondoa wavamizi katika msitu wa Zigua iliyoundwa na wilaya tatu za Kilindi, Handeni na Bagamoyo, Alhaji majid Mwanga, wakati wa kufunga  oparesheni maalum ya kuondoa wavamizi ndani ya msitu wa Zigua.

Mwanga ambae ni Mkuu wa wilaya ya bagamoyo, Alisema kufuatia Elimu waliyoipata katika zoezi hilo, watendaji hao wa Vijiji Kata na Vitongoji wanapaswa kuitisha mikutano ya hadhara ili elimu hiyo iwafikie wananchi wote wanaozunguuka Hifadhi ya Msitu wa Zigua.

Nae Mtendaji mkuu wa wakala wa huduma za misitu Tanzania (TFS) Prof. Dos Santos Silayo amewataka wale wote waliohamishwa ndani ya Msitu wa Zigua ambao waliuziwa maeneo hayo na wenyeviti wa vijiji kutoa ushirikiano ili wenyeviti waliohusika wachukuliwe hatua za kisheria.

Alisema wale wote waliohusika kuhujumu rasilimali za Taifa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ili kukomesha Tabia hiyo katika misitu yote hapa nchini.

Prof. Silayo, alizipongeza kamati za ulinzi na usalama za wilaya hizo tatu kwa kazi bzuri za kuwaondoa wavamizi ndani ya msitu wa zigua, zikiongozwa na wakuu wao wa wilaya ambao ndio wenyeviti wa kamati hizo.

Aidha, Prof. Silayo alichukua nafasi hiyo kuwapongeza Mkuu wa mkoa wa Pwani, Mhandisi Evarist Ndikilo na Mkuu wa mkoa wa Tanga Martine Shigella kwa kutoa umuhimu wa zoezi hilo na kusimamia majeshi yao ili kuwaondoa wavamizi ndani ya msitu huo.

Hata hivyo licha ya mafanikio hayo Prof. Silayo alisema Hifadhi za misitu hapa nchini zinakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo ugumu wa kufikia misitu hiyo jambo ambalo linapelekea wavamizi kuingia wakiona kama ni mapori ambayo hayana wenyewe.

Alisema kwa sasa Serikali kupitia Wakala wa huduma za Misitu Tanzania TFS wamejipanga kuilinda misitu yote na kwamba ulinzi huo utakuwa shirikishi na endelevu. 

Kwa upande wao, Mkuu wa wilaya ya Handeni,  Godwin Gondwe na Mkuu wa Wilaya ya Kilindi, Sauda Mtondoo, wamesema Tayari wameanza kuwashughulikia viongozi wa vijiji waliohusika kuuza maeneo ya Hifadhi ya msitu wa Zigua na kwamba kila atakaebainika kuhusika atachukuliwa hatua za kisheria.

Awali akisoma Taarifa ya utekelezaji wa opesheni hiyo ya kuondoa wavamizi ndani ya msitu wa Zigua, Mkaguzi msaidizi wa Zimamoto, Henry Mwaluseka, alisema jumla ya nyumba zilizobomolewa katika zoezi hilo ni nyumba za bati 62, za nyasi 863, mazizi ya mifugo 112, Magala ya asili 19.

Aidha, katika zoezi hilo hakuna mtu aliyejeruhiwa wala kupata madhara yoyote na kuongeza kuwa hakuna pingamizi lolote kutoka kwa mtu yeyote wala kikundi cha aina yoyote.

Alisema katika operesheni hiyo mazao ya muda mfupi yaliyopandwa ndani ya msitu hayakuharibiwa na badala yake wahusika wamepewa muda wa ili wavune mazao yao na kusisitizwa kutorudia kufanya shughuli za kilimo na shughulizingine zote za kibinadamu ili kuuacha huru msiru huo uweze kurudisha uoto wake wa asili na kuhifadhi vyanzo vya maji na wanyama wanaoishi humo. 

Msitu huo wa Zigua una jumla ya Hekta 24, 436 ukiwa na urefu wa kilomita 172 ambao umepakana na  wilaya ya za Bagamoyo, Handeni na kilindi, ambapo katika wilaya ya Bagamoyo sehemu kubwa ya Msitu huo unapatikana kata ya Kibindu katika Halmashauri ya Chalinze.
 Wakuu wa wilaya hizo tatu kutoka kulia ni Mwenyekiti wao Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Alhaj, Majid Mwanga, katikati ni Mkuu wa wilaya ya Kilindi, Sauda Mtondoo, na kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Handeni, Godwin Gondwe, walipokutana eneo la Msata wilayani Bagamoyo kufanya Tathmini ya zoezi la kuwaondoa wavamizi ndani ya Hifadhi ya msitu wa Zigua. 

Kamati za ulinzi na usalama za wilaya za Handeni, Kilindi na Bagamoyo, picha ya juu na chini, Picha ya chini ni Washauri wa Mgambo wa wailaya hizo tatu kutoka kushoto ni mshauri wa mgambo wilaya Handeni, Katikati ni mshauri wa Mgambo wilaya ya Bagamoyo, na Kulia ni mshauri wa mgambo wilaya ya Kilindi.

 Mtendaji mkuu wa wakala wa huduma za misitu Tanzania (TFS) Prof. Dos Santos Silayo akizungumza wakati hafla fupi ya kufanya Tathmini ya zoezi hilo.
  Mkaguzi msaidizi wa Zimamoto, Henry Mwaluseka, akisoma Taarifa ya utekelezaji wa Oparesheni ya kuondoa wavamizi ndani ya Hifadhi ya msitu wa Zigua.
Askari walioshiriki zoezi hilo wakijipongeza kwa nyimbo za kutiana hamasa baada ya kumaliza oparesheni hiyo kwa usalama na amani.




Kutoka kulia ni Mkuu wa Oparesheni mkoa wa pwani, Mrakibu wa Polisi, SP. Rajabu Shemndolwa, wa pili kulia ni mkuu wa Polisi wilaya ya Kilindi Mrakibu wa Polisi, SP. Richard Nyansamdo. wa tatu kulia ni Mkuu wa Polisi Wilaya ya Handeni, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, SSP. William Alloyce Nyello, na wakwanza kushoto ni Mkuu wa Plisi wilaya ya Kipolisi Chalinze, Mrakibu Mandamizi wa Polisi, SSP. Janet Magomi.

No comments:

Post a Comment