Wednesday, February 21, 2018

NAIBU WAZIRI WA NISAHATI AKAGUA MITAMBO YA UMEME ITAKAYOFUNGWA MTWARQ



Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu amekagua mitambo miwili ya umeme yenye uwezo wa kuzalisha megawati 2 kila mmoja itakayofungwa katika kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia cha Mtwara.

Amekagua mitambo hiyo tarehe 21 Februari, 2018 katika eneo la Mkandarasi, jijini Dar es Salaam ambapo kampuni ya Mantrac ndiyo iliyopewa kazi ya kufunga mitambo hiyo.

Baada ya kukagua mitambo hiyo, Naibu Waziri alisisitiza kuwa, Serikali inafuatilia kwa karibu utekelezaji wa  kazi  hiyo lengo likiwa ni kuhakikisha kuwa  mitambo hiyo inafikishwa na kusimikwa mkoani Mtwara mapema iwezekanavyo ili kuboresha hali ya upatikanaji wa umeme katika mkoa wa Mtwara pamoja na Lindi.

Kabla ya kukagua mitambo hiyo, Naibu Waziri Mgalu alifanya kikao na watendaji wa kampuni hiyo ya Mantrac pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) lengo likiwa ni kufahamu maendeleo ya kazi hiyo.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi Mtendaji wa Mantrac, Ahmed Saleh alimweleza Naibu Waziri kuwa mpaka sasa mitambo hiyo tayari imewasili jijini Dar es Salaam na kinachosubiriwa kwa sasa ni kuwasili kwa kontena maalum zitakazotumika kuwekea mitambo hiyo kabla ya kusafirishwa kuelekea mkoani Mtwara.

Aliongeza kuwa, kazi ya usafirishaji wa mitambo hiyo kwenda mkoani Mtwara itafanyika mwanzoni mwa mwezi Aprili mwaka huu na kwamba kazi ya kufunga mitambo hiyo, majaribio na makabidhiano itafanyika tarehe 9 hadi 30 mwezi Aprili mwaka huu.

Kituo cha kuzalisha umeme kwa Gesi asilia mkoani Mtwara kina mitambo Tisa yenye uwezo wa kuzalisha megawati 2 kila mmoja. Kituo kwa sasa kinazalisha umeme wa kiasi cha megawati 16 kufuatia mtambo namba Tisa kuwa nje kwa matengenezo.

Kuongezeka kwa mashine hizo mbili mpya (4 MW) kutafanya uwezo wa kituo hicho kuongezeka na  kufikia megawati 22 na hivyo kuboresha hali ya upatikanaji wa umeme katika mikoa ya Lindi na Mtwara.



Sunday, February 18, 2018

NAIBU WAZIRI NISHATI ATOA WIKI MOJA KWA WAKANDARASI WA REA.


Naibu waziri wa Nishati Subira Mgalu ametoa wiki moja kuanzia leo Tarehe 18 February 2018,  kwa  wakandarasi wote nchini wanaofanya kazi ya kusambaza umeme kupitia Mradi wa Umeme vijijini (REA) kuhakikisha wanapima (survey)  kwenye taasisi za uma zikiwemo Vituo vya Afya, Zahanati, na Shule .

Alisema lengo la Mradi huo ni kuhakikisha wananchi wa vijiini wanapata umeme huku sehemu zao za kupata huduma, Vituo vya Afya, Zahanati na shule  zikipewa kipaumbele katika kufikisha umeme.

Naibu waziri huyo wa Nishati ametoa kauli hiyo Wilayani Bagamoyo alipokuwa akizindua mradi wa umeme vijijini (REA) awamu ya tatu kitongoji cha Migude kata ya Kiromo. 

Aliwataka wakandrasi hao kuhakikisha maeneo yote ya Zahanati, Vituo vya Afya, Shule na Miradi ya maji yanapimwa (yanafanyiwa  survey) kwakuwa agizo la serikali maeneo hayo yafikiwe na huduma ya Nishati katika utekelezaji wa REA awamu ya tatu. 

Alisema maeneo hayo yanapaswa kufanyiwa matayarisho ya miundombinu ikiwa ni pamoja na upimai (survey) ili yafikiwe na Umeme.

Aliongeza kwa kusema kuwa,  Mkandarasi atakaeshindwa kufuata maelekezo ya serikali atakuwa ameshindwa kazi na mkataba wake utasitishwa ili apatikane mkandarasi atakaeweza kufanya kazi kwa mujibu wa maelekezo ya serikali.

Kauli hiyo imekuja kufuatia Diwani wa kata ya Kiromo Wilayani Bagamoyo, Hasan Usinga (Wembe) kutoa taaraifa ya hali ya umeme katika kata yake ambapo alisema umeme huo haujafikishwa kwenye Zahanati.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Dkt. Shukuru Kawambwa amepongeza utendaji kazi wa wizara ya Nishati chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli kwa namna inavyoweza kufikisha umeme vijiini.

 Naibu waziri wa Nishati Subira Mgalu (katikat) akikagua utekelezaji wa Miradi ya Umeme Vijijini (REA) awamu ya tatu katika Kitongoi cha Migude kata ya Kiromo Wilayani Bagamoyo, kulia ni Diwani wa kata ya Kiromo, Hassan Usinga (Wembe) na kushoto ni Mwenyekiti wa kitongoji cha Migude, Kitumboy Bushiri.
 Diwani wa kata ya Kiromo, Hassan Usinga (Wembe)wa kwanza kulia akifurahia ambo na Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Dkt. Shukuru Kawambwa.
Madiwani wa viti Maalum wa Halmashauri ya Bagamoyo wakifuatilia hutuba ya naibu waziri wa Nishati ( hayupo pichani) kutoka Kulia ni Hafsa Juma Kilingo, wa katikati ni Shumina Ismail Rashid na wa kwanza kushoto ni Togo Omari Hega.
Wananchi waliohudhuria kumsikiliza Naibu waziri wa Nishati kitongoji cha Migude 
 Naibu waziri wa Nishati Subira Mgalu, akipeana mkono na Mwenyekiti wa Kitongoji cha Migude, Kitumboy Bushiri ikiwa ni ishara ya kuzindua Mradi wa REA awamu ya tatu katika kitongoi hicho.

Wananchi wa Kitongoji cha Migude wakifurahi umeme baada ya Naibu waziri wa Nishati, Subira Mgalu kuwahakikishia umeme utapatikana katika eneo hilo na nchi nzima.

JAFO AAGIZA MKANDARASI KUFANYA KAZI KWA BIDII KUKAMILISHA DARAJA LA KIMALAMISALE



Waziri wa  Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Selemani Jafo amemuagiza mkandarasi anayejenga daraja wa Kimalamisale wilayani Kisarawe kufanyakazi usiku na mchana ili daraja hilo liweze kukamilika kabla ya Mvua za masika hazijaanza.

Waziri Jafo ametoa agizo hilo alipotembelea kukagua mradi wa ujenzi wa daraja hilo ambao unagharimu kiasi cha Sh.Milioni 390.

Hatua hiyo ya Jafo imetokana na mradi huo kuchelewa hapo awali kutokana na Mvua kubwa za vuli zilizokuwa zinanyesha.

Amesema mradi huo unatarajiwa kuwa kiungo muafaka kwa barabara ya Kimalamisale ambapo kukamilika kwa daraja hilo kutakuwa ukombozi mkubwa kwa wananchi.

Amebainisha kuwa kwasasa mvua zinaponyesha magari yanashindwa kupita kutokana kujaa maji mengi katika mto Muyombo unaotenganisha wilaya ya Kibaha na Kisarawe mkoani Pwani. 

Katika ukaguzi huo, Mkandarasi wa mradi huo amemwambia Waziri Jafo kuwa ameshanunua jenerata kubwa ambalo watalitumia wakati wa usiku ili aweze kukamilisha ujenzi huo.

Ameahidi kwamba watajitahidi kufanyakazi kwa kasi kubwa ili kuwahi  Mvua za masika na wasipate hasara ya kuchelewesha mradi.

Wananchi wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI Selemani Jafo.

SERIKALI KUFANYA UCHUNGUZI WA KIFO CHA MWANAFUNZI ALIYEPIGWA RISASI.



Waziri wa Elimu na Mafunzo Profesa Joyce Ndalichako na Naibu waziri wa Mambo ya Ndani Injinia Hamad Yusuph Masauni wakimfariji mama mzazi wa marehemu Akwiline Baftaha Mwanafunzi wa Cho cha Usafirishaji NIT aliyefariki kwa majeraha  baada ya kujeruhiwa na  risasi juzi. 

Akiwa kwenye daladala. Kufuatia vurugu za maanamano ya wafuasi wa Chadema ,Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania Dk. John Pombe Magufuli ametuma salami za rambirambi kwa familia kufuatia kifo hicho.
....................................

Serikali imewahakikishia Watanzania kuwa vyombo vya ulinzi na usalama vinafanya uchunguzi kufuatia kifo cha mwanafunzi wa Chuo cha Usafirishaji (NIT) Akwilina Baftaha Akwilini, aliyefariki kwa kupigwa risasi mwishoni mwa wiki iliyopita jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari, leo jijini Dar es Salaam, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Hamad Masauni amesema kuwa Serikali itahakikisha uchunguzi huo unafanyika kwa weledi na utaalamu ili haki iweze kupatikana na yeyote aliyehusika atachukuliwa hatua za kisheria ili iwe fundisho kwa wengine.

“Nawasihi watanzania kuwa na subira ili uchunguzi ufanyike na tutahakikisha uchunguzi huo unafanyika haraka iwezekanavyo na baada ya kukamilika wote waliohusika watachukuliwa hatua za kisheria”, alisisitiza Masauni.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Joyce Ndalichako alisema kuwa Serikali imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha mwanafunzi huyo ambacho kilitokea wakati wa kudhibiti maandamano yaliyokuwa yakifanyika katika eneo la Mkwajuni, wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam.

“Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli amepokea kwa masikitiko makubwa kifo cha mwanafunzi Akwilina na anaungana na wazazi, familia, ndugu, jamaa na watanzania wote kuwapa pole za dhati kutokana na msiba huo”, alisema Ndalichako.

Aidha Ndalichako alibainisha kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia itagharamia shughuli zote za mazishi ya mwanafunzi huyo na amemuagiza Katibu Mkuu wa wizara hiyo kusimamia shughuli zote za msiba huo.
Pia Ndalichako alitoa rai kwa watanzania kujiepusha na vitendo vyote ambavyo vinaweza kusababisha maafa kwa watu wasio na hatia.

Wednesday, February 14, 2018

WAZIRI KALEMANI ATOA WIKI MOA KWA MKANDARASI ANAYESAMBAZA UMEME VIJIJI


Waziri wa Nishati ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Chato,Dk Medard Kalemani akitoa maagizo ya utekelezaji wa usambazaji wa umeme kwenye maeneo ya vijiji na Kata za  Iparamasa pamoja  Kalembela wakati alipokuwa akizungumza na wananchi kwenye mojo kati ya ziara zake za kukagua utekelezaji wa usambazaji wa umeme wa REA awamu ya tatu.
...............................................
Waziri wa Nishati,Dkt Medard Kalemani amemwagiza mkandarasi
shirika la White City  International ambaye anasambaza umeme wa rea
awamu ya tatu kwenye Vijini na kata za Iparamasa na Kalembela kuhakikisha anafanya kazi hiyo kwa haraka zaidi ili kuwasaidia wananchi ambao wamekuwa na kilio cha muda mrefu cha uhitaji wa nishati ya umeme.

Hayo aliyasema wakati alipokuwa kwenye ziara ya Kukagua na
kuangalia utekelezaji wa mradi wa usambazaji umeme vijijini  Wilayani Chato.

Ambapo Diwani wa kata ya Iparamasa Amos Jiji ,amemweleza Waziri wa
nishati ambaye pia ni mbunge wa Jimbo hilo matatizo ambayo yameendelea kujitokeza kutokana na kukosekana  kwa umeme kwenye  kata yake  na kwamba kwa sasa kuna nguzo ambazo zimekaa
kwa muda wa miezi mitatu bila ya kusambazwa kwa wananchi ambao wanashida na huduma hiyo.

 Mmoja kati ya wananchi wa kata hiyo ,Bw Peter Mabula ameelezea
kukosekana kwa umeme ni chanzo kikubwa ambacho kinakwamisha utendaji kazi hususani kwa upande wa biashara kutokana na wengi wao kutegemea nishati hiyo ili waweze  kuendesha  biashara zao.

Aidha kutokana na maombi hayo kutoka kwa Diwani pamoja na wananchi
Mbunge wa Jimbo la Chato na waziri wa nishati Dk Kalemani alitoa maagizo
kwa Mkandarasi kuhakikisha nguzo ambazo zimelala ndani ya miezi mitatu zisimame na kufikia siku ya alhamisi vijiji hivyo na kata hizo ziwe zimepata umeme.
“Nimesikia kuwa nguzo zimelala tu chini ndani ya miezi mitatu na kwamba mkandarasi alivyosikia nakuja ndio ameanza kazi sasa namwagiza kuwa ahakikishe alhamisi wiki ijayo awe amewasha umeme kwenye kata ya iparamasa na vijiji vyote na mimi siondoki hapa nitahakikisha namsimamia”Alisisitiza Kalemani.

Mradi wa usambazaji wa umeme vijijini  Mkoani
Geita,unatekelezwa na mkandarasi  wa Shirika la White City
International ambapo unatarajia kufanyika ndani ya miezi  16 kwenye
jumla  vijiji  220 vilivyopo  mkoani humo na jumla ya fedha ambazo
zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza mradi huo ni  Sh Bilioni 78.56.

MADIWANI BAGAMOYO WAIKATAA TAARIFA YA UTEKELEZAI WA ILANI.


Diwani wa kata ya Yombo, Mohamed Usinga akitoa msimamo kwa Mwenyekiti wa Halmashauri kuhusu kuiktaa Taarifa ya utekelezaji wa ilani.
............................................

Madiwani wa Halmashauri ya Bagamoyo wameikataa taarifa ya utekelezaji wa ilani ya 2017 kufuatia taarifa hiyo kuwa na mapungufu kadhaa.

Madiwani hao wakiongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bagamoyo, Ally Ally Issah wameikataa taarifa hiyo mara ilipofika katika utekelezai wa miradi inayohusu idara ya uvuvi ambapo miradi iliyoainishwa ndani ya taarifa hiyo haipo katika maeneo husika jambo liliwatia hasira madiwani hao na kuamua kuirudisha Taarifa yote kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ili ifanyiwe marekebisho.

Akitoa maamuzi ya Baraza Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bagamoyo, Ally Ally alisema wanairudisha taarifa yote ka Mkurugenzi ili ipitiwe upya na kunyiwa marekebisho katika maeneo ambayo madiwani hawakuridhika nayo.

Kabla ya Mwenyekiti wa Halmashauri kutoa msimamo huo wa Baraza, madiwani hao walisema ifike wakati sasa wataalamu wa Halmashauri wafanye kazi kwa kuzingatia sheria na kanuni za kazi ili kila mmoja achunge mipaka yake.

Walisema katika kikao cha Baraza kuleta tarifa inayokwenda kinyume na uhalisia katika utekelezaji wa miradi ni kukiuka sheria, na kwamba baraza halitasita kumuwajibisha mtumishi yeyote anaekiuka sheriaa kwa kushindwa kutoa taarifa sahihi za utekelezaji wa ilani.

Walisema madiwani ni viongozi wanaochaguliwa na wananchi kwa lengo la kusimmamia utekelezaji wa miradi mbalimbali kwa manufaa ya wananchi hivyo si vyema wataalamu wa Halmashauri wanaposhindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo ni wazi kuwa wanawatengezea mazingira magumu madiwani ambao watarudi kwa wananchi kuomba kura kwaajili ya kurudi tena madarakani.

Aidha, Madiwani hao waliwataka wataalamu wa Halmashauri wanapofika katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenye maeneo mbalimbali wawasiliane na viongozi wa kata husika ili kuleta ushirikiano kati ya wataalamu hao na viongozi wa kata wakiwemo watendai wa kata na madiwani ili kuondoa sintofahamu inayoweza kujitokeza siku ya kuwasilisha taarifa.

Katika taarifa hiyo idara ya uvui imetaja kujenga kwa mabwawa ya samaki katika baadhi ya maeneo huku madiwani wakishangaa kwakuwa hawajawahi kuyaona mabwawa hayo kwenye maeneo yao.
 Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bagamoyo, Fatuma Latu amekiri kupokea taarifa hiyo na kwenda kuifanyia marekebisho na wataalamu wake ili baadae iwasilishwe ikiwa imekamilika.
Wakati huohuo Katibu wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Salum kamote amewaonya wakuu wa idara ambao wanatabia ya kutoa taarifa zisizo sahihi kwani kwa kufanya hivyo wanachangia kuidhoofisha chama tawala katika mikakati yake ya kusimamia utekelezaji wa ilani uchaguzi jambo linaidhoofisha serikali iliyopo madarakani kwa ujumla.

Alisema ni vyema taarifa ikawa wazi kama kuna mradi haujatekelezwa ili chama kijue wapi kwenye madhaifu ili nguvu zielekezwe hapo na kuhkikisha miradi hiyo inateekelezwa kuliko kutoa taarifa za uongo.
Aidha, katibu huyo wa CCM wilaya ya Bagamoyo amewapongeza madiwani Halmashauri ya Bagamoyo kwa uwasilishaji mzuri wa taarifa za kata na hatua waliyochukua kuikataa taarifa ya utekelezaji wa ilani.

Alisema Madiwani ndio wasimamizi wa miradi hivyo wanapaswa kuwa imara katika kuhakikisha miradi yote iliyopangwa na kutengewa mafungu inatekelezwa kwa ukamilifu wake ili kujenga imani kwa wananchi ambao ndio walipewa ahadi za kutekeleza mambo mbalimbali.

Kikao hicho cha Baraza la madiwani Halmashuri ya Bagamoyo kimeanza leo jumatano February 14 ambapo kimejadili taarifa za robo ya pili ambapo madiwani waliweza kuwasilisha taarifa za kata zao.
 Madiwani wa Halmashauri ya Bagamoyo wakifuatilia kwa karibu uwasilishwaji wa taarifa za kata pamoja na kupokea taarifa ya utekelezaji wa ilani ambayo baadae waliikataa kwa pamoja na kumrudishia Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bagamoyo Fatuma Latu kwaajili ya Marekebisho.

 Madiwani wa Halmashauri ya Bagamoyo wakifuatilia kwa karibu
 uwasilishwaji wa taarifa za kata pamoja na kupokea taarifa ya utekelezaji wa ilani ambayo baadae waliikataa kwa pamoja na kumrudishia Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bagamoyo Fatuma Latu kwaajili ya Marekebisho.

BIL. 161.9 ZIMETUMIKA KUBORESHA VITUO VYA AFYA 170.



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imetumia sh. bilioni 161.9 kuboresha vituo vya afya 170 nchini pamoja na kugharamia huduma ya Afya ya Mama na Mtoto kwa lengo la kuokoa maisha yao.

Amsema Serikali itaendelea kukarabati na kupanua miundombinu ya kutolea huduma pamoja na kununua vifaa vya kisasa katika Hospitali za Mloganzila, Benjamini Mkapa, Dodoma na Hosptali za Rufaa katika Mikoa na Kanda.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatano, Februari 14, 2018) wakati akizindua jengo  jipya la mama na mtoto katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa-Amana iliyopo wilayani Ilala jijini Dar es Salaam.

Jengo hilo la ghorofa mbili limejengwa kwa ufadhili wa kundi la kampuni za AMSONS na lina thamani ya sh bilioni 1.2.

Amesema uzinduzi wa jengo hilo  unakwenda sambamba na azma ya Rais Dkt. John Magufuli za kuimarisha sekta ya afya na kuifanya kuwa miongoni mwa sekta za kipaumbele.

Amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha inasogeza huduma za afya karibu na wananchi. “Mfano, Hospitali za Rufaa za Amana, Mwananyamala na Temeke, zimeendelea kuhudumia wagonjwa kutoka Zahanati, Vituo vya Afya vya Serikali, binafsi na vya dini kutoka mikoa jirani ya Pwani, Morogoro na Lindi.

Pia amesema Serikali itaendelea kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015 – 2020, kuhusu kuwapatia wananchi huduma bora za afya pamoja na kujenga hospitali nyingine za Rufaa kwa ajili ya Kanda ya Kusini, Kati na Magharibi.

Akizungumzia kuhusu changamoto ya idadi ndogo ya watumishi na ukosefu wa huduma za uangalizi maalumu (ICU) katika hospital ya Amana, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kufanyia kazi changamoto zote zilizopo katika sekta ya afya zikiwemo n aza hospital hiyo. 

Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuthamini na kutambua mchango wa wadau mbalimbali pamoja na kuendelea kushirikiana nao katika kuhakikisha kuwa huduma za afya nchini zinaboreshwa.

Hivyo, alitumia fursa hiyo  na kulipongeza kundi la kampuni za AMSON’s lililoamua kujenga jengo la mama na mtoto katika hospital hiyo kwa ushawishi wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Paul Makonda.

Awali, Mganga Mkuu Hospitali ya Rufaa ya Mkoa – Amana, Dkt. Meshack Shimwella alisema wazazi wanaolazwa katika hospitali hiyo kwa siku ni 180 hadi 250 na uwezo wa hospitali ni vitanda 353, ambapo vitanda 250 vinatumika wodi ya wazazi.

Alisema idadi hiyo hailingani na idadi ya wagonjwa, hivyo kusababisha wakati mwingine wagonjwa kulala zaidi ya mmoja kwenye kitanda kimoja kutokana na kasi ya ongezeko wa wagonjwa wanaolazwa hususani wodi ya watoto na akinamama.

Dkt. Shimwella alisema wamefanikiwa kuongeza jingo la kutolea huduma ya mama na mtoto lenye ghorofa mbili ilililojengwa kwa ufadhili wa AMSONS lenye uwezo wa vitanda 100, ambalo ndilo liliongeza idadi ya vitanda kutoka 253 hadi kufikia 353.

“Kutokana kukamilika kwa jengo hilo kwa sasa akinamama wanaonyonyesha wanalala wakiwa mmoja mmoja, watoto wachanga wanahudumiwa katika mazingira mazuri yanayofanana na viwango Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.”

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Makonda aliwashukuru wafadhili waliojenga jengo hilo kwa sababu si kila mtu anayekwenda hospitali na kukuta changamoto na akaamua kuzifanyia kazi.

Bw. Makonda alisema awali akinamama walikuwa wanalala hadi watatu katika kitanda kimoja, hivyo madhumuni ya ujenzi wa jego hilo ni kupunguza msongamano katika wodi ya wazazi.

MADIWANI CHALINZE WAMUOMBA RAIS AINGILIE KATI KILIO CHA MAJI.



BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Chalinze ,limemuangukia rais Dkt. John Magufuli kwa kumuomba aende kujionea mradi wa maji awamu ya tatu WAMI-CHALINZE ambao umekwama huku wananchi wakiwa hawana maji kwa takriban miezi mitatu sasa.

Wamesema Rais ,ndio mwenye mamlaka za mwisho kwani waziri mkuu alishafika kujionea mradi huo ambapo mkandarasi aliongezewa muda lakini mkataba umekwisha na hakuna kilichofanyika.

Wakitoa kilio hicho ,wakati wa kikao cha bajeti ,baadhi ya madiwani akiwemo diwani wa Talawanda ambae pia ni mwenyekiti wa halmashauri hiyo,Saidi Zikatimu alisema kuna kila sababu serikali ikaingilia kati na kutoa tamko ili kurejesha imani kwa wananchi.

Alieleza tatizo hilo ni kubwa kwani zipo baadhi ya shule hazina maji safi na salama na wanahofiwa wanafunzi kupata magonjwa ya mlipuko.

“Maji ni tatizo mradi wa WAMI -CHALINZE, kamati ya fedha tulishaenda lakini majibu ya meneja wa CHALIWASA Christer Mchomba  hayakuturidhisha “

“Baraza hili linaimani na Mh.Rais jambo hilo lichukuliwe ufumbuzi wa haraka zaidi ya miezi miwili ama mitatu hakuna maji, serikali itoe tamko kuhusiana na mradi huo “; alisema Zikatimu .

Zikatimu alisema zipo shule za sekondari ya Kikalo ,Miono ,Chalinze hazina maji na wanafunzi wameshaanza kusumbuliwa na magonjwa ya matumbo kutokana na ukosefu wa maji.

Aliomba serikali kuu,CCM na halmashauri ishirikiane kwa hilo ili kupata ufumbuzi.

Zikatimu alieleza kwasasa, wamechukua hatua ya kuzungumza na watu wenye maboza ya kusambaza maji kwenye maeneo muhimu ya kijamii kama mashuleni kwani meneja wa CHALIWASA  aliwaambia kuna uwezekano wa kuchukua maji katika chanzo chao cha maji ambayo yatawasaidia wakati suluhu ikiendelea kutafutwa .

Nao diwani wa kata ya Miono Juma Mpwimbwi,Diwani wa Lugoba Rehema Mwene na diwani wa Kimange Hussein Hading’oka walisema hali ya mradi mkubwa wa aina hiyo iliyofikia ni mbaya na haileti taswira nzuri kwa jamii.

Diwani wa kata ya Miono ,Juma Mpwimbwi,alisikitika kutokuwa na maji ya uhakika kwa miaka mingi hali ambayo inakatisha tamaa wananchi.

“Rais aje kujionea labda kauli yake itasaidia kutatua changamoto ya mradi huu:;”Mradi huu sio rafiki tena na jamii shule hazipati maji na unasababisha usumbufu kwa wanafunzi ambao wakati mwingine inabidi waache masomo wakatafute maji ;” alifafanua Mpwimbwi.

Mpwimbwi alisema ,amehamasisha kila kaya katika kata ya Miono kutoa 2,000 itakayosaidia kulipia maboza yanayosambaza maji yatakayowezesha kusaidia wanafunzi .

“Kuna shule hizi za sekondari ya Miono na Kikalo zinapata shida,walimu wanaogopa kuchangisha wanafunzi kutokana na suala la elimu bure,kila trip moja ya boza kwa wiki ni sh.100,000 ,mkuu gani wa shule atamudu kulipia ama diwani ” alisema Mpwimbwi.

Mkazi wa Bwilingu,Chalinze Zulfa Hassan alieleza wanalazimika kununua madumu ya maji matano hadi kumi kwa siku kwa ajili ya matumizi ya familia.

Alisema uwezo wa kutoa sh.2,500 na 5,000 kila siku hawana hivyo wnaiomba serikali itatue changamoto ya maji Chalinze.

Kwa upande wake ,mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Bagamoyo alhaj Abdul Sharif ,alisema ukienda kwa meneja wa CHALIWASA hupati majibu ya kuridhisha hivyo viongozi kukosa majibu mazuri ya kuwaeleza wananchi.

Alisema ni vyema wizara ya maji ikaeleza kinaga ubaga kinachofuata kwenye mradi baada ya mkataba wa ujenzi wa mradi wa maji WAMI-Chalinze kuisha.

Alhaj Sharif alisema, serikali inafanya juhudi kubwa kuendeleza viwanda na Chalinze ni moja ya halmashauri yenye viwanda na wawekezaji lakini kukosekana kwa maji miezi mitatu anahofu ya kukatisha tamaa baadhi ya wawekezaji .

Meneja wa Chaliwasa alielezea serikali inaendelea kuchukua hatua na kufanya jitihada za kuondoa tatizo la maji tangu mwaka 2001 ,ilipoanza kutekeleza mradi wa maji Chalinze kwa awamu mbalimbali.

Mapema sept mwaka jana Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alitembelea baadhi ya viwanda mkoani Pwani ,na kutoa agizo la wiki mbili kwa waziri wa maji kutathmini matokeo ya mwenendo wa mradi wa maji wa mradi wa WAMI CHALINZE ,;:      ili kutoa utaratibu na kama sheria ingeruhusu kuvunja mkataba ikiwa mkandarasi ameshafikia kiwango cha asilimia 50 ya utekelezaji.

Monday, February 12, 2018

MAKAMU WA RAIS AZINDUA MRADI WA KUENDELEZA UTALII UKANDA WA KUSINI (REGROW)


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla kabrasha lenye Andiko la  mradi wa REGROW na Mikataba ya Fedha na utekelezaji wa mradi mara baada ya kuuzindua mradi huo katika eneo la Kihesa Kilolo mkoani Iringa.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa mradi wa kuendeleza utalii ukanda wa kusini mwa Tanzania (REGROW) ,Kihesa Kilolo mkoani Iringa.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipata maelezo ya mpango wa uwekezaji katika miundo mbinu ya mradi wa kuendeleza utalii ukanda wa kusini mwa Tanzania kutoka kwa Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla wakati alipotembelea mabanda ya maonyesho kabla ya kuzindua mradi wa REGROW. 

Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais.

WAZIRI WA NISHATI AZINDUA HUDUMA YA UMEME KIGWE



Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amezindua rasmi huduma ya umeme katika Kata ya Kigwe iliyopo wilayani Bahi, Mkoa wa Dodoma.

Uzinduzi huo uliofanyika mwishoni mwa Juma, Jumamosi Februari 10 mwaka huu, ulienda sambamba na ufunguzi wa Mtambo wa Maji ambao umeweza kufanya kazi kutokana na upatikanaji wa huduma hiyo ya umeme.
Waziri Kalemani alifanya uzinduzi huo akiwa katika ziara ya kazi wilayani Bahi kukagua miradi ya umeme inayotekelezwa wilayani humo.

Awali, akiwa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Binilith Mahenge kumweleza nia ya ziara yake, Waziri alisema kuwa wananchi zaidi ya 200 wataanza kupata umeme kufuatia tukio la kurasimishwa kuwashwa kwa nishati hiyo Kigwe.

“Tunatoa kipaumbele sana kwa Mkoa wa Dodoma kwa sasa kwani ni Makao Makuu. Tunaweka juhudi za makusudi kuhakikisha kwamba wananchi wengi wanapata umeme na huduma hiyo inakuwa ya uhakika,” alisema Dkt. Kalemani.

Akifafanua zaidi, alisema kuwa, Serikali imeanzisha harakati za kufanya ukaguzi kwenye utekelezaji wa Miradi yote ya umeme mkoani humo. 

Alieleza kuwa lengo la kufanya hivyo siyo tu kwa sababu Dodoma ni Makao Makuu bali pia kama Mkoa, imebainika kuwa miundombinu yake katika baadhi ya maeneo imepoteza ubora, hasa nguzo. 

Hii ni kwa sababu eneo hili ni tambarare na hivyo mvua ikinyesha maji yanatuama na kuharibu nguzo mara kwa mara.
“Kwa hiyo tunaendelea na ukaguzi wa miundombinu ili kuhakikisha Dodoma inaendelea kupata umeme wa uhakika muda wote.”

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa pamoja na kupongeza jitihada ambazo Wizara ya nishati imekuwa ikifanya nchi nzima katika kuhakikisha huduma ya umeme inapatikana katika maeneo mbalimbali, pia alimwomba Waziri Kalemani kuupa upendeleo Mkoa huo kwa kuwa ni kitovu cha nchi.

Akiwa katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Bahi katika ziara yake, Waziri Kalemani aliwasisitiza wananchi kufanya maandalizi ili umeme utakapounganishwa katika maeneo yao waweze pia kuunganisha katika makazi yao na katika maeneo yao mbalimbali ya kazi.

Aidha, alitumia fursa hiyo kuwataka viongozi wa Halmashauri mbalimbali za vijiji kote nchini, kuhakikisha wanajiandaa kwa ajili ya kuunganishiwa umeme katika taasisi zote za umma zikiwemo Shule, Vituo vya Afya, Miradi ya Maji, Masoko na nyinginezo.

Vilevile, alikumbushia umuhimu wa kila mmoja kuhakikisha baada ya kuunganishiwa umeme katika eneo lake anakumbuka kulipa bili za huduma hiyo muhimu.

“Usipolipa, Serikali itakukatia umeme hivyo kurudisha nyuma maendeleo yako,” alisisitiza.

Jambo jingine ambalo Waziri Kalemani alisisitiza ni kwa wakandarasi kuhakikisha wanawagawia bure wateja 200 wa kwanza watakaojitokeza kuunganishiwa umeme wa REA, kifaa cha Umeme Tayari (UMETA) kama ilivyoelekezwa na Serikali na siyo vinginevyo.

“Kifaa hicho hakiuzwi kwa sasa hadi wateja 200 wa mwanzo wakamilike na kugawiwa bure ikiwa ni njia ya kuhamasisha wananchi wengi vijijini kujitokeza kuunganisha umeme. Mkandarasi yeyote atakayebainika kuwauzia wananchi au kutowapatia kifaa hicho wale wateja 200 wa kwanza kama tulivyoelekeza, tutamchukulia hatua.”

Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika ziara hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Bahi Elizabeth Kitundu na Mbunge wa Jimbo hilo, Omari Baduel walipongeza jitihada za Serikali kupitia Wizara ya Nishati katika kuhakikisha wananchi, hususan wa vijijini wanafikiwa na huduma muhimu ya umeme.

Akiwasilisha taarifa ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), kwa Waziri Kalemani katika ziara hiyo, Meneja wa Shirika hilo wa Wilaya ya Bahi, Kitila Bryceson alisema kuwa, Wilaya hiyo ina jumla ya wateja 1498 wa umeme hadi kufikia mwezi Januari mwaka huu na kwamba ina laini ya umeme yenye urefu wa jumla ya kilomita 78.8 na jumla ya Mashine Poozo (Transfoma) 35 zinazohudumia wananchi, taasisi na viwanda.