Sunday, October 1, 2023

WAZIRI MKUU, MAJALIWA AMPA RUNGU RC PWANI KUNYANG'ANYA VIWANJA VILIVYOMILIKIWA NA WAWEKEZAJI KWA MUDA MREFU BILA KUENDELEZWA.

 

Na Scolastica Msewa, Mafia.


Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassimu Majaliwa amempa rungu Mkuu wa mkoa wa Pwani Mheshimiwa Abubakari Kunenge kunyang'anya Visiwa na viwanja uwekezaji wa Utalii Wilayani Mafia vilivyong'ang'aniwa na wawekezaji miaka mingi bila kuendelezwa kwa kutofanya chochote ili vigawiwe kwa wawekezaji wengine.


Amesema hayo wakati akifunga siku tatu za maonyesho ya uwekezaji wa katika uchumi wa buluu na kutangaza Utalii mazao ya bahari katika kisiwa cha Mafia mkoani Pwani Mheshimiwa Majaliwa amesema hatua hizo zifanyike kwa kuzingatia taratibu na Sheria za nchi kwani muda wa mwekezaji kumiliki eneo la uwekezaji bila kuendeleza ni miezi 36. "Kweli nyinyi mnawaacha tu? Sheria sizipo? Watu wa ardhi simpo?"


Amesema "Mkuu wa mkoa uwekezaji katika viwanja ni miezi 36 hujaendeleza nyang'anya chukua tunampa mtu mwingine".


"Na nyinyi Wakuu wa Wilaya wengine mwende mkaainishe maeneo ya fulsa za uwekezaji wa Utalii mliyonayo yaliyoshikiriwa na wawekezaji kwa miaka mingi hayana kazi yoyote wala bila kuendelezwa kwani sisi tunatangaza fulsa za uwekezaji wa Utalii miaka kumi bila uendelezwaji wowote nyang"anya kwa mujibu wa sheria maana Sheria tunazo ili tukabidhi kwa wawekezaji wengine wawekeze"

 

Mheshimiwa Mkuu wa mkoa ukiona kuna mwekezaji anamiliki kisiwa bila kuendeleza nyang'anya Sheria tunazo, watu wa ardhi mpo, hujaendeleza tunachukua tunampa mwekezaji mwingine.


"Tunatangaza fulsa, tunaita Watalii, tunaita wawekezaji halafu Kuna mtu anamiliki bila kuendeleza nyang'anya tukabidhi wengine wawekeze hayo ndio maelekezo yangu" 





MAGAZETI YA LEO TAREHE 01 OKTOBA 2023.

 













Saturday, September 30, 2023

MUFTI ZUBEIR, AKAMILISHA ZIARA YAKE LEO NCHINI UINGEREZA.

 

Na Hamimu Mussa,
Afisa Habari Mkuu
Bakwata Online Academy
Ofisi Ya Mufti-Tanzania

Leo tatehe 30/09/2022, ndio siku ya mwisho ya ziara ya Mheshimiwa Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania Dkt Abubakar Zubeir Bin Ally Nchini Uingereza ambapo ameweza kuitembelea miji mbalimbali na hasa yenye Waislaamu wengi Watanzania wanaoishi huko.


Jana tarehe 29/09/2023 akiwa katika Mji wa Leeds-Bangaladesh Center, aliweza kuwaaga diaspora wetu Nchini humo pamoja na wale wote walioshiriki katika Mkutano huo, ikiwa ni ishara ya ziara hiyo kufikia mwisho.


Inatajwa ni miongoni mwa ziara Bora kuwahi kufanywa na Viongozi wa kidini kutoka katika Mataifa ya kiafrika, na hii ni kwa sababu ya ujumbe aliokuwa nao kiongozi huyo Mkuu wa kidini Nchini Tanzania.


Ziara hiyo ilibeba ujumbe mzito kwa ulimwengu ikiwemo Amani kwa watu wote, uchumi, elimu, afya, chakula, teknolojia, usawa, haki na wajibu, maridhiano, mshikamano na umoja, uongozi na utawala bora pamoja utunzaji wa mazingira kwa kuvilinda viunbe hai.


Zaidi ya hapo, Mheshimiwa Mufti ameitumia ziara hiyo kwa kuwakumbusha Watanzania waishio katika Mataifa mengine (Diaspora) kuwekeza mitaji yao nyumbani ili iwe ni faida kwa Nchi na Watanzania kwa ujumla.





BAGAMOYO YATEKELEZA USAFI WA MWISHO WA MWEZI.

 

Viongozi mbalimbali katika Halmashauri ya Bagamoyo leo Tarehe 30 Septemba 2023 wameshiriki katika zoezi la usafi wa mazingira kwa kushirikiana na wananchi katika maeneo mbalimbali ya mji wa Bagamoyo.


Akiongoza zoezi hilo la usafi wa mazingira ambalo hufanyika kila jumamosi ya mwisho wa mwezi, kwaniaba ya Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Bagamoyo Shauri Selenda amesema usafi wa mazingira ni jambo la lazima kwa kila mwananchi ili kuepuka magonjwa ya mlipuko.


Alisema swala la usafi wa mazingira sio hiyari kulitekeleza kwani mazingira safi humuacha mtu akiwa salama ki afya na muonekano.


Amewataka wananchi kufanya usafi wa mazingira kila siku, kila wiki na kujumuika pamoja kila jumamosi ya mwisho wa mwezi.















MBUNGE PROF. MUHONGO NA WADAU WAFANIKISHA HARAMBEE UJENZI WA ETARO SEKENDARI KISIWA CHA RUKUBA

 


Na Mwandishi Wetu, Musoma Vijijini.


MBUNGE wa Jimbo la Musoma Vijijini, Prof. Sosepter Muhongo kwa kushirikiana na viongozi wakiwemo wakuu wa Wilaya ya Musoma na Halmashauri yake (Musoma DC), waemeendesha Harambee ya ujenzi wa Shule ya Sekondati Etaro, ambayo itakuwa ya Kata hiyo katika kisiwa cha Rukuba.


Katika tukio hilo lililofanyika Septemba 27,2023 kwenye Kisiwa hicho,

Wafanyakazi wa kada mbalimbali, wakiwemo Walimu, Kamati ya Siasa ya Wilaya na Wadau wengine wameshiriki


Kwa mujibu wa Ofisi ya Mbunge kupitia taarifa yake kwa umma, mapema leo Septemba 30,2023, imebainisha kuwa, Michango iliyopatikana kwenye Harambee hiyo ni pamoja na: 


"Wakazi na Wazaliwa wa Kisiwa cha Rukuba-Saruji Mifuko 167, Kamati ya Siasa ya Kata CCM-Saruji Mifuko 22, Kamati ya Siasa ya Wilaya CCM-Saruji Mifuko 15 na DED na wenzake-Saruji Mifuko 20.


Wengine waliochangia kwenye Harambee hiyo ni: "DC na wenzake- Saruji Mifuko 62, Mbunge wa Jimbo hilo la Musoma Vijijini-Saruji Mifuko 200,


Aidha,Fedha taslimu,Tsh248,000 (zikiwemo Tsh 105,000 za Walimu Makada wa CCM).


"Karibuni tujenge Sekondari ya Kisiwa cha Rukuba cha Musoma Vijijini.


Furaha na shauku ya ujenzi wa Sekondari Kisiwani Rukuba ni yetu sote" Imeeleza taarifa hiyo.


Kisiwa cha Rukuba ni moja ya vijiji vinne vya Kata ya Etaro ambapo Wanafunzi wa sekondari kutoka Kisiwani humo wanasoma nchi kavu kwenye sekondari ya Kata yao (Etaro Sekondari).


Ambapo imeelezwa kuwa, Wanafunzi hao wanakumbana na matatizo mengi ambayo yanadhoofisha maendeleo yao kielimu hivyo wakazi hao wameamua kujenga sekondari yao Kisiwani humo.


TOENI USHIRIKIANO KWA MIRADI YA TASAF- Ridhiwani Kikwete

 

Watumishi pamoja na wananchi wametakiwa kutoa ushirikiano kwa watendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii ( TASAF)  ili kuwainua watu wenye uhitaji



Ushauri huo umetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora Ndg. Ridhiwani Kikwete alipokuwa anaongea na wananchi wa kata ya Msata na Msoga katika mikutano baada ya kukagua maendeleo ya miradi inayotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).


Akizungumza baada ya kukagua ujenzi wa jengo la kuhifadhia maiti katika hospitali ya Wilaya Msoga , na baadae kuona mafanikio ya miradi ya kuwezesha wananchi na miradi ya miundombinu ya jamii, 


Naibu Waziri aliwaomba wananchi na Halmashauri kuendelea kushirikiana na Miradi ya TASAF ili kuwanyanyua wananchi wenye uhitaji. 


Katika mkutano huo, Naibu Waziri aliwapongeza Halmashauri kwa kutenga pesa za kukopesha vikundi vya maendeleo vikiwemo vikundi vya wanufaika wa miradi inayotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).


Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi wameshukuru TASAF kwa jitihada za kuwakomboa katika hali mbaya ya umaskini na pia kuishukuru Halmashauri kwa kuendelea kutenga pesa kwa vikundi vikiwemo vya TASAF na mafanikio yanayoonekana ni kwa sababu ya mipango hii kufanywa pamoja. 

Halmashauri ya Chalinze imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya kusaidia makundi mbalimbali na katika mkutano huo pamoja na makundi mengine, vikundi viwili vya Pain For Success na Muungano ambavyo kila kimoja kilikopeshwa shilingi Milioni 10 vilitoa ushuhuda wa jinsi mipango hivyo ilivyofanikiwa kwa kuonyesha bidhaa mbalimbali walizotengeneza na miradi waliyoshiriki. 


MAGAZETI YA LEO TAREHE 30 SEPTEMBA 2023










WAZIRI MKUU AFUNGA MAFUNZO YA UHAMIAJI, AHIMIZA UADILIFU

 

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wahitimu 521 wa mafunzo ya Kozi Na. 01/2023 wakatumie vema ujuzi na maarifa waliyoyapata katika kudhibiti vitendo vya uhalifu hususan maeneo ya vipenyo, vituo na mipakani.

Ametoa wito huo leo Ijumaa (Septemba 29, 2023) alipofunga mafunzo hayo kwa askari wa Uhamiaji katika Chuo cha Mafunzo ya Uhamiaji cha Raphael Kubaga, Wilayani Mkinga, katika Mkoa wa Tanga.

Waziri Mkuu amemshukuru Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutekeleza kwa vitendo mpango wake wa kuvijengea uwezo vyombo vya ulinzi na usalama nchini.

Mheshimiwa Majaliwa pia amewataka wahitimu hao wakafanye kazi kwa uzalendo, weledi na kutanguliza kwanza maslahi ya Taifa katika kazi zao za kila siku. “Kila mmoja akazingatie maadili na miiko ya kazi na akawe mfano bora wa uadilifu katika kituo atakachopangiwa,” amesisitiza.

Aidha, Waziri Mkuu amewataka viongozi wa Jeshi la Uhamiaji wawachukulie hatua kali za kisheria wahitimu ambao watabainika kuwa wanajihusisha na vitendo viovu ikiwemo rushwa, wizi wa maduhuli ya Serikali, ama kujiunga na mitandao ya uhalifu wa kiuhamiaji.

Mheshimiwa Majaliwa amesema kutokana na kuongezeka kwa teknolojia za kisasa na makosa ya kiuhalifu hususan biashara haramu ya usafirishaji wa binadamu na uhamiaji haramu, wahitimu hao wanapaswa kuhakikisha wanapata maarifa mapya mara kwa mara ili waweze kukabiliana na mabadiliko hayo ya kiteknolojia.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amemuagiza Meneja wa TARURA mkoa wa Tanga ahakikishe kuwa hadi kufikia mahafali ya mwaka 2024 awe ameijenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka barabara kuu inayoingia chuoni hapo.

Kuhusu changamoto ya maji kwa chuo pamoja na wananchi wa vijiji jirani, Mheshimiwa Majaliwa ameiagiza Mamlaka za maji za Mkoa wa Tanga zihakikishe taasisi hiyo inaunganishwa kwenye mtandao wa maji. “Lakini pia Katibu Mkuu upo hapa, ona namna ya kuwezesha chuo hiki fedha kwa ajili ya ujenzi wa tanki la kuhifadhi kama yalivyo mahitaji ya chuo.”

Mapema, Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhandisi Hamad Masauni alisema awali Jeshi la Uhamiaji halikuwa likitoa mafunzo kwa watumishi wake.

"Mwaka jana ndiyo tulitoa kundi la kwanza la wahitimu, tunamshukuru Mhe Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kutoa sh. bilioni 1.5 za kuendeleza majengo. Hatukuwa na ajira mpya katika idara ya uhamiaji, tunamshukuru kwa kuongeza ajira wakiwemo hawa 521 wanaohitimu leo," alisema.

Naye, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii ambaye ni Mbunge wa jimbo la Mkinga, Bw. Dunstan Kitandula alisema anashukuru Serikali kwa uwepo wa chuo hicho na kuongeza: "Tunaiomba Serikali iendelee kuboresha chuo hiki kwa sababu matamanio yetu ni kuona chuo kinasaidia Afrika Mashariki yote."

Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala aliiomba Serikali isaidie kuboresha miundombinu ya chuo hicho ikiwemo barabara ya kuingia chuoni na uwanja wa gwaride. Pia aliomba wajengewe tanki la lita 250,000 ili kutatua shida ya maji chuoni hapo na kwenye vijiji vya jirani.


Friday, September 29, 2023

TANZANIA KUSIMAMIA MATUMIZI SALAMA YA KEMIKALI NA TAKA ZA KEMIKALI

 


Na. WAF - Bonn, Ujerumani

Serikali ya Tanzania kupitia wizara ya Afya imesisitiza kuendelea kusimamia matumizi salama ya Kemikali na taka zitokanazo na Kemikali ili kuzuia athari kwa  wananchi.


Hayo yamebainishwa leo Septemba 29, 2023 na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. Grace Magembe wakati akiwasilisha tamko la Tanzania katika Mkutano wa tano wa Kimataifa wa Usimamizi wa matumizi salama ya Kemikali Duniani (ICCM5) kwa niaba ya Mhe Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu.


Aidha, Dkt Magembe alieleza kuwa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe Rais, Dkt Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuchukua hatua madhubuti kudhibiti matumizi mabaya ya Kemikali ili kuhakikisha usalama wa wananchi na mazingira nchini kwa kutekeleza kwa vitendo malengo endelevu ya maendeleo ya Dunia na katika kujenga uchumi endelevu wa nchi.


“Pamoja na kuwa matumizi ya Kemikali  ni muhimu na zipo faida nyingi zitokanazo na kemikali hasa katika sekta za Afya, Kilimo, Elimu, Viwanda nk, shughuli za kemikali zisiposimamiwa vizuri, zinaweza kuwa na athari kubwa kwa afya ya binadamu,  mazingira, usalama mahala pa kazi, ulinzi na usalama wa nchi”. Amesema Dkt. Magembe.


Pia Dkt. Magembe amesema kuwa takwimu za Shirika la Afya Duniani zinaonyesha, takribani vifo milioni mbili duniani  kwa mwaka vinatokana na matumizi mabaya ya Kemikali yakiwemo madhara mengine kama ulemavu, kuharibika kwa mimba, magonjwa ya mfumo wa hewa na saratani.


Sambamba na hilo Dkt. Magembe amebainisha mipango ya Tanzania katika matumizi ya kemikali hizo ikiwa ni Pamoja na kuimarisha uratibu na usimamizi wa Kemikali ndani ya nchi Pamoja na kutenga rasilimali za kutosha ikiwemo fedha ili kuwezesha utekelezaji wa mpango mkakati huo, hususani kuziwezesha nchi zinazoendelea kuzuia na kudhibiti madhara yatokanyo na matumizi ya Kemikali.


Aidha Dkt. Magembe ameziomba nchi zilizoendelea kushirikiana na nchi zinazoendelea katika kuwekeza kwenye teknolojia za kisasa kwenye viwanda vinavyozalisha dawa, vifaa tiba, mbolea, viuatilifu  na bidhaa nyinginezo kwa lengo la kuzalisha bidhaa rafiki kwa afya ya binadamu na mazingira na pia kudhibiti taka zitokanazo na bidhaa hizo.