Waziri wa
Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi amewaasa watu wanaotoa kauli za
kichochezi katika mitandao ya kijamii, majukwaa ya kisiasa na maeneo mbalimbali
ambapo kauli hizo za kibaguzi na kichochezi zinahusu Muungano wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Viongozi mbalimbali wa serikali au wa dini.
Waziri
Katambi ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na waumini wa Msikiti wa Mukadam uliopo
Kata ya Chang’ombe iliyopo wilaya ya Dodoma Mjini ambapo kumefanyika Mashindano
ya Quran na Harambee ya Ujenzi wa Msikiti huo.
“Taifa hili
limejengwa kwa maumivu makubwa ya waasisi, limejengwa kwa jasho na hata damu
ilipobidi ili Taifa Tanzania liwepo, nitumie fursa hii kuwaomba sana na kuwaasa
wale wote ambao wanatumia majukwaa ya kisiasa kuchonganisha wananchi, kuwajaza
chuki, kuchochea lakini pia kuhamasisha kufanya uhalifu na wanaounda magenge ya
uhalifu yanayolenga kuharibu taifa letu, niwasihi na kuwaomba waache mara moja
kwasababu kufanya hivyo hakuna ambae atabaki salama tutaathirika sisi
Watanzania wote na athari hii italiathiri taifa kisiasa, kiuchumi na
kiutamaduni.” amesema Waziri Katambi.
“Tutarudi
nyuma kimaendeleo,tutashindwa kuswali, tutashindwa kwenda kanisani, tutashindwa
kufanya kazi za kiuchumi, tutashindwa kujenga nchi yetu, tutashindwa kujenga
uchumi wa mtu mmoja mmoja, tuwakanye na kuwaelekeza vijana wetu wakaishi
mwenendo mwema na uzalendo kwa taifa lao na pale yanapotolewa maonyo na
maelekezo ya vyombo vya ulinzi na usalama wasikaidi kwani kwenda kinyume ni
kuvunja sheria, katiba na taratibu.” aliongeza Waziri Katambi.





No comments:
Post a Comment