Tuesday, June 23, 2026

TWPF YAKAGUA ENEO LAKE LA KIMKAKATI DODOMA

 

 

Na Oscar Mbuza, MNRT

 

BODI ya Mfuko wa Kuhifadhi Wanyawapori (TWPF) imetembelea kiwanja kinachomilikiwa na Mfuko huo  eneo la Njedengwa katika Manispaa ya Dodoma ambacho kitapangiwa matumizi yake hivi karibuni.

 

Msafara wa Bodi hiyo umeongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya TWPF Profesa Jafari Kideghesho akiambatana na  Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Alexander Lobora na baadhi ya wajumbe wa Bodi.

 

Wajumbe wengine ambao wameshiriki  ziara hiyo ni Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) Dkt. Eblate Mjingo na  Kamishna wa Uhifadhi kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Mlage Kabange.

 

Aidha ujumbe huo pia ulimjumuisha  Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCCA), Victoria Shayo aliyemwakilisha Kamisha wa Uhifadhi wa NCCA.

 

Akizungumza baada ya kukagua eneo hilo lililopo Kitalu Namba 16, lenye ukubwa wa mita za mraba 39,700, Profesa Kideghesho amesema ameridhishwa na usimamizi na uhifadhi wa kiwanja hicho ambacho kitapangiwa matumizi yake hususani kwenye maendeleo ya uhifadhi wa wanyamapori hivi karibuni.

 

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Wanyamapori, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Lobora amesema wizara italitumia eneo hilo kama eneo la mkakati la uendeshaji wa shughuli za uhifadhi wa wanyamapori nchini.

 

Mfuko wa Hifadhi ya Wanyamapori Tanzania ni wa kudumu maalum kwa ajili ya kusaidia kutatua baadhi ya changamoto zinazohitaji fedha kwenye uhifadhi.

 

Madhumuni ya Mfuko ni kurahisisha na kusaidia uhifadhi wa wanyamapori, ndani na nje ya maeneo yaliyohifadhiwa. Bodi ya TWPF ina wajumbe tisa.

                


No comments:

Post a Comment