Tuesday, June 23, 2026

TANROADS YATANGA BARABARA SITA ZA PPP KUUNGANISHA MIKOA YA DAR, PWANI, DODOMA, SINGIDA NA TANGA KM 969

 

Katika hatua nyingine kubwa ya kuharakisha maendeleo ya miundombinu na kuimarisha ukuaji wa uchumi wa Taifa, Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) umetangaza fursa za uwekezaji katika miradi sita mikubwa ya barabara yenye urefu wa kilomita 969 kupitia mfumo wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP).

 

Tangazo hilo la kimataifa la kutafuta wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kubuni, kujenga, kugharamia, kuendesha, kutunza na hatimaye kukabidhi miradi hiyo kwa Serikali kupitia mfumo wa Design, Build, Finance, Operate, Maintain and Transfer (DBFOMT), linaendelea kudhihirisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutumia nguvu ya sekta binafsi kuharakisha utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo.

 

Hatua hiyo pia inaakisi mafanikio ya mageuzi makubwa yanayosimamiwa na Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC) chini ya Mkurugenzi Mtendaji David Kafulila, ambaye amekuwa mstari wa mbele kuhamasisha ushiriki wa sekta binafsi katika uwekezaji wa miundombinu na huduma za kijamii nchini.

 

Miradi iliyowekwa mezani kwa wawekezaji ni pamoja na upanuzi wa Barabara ya Morogoro–Dodoma yenye urefu wa kilomita 260 kuwa njia nne, Barabara ya Handeni–Kiberashi–Chemba–Kwamtoro–Singida yenye kilomita 384, upanuzi wa Barabara ya Chalinze–Segera–Tanga yenye kilomita 246 kuwa njia nne pamoja na ujenzi wa Kitonga Escarpment Bypass yenye kilomita 27.

 

Miradi mingine ni Dar es Salaam Port–Kibaha Expressway yenye kilomita 42 na Dar es Salaam CBD–Julius Nyerere International Airport Expressway yenye kilomita 10.

 

Kwa mujibu wa TANROADS, miradi hiyo inalenga kupunguza msongamano wa magari, kuboresha usafirishaji wa watu na mizigo, kuongeza ushindani wa uchumi wa Tanzania na kuimarisha nafasi ya nchi kama kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

 

Kwa ujumla, miradi hiyo ina urefu wa kilomita 969. Kwa makadirio ya wastani ambapo kilomita moja ya barabara inaweza kugharimu takribani Dola za Marekani milioni moja sawa na karibu tsh trilioni tatu za Kitanzania kwa zote.


No comments:

Post a Comment