Thursday, January 3, 2019

RPC MOROGORO AIPONGEZA TIF.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, (SACP) Wilbroad Mutafungwa, (kushoto) akisalimiana na Mwenyekiti wa The Islamic Foundation (TIF).
..................................... 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, (SACP) Wilbroad Mutafungwa,  ameipongeza Taasisi ya The Islamic Foundation yenye makao yake makuu Mkoani humo kwa kazi inayofanya katika kuihudumia jamii.

Kamanda Mutafungwa amesema Taasisi hiyo imekuwa mfano wa kuigwa katika shughuli zake ambazo zinafanywa na kusimamiwa kwa weledi huku huduma zake zikiwa hazibagui dini, rangi wala kabila.

Akizungumzia vyombo vya habari vinavyomilikiwa na Taasisi hiyo  Kamanda Mutafungwa amesema vyombo hivyo vimekuwa msaada mkubwa kwa jeshi la polisi mkoani humo kutokana na vipindi vyake vya kuelimisha jamii kuhusu amani, na usalama barabarani hali iliyopelekea kupungua kwa kiasi kikubwa kwa ajali za barabarani.

Aliongeza kwa kusema kuwa, vyombo vya habari vinaweza kuwa chanzo cha uvunjifu wa amani mahali popote pale na kwamba vikitumika vizuri vinakuwa msaada mkubwa kwa serikali katika kulinda amani ya sehemu husika.

Alisema jeshi la polisi linahitaji ushirikiano katika kutekeleza majukumu yake hivyo kinachofanywa na Taasisi ya The Islamic Foundation ni kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo ili kurahisisha utendaji kazi wa polisi.

Alifafanua kuwa, jeshi la polisi kazi yake ni kulinda usalama wa raia na mali zao huku wajibu wa raia ni kutii sheria bila ya shuruti na kwamba anaevunja sheria anachukuliwa hatua kwa mujibu wa kosa alilotenda.

Alisema katika hali hiyo, raia wakielewa kazi ya polisi, na wajibu wao wa kutii sheria kama raia, hakutakuwa na uhasama miongoni mwao na kwamba uendeshaji wa shughuli mbalimbali za kijamii utafanywa kwa ushirikiano.

Akizungumzia ajali za barabarani, Kamanda Mutafungwa amesema kwa sasa ajali zimepungua kwa kiasi kikubwa na kwamba utii wa sheria hasa kwa madereva wa bodaboda upo kwa kiwango kikubwa mkoani humo.

Alimalizia kwa kuwataka wananchi wote mkoani humo kutoa ushirikiano kwa jeshi la Polisi ili kukomesha vitendo vyote vya uvunjifu wa sheria, ikiwemo zile za barabarani na uhalifu wa aina zote.

Nae Mwenyekiti wa Taasisi ya The Islamic Foundation, Aref  Nahd amelipongeza Jeshi la polisi mkoani humo kwa kutoa ushirikiano wao na Taasisi hiyo hali inayaopelekea kuendesha vipindi vya usalama barabarani kupitia Tvimmaa na Redio imaan ambapo elimu hiyo imewasaidia sio tu wakazi wa mkoa wa Morogoro, bali kila sehemu vinaposikika vyombo vya habari vya imaan.

Alisema Taasisi hiyo pamoja na kujishughulisha na huduma za kiroho lakini pia inatekeleza miradi mbalimbali ya kijamii kwa lengo la kuisaidia serikali katika kuleta maendeleo.

Aidha, Mwenyekiti Aref Nahdi,  alimueleza Kamanda Mutafungwa kuwa, Taasisi hiyo imekuwa ikitoa elimu mbalimbali kuhusiana na kulinda amani na kwamba katika hilo inashirikiana na wahadhiri mbalimbali wa ndani na nje ya nchi kwa lengo la kudumisha amani.

Aliongeza kuwa, wamefanikiwa kuandaa makongamano ya kuelimisha jamii umuhimu wa amani ndani ya mkoa wa Morogoro na nje ya mkoa huo na kwamba muitkio unakuwa mkubwa hali inayoashiria kuwa elimu iliyokusudiwa inafika ipasavyo.

Kamanda wa  Polisi Mkoa wa Morogoro, alitembelea ofisi za The Islamic Foundation (TIF) zilizopo msamvu mjini Morogoro kwa kutambuana na viongozi wa Taasisi hiyo ambapo aliweza kukutana na Mwenyekiti wa The Islamic Foundation, Aref Nahd, Mkurugenzi Mtendaji wa Taassi hiyo, Sheikh Ibrahim Twaha, na Katibu Mkuu Haroun Rajab.

Akiwa katika ofisi za The Islamic Foundatio, Kamanda Mutafungwa alijionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na taasisi hiyo huku kumbukumbu zikiwa makao makuu ya ofisi.

Miongoni mwa shughuli alizoweza kuona kumbukumbu zake ni pamoja na ujenzi wa Misikiti, uchimbaji wa visima, utoaji wa misaada mbalimbali, vituo vya kulelea watoto yatima na uendeshaji wa shule za msingi na sekondari.

Kamanda Mutafungwa ameipongeza The Islamic Foundation kwa miradi mbalimbali ya maendeleo na kuahidi kushirikiana nao katika kipindi chake chote atakachokuwepo Mkoani Morogoro.

  Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, (SACP) Wilbroad Mutafungwa, akimsikiliza Mwenyekiti wa Taasisi ya The Islamic Foudation (TIF), Aref Nahdi, alipotembelea Makao ya Taasisi hiyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, (SACP) Wilbroad Mutafungwa, akiwa anazungumza na Tvimaan nje ya ofisi mara baada ya kumaliza kuzungumza na viongozi wa Taasisi ya The Islamic Foundation (TIF) Makao makuu ya Taasisi hiyo iliyopo Msamvu Mkoani Morogoro.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya The Islamic Foundation (TIF) Sheikh Ibrahim Twaha, (Kulia) Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, (SACP) Wilbroad Mutafungwa (katikati) Mwenyekiti wa The Islamic Foundation, Aref Nahdi, (kushoto) wakiangalia kitabu cha utekelezaji wa miradi ya TIF.

 Mwenyekiti wa The Islamic Foundation, Aref Nahdi, (kulia) akimkabidhi zawadi ya ngao, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, (SACP) Wilbroad Mutafungwa (katikati) anaeshuhudia kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya The Islamic Foundation (TIF) Sheikh Ibrahim Twaha.
Katibu Mkuu wa The Islamic Foundation, Haroun Rajab (kulia) Mwenyekiti, Aref Nahd, (katikati) wakifurahia jambo na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, (SACP) Wilbroad Mutafungwa.

WAZIRI LUGOLA APIGA MARUFUKU POLISI KUWAKAMATA WAENDESHA BODABODA WAKIWA HAWAJAVAA SARE

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kushoto) akitoka Kituo Kikuu cha Polisi cha mjini Bukoba mara baada ya kufanya ziara ya kushtukiza katika Kituo hicho, leo, kwa kufuatilia utendaji kazi wao. Katikati ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Revocatus Malimi, na kulia ni Mkuu wa Jeshi la Magereza Mkoani humo, ACP Raymond Mwampashe. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola akizungumza na mamia ya wananchi mjini Bukoba Mkoani Kagera, katika mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa Uhuru, Mayunga mjini humo, leo. Lugola licha ya kuwa amewataka waendesha bodaboda wafuate sheria za usalama barabarani, lakini ametoa onyo kwa Polisi mjini humo kuacha  kuwakamata waendesha bodaboda wakiwa hawajavaa sare.
............................................

Na Felix Mwagara, MOHA-Bukoba.

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amepiga marufuku tabia ya baadhi ya Askari Polisi nchini kukamata pikipiki wakiwa hawana sare za Jeshi.

Akizungumza na mamia ya wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa uhuru, Mayunga, mjini Bukoba Mkoani Kagera, leo, Lugola alisema polisi wanapaswa kufuata utaratibu wa kijeshi hasa wanapokamata vyombo vya moto na siyo kuvunja utaratibu.

Lugola aliongeza kuwa, bodaboda zinazovunja sheria za usalama barabarani zinapaswa kukamatwa bila kuwaonea huruma, ila ni kosa Polisi kuwanyanyasa vijana hao ambao wanapata ridhiki kupitia biasahara hiyo.

“Mnapaswa kukamata hizi bodaboda zinapofanya makosa, tabia ya kukurupuka huku mkitafuta fedha zisizo halali, huko ni kuwaonea waendesha bodaboda,” alisema Lugola.

Pia Lugola aliwataka waendesha bodaboda mjini Bukoba na Tanzania kwa ujumla wafuate sharia za usalama barabarani zikiwemo kuvaa kofia ngumu, kutokubeba abiria zaidi ya mmoja na pia wakiendesha wanapaswa kuwasha taa.

Lugola ameanza ziara yake ya siku nane mkoani humo akitembelea Wilaya zote za Mkoa huo akisikiliza kero za wananchi pamoja na kufuatilia maagizo yake aliyoyatoa kwa vyombo vya ulinzi na usalama vilivyopo ndani ya Wizara yake.

Lugola mwaka jana alitoa maagizo kwa makamanda wa mikoa nchini ambayo ni dhamana zitolewe saa 24 katika vituo vyote vya polisi nchini, na pia kupiga marufuku tabia ya baadhi ya Polisi kubambikizia kesi wananchi, na pamoja na agizo la pikipiki zote zilizopo vituoni ziondolewe.

Waziri Lugola tayari amemaliza ziara yake kwa Wilaya ya Bukoba na Kesho ataanza ziara Wilaya za Misenyi, baadaye Karagwe, Kyerwa, Ngara, Biharamulo na Januari 8, 2019 atamalizia ziara yake Wilaya ya Muleba ambapo katika Wilaya hizo pia atazungumza na wananchi pamoja na watumishi waliopo ndani ya Wizara yake ambao ni Jeshi la Polisi, Idara ya Uhamiaji, Jeshi la Magereza, Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, pamoja na Idara ya Probesheni ambayo jukumu lake kuu ni kupunguza msongamano gerezani na kusimamia wafungwa waliopewa adhabu mbadala na Mahakama au wafungwa waliopata msamaha kupitia sheria ya huduma kwa jamii na kutumikia kifungo chao nje ya Gereza.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kushoto) akimsikiliza Mkazi wa mjini Bukoba alipokuwa anaeleza kero yake mara baada ya Waziri huyo kuwaita wananchi hao mbele waweze kutoa kero zao, mara baada ya kumaliza kuzungumza na wananchi hao katika mkutano wa hadhara  uliofanyika Uwanja wa Uhuru, Mayunga mjini humo, leo. Lugola licha ya kuwa amewataka waendesha bodaboda wafuate sheria za usalama barabarani, lakini ametoa onyo kwa Polisi mjini humo kuacha kuwakamata waendesha bodaboda wakiwa hawajavaa sare.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kushoto) akimsalimia Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt Bashiru Ally, wakati alipoonana naye Uwanja wa Ndege wa Bukoba, leo. Lugola yupo Mkoani Kagera kwa ziara ya kikazi akitembelea Wilaya zote, akisikiliza kero mbalimbali za watumishi wa Wizara yake pamoja na wananchi mkoani humo.

Wednesday, January 2, 2019

TAARIFA KUTOKA JESHI LA POLISI MKOANI MWANZA LEO

Jeshi la Poliisi Mkoa wa Mwanza kwa kutumia kikosi chake kabambe chenye uweledi uliotukuka tumefanikiwa kuwakamata watu watatu kwa kosa la kupatikana na dawa za kulevya aina ya bhangi kiasi cha kilogramu 110, huko mtaa wa Ngumo “A”, Wilayani Kwimba.

Tukio hilo limetokea tarehe 01.01.2019 majira ya saa 21:00hrs, hii ni baada ya kikosi hicho mahiri cha askari wakati kikiwa doria na misako kilipokea taarifa toka kwa wasiri kwamba katika mtaa wa Ngumo ”A” na Safari club wapo watu wanaojihusisha na utumiaji na uuzaji wa dawa za kulevya. 

Ndipo askari walifanya ufuatiliaji na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa hao watatu wakiwa na kiasi hicho cha dawa za kulevya aina ya bhangi.

Watuhumiwa waliokamatwa na dawa hizo za kulevya aina ya bhangi ni;

Consolatha Elias, miaka 52, mkazi Ngumo “A”, huyu amekamatwa na dawa za kulevya aina ya bhangi kiasi cha kilogramu 100.

Emmanuel Lucas, miaka 21, mkazi wa kijiji cha Manguluma, na
Rehema Joseph, miaka 27, mkazi wa Chato, hawa wawili wamekamatwa na dawa za kulevya aina ya bhangi kiasi cha kilogramu 10.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza tunaendelea na mahojiano na watuhumiwa wote watatu ili kuweza kubaini watu wanaoshirikiana nao katika uuzaji, utumiaji na usafirishaji wa dawa hizo za kulevya aina ya bhangi. Aidha pindi uchunguzi ukikamilika watuhumiwa wote watatu watafikishwa mahakamani ili hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza, tunatoa onyo kwa baadhi ya wananchi waojihusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya kuwa waache kwani ni kinyume na sheria na endapo mtu atabainika hatua stahiki za kisheria zitachukuliwa dhidi yake. 

Vilevile tunawaomba wananchi waendelee kutupa ushirikiano kwa kutupa mapema taarifa za uhalifu na wahalifu ili waweze kukamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria.
Imetolewa na;

Jonathan Shanna – ACP
Kamanda wa Polisi (M) Mwanza.
02 January, 2019.

MAGAZETI YA LEO JANUARI 02, 2019.

Tuesday, January 1, 2019

MWENYEKITI WA CCM BAGAMOYO ATOA SALAM ZA MWAKA MPYA.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi wilaya ya Bagamoyo, Abduli Sharifu, ametoa salamu za mwaka mpya 2019 huku akisema kuwa anathamini michango ya watu wa vyama vyote.

Katika salamu zake hizo, Sharifu amewataka wa CCM na wanachama wa vyama vingine kuishi kwa umoja na kushirikiana katika mambo mbalimbali ya maendeleo.

Alisema maendeleo hayana chama hivyo kila mtanzania bila ya kujali chama chake anapaswa kushiri shughuli za maendeleo katika eneo lake.

Alisema katika uongozi wake ndani ya CCM wilaya ya Bagamoyo, atahakikisha wana siasa wote wanaishi kwa amani na utulivu na kuthamini mawazo ya watu wote.

Aliongeza kuwa, kukosolewa ni miongoni mwa chaangamoto kuona wapi panahitaji marekebisho ili kuboresha zaidi.

Katika hatua nyingine Mwenyekiti huyo wa CCM wilaya ya Bagamoyo alisema katika kipindi hiki ambacho anatimiza mwaka mmoja katika uongozi wake ameweza kusimamia vyema utekelezaji wa ilani ya uchaguzi pamoja na kusimamia katiba ya CCM.

Alisema miongoni mwa mambo ambayo ameyafanya katika kipindi cha mwaka mmoja ni pamoja na kujenga mahusiano mema kati ya chama na serikali na kuamsha ari kwa wanachama wa CCM.


DC BAGAMOYO AKABIDHI VITAMBULISHO KWA WAJASILIAMALI.

 Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Zainabu Kawawa, akimkabidhi kitambulisho mmoja wa wafanyabiashara ndogo ndogo, zoezi ambalo lilifanyika katika ofisi ya Mkuu wa wilaya.
 
Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Zainabu Kawawa, akizungumza na wafanyabiashara ndogo ndogo.
................................................ 

Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo, Zainabu Kawawa, amezindua rasmi zoezi la ugawaji wa vitambulisho kwa wafanya biasahara ndogo ndogo kama alivyoelekeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mkuu huyo wa wilaya aliwataka wafanyabiashara hao kuzingatia vigezo villivyowekwa kwa mfanyabiashara anaestahiki kupata kitambulisho hicho.

Alisisitiza kuwa, mfanyabiashara atakaekiuka masharti yaliyowekwa na kusema uongo atachukuliwa hatua kali za kisheria.

Aidha, amewaagiza maafisa biashara na wale wa Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) kutoa elimu kwa wafanyabiashara ili wale wanokidhi vigezo waweze kupatiwa vitambulishi hivyo.

Katika hatua hiyo ya uzinduzi, Mkuu huyo wa wilaya amewakabidhi wafanyabiashara ndogo ndogo 10 wa awali ambapo baada ya hapo zoezi litaendelea kwa kushirikiana kati ya Maafisa wa biashara na wale wa Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) pamoja na watendaji wa kata kwaajili ya kuwatambua wafanyabiashara ndogo ndogo wenye sifa ya kupata vitambulisho hivyo.

Tayari zoezi la awali limeshafanyika la kuwatambua wafanyabiashara ndogo ndogo ambapo mitaji yao haizidi milioni 4.

Katika hatua ya awali kwa Halmashauri ya Bagamoyo jumla ya wafanyabiashara ndogo ndogo 4,400 wamekidhi vigezo na kustahiki kupewa vitambulisho hivyo.

Kwa upande wao wafanyabiashara ndogo ndogo, wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli kwa hatua hiyo ambayo itawaondolea kero wafanyabiashara wadogo wadogo.

Walisema awali walikuwa wakisumbuliwa na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) hata kama biashara ikiwa ndogo unatakiwa kukadiriwa kodi hali iliyopelekea watu wengi kushindwa kuendesha biashara zao.

Waliongeza kwa kusema kuwa, utaratibu huu wa sasa ni mzuri kwa upande wao kwani kila mmoja ataweza kuiingizia serikali mapato kulingana na uwezo wake.

Hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alitoa vitambulisho kwa wafanyabiashara ndogo ndogo nchini wenye mitaji isiozidi shilingi milioni nne 4,000,000/= ili waepukane na usumbufu wanaoupata kutoka TRA na mgambo wa jiji.

Jumla ya vitambulisho laki sita na sabini elfu 670,000 vilitolewa na kugawanywa kwa wakuu wa mikoa nchi nzima ambapo kila mkuu wa mkoa alipewa vitambulisho 25,000 avigawanye kwenye wilaya zake.
Baadhi ya wafanyabiashara ndogo ndogo waliokabidhiwa vitambulisho vyao na Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo.
Sehemu ya wafanyabiashara ndogo ndogo waliofika ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo kupata vitambulisho vyao.

Monday, December 31, 2018

RAIS WA ZANZIBAR DKT. SHEIN ATOA SALAMU ZA MWAKA MPYA 2019

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akitoa salamu za Mwaka Mpya wa 2019, Ikulu Zanzibar.(Picha na Ikulu)

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wananchi  wa Zanzibar kuendelea kuidumisha hali ya amani na utulivu ambayo ndio msingi wa mafanikio yanayoendelea kupatikana hivi sasa na yatakayopatikana hapo baadae.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika risala yake ya kuukaribisha mwaka mpya wa 2019 aliyoitoa kupitia vyombo vya habari, Ikulu mjini Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisema kuwa katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya mwaka 2018 mafanikio makubwa yamepatikana ambayo yamechangiwa na kuwepo kwa amani, mshikamano, umoja na mapenzi yaliopo.

Katika risala yake hiyo Rais Dk. Shein alieleza kuwa hali ya amani, umoja na mshikamano uliopo nchini ni jambo muhimu linalowavutia Washirika wa maendeleo ambao wanaridhika na jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na ndio maana wanaiunga mkono katika mipango yake ya maendeleo.

Alisema kuwa hapana shaka kwamba iwapo amani, usalama na utulivu vitadumishwa na kufanya kazi kwa bidii Washirika wa Maendeleo watakuwa pamoja na Zanzibar katika kuisaidia ili kuweza kutekeleza malengo yaliyopangwa.

Rais Dk. Shein alitoa shukurani kwa wananchi wote kwa kuunga mkono juhudiza serikali za kuiletea maendeleo Zanzibar na kueleza kuwa moyo wao huo wa umoja na mshikamano umewezesha kuimarisha vizuri hali ya uchumi wa Zanzibar.

Hata hivyo, Dk. Shein alitoa shukurani nyingi kwa wananchi wote kwa kuunga mkono juhudi za Serikali za kuiletea maendeleo Zanzibar ambapo moyo wao huo wa umoja na mshikamano umewezesha kuimarisha vizuri hali ya uchumi wa Zanzibar.

“Tukiwa tunaukaribisha mwaka mpya wa 2019, nachukua fursa hii kwa niaba ya wananchi wote  wa Zanzibar kuwashukuru kwa dhati  Washirika wetu wa Maendeleo kwa kuendelea kutuunga mkono, tunathamini mikopo, misaada na ushauri tulioupata kutoka kwao”, alisema Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa wakati unakaribishwa mwaka 2019 ni wajibu wa kila Taasisi ya Serikali ikajipima namna inavyoendelea kutekeleza mambo yaliyoagizwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015-2020.

“Nawakumbusha viongozi wenzangu viongozi wenzangu wote wa CCM tuliochaguliwa na wananchi katika Uchaguzi Mkuu wa 2015, uliorudiwa mwezi Machi, 2016. Kadhalika jukumu hili wanapaswa walizingatie na wale wote niliowateua katika nyadhifa mbali mbali”,alisema Dk. Shein katika risala yake hiyo.

Katika risala yake hiyo Rais Dk. Shein alizitaja kumbukumbu za matukio yalitokea katika mwaka 2018 ikiwa ni pamoja na utiaji wa saini wa Mkataba wa Mgawanyo wa Uzalishaji wa Mafuta na Gesi Asilia (PSA), baina ya Kampuni ya Maendeleo ya Mafuta na Gesi Asilia na kampuni ya RAK GAS ya Ras Al Khaimah.

Aliongeza kuwa tukio jengine la kihistoria ni kufanyika kwa Tamasha la Utalii la Kimataifa ambalo lilihudhuriwa na Makampuni 150 ya Utalii ya ndani na nje ya nchi ambalo lilileta mafanikio katika kuwaunganisha wafanyabiashara wa utalii wa Zanzibar na wale wa Kimataifa na kuitangaza Zanzibar katika masoko ya Kimataifa.

Alieleza kuwa mwaka 2018 umefungua milango katika utekelezaji wa dhamira ya kuendeleza kilimo cha mpunga kwa njia ya umwagiliaji maji na utumiaji wa zana za kisasa ambapo tarehe 6 Disemba, 2018 Serikali ilitiliana saini Mkataba wa Ujenzi wa Miundombinu ya Kilino cha Umwagiliaji maji na Kampuni ya Kokon Hansol JV ya Jamhuri ya Korea kupitia Shirika la Maendeleo la nchi hiyo.

Pia, Rais Dk. Shein alieleza kuwa katika lengo la kuungana na nchi nyengine katika kuendeleza uchumi wa Bahari tarehe 26 hadi 28 aliongoza Ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mkutano wa Kimataifa uliofanyika Nairobi nchini Kenya.

Alisisitiza kuwa kwa upande wa Zanzibar inauanza mwaka 2019 ikiwa imejipanga kwa kutafuta njia bora za kutumia rasilimali za bahari kwa kuitumia vizuri bahari ya Hindi iliyoizunguka kwani hili ni eneo muhimu kwa uchumi wa Zanzibar.

Akieleza jambo jengine muhimu ambalo limefanyika katika mwaka 2018, Rais Dk. Shein alisema kuwa tukio linalohusu jitihada za Serikali za kuwakinga wanawake wa Zanzibar na janga la saratani ya shingo ya kizazi ambapo mnamo April 10 Mama Mwanamwema Shein alizindua rasmi Mpango wa Chanjo dhidi ya Ugonjwa wa Saratani ya Shingo wa Kizazi.

Vile vile, tarehe 5 Disemba 2018 alizindua Mpango wa Miaka Minne wa Uchunguzi wa Saratani ya Shingo ya Kizazi ambao unawajumuisha wanawake wenye umri wa miaka 21 hadi 65 kazi ambayo itafanywa kwa kushirikiana na Wataalamu kutoka Jamhuri ya Watu wa China ambapo huduma zote pamoja na matibabu zitatolewa bure.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Zanzibar inasifika kwa uzuri wake, historia yake na khulka nzuri za watu wake na hali ya usalama iliyopo ambapo Serikali nayo inafanya jitihada za kuhakikisha kwamba sifa njema ya Zanzibar ya kuwa ni sehemu salama yenye utulivu inaendelea kwua ni kichocheo cha kuwavutia wageni, watalii na wawekezaji sambamba na kurahisiha utekelezaji wa mipango ya kamedneleo.

Hivyo, mnamo tarehe 3 Novemba 2018 ulizinduliwa rasmi  Mradi wa Ulinzi wa Mji Salama ambao lengo lake ni kuhakikisha hali ya usalama kwa kutumia CCTV na vyombo vyengine vya kisasa ambapo dhamira ni kuendeleza mradi huu katika Mikoa mengine ya Unguja na Pemba hatua kwa hatua.

Licha ya mafanikio hayo yaliopatikana mwaka 2018, Rais Dk. Shein alieleza kuwa bado kunahitajika kuzidisha mapambano dhidi ya udhalilishaji wa wanwake na watoto na unyanyasaji wa kijinsia kwa vile kesi za vitendo hivyo bado zinaendelea kuripotiwa kwenye maeneo mbali mbali.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwaahidi wananchi wote kwamba wale wote watakaobainika kwamba wamehusika kwenye tukio la uvujaji wa mitihani ya kidato cha Pili kwenye sekta ya elimu watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Aliongeza kuwa tukio hilo ni la kusikitisha, linalokwenda kinyume na mipango ya maendeleo ya elimu ambalo halijengi mustakbali mwema wa elimu kwa watoto na kuwataka wananchi kujifunza athari za tukio hilo kwa Serikali, Wizara, Walimu, Wazazi, Wanafunzi na nchi kwa jumla.

Akimalizia risala yake hiyo, Rais Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi wote kushiriki kwa wingi katika shughuli mbali mbali za kuadhimisha miaka 55 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964 zitakazofanyika katika maeneo yao kwani hizo ni sherehe zao kila mmoja ahakikishe anashiriki ipasavyo katika hatua zote.

IGP SIRRO AZINDUA RASMI CHAMA CHA WASTAAFU WA JESHI LA POLISI (TARPOA)

Mwenyekiti wa Chama cha Wastaafu wa Jeshi la Polisi (TARPOA) Kamishna Mstaafu CP Suleiman Kova (Kushoto), akimkabidhi zawadi Kamishna wa Kamisheni ya Ushirikishwaji wa Jamii Mussa Ali Mussa kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini, katika sherehe za Uzinduzi Rasmi wa chama hicho zilizofanyika mwishoni mwa juma katika bwalo la maafisa wa Polisi Oysterbay jijini Dar es salaam. Picha na Jeshi la Polisi.

Mgeni Rasmi Kamishna wa Kamisheni ya Ushirikishwaji wa Jamii CP Mussa Ali Mussa kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini, akiwaongoza aliyekuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi Mstaafu IGP Said A. Mwema (kulia) na kamishna mstaafu suleiman Kova ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Wastaafu wa Jeshi la Polisi (TARPOA) katika zoezi la kukata utepe wakati wa sherehe za Uzinduzi Rasmi wa Chama hicho zilizofanyika mwishoni mwa juma katika bwalo la maafisa wa Polisi Oysterbay jijini Dar es salaam. Picha na Jeshi la Polisi.
Baadhi ya Wastaafu wa Jeshi la Polisi ambao pia ni Wanachama wa Chama cha Wastaafu wa Jeshi hilo TARPOA wakifuatilia matukio mbalimbali yaliyokuwa yakiendelea wakati wa sherehe za Uzinduzi Rasmi wa Chama hicho kilichoanzishwa mwaka 2006 na aliyekuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi IGP Mstaafu Said Mwema. Picha na Jeshi la Polisi.

SHARIFU AWATAKA VIONGOZI WA CCM BAGAMOYO WASHIRIKIANE

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Bagamoyo Abduli Sharifu akizungumza katika semina ya siku mbili iliyoandaliwa na Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo ambayo imelenga kuwajengea uwezo watendaji wa CCM kata na makatibu wa Elima na Malezi.
...................................

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Bagamoyo Abduli Sharifu amewataka wanachama wa CCM wilayani humo kuwa na ushirikiano katika kutekeleza majukumu yao ili kukiletea maendeleo chama hicho.

Akizungumza katika semina ya siku mbili iliyoandaliwa na Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo ambayo imelenga kuwajengea uwezo watendaji wa CCM kata na makatibu wa Elimu na Malezi, Mwenyekiti Sharifu amesema siri pekee ya mafanikio ndani ya Chama ni ushirikiano katika kutekeleza majukumu.

Sharifu ameongeza kwa kusema kuwa,  Mwenyekiti wa CCM Taifa Dkt. John Magufuli anahimiza viongozi kujituma na kuzingatia maadili ya uongozi hivyo ni vyema kila kiongozi atekeleze wajibu wake katika nafasi yake aliyo nayo.

Aliwataka wanajumiya hao ambao wamepata semina ya uongozi na maadili kuyafanyia kazi yale waliyofundishwa katika semina hiyo ili kuleta maendeleo ndani ya jumuiya ya wazazi na chama kwa ujumla.

Alisisitiza kuwa, CCM wilaya ya Bagamoyo haitamvumilia kiongozi yeyote mzembe asietimiza wajibu na kwamba hatua zitachukuliwa dhidi ya viongozi wenye kuzembea kwenye nafasi zao.

Mwenyekiti huyo wa CCM wilaya ambe awali aliwahi kuwa Mwenyekiti wa jumuiya ya wazazi wilaya, amempongeza Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo Aboubakari Mlawa kwa kusimamia vizuri jumuiya hiyo na kuleta mabadiliko mbalimbali ya kimaendeleo.

Aidha, ametoa wito kwa jumuiya zote ndani ya chama kuhakikisha kuwa wanashirikiana na kuacha makundi katika kipindi cha utendaji kazi.

Alisema imezoeleka kuwa na makundi katika vipindi vya uchaaguzi lakini mara chaguzi zinapoisha ni vyema wanachama wote wakawa kitu kimoja ili kushirikiana kukijenga chama.

Alitumia nafasi hiyo kumtambulisha rasmi Katibu mpya wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Salum Mtelela ambae anachukua nafasi ya Kombo Kamote aliyestaafu kwa mujibu wa sheria.

Mwenyekiti huyo wa CCM wilaya, alimtaka Katibu anaeanza kazi katika wilaya hiyo kufanya kazi zake kwaa kuzingatia katiba ya CCM, Kanuni, Busara na miongozo mbalimbali iliyotolewa kwa mujibu wa sheria bila ya kumuogopa mtu yeyote.

Alisema Chama Cha Mapinduzi kina Dira inayowaongoza watendaji wote katika kutekeleza majukumu yao hivyo atakaekwenda kinyume katibu ya chama itamuhukumu.

Kwa upande wake Katibu wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Salum  Mtelela amesema anashukuru kwa mapokezi aliyoyapata na kwamba ameahidi kushirikiana na viongozi mbalimbali kwa lengo la kuimarisha chama ndani ya wilaya.

Amewataka viongozi na wanachama kwa ujumla kumpa ushirikiano ili CCM iendelee kuchukua ushindi katika chaguzi mbalimbali zinazokuja.
 
Katibu wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Salum Khalfani Mtelela akizungumza katika semina hiyo.

Kutoka kulia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aboubakari Mlawa, Katibu wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani, Juma Gama, Mwenyekiti wa CCM tawi la Tandika Bagamoyo, Katibu Mwenezi wilaya ya Bagamoyo, Francis Bolizozo, Mjumbe wa kamati ya utekelezaji jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo, Mariamu Hassan.