Monday, December 31, 2018

MKURUGENZI WA TIBA ATOA TAARIFA KWENDA KWA WAMILIKI WA MAABARA BINAFSI ZA AFYA KUHUSU UTEKELEZAJI WA SHERIA YA UMILIKI WA MAABARA BINAFSI ZA AFYA.

Mkurugenzi wa Tiba, Wizara ya Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima akisisitiza jambo katika mkutano na Waandishi wa Habari kuhusu utekelezaji wa sheria ya umiliki wa maabara binafsi za Afya.
.................................................


Dkt. Dorothy Gwajima, Mkurugenzi wa Tiba wa WAMJW ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Maabara Binafsi za Afya (Private Health Laboratory Board) (PHLB). amewatakia heri ya mwaka mpya 2019 na hongera wamiliki wa maabara binafsi za afya kwa kazi kubwa waliyofanya mwaka 2018 ya kushirikiana bega kwa bega na sekta ya afya katika kuhakikisha taarifa sahihi zinawafikia wananchi na wadau wote kokote waliko.

Katika kufikisha salaam zangu kwa wamiliki wa maabara binafsi, amewashukuru wamiliki hawa kwa kuchagua kuwekeza katika sekta ya afya nchini Tanzania, na kuwapongeza wale wote waliowekeza huku wakihakikisha wanafuata taratibu zote za kisheria za uwekezaji huo.

Aidha, amewakumbusha wamiliki wa maabara binafsi kuwa, umiliki huu unasimamiwa na sheria namba 10 ya mwaka 1997 inayowataka wamiliki wote kusajiliwa na kutambuliwa na PHLB kisheria. Hii ni hata kama maabara husika inajitegemea au iko ndani ya kituo cha kutolea huduma za tiba cha aina yoyote cha ngazi yoyote ile, maabara husika inatakiwa itimize matakwa ya kisheria.

Amesema  kufikia Septemba, 2018 PHLB ilikuwa inazitambua jumla maabara 641 zinazojitegemea na 719 zilizoshikizwa kwenye vituo vya tiba vya watu binafsi vya ngazi mbalimbali.

Katika utekelezaji wa majukumu yake, Bodi imeendelea kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa shughuli za maabara binafsi kama sheria inavyotaka, na kupitia utekelezaji huo imebaini wako baadhi ya wamiliki ambao, hawatimizi matakwa ya kisheria.


Kutotekeleza matakwa ya kisheria siyo tu kunaifanya maabara husika kuwa mbali na macho ya Bodi katika kuhakikisha usimamizi wa ubora wa huduma, bali kunamfanya mmiliki husika kukwepa wajibu wake wa msingi kwa serikali ikiwemo kulipa tozo na ada stahiki zitokanazo na biashara anayofanya na hii ni kukwamisha juhudi za Serikali katika kuwaletea wananchi maendeleo kulingana na mipango yake. Hili halikubaliki hata kidogo.

 Kanuni za kumiliki maabara binafsi zinataka mmiliki kutekeleza mambo makubwa yafuatayo;-

1. Kufuata utaratibu wa kusajiliwa (kwa maabara zinazojitegemea) na kufuata utaratibu wa kujiandikisha na kutambuliwa na Bodi husika kwa maabara ambazo zimesajiliwa pamoja na vituo vya tiba (zilizoshikizwa).
2. Kulipa ada stahiki kila mwaka ambazo ni ada ya uhakiki wa ubora wa huduma na ingine ni ada ya ukaguzi.


Kutokana na baadhi ya wamiliki wa maabara binafsi hususan zilizoshikizwa kutofuata maadili ya uwajibikaji kisheria, bodi imebaini kuwa, kufikia Septemba 2018, kati ya vituo vya tiba 1731 vya watu binafsi vyenye maabara ndani ni maabara 1012 (58%) tu ndiyo zilikuwa zimetimiza wajibu wake wa kujiandikisha kwenye Bodi ya Usimamizi wa Maabara Binafsi na kutekeleza matakwa yote ya kisheria kama nilivyoeleza hapo awali.

Ni kweli kwamba, vituo hivi vya maabara binafsi viko ndani ya vituo vya tiba ambavyo, vinasimamiwa na Sheria ya Usajili wa Vituo Binafsi (PHAB) lakini, hili haliondoi utekelezaji wa sheria ya PHLB yenye dhamana ya kusimamia maabara binafsi. Wizara inakubalina na hoja kuwa, vema sheria hizi zikajumuishwa, na tayari imeanza kufanyia kazi na wadau wote wanafahamu na wameshiriki hivyo, hii haiwezi ikawa ndiyo sababu ya kutowajibika kutekeleza sheria halali ambazo bado ziko hai.

Wizara kupitia Bodi husika imeendelea kuelimisha na kufafanua juu ya mamlaka tofauti za sheria hizi mbili, lakini bado baadhi ya wamiliki wa maabara binafsi wamekuwa wakikwepa tu kuwajibika kwa makusudi.

Aidha, leo hii, watendaji wa sekretarieti ya bodi ya PHLB kwa kushirikiana na sekretarieti ya PHAB na viongozi wa sekta ya afya ngazi zote wakiwemo OR TAMISEMI, Ofisi za Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya mbalimbali, tumehitimisha ziara ya kufuatilia utekelezaji wa shughuli za maabara binafsi za afya katika mikoa mbalimbali ukiwemo mkoa wa Dar es Salaam.

Kupitia ziara hii, tumechambua na kubaini kuwa, wamiliki wengi wasiotekeleza sheria ya umiliki wa maabara binafsi wanatokea miongoni mwa wanaomiliki maabara zilizoshikizwa yaani, zilizomo ndani ya vituo vya tiba ngazi mbalimbali. Aidha, katika kundi hili, wapo watu ambao, kimsingi huwezi kuwatarajia kutokana na elimu zao, kazi zao na Imani zao kwa jamii inayowazunguka (wao wanajijua). Hii haivumiliki kabisa.

Kwa kuwa nilikuwa mstari wa mbele kuwafikia wale wamiliki wa maabara binafsi walioripotiwa kuwa eti wameshindikana, nimewafikia baadhi yao na kusikiliza hoja zao na kubaini kuwa, hazina mashiko kabisa. Eti, hoja yao ya msingi ni kuwa, wanapolipa kusajili kituo cha tiba huwa wanadhani kuwa, tayari na maabara imejumuishwa humo.

 Utetezi huu siyo wa kweli kwa kuwa, sheria ya kusimamia umiliki wa vituo binafsi vya tiba iko wazi na ina bodi yake na hii ya kusimamia umiliki wa maabara binafsi nayo iko wazi na ina bodi yake na siku zote wamekuwa wakielimishwa na mimi nimeshiriki mara nyingi kutoa elimu hiyo.

Nimeona leo nirudie tena kufafanua kuwa, bodi ya usajili wa vituo vya Tiba inajukumu lake na haiingiliani kabisa na sheria ya bodi ya usimamizi wa kumiliki maabara binafsi.

Kwa kuwa wako wamiliki wa maabara binafsi ambao, wameamua kuamini kwenye kufuatiliwa kila siku, sasa ufuatiliaji na uelimishaji uliokwisha fanyika awali unatosha, wakati wa kuelewa somo umepita sasa ni saa ya KAZI TU !. Imefika zamu ya wamiliki wa maabara binafsi waliokuwa hawajatekeleza wajibu wao wa kumiliki maabara hizo kisheria kuchukua hatua mara moja za kwenda kutimiza wajibu wao bila shurti tena pasipo kuendelea kuisababishia Serikali gharama za ziada za kuwafuatilia. 


Hivyo, ifikapo tarehe 15/1/2019 ambaye hajatimiza wajibu wake ni kwamba, atafungiwa bila taarifa ya ziada na kushtakiwa. Iwapo kuna ambaye anayejiandaa kutotimiza matakwa hayo, bora atumie muda huu kufunga ofisi yake kabisa ili kuepuka usumbufu usio wa lazima. Hata hivyo, kufunga ofisi hakutamuepusha mvunja sheria yeyote yule kuwajibika kwa uvunjifu wa sheria alioufanya awali.

Naomba ifahamike kuwa, kutimiza wajibu wa matakwa ya kisheria kwa wamiliki husika wa mabaara binafsi ni pamoja na;-

1. Kila mmiliki kuhakikisha amekidhi vigezo vyote vya kumiliki maabara binafsi kama ambavyo amekuwa akielekezwa na wataalamu walioko kila halmashauri na mikoa husika, pamoja na

 
2. Kuhakikisha amelipa ada na tozo stahiki zikiwemo malimbikizo ya nyuma na faini zote stahiki.

 
3. Amepata risiti halali za malipo hayo

 
4. Anaendelea kulipa tozo stahiki kila mwaka ili, kuwezesha bodi husika kutimiza wajibu wake wa kufanya uhakiki wa ubora wa huduma kwa kila kituo kila mwaka na kufanya ukaguzi maalumu wa vituo husika kama vinaendelea kuwa katika viwango stahiki kama siku vilipopewa kibali cha kutoa huduma husika.


Kwa kuwa tumebaini kuwa, wasiofuata sheria wanatoa huduma bubu mita chache tu toka serikali za mitaa, Bodi imeendelea kuimarisha ushirikiano wake na vyombo vyote vya Serikali ngazi zote kuanzia OR TAMISEMI na ngazi zake zote za Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na sasa, Bodi inaandaa orodha ya maabara binafsi nchi nzima na itaweka katika gazeti la Serikali na vyombo vya habari na itasambaza kwa wadau wote.

Hivyo, yeyote ambaye hayumo katika orodha hiyo asithubutu kutoa huduma hizo maana, mamlaka za Serikali za mitaa zitambaini na taarifa zitafika mahali sahihi mara moja na hatua kali zitachukuliwa.
Aidha, natoa wito kwa mamlaka zote za Serikali ngazi zote tuendelee kupeana taarifa kwa haraka zaidi na kujipanga vema zaidi katika kuhakikisha hakuna mvunja sheria anathubutu kutoa huduma za kijamii bila kibali.


Ni matumaini yangu kuwa mtatumia umahiri wenu katika kuhakikisha ujumbe huu unawafikia wadau wote kwa usahihi. Aidha, nina Imani kuwa, wadau husika sasa wataacha utetezi dhaifu na watatimiza wajibu wao mara moja.

Mwisho, naomba kuwakumbusha wadau wote sekta ya afya kuwa, katika kujenga taifa letu, ni budi kila mmoja atimize wajibu wake ili, tuongeze kasi, kwa kuwa hakuna mtazamaji bali wote tuna majukumu na wajibu kamili.

Kaimu Msajili wa Bodi ya Maabara Binafsi za Afya akijibu maswali ya Waandishi wa habari wakati wa mkutano na Waandishi wa Habari uliohusu utekelezaji wa sheria ya umiliki wa maabara binafsi za Afya.

Wajumbe wa Sekretariet ya Maabara binafsi pamoja na kamati ya Afya ya msingi za manispaa za jiji la Dar es salaam wakifuatilia maelekezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Tiba, Wizara ya Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima kuhusu utekelezaji wa sheria ya umiliki wa maabara binafsi za Afya katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es salaam.

ASKOFU KANISA KATOLIKI ZANZIBAR AITAKA JAMII KUWALEA WATOTO KATIKA MAADILI MEMA

Na Masanja Mabula -PEMBA

 ASKOFU wa kanisa katoliki Zanzibar Agustino Shao ameitaka jamii kuwalea watoto katika maadili mema , na kuhakikisha wanawalinda na vikundi viovu ili kuwafanya wawe nashuhuda wa ukweli.

Amesema ni jukumu la kila mzazi na mlezi kuhakikisha mtoto wake anaishi kwa hofu ya mungu kwa kufuata mafundisho ya dini.

 Askofu shao, ameyasema hayo wakati akizungumza na watoto wa haki na amani katika maadhimisho ya kumbukumbu ya watoto mashahidi iliyofanyika kitaifa  katika kanisa kuu wete pemba.

Amesema wazazi wanajukumu la kumtayarisha mtoto kuweza kutambua leo yake paamoja na kesho yake, pamoja na kuwapatia elimu ambayo ndio mkombozi wao.

“Kila mzazi analojukumu la kuhakikisha mtoto wake anapata malezi bora ambayo yatamsaidia kuishi kwa hofu ya Mungu na kujiepusha na makundi maovu ”alifahamisha.

 Aidha amelaani tabia ya baadhi ya wazazi ya kuwakosesha haki ya elimu watoto wa kike , na kusema wote wanahaki ya kupata elimu.
Amesema mipango ya Mungu iko juu kuliko ya mwanadamu , na kuitaka jamii kumtegemea Mungu katika kazi zao za kila siku.

Kwa upande wao walezi wa watoto wa haki na amani akiwemo Frola Vicent John kutoka Pemba na Jenister Mvula kutoka Unguja wamesema changamoto kubwa inayowakabili ni wazazi kutokuwa na mwamko wa kuwaruhusu watoto kushiriki utume.

Wamesema pamoja na juhudi wanazochukuwa kuwafuatilia watoto, lakini bado baadhi ya wazazi wanaonekana kuwa ni kikwazo katika kuwahimiza watoto kushiriki mafundisho.

“Tunapa changamoto kutoka kwa wazazi kwani baadhi yao wanakwamisha  mipango yetu kwa kutowahimiza watoto wao kushiriki mafundisho “alisema Frola.

Watoto wa haki na amani Judith Damian Modest na Mikael Costa Gerevas wameitaka kuwalinda watoto dhidi ya matendo ya udhalilishaji ili waishi kwa amani na upendo.

Mikael ameiomba serikali kuwachukulia hatua wanahusika na vitendo vya kuwabaka watoto wadogo, ili kuwalinda na kuwafaanya watoto waishi kwa amani na upendo kutoka kwa wazazi wao.

Maadhimisho hayo ya kumbukumbu ya watoto mashahidi , zaidi ya watoto mia moja na ishirini kutoka Unguja na Pemba wameshiriki.

MAGAZETI YA LEO DESEMBA 31, 2018.

TFS YATOA UFAFANUZI WA UKAMATAJI WA MAZAO YA MISITU

Sunday, December 30, 2018

MLAWA ATOA WITO KWA WAZAZI BAGAMOYO.

  Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aboubakari Mlawa, akizungumza wakati wa kufunga semina ya siku mbili ya watendaji wajumuiya hiyo na makatibu Elimu, Malezi na Mazingira wa kata iliyofanyika Nianjema Bagamoyo, kulia ni Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Bagamoyo, Abduli Sharifu na kushoto ni Katibu wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani, Juma Gama.
..............................

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aboubakari Mlawa amewataka wazazi na walezi kuhakikisha wanawaandikisha watoto wenye umri wa kuanza shule ya msingi ili wapate haki yao ya kupata elimu huku wale wanaotakiwa kujiunga na kidato cha kwanza wapelekwe kwenye shule walizopangiwa haraka iwezekanvyo.

Mlawa ameyasema hayo leo Desemba 30, 2018 wakati wa kufunga semina elekezi ya siku mbili kwa watendaji wa Jumuiya ya wazazi, kata pamoja na makatibu Elimu na Malezi wa kata iliyofanyika kata ya Nianjema Halmashauri ya Bagamoyo.

Alisema Jumuiya ya wazazi pamoja na majukumu mengine ni pamoja na kusimamia Mazingira na Malezi pamoja na maadili kwa watoto hivyo ni lazima jumuiya ihakikisha inasimamia vyema majukumu hayo na kuwahimiza wazazi na walezi kutekeleza hilo.

Aliongeza kwa kusema kuwa licha ya kuwa wilaya ya Bagamoyo ni wilaya inayoongoza kitaaluma katika mkoa wa Pwani, lakini pia ndio wilaya ambayo watoto wengi hawaandikshwi kuanza darasa la kwanza na kuendelea na kidato cha kwanza.

Aidha, ametumia fursa hiyo kusisitiza umoja na mshikamano ndani ya jumuiya kuanzia ngazi ya kata mpaka wilaya kwani hiyo ndio siri ya mafanikio yanayopatikana ndani ya jumuiya ya wazazi.

Alisema jumuiya hiyo wilaya iko imara na kwamba haiwezi kutetereka kwakuwa inafanya kazi kama timu moja na hivyo inaweza kupambana na changamoto mbalimbali zinazoweza kujitokeza kwaajili ya kukwamisha maendeleo.

Mwenyekiti huyo wa jumuia ya wazazi aliwaataka washiriki wa semina hiyo kutumia mafunzo hayo kama njia ya kuongeza uwajibikaji kwa ufanisi zaidi na kuongeza wigo wa wanachama ndani ya jumuia na chama kwa ujumla.

Alisema jumuiya ya wazazi ikitekeleza majukumu yake ipasavyo ndio njia pekee ya kuipatia ushindi CCM katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka 2019 na hata ule wa Rais, madiwani na wabunge 2020.

Aliendelea kusema kuwa,  jumuiya hiyo inatekeleza majukumu yake kwa weledi katika kusimamia maadili kila mmoja kwenye eneo lake anapaswa kuhakikisha anapinga vitendo vya rushwa ili kila hatua inayofikiwa katika chaguzi mbalimbali ifikiwe kwa haki na uadilifu.

Kwa upande wake Katibu wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani Juma Gama ametoa wito kwa wana jumuiya kuinua uchumi wa mmoja mmoja, na jumuiya kwa ujumla kwa kuanzisha miradi mbalimbali ikiwemo ya ufugaji wa nyuki ili kujiletea maendeleo.

Alisema kiongozi atakapojiimarisha kiuchumi ataweza kutekeleza majukumu yake ipasavyo na kujenga uaminifu katika jamii kwakuwa hatapita kuomba omba.

Alisema kama jumuiya ya wazazi inapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika kujiinua kiuchumi ili utekelezaji wa majukumu ya jumuiya na chama uende kwa ufanisi na sio kwa utapeli.

Aidha, aliwaonya wale wote waliochaguliwa ndani ya jumuiya na wanashindwa kutekeleza majukumu yao ni vyema sasa sheria ikachukua mkondo wake kwa kumsimamisha ili nafasi yake izibwe na mtu mwingine.

Alisema uongozi ni uwajibikaji hivyo yule ambae hawezi kuwajibika anastahili kuwekwa pembeni ili watu wenye nia ya dhati na jumuiya hiyo waweze kusonga mbele.

Washiriki wa semina hiyo wamesema wamefaidika na kile walichofundishwa na kwamba wataleta mabadiliko kwenye maeneo yao.

Katika semina hiyo ambayo imeandaliwa na Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo na kukusanya washiriki kutoka kata zote za wilaya hiyo wamejifunza mipaka ya uongozi, uandaaji wa mihutasari, Barua, Taarifa na kazi pamoja na mambo mbalimbali yanayohusu itifaki ndani ya Chama Cha Mapinduzi.
 
Muwezeshaji Hassan Tambaza akitoa mafunzo kwa washiriki
 
Muwezeshaji Mwinyi Sangaraza akitoa mafunzo kwa washiriki

 Katibu wa Jumuiya ya wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aeshi akizungumza na washiriki katika semina hiyo.

Washiriki wakifuatilia mada zilizowasilishwa katika semina hiyo
 
Washiriki wakifuatilia mada zilizowasilishwa katika semina hiyo
   Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo, Aboubakari Mlawa, (kulia) na Katibu wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani, Juma Gama (kushoto) wakifuatilia semina hiyo.

WAZIRI HASUNGA AZIAGIZA BODI ZA MAZAO NCHINI KUWASAJILI WAKULIMA WOTE.

Waziri wa Kilimo, Mhe. Japhet Hasunga (Mb) akisisitiza jambo wakati akizungumza na Wenyeviti wa Bodi za Mazao pamoja na Wakurugenzi wa Bodi hizo za Mazao, kwenye ukumbi wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Jijini Dodoma jana tarehe 29 Disemba 2018
.......................................................


Waziriwa Kilimo, Mhe. Japhet Hasunga (Mb)  amewaagiza Wakurugenzi wa Bodi za Mazao kuanza mara moja zoezi la kuwatambua na kuwasajili wakulima wa mazao yote nchini lengo likiwa kuwatambua ili kupanga mipango sahihi yenye kuongeza tija na uzalishaji katika mazao yote.


Ametoa agizo hilo jana tarehe 29 Disemba 2018 wakati akizungumza na Wenyeviti wa Bodi za Mazao pamoja na Wakurugenzi wa Bodi hizo za Mazao, kwenye ukumbi wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Jijini Dodoma.


Mhe. Hasunga amesema ili kuongeza tija na uzalishaji katika Sekta ya kilimo na kuandaa mipango madhubuti ya kuendeleza mazao yote ni vyema kuwatambua Wakulima wote nchini na kuongeza kuwa Wakulima wa zao la korosho wametoa funzo kubwa kwa Wizara yake kufanya jambo kama hili katika mazao mengine hapa nchini.


Itakumbukwa kuwa wiki tatu zilizopita, Waziri Hasunga alitoa agizo kwa Bodi ya Korosho agizo kuandaa daftali maalumu la kuwatambua Wakulima wa korosho kote nchi ambapo moja ya taarifa ambazo zitajumuishwa katika daftali hilo ni pamoja na

Jina Kamili la Mkulima,  Mkoa, Wilaya, Kata na Tarafa anayotoka.


Mambo mengine ni pamoja na Kitongoji, Mtaa au Jina la Kijijini anapotoka, mahali lilipo shamba pamoja na ukubwa wa shamba lake.


Waziri Hasunga ameongeza kuwa mipango sahihi ya kuwaendeleza Wakulima kuanzia kwenye kilimo chenyewe hadi kufikia katika hatua ya kuvuna, kuhifadhi na kulifikia soko ni vyema kuwa na mfumo maalumu wa kanzi data (Database) ya kuwafahamu ili kushughulikia mahitaji yao kisasa na kwa haraka zaidi.


Waziri Hasunga alienda mbali na kushauri matumizi ya TEHAMA na ya Mfumo wa GPS ili kuboresha daftari hilo kwa lengo la kuboresha uwekaji wa taarifa za Wakulima na

maeneo wanayotoka Wakulima kwa usahihi zaidi.


“Tumepata changamoto kadhaa wakati wa kuwahakiki Wakulima wa korosho katika mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na Ruvuma na kama Bodi ya Korosho ingekuwa makini kuandaa daftari la Wakulima zoezi la uhakiki lingekuwa rahisi, kwa ajili hiyo niliwaagiza Bodi ya Korosho kukamilisha zoezi hili mpaka Mwezi Machi, 2019 na Bodi za Mazao zilizobaki ukiacha Bodi ya Tumbaku ambao wao tayari walishafanya hivyo, kukamilisha Mwezi June, 2019”. Amekaririwa Mhe. Hasunga.


Waziri ameitisha kikao maalumu na Viongozi wa Bodi za Mazao, Wakala na Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Kilimo kwa lengo la kuboresha mikakati na kuongeza ufanisi katika utendaji wa Wizara pamoja na kujitathmini kabla ya kufikia nusu mwaka wa utekelezaji wa vipaumbele vya bajeti ya Wizara ya mwaka 2018/2019 ili kujipanga kwa ajili ya utekelezaji wa bajeti ya Wizara ya kilimo ya mwaka ujao wa 2019/2020.


Bodi za Mazao zilizoshiriki mkutano huo ni pamoja na Bodi ya Korosho, Bodi ya Pamba, Bodi ya Mkonge, Bodi ya Pareto, Bodi ya Chai, Bodi ya Kahawa, Bodi ya Tumbaku, Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko na Bodi ya Sukari.


Wakala zilizoshiriki ni pamoja na  Wakala wa Taifa wa Mbolea (ASA) Wakala wa Wakulima Wadogo wa Chai (TSHTDA).


Taasisi nyengine za Wizara ya Kilimo zilizoshiriki ni pamoja na Taasisi ya Udhibiti wa Mbegu (TOSCI), Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO), Taasisi ya Utafiti wa Viuatilifu vya Ukanda wa Kitropiki (TPRI), Mfuko wa Pembejeo za Kilimo (AGITF), Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA),


Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea (TFRA), Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI), Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Kampuni ya Taifa ya Mbolea (TFC) na Bodi ya Leseni za Maghala.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe akifatilia mkutano wa Wenyeviti wa Bodi za Mazao pamoja na Wakurugenzi wa Bodi hizo za Mazao,  uliongozwa na Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) kwenye ukumbi wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Jijini Dodoma jana tarehe 29 Disemba 2018.
 
Wenyeviti wa Bodi za Mazao pamoja na Wakurugenzi wa Bodi hizo za Mazao,  wakifatilia mkutano wa kazi ulioongozwa na Waziri wa Kilimo, Mhe. Japhet Hasunga (Mb) kwenye ukumbi wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Jijini Dodoma jana tarehe 29 Disemba 2018.


(Picha Zote Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo)

CHAHUA WAKUMBUKA HOFU YA RIDHIWANI KIKWETE KUHUSU MAJI

Wakazi wa kitongoji cha Chahua, kata ya Bwilingu Halmashauri ya Chalinze wilayani Bagamoyo wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wao mara baada ya zoezi la usafi la kila mwisho wa mwezi ambapo wakazi hao walijumuika kwenye Zahanati yao kwaajili zoezi hilo, Picha na Omary Mngindo.
 ..............................................................


Na Omary Mngindo, Chahua 


MWENYEKITI wa Kitongoji cha Chahua, Kata ya Bwilingu Halmashauri ya Chalinze mkoani Pwani Rashid Maisha, amekumbuka hofu iliyooneshwa na Mbunge wao Ridhiwani Kikwete, aliyeionesha wakati ikitolewa ahadi ya upatikanaji wa maji jimboni humo, ifikapo Des 31 mwaka huu.

Maisha ametoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki, akizungumza na mwandishi wa habari hizi muda mfupi mara baada ya kumalizika kwa zoezi la usafi wa mwishoni mwa mwezi, ambapo wakazi hao walijumuika kwenye jengo la Zahanati kwa ajili ya zoezi hilo.

Alisema kwamba, kwenye mkutano uliofanyika hivi karibuni mbele ya Makamu wa Rais Mama Samoa Suluu Hassani katika viwanja vya Polisi Bwilingu, Mtendaji Mkuu wa DAWASA lipotoa ahadi ya kupatikana kwa maji Des 31, Ridhiwani alionesha hofu ya kukamilika kwake, huku akimuomba Mtendaji huyo wafanye ziara ya kukagua namna ya utekelezwaji wa mradi unavyokwenda.

Alisema kwamba mradi huo mpaka sasa hauna matumaini ya kukamilika hivi karibu, ambapo wananchi wakiendelea kutaabika kupata huduma hiyo, huku matumaini ya kumalizika kwa adha hiyo yakigonga mwamba.

"Wakati Mbunge wetu Ridhiwani Kikwete akionesha hofu ya kukamilika kwa mradi, wengi wetu hatukumuelewa hiyo imetokana na ahadi hiyo kutolewa mbele ya Makamu wa Rais Mama Samia, lakini leo tumeamini, hofu yake imekuwa na mashiko, mradi hauna dalili za kukamilika leo wala kesho," alisema Maisha.

Kwa upande wao wakazi wakazi Mwanahamisi Lomano na Mariana Mtamani walielezea adha ya maji wanayokabiliana nayo huku wakisema kwamba mara ya mwisho kupata huduma hiyo ilikuwa mwezi wa Novemba na kuwa mpaka sasa hawana maji.

"Mpaka leo tuna mwezi mmoja hakuna maji, wananchi tunaendelea kuteseka kwa kutafuta maji kwenye malambo yasiyo safi na salama, hii kero si huku Chahua tu hata kwa wenzetu wa Chalinze pia wanakabiliwa na adha kama hii," alisema Lomano.

Mtamani aliiomba Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Chalinze (CHALIWASA) kuhakikisha wanaboresha upatikanaji wa huduma hiyo, ili wananchi waondokane na adha hiyo ya miaka kwa miaka.

MAJALIWA AWASILI MTWARA AKIWA NJIANI KWENDA RUANGWA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Gelasius Byakanwa wakati alipowasili kwenye uwanja wa ndege wa Mtwara akiwa njiani kwenda Ruangwa, Desemba 30, 2018.
 

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Mtwara, Dkt. Jilly Elibariki Maleko  wakati alipowasili kwenye uwanja wa ndege wa Mtwara akiwa njiani kwenda Ruangwa, Desemba 30, 2018. Wapili kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Gelasius Byakanwa, watatu kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi na kushoto ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi, Bibi  Rehema Madenge.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akislimiana na viongozi wa mkoa wa Mtwara wakati alipowasili kwenye uwanja wa ndege wa Mtwara akiwa njiani kwenda Ruangwa, Desemba 30, 2018. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu

RAIS DKT.JOHN POMBE MAGUFULI AMJULIA HALI MAMA YAKE MZAZI BIBI. SUZANA MAGUFULI ANAYEPATIWA MATIBABU JIJINI DAR ES SALAAM

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Wasaidizi wake wakimuombea Mama yake Mzazi Bibi. Suzana Magufuli anayepatiwa Matibabu  Jijini Dar es Salaam. Desemba 30, 2018. 

Bibi Suzana Magufuli anasumbuliwa na ugonjwa wa Kiharusi ambapo amekuwa akipatiwa matibabu kwa takribani miezi mitatu sasa.

PICHA NA IKULU

TAARIFA KWA UMMA KUHUSU AKAUNTI HALALI ZA MITANDAO YA KIJAMII YA INSTAGRAM NA TWITTER ZA KANGI ALPHAXARD LUGOLA, WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI

Baada ya kuwepo kwa akaunti feki ya Mtandao wa Kijamii wa Instagram ambao ulikua unatoa taarifa mbalimbali kwa jamii kuhusu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Wizara kwa ujumla, kuanzia leo Disemba 30, 2018, Wizara inatangaza rasmi kwa jamii, akaunti halali zilizosajiliwa kwa jina la Mheshimiwa Waziri Kangi Lugola, kama ifuatavyo;
  • officialkangi_lugola (Instagram)
  • @kangi_lugola (Twitter)
Taarifa zote zitakazotolewa katika kurasa za akaunti hizi zitakua sahihi.
Kwa hatua hiyo, Wizara inaendelea kutoa onyo kali kwa mtu yeyote atakayejihusisha kwa kutumia jina la Kangi Lugola kusajili akaunti yoyote na kutoa taarifa za Waziri huyo kupitia akaunti feki hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.

Aidha, Wizara inawaomba Watanzania waendelee kupata taarifa zake zaidi kupitia tovuti yenye anuani; www.moha.go.tz na twitter ya Wizara kwa akaunti ya Msemaji Mambo ya Ndani.