Thursday, February 27, 2020

DC BAGAMOYO APIGA MARUFUKU NGOMA ZA VIGODORO

Image may contain: 1 person

NA VICTOR MASANGU, BAGAMOYO

MKUU wa Wilaya ya Bagamoyo Zainabu Kawawa ambaye pi ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama (KUU) amepiga marufuku ngoma  na miziki ambayo inafanyika nyakati za usiku bila utaratibu  maarufu kama ‘Vigodoro’ kwani zimekuwa zikichangia kwa kiasi kikubwa mmomonyoko wa maadili kwa wananchi.


Agizo hilo amelitoa  wakati akizungumza na wananchi wa Kata ya Nianjema, wadau wa maendeleo pamoja na wakuu mbali mbali wa idara wakati wa mkutano wake wa kikazi kwa ajili ya kusikiliza kero na changamoto mbali mbali za wananchi kwa lengo la kuweza kuzitafutia ufumbuzi pamoja na kuweka mipango  madhubuti kwa ajili ya kuleta chachu ya maendeleo.


Zainabu alisema kwamba  katika baadhi ya maeneo ya Wilaya yake kumekuwepo  wimbi la ngoma ambazo zinachezwa nyakati za usiku na kupelekea kero na usumbufu mkubwa kwa watu wengine hivyo ameamua kuchukua hatua ya  kupiga marufuku hali hiyo kwa lengo la kuondokana na mambo mbali mbali ambayo yamekuwa yakijitokeza hasa katika wakati wa usiku.


“Kuanzia leo katika mkutano huu napenda kusema napiga marufuku kabisa mambo ya vigodoro vya usiku kwani vimekuwa ni kero sana na vinachangia kwa kiasi kikubwa katika kuvunja maadili ya Mtanzania na kwamba katika hili nitahakikisha ninalisimamia kwa ukaribu mno ili kukomesha kabisa kuwepo kwa hali hii katika Wilaya ya Bagamoyo,”alifafanua Zainabu.


Aidha Mkuu huyo alibainisha kwamba wananchi wa Bagamoyo kwa sasa wanatakiwa kubadilika na kuwa na mtazamo chanya kwa kushiriki kikamilifu katika shughuli mbali mbali za miradi ya maendeleo kuliko kutumia muda wao mwingi katika kukesha nyakati za usiku wakicheza ngoma ambazo hazina faida yoyote katika Taifa la Tanzania.


“Mimi kikubwa ninachotaka kuwaambia hasa wananchi wa Wilaya ya Bgamoyo tuachane kabisa na kujikita zaidi katika kukesha kwenye vigodoro,  ni vyema zaidi mkatumia fursa mbali mali zilizopo mkajishughulisha katika shughuli za kujipatia kipato ili kuweza kuondokana na  wimbi la umasikini hivyo ni rai yangu wote tukashirikiana katika kuleta maendeleo na sio kukesha kwenye vigodoro ambavyo ni havina faida yoyote ile,”alisema Zainabu.


Pia Mkuu huyo wa Wilaya alifafanua kwamba mtu yoyote ambaye anahitaji kufanya shughuli yake ya usiku ni lazima apatiwe kibali maalumu kutoka katika Ofisi yake kwa kuzingatia sheria na utaratibu ambao utakuwa umewekwa,ili kuhakikisha mambo yote ambayo yanakuwa yanajitokeza nyakati za usiku ikiwemo masuala ya  uhalifu  na wizi yanakomeshwa kwa kiasi kikubwa.


Katika  hatua nyingine ametoa onyo kali kwa wale wote ambao watabainika kukiuka agizo lake ambalo amelitoa na kwamba atahakikisha anawachukulia hatua kali za kisheria wale wote ambao watabainika bado wanaendeleo kinyemela  kujihusisha na masuala ya kupiga ngoma za usiku na vigodoro bila ya kuwa na kibali maalumu.


Nao baaadhi ya wananchi ambao hawakuta kutaja majina yao walimpongeza Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo kwa hatua ambayo ameifanya ya kupiga marufuku kabisa mambo ya vigodoro hasa katika nyakati za usiku kwani yamekuwa ni tatizo kubwa kutokana na kuwepo kwa matukio mbali mbali ambayo yanasabisha momonyoko wa maadili hasa kwa vijana.


“Kwa kweli sisi kama wananchi wa Wilaya ya Bgamoyo hili agizo la Mkuu wetu kupiga marufuku ngoma za usiku maarufu vigodoro sisi tunamuunga mkono kwa asilimia mia moja kwani imekuwa ni kero sugu ya siku nyingi na wakati mwingine yani watu hatulali kabisa na kingine kuna baadhi ya matukio ambayo yanafanyika hivyo kwa hatua hii itaweza kusaidia kuondoa na kupunguza kabisa changamoto amabzo zimekuwa zikijitokeza katika maeneo ambayo tunaishi,”walisema.


Kwa upande wake mmoja wa wadau wa maendeleo ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Nianjema Abdul Pyalla, alisema kwamba suala hilo la vigodoro  ni kweli limekuwa ni kero kubwa kwa wananchi hivyo atahakikisha anashirikiana bega kwa bega na Mkuu wa Wilaya  pamoja na wananchi husika katika mitaa mbali mabli kwa lengo la kuwaelimisha zaidi kuhusu umuhimu wa kutumia muda wao katika shughuli za maendeleo kuliko kukesha kwenye ngoma.


Baadhi ya Wananchi wa Wilayani Bagamoyo wakiwa wametulia kwa makini kumsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo ambaye aliitisha Mkutano maalumu kwa ajili ya kuzungumzia mambo mbali mbali ya maendeleo kwa wakazi wa kata ya Njia njema pamoja na kuwasikiliza changamoto zao. (PICHA NA VICTOR MASANGU)

Wednesday, February 26, 2020

MGALU ATAKA UMEME VIJIJINI UONGEZE UFAULU KWA WANAFUNZI.

NA HADIJA HASSAN, LINDI.

NAIBU Waziri wa Nishati Subira Mgalu ametoa Rai kwa vijiji vyote ambavyo tayari vimeunganishwa na huduma ya Umeme, kupitia Mradi wa Umeme Vijijini (REA) kuitumia fursa hiyo kuboresha ufaulu pamoja na kuinua kiwango cha elimu katika Maeneo yao.

Mgalu aliyasema hayo alipofanya ziara ya siku moja katika Wilaya ya Liwale Mkoani Lindi kwa lengo la kukagua maendeleo ya Mradi huo wa Umeme vijijini (REA) pamoja na kuwasha umeme katika vijiji vya Naluleo, Makata na Mengele Wilayani humo.

Akizungumza na wananchi, Walimu pamoja na Wanafunzi baada ya kuwasha umeme katika Shule ya Msingi Naluleo, Mgalu alisema ni mategemeo ya Serikali kuwa baada ya umeme kufika katika maeneo yao utaboresha na kuongeza kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi kutokana na mazingira wezeshi ya kusoma na kujifunzia muda wote.

Aidha, Mgalu pia aliwaasa wanafunzi wa kike hapa Nchini kuepuka vishawishi kwa vijana wakiume pamoja na kuwataka walimu pamoja na Wazazi kuwa walinzi namba moja wa wanafunzi hao wakike kuhakikisha hawakatishi masomo yao kwa kupata ujauzito.

“Niwaombe sana hii sio kazi ya mzazi au mwalimu peke yake, nikazi yetu sote tunapomuona mtoto wa kike anafanya vitendo hivyo tumkemee, sisi walimu tuwe chachu hasa walimu wa kiume inatia uchungu kuona mwanafunzi wa kike anapata ujauzito kisha mwalimu ndio anahusishwa iwe ni ya kweli au kwa kusingiziwa hiyo sio sawa” alisema Mgalu.

Nae Mkuu wa Wilaya ya Liwale Sara chiwamba alisema kuwa Swala la kutokomeza mimba kwa wanafunzi ni miongoni mwa mambo yanayopewa kipaumbele katika Mkoa huo wa Lindi hasa kupitia kampeni ya “tumsaidie akue asome mimba baadae” yenye lengo la kumfanya mtoto wa kike atimize ndoto zake.

Kwa upande wake Abdull Mohamdi mwanafunzi wa darasa la sita katika shule ya Msingi Naluleo alisema kuwa upatikanaji wa umeme huo utakuwa mkombozi kwa walimu na wanafunzi hasa wakati wa kujiandaa na mitihani kuweza kujisomea nyakati za usiku.

“Baada ya umeme huu sasa wanafunzi tutakuwa na muda wa kutosha wa kuweza kujisomea kwa sababu hatutakuwa na shida tena ya kutafuta nishati ya umeme kama zamani “ alieleza.

DC BAGAMOYO KUFUATILIA FEDHA ZA TASAF KWA KAYA MASIKINI.

Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Zainabu Kawawa (kati kati) akizungumza na wananchi wa kata ya Nianjema hawapo pichani katika mkutano wa hadhara ambao aliuandaa kwa lengo la kusikiliza kero na changamoto za wananchi hao.
 ...............................................


NA VICTOR MASANGU, BAGAMOYO.

BAADHI ya wazee wanaoishi katika kaya masikini na mazingira magumu  Wilayani Bagamoyo Mkoa wa Pwani wameiomba serikali ya awamu ya tano kuingilia kati sakata la kero yao kubwa ya kuonewa kwa  kipindi kirefu kutokana na  kutopatiwa fedha ambazo zinatolewa na mfuko wa maendeleo ya jamii (TASAF) kwa ajili ya kujikimu kimaisha pamoja na kuanzisha miradi midogo midogo.


Hayo yalibainisha wakati wa mkutano wa hadhara ambao umeandaliwa na Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Bi Zainabu Kawawa kwa wananachi wa Kata ya Nianjema kwa lengo la kusikiliza kero na changamoto mbali mbali zinazowakabili ili kuzitafuatia ufumbuzi pamoja na kuweka mikakati ya kuleta maendeleo kwa wananchi kwa ushirikiano wa serikali na jamii kwa ujumla.


Aidha mmoja wa wazee hao akizungumza kwa  niaba ya wezake wanaoishi katika kaya masikini Ole Shamba alisema kwamba wamekuwa wakipata usumbufu mkubwa katika suala zima la upatikanaji wa fedha kutoka TASAF hivyo wanajikuta maisha yao yanakuwa ni magumu kutokana na kukosa mahitaji muhimu wao na familia zao.


“Kwa kweli huu mpango kiukweli unatusumbua sana na leo hii kwa kuwa amekuja Mkuu wetu wa Wilaya Zainabu Kawawa tumeona ni bora tuseme kilio chetu ambacho kimekuwa ni kero kubwa ya siku nyingi maana hata sasa nimesahau kutokana na kipindi kimekuwa ni kirefu sana na ukizingatia taratibu zote tumeshazikamilisha sasa nashindwa kuelewa kwa hiyo tunaomba sana serikali yetu itusaidia katika suala hili,”aslisema Shamba.


Aidha katika hatua nyingine wazee hao walimpongeza Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo kwa kuwa na utaratibu wa  kufanya mikutano na wananchi wake kwa lengo la kusikiliza changamoto zinazowakabili na kumuomba alichukue suala hilo kwa uzito mkubwa ili fedha zote ambazo zinatolewa ziweze kuwafikia walengwa na sio vinginevyo.


Kwa upande wake MKUU wa Wilaya ya Bagamoyo Zainabu Kawawa baada ya kusikiliza kilio hicho ameahidi kulivalia njuga suala hilo na kuwaagiza watendaji wa TASAF kuhakikisha fedha zote zinazotolewa zinawafikia walengwa kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa bila ya ubaguzi na upendeleo  na kuachana kabisa na vitendo vya  kufanya ubadhilifu kwa maslahi yao binafsi kwani atakayebainika atachukuliwa hatua kali za kisheria.


Pia ,Mkuu huyo alibainisha kwamba lengo kubwa la serikali ya awamu ya tano ni kuhakikisha inawaletea wananchi maendeleo kupitia miradi mbali mbali na mifuko ambayo imeanzishwa hivyo atahakikisha kwamba wale walengwa wote ambao wanaishi katika mazingira magumu pamoja na kaya ambazo ni masikini wanawekwa katika utaratibu wa kusaidiwa fedha  kwa kuzingatai vigezo mbali mbali ambavyo vimetolewa na TASAF.


“Kwa kweli katika hili jambo mimi nitalisimamia kweli kweli kwa kushirikiana na viongozi wangu wengine pamoja na watendaji wa mamlaka husika lakini kikubwa fedha hizi ni lazima ziwafikie watu ambao ni walengwa na wanaoishi katika kaya masikini, na kitu kingine watendaji inabidi kuchunguza uhalisia wa kaya husika kama ni masikini au la na wananchi msiwe wadanganyifu ili wananchi wa maeneo husika waweze kupata haki zao, awe bibi au babu sio anakaa Mkuranga unamwandikisha Bagamoyo hii hapana,”alisema Zainabu.


Kwa  upande wake Mratibu wa ….TASAF Wilaya ya Bagamoyo Dionise Mahilane amesema kwamba kwa sasa wamejipanga kuondokana na changamato ya kuwepo kwa baadhi ya wananchi kuwa wadanganyifu katika utoaji wa taarifa zao ili kuhakikisha inawasaidia wale ambao ni walengwa na wanaishi katika kaya masikini kwa kuzingatia vigezo vilivyoweka sambamba na kutoa elimu jumuishi kwa jamii.
    

Naye Diwani wa Kata ya Nianjema Abdul Pyalla alisema kuwa kwa sasa kutokana na kuwepo kwa changamoto ya baadhi ya kaya masikini kutokupata fedha hizo watafanya zoezi la kupita katika mitaa ili kutoa elimu ya watu ambao wanastahili kusaidiwa sambamba na kuhakiki orodha ya kaya  ambazo zinatakiwa kupatiwa msaada lengo ikiwa ni kuondokana na kero hiyo ambayo imekuwa ni usumbufu mkubwa.
Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Kulia Zainabu Kawawa akiwa anasikiliza moja na hoja ambazo zilikuwa zinatolewa na wananchi wa kata ya Nia njewa wakati wa mkutano huo amabao ulifanyika katika viwanja vya shule ya msingi nia njema.

 Mkuu wa kituo cha Polisi Bagamoyo, Mrakibu Msaidizi wa Polisi, (ASP) Michael Kakoshi licha ya kulinda hali ya usalama katika eneo hilo la mkutano wa hadhara akiwa anasikiliza changamoto mbali mbali ambazo zilikuwa zikitolewa na wananchi wa kata hiyo ya Nianjema.

Baadhi ya wazee wa Kata ya Nianjema Wilayani Bagamoyo wakiwa wanamsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo katika mkutano huo wa hadhara ambao ulihudhuriwa na wadau mbali mbali wa maendeleo pamoja na viongozi wa serikalia na wakuu wa Idara.

Diwani wa Kata ya Nianjema Abdul Pyalla akizungumza jambo na wananchi katika Mkutano wa hadhara ambao uliandaliwa na Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo kwa lengo la kuwasikiliza wananchi kero zao ili kuweza kuzitafutia ufumbufu. (PICHA ZOTE NA VICTOR MASANGU)