Sunday, September 22, 2024

MACHIFU WAMPONGEZA RAIS SAMIA KWA KUENZI UTAMADUNI.

 

Wasema atasaidia kurejesha maadili yanayoendelea kuporomoka


Na Mwandishi Wetu


VIONGOZI wa Kimila kutoka mikoa mbalimbali nchini, wamemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha Tamasha la Utamaduni la Kitaifa pamoja na kuongeza thamani ya viongozi wa mila iliyoonekana kushuka kwa miaka mingi.


Wamesema hatua hiyo ya kuthamini, kufufua misingi na kuenzi tamaduni zilizokuwa zimeanza kuwekwa kando itasaidia kwa kiwango kikubwa kulinda maadili na tamaduni za Kitanzania.


Wakizungumza kwa nyakati tofauti mkoani Ruvuma linakofanyika kongamano hilo la tatu la utamaduni la kitaifa, viongozi hao wa kimila wamesema kwa miaka mingi mila na tamaduni za Kitanzania zilionekana kutokuthaminiwa lakini Rais Samia ametambua umuhimu wake na kufufua.


“Tunamshukuru Chifu Hangaya (Rais Samia), yeye kama kiongozi namba moja wa Machifu wote Tanzania, ameona umuhimu wa kuenzi mila na tamaduni zetu ambazo zilikuwa zimeachwa kupewa kipaumbele sana, kwa kifupi ni kwamba amezifufua na kuupa thamani kubwa utamaduni wa Mtanzania, na kwa kuwa yeye ndiye msimamizi mkuu, tunaamini maadili ya nchi yetu yatalindwa zaidi,”amesema Chifu Nyamironda, ambaye ni Katibu Mtendaji wa Umoja wa Machifu Tanzania.


“Leo hii viongozi wa kimila wanakaa pamoja, wanajadili mstakabali wa taifa lao, hili  ni jambo jema sana na tunaamini hili litazidi kulinda pia utulivu na amani kwenye nchi yetu kwa sababu viongozi wa kimila wana nafasi na nguvu kubwa kutoka kwenye jamii zao wanazoziongoza.”


Belinje Yasini, Mwenyekiti wa Machifu mkoa wa Dodoma, amesema kati ya tunu ya kujivunia ni kuwa Mtanzania na kwamba, umoja na mshikamano uliopo mpaka sasa, unapaswa kulindwa zaidi.


“Amani, umoja na mshikamano tulionao ni vya kulindwa sana kwa sababu kuna baadhi ya mataifa yanatamani kuwa kama sisi lakini hayawezi, sisi tunakaa pamoja, tunazungumza lugha moja, ni wakarimu, wenye upendo na utulivu licha ya kuwa tuna makabila mengi, lakini bado tunadumisha na kulinda umoja wetu tofauti na ilivyo kwa mataifa mengine,”anasema Chifu Yasini.


“Yaani tungekuwa na ukabila, tukabaguana, tukatengana, tungeenda kuishi wapi, lakini taifa teule, lililobarikiwa kuliko mataifa yote, tunamshukuru Mungu bado tumezidi kuwa na mshikamano na amani, ni vema tukaendelea kulinda tunu hii ambayo tumepewa na Mwenyezi Mungu."


Chifu Yasini alisema kitendo cha Rais Samia kutambua mchango wa viongozi hao wa dini ni jambo jema na anapaswa kupongezwa na kuungwa mkono kutimiza azma yake ya kuhakikisha Tanzania inaendelea kulinda tamaduni na maadili yake.


“Tumekuwa na viongozi wengi waliopita katika nafasi hiyo ya Rais, lakini hawakuzipa nguvu kubwa tamaduni zetu kama ilvyo kwa Rais Samia, kwa hiyo tunamsifu katika hili, tumuunge mkono ili kurejesha tamaduni zetu na kupambana na tamaduni potofu zisizo zetu ambazo zimeanza kuchangia mmonyoko wa maadili kwenye taifa letu,”alisema Chifu Yasini.


 “Tushirikiane na Rais Samia kupambana na vitendo vinavyochangia mmomonyoko wa maadili katika taifa letu, yeye ameonyesha njia na sisi tufuate.Tunapoona leo kuna unyanyasi, ukatili wa kijinsia na vitendo vingine vinavyotokea sasa, kazi ya kupambana navyo siyo ya serikali pekee, ni ya sisi sote jamii,” alisema


Alisema viongozi wa mila wana mchango wa kipekee katika kujenga taifa lenye mshikamano, amani, utulivu na kuchangia katika maendeleo endelevu yanayozingatia urithi wa kitamaduni na maadili ya kitaifa.


Chifu Yasini alisema viongozi hao wa kimila wamekuwa hawashirikishwi kwenye mambo mengi kwa kutokuthamini umuhimu wao.


“Unakuta mtu anatoka mbali huko anakuja anakusanya watu kupiga kampeni lakini kiongozi wa mila wa eneo husika hashirikishwi na ndio maana wakati mwingine baadae huwa mambo yanakuja kutugharimu au kuharibika, kwa hiyo thamani aliyoionyesha Rais Samia kwa sasa kwa viongozi hawa liwe funzo kwa wengine na naamini tutafika mbali,”alisema Chifu Ismail Hassan kutoka Nachingwea mkoani Lindi.


Saturday, September 21, 2024

TASSIM YAANDAA MAONYESHO YA VIWANDA VIDOGO DODOMA.

 




Na  Mwandishi Wetu

SERIKALI imewaalika wananchi na wadau mbalimbali kuhudhuria mkutano wa kukusanya maoni kuhusu Sera mpya ya biashara ndogo ndogo (SMEs) utakaofanyika mkoani Dodoma .

Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Dk. John  Simbachawene, wakati akizungumza kwenye uzinduzi wa siku ya viwanda vidogo vidogo (TAMISID).

Siku ya viwanda vidogo vidogo inayotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu mkoani Dodoma inaratibiwa na Chama cha Wenye Viwanda Vidogo Tanzania Association of Small Scale Industries and Manufacturers (TASSIM).

Alisema serikali ilikusanya maoni ya watu mbalimbali kwenye awamu ya kwanza hivyo imeamua kuandaa mkutano wa awamu ya pili kuchukua maoni kwa wale ambao walikosa nafasi kwenye awamu ya kwanza.

Alisema mkutano huo utafanyika wiki hii mkoani Dodoma na kuwataka wananchi,  wajasiriamali, wafanyabiashara kushiriki kwenye mkutano huo ili watoe maoni ya kuchangia kuboresha sera hiyo.

“Wizara inaendelea kuifanyia kazi Sera mpya ya viwanda  na tumeitisha mkutano wa wadau mbalimbali mkoani Dodoma waje kutoa maoni yao kwa awamu ya pili kwa ambao hawakutoa maoni yao ili tukamilishe hiyo Sera na  iweze kutoa mchango wake kwenye taifa letu na tuweze kuizindua rasmi,” alisema Dk. Simbachawene

Alisema malengo makuu ya siku ya viwanda vidogo ni pamoja na kuongeza uelewa wa mchanago wa viwanda vidogo katika uchumi na kukuza ubunifu kwenye sekta.

”Kama tulivyoona wakati tunatembelea maonyesho zipo bidhaa ambazo zimetengenezwa na wajasiriamali wadogo ambazo ni bora na zinaweza kushindana kimataifa kwa hiyo nawasisitiza wajasiriamali waendelee kuwa wabunifu wa bidhaa,” alisema

Aidha, alisema kuanzishwa kwa taasisi hiyo kutakuwa ni jukwaaa la kuwaunganisha wadau wawekezaji na washirika wa maendeleo katika kuendeleza viwanda vidogo na kuwajengea uwezo kupitia mafunzo.

Alisema TASIM inafanya maandalizi ya maonyesho ya viwanda vidogo Tanzania yatakayofanyika tarehe 28 Oktoba hadi Novemba Mosi kwenye ukumbi wa Jakaya Kikwete mkoani Dodoma na kuwataka wajasiriamali kuitumia kama fusa kwao kuongeza ufanisi.

“Tunatarajia kufanya maonyesho rasmi Dodoma tutumie nafasi hii kama TASIM tujitangaze kwenye vyombo vya habari ili wafanyabiashara washiriki na kutangaza bidhaa zao na tutangaze kwenye balozi zilizopo hapa nchini ili zione namna ya kusaidia wajasiriamali,” alisema

Alisema viwanda vidogo vidogo vimekuwa na mchango mkubwa kwenye uchumi wa Tanzania kwa kuchangia kutoa ajira nyingi na kupunguza kiwango cha umaskini.

Dk. Simbachawene alisema viwanda vidogo ni injini ya ukuaji wa uchumi kwa kuzalisha bidhaa na huduma muhimu na kukuza ujasiriamali wa ndani kwa watanzania walio wengi ambao wako kwenye sekta isiyo rasmi.

Mwenyekiti wa TASSIM, Masoud Ali alisema lengo la kuanzishwa kwa chama hicho ni kuinua viwanda vidogo vidogo ambavyo ndivyo uti wa mgongo wa uchumi wa nchi na kuunga mkono juhudi zinazofanywa na serikali kwenye sekta ya viwanda.

Alisema imekadiriwa kuwa zaidi ya asilimia 99 ya viwanda vyote nchini viko kwenye makundi ya viwanda vidogo sana, viwanda vidogo sana na viwanda vya kati kwa maana ya small, micro and medium industries.

 “Kwa hiyo sisi wawakilishi wa haya makundi tuna mchango mkubwa sana kwenye maendeleo ya nchi yetu na kauli mbiu ya TAMISID 2024 ni kusherehekea nguvu ya viwanda vidogo,kujenga Tanzania imara na kuwekeza kwenye mustakabali wetu kwa kuwekezesha watu wetu,” alisema

Alisema kauli mbiu hiyo inaonyesha dhamira ya dhati ya chama hicho kuinua vianda vidogo vidogo na kuvitumia ipasavyo kama injini ya ukuaji wa uchumi na kuomba wadau kujitokeza kuwekeza kwenye sekta ya viwanda.

RAIS SAMIA AKUTANA NA MKUU WA JESHI LA POLISI IGP WAMBURA

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania (IGP) Camillus Wambura pamoja na Makamishna wa Jeshi hilo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es salaam tarehe 20 Septemba, 2024





Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania (IGP) Camillus Wambura pamoja na Makamishna wa Jeshi hilo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es salaam tarehe 20 Septemba, 2024


TAMASHA LA UTAMADUNI KITAIFA LAFUNGULIWA SONGEA.





Na Mwandishi Wetu, RUVUMA

WAZIRI wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Damas Ndumbaro amewaasa watanzania kuzingatia miiko, mila na desturi za kitanzania na kuwarithisha watoto na vijana ili kujiepusha na tamaduni za kigeni zisizofaa kwa jamii.

Aidha, ameitaka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuwachukulia hatua kali wale wanaoua mila na desturi za watanzania kwenye mitandao ya kijamii.

Akizindua Tamasha la tatu la Utamaduni Kitaifa kwenye uwanja wa Majimaji mjini Songea, alisema kusipokuwa na utamaduni hakutakuwa na utu na wasipouenzi hawatauendeleza.

“Ili Taifa liwe hai lazima tuenzi na kuendeleza utamaduni wetu, na lazima turithishe utamaduni wetu kwa vijana na watoto na lazima tuwafundishe watoto wetu mila na desturi za kitanzania, Kiswahili tuwafundishe miiko mbalimbali na historia yetu kwa kuwa hawa watoto ni taifa la kesho,”alisema.

Alisema katika maadhimisho ya tamasha hilo ilitolewa semina ya maadili na utamaduni iliyofundisha jinsi ya kuenzi utamaduni na namna ya kukabiliana na madhara ya sayansi na teknolojia katika kulinda, kuenzi na kuendeleza mila na desturi.

“Sasa hivi duniani kuna suala linaitwa haki za binadamu ni jambo linalopaswa kuliheshimu na kulizingatia lakini tusitumie haki za binadamu kuingiza tamaduni za kigeni zisizofaa katika jamii yetu,”alisema.

“Taasisi za elimu kuanzia chekechea hadi chuo kikuu ni muhimu kurithisha utamaduni wetu una mila zetu katika kupambana na mmonyoko wa maadili,”alisema.
 

Alikemea tabia ya familia kulaumu mmonyoko wa maadili badala ya kujikita kutoa elimu kwa watoto na vijana ili kuishi kwenye tamaduni za mtanzania.
 

Hata hivyo, alisema taasisi za dini zina nafasi ya kukabiliana na mmonyoko wa maadili na kurithisha utamaduni kwa watoto na vijana.


“Tuwafundishe maadili mema watoto wetu, viongozi wa dini mna kazi kubwa sana na maadili mengi ya dini yanatusaidia kulinda tamaduni zetu,”alisema.


Awali, Dk.Ndumbaro alibainisha kuwa Septemba 8, 2021 katika maadhimisho ya utamaduni Bujora mkoani Mwanza Rais Samia Hassan Suluhu alitoa maelekezo kwa Wizara hiyo kuandaa tamasha la kitaifa litakalofanyika kila mkoa.
 

“Maelekezo yale yametufanya tuwe Songea leo, uwepo wetu hapa ni maelekezo ya Rais Samia kudumisha tamaduni zetu, ”alisema.

 Alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na makabila zaidi ya 120 na lugha za kijamii zaidi ya 150 na ni utajiri wa kiutamaduni.

“Utamaduni wetu unategemea nguzo zifuatazo moja ni upendo, mshikamano, umoja, amani na utulivu, yote tunayoyafanya ili kuendeleza nguzo hizi,”alisema.

Tuesday, September 17, 2024

MADAKTARI BINGWA WA MAMA SAMIA WAWEKA KAMBI MKOANI LINDI

 

Na Hadija Omary, LINDI.


Wananchi Mkoani Lindi wametakiwa kutumia siku sita za ujio wa madaktari bingwa na ubingwa bobezi wa Rais Samia kupata huduma za kibingwa kwa karibu katika hospitali za Wilaya  za Mkoa huo


 

Rai hiyo imetolewa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Lindi Dkt Kheri Kagya Jana  septemba 16, 2024 wakati wa kuwapokea madaktari hao bingwa na bingwa bobezi wa Rais Samia katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa lindi kisha kuwakabidhi kwa waganga wakuu wa halmashauri sita za mkoa huo



Madaktari hao watakuwepo kwa muda wa siku 6 kuanzia Jana Septemba 16 hadi 21 wakitoa huduma za kibingwa kwenye hospitalli zote za halmashauri Mkoani Lindi lengo likiwa  kusogeza huduma za kibingwa na ubingwa bobezi karibu zaidi na wananchi pamoja na kuwajengea uwezo wataalam wa afya kwa ngazi ya halmashauri kutoa huduma hizo za kibingwa.



Dkt. Kagya ametaja madaktari waliopokelewa ni pamoja na madaktari bingwa wa huduma za magonjwa ya kike na uzazi, upasuaji, mfumo wa mkojo, magonjwa ya ndani, huduma za mifupa, watoto, ganzi na usingizi.



Amesema huduma hizo zitatumia bima na kwa wagonjwa wasio na bima watamuona daktari na Kuchangia Kiasi kidogo kwa utaratibu wa kawaida kama atahitajika kupata huduma nyingine ikiwemo vipimo, upasuaji na dawa.



Awali, akizungumza Mwakilishi kutoka Wizara ya afya ambaye pia na mratibu wa madaktari hao waliotoka hospitali mbalimbali hapa Nchini  Faraja Mgeni amewakumbusha Madaktari kwenda kufanya kazi kwa kujituma zaidi na kuzingatia maadili ili kutimiza lengo la Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania na Wizara ya Afya kwa wananchi huku akiomba waganga wakuu kwenye halmashauri kuwapa ushirikiano wa kutosha ili waweze kutimiza majukumu yao.





Thursday, September 12, 2024

MAGEUZI MAKUBWA WAKALA WA VIPIMO (WMA)

 

Na Albert Kawogo 


SERIKALI kupitia Wakala wa vipimo nchini (WMA)imefanya mageuzi makubwa yanayolenga kumlinda mlaji kwenye huduma na ubora wa vipimo vinavyotumika kwenye sekta za biashara, afya na mazingira.


 Mtendaji Mkuu wa WMA Alban Kiula amesema hayo jana wakati akiongea Jijini Dar es Salaam na Wahariri kutoka Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) ukiwa ni mfululizo wa vikao vya Taasisi za Umma zilizoko chini ya msajili wa hazina. 


Kiula alisema WMA ina jukumu kubwa la kuilinda jamii kwenye athari zinazotokana na matokeo ya upimaji usio sahihi katika biashara na maeneo mengine mtambuka.


"Unaweza usiione hii hali lakini kuna madhara makubwa kijamii yatokanayo na upimaji usio sahihi hasa kiuchumi" Alisema Kiula


Mtendaji Mkuu alisema jukumu la WMA  haliishii tu kwenye kusimamia na kudhibiti vipimo bali pia taasisi hiyo inatoa ushauri wa kitaalam kuhusiana na vipimo Kwa serikali, mashirika ya umma na Taasisi binafsi.


Pia Kihula alisema moja ya mafanikio makubwa ya WMA ni kuongezeka kwa idadi ya vipimo vinavyohakikiwa na kuendelea na ununuzi wa vifaa vya kitaalam ambapo yote haya yameipa thamani taasisi hiyo


Akizungumza kwa niaba ya Wahariri Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania TEF Deodatus Balile alisema kazi kubwa ya kupongezwa imefanywa na WMA lakini bado changamoto ipo kwenye uchache wa watendaji kwakuwa jukumu lao kama WMA lina wigo mpana wa kiutendaji hasa kwenye yale maeneo yanayogusa walaji Kwa bidhaa za chakula na vifaa vya ujenzi.

Tuesday, September 10, 2024

SHARIFA MKWANGO MWENYEKITI MPYA TWFA MKOA WA LINDI

 






NA HADIJA OMARY, LINDI.

Sharifa Mkwango ameshinda kuwa Mwenyekiti mpya wa chama cha mpira wa miguu Wanawake  (TWFA) Mkoa wa Lindi atakaehudumu nafasi hiyo kwa muda wa miaka mitano  baada ya kushinda kwa Kura za ndio

Uchaguzi huo umefanyika Jana huko Manispaaa ya Lindi ambao ulihusisha pia nafasi za wajumbe wawili wa kamati tendaji ambao ni Bi. Subira  Mwangata na Beatrice Victor pamoja na nafasi ya mjumbe wa Mkutano Mkuu Taifa (TWFA) Bi.Sifa Mwaya 

Akifungua mkutano huo  Afisa Michezo wa Manispaa  ya Lindi Jamal Lisuma  kwa niaba ya Katibu tawala wa Wilaya ya Lindi hudhaifa Rashid aliwataka  viongozi watakaochaguliwa kutatua changamoto zilizopo Katika Mkoa wa Lindi upande wa soka la Wanawake ikiwemo kuongeza vilabu vya timu za Wanawake na kuanzisha ligi ya Wanawake Ngazi za Wilaya na Mkoa 

Amesema lengo la hayo yote ni   kutafuta vipaji vya wachezaji  hao wanawake wanaoweza kuunda timu ya Mkoa inavyoweza kushiriki ligi kuu ya Wanawake Tanzania Bara.

Kwa upande wake Bi Sharifa Mkwango Mwenyekiti mpya wa (TWFA) ameahidi kufanya uhamasishaji kwa Jamii kuona Umuhimu wa kuwekeza Katika Michezo kwa watoto wa Kike.

Katibu wa kamati ya Uchaguzi Fidea Mnunduma amewapongeza wajumbe kwa kutimiza wajibu wao na kutenda haki  kwenye uchaguzi huo  na kwamba Kura zimepigwa vizuri hakuna zilizoharibika kila Mmoja ametumia  haki yake kwa kutimiza wajibu wake


"Kamati ya uchaguzi inawashukuru wajumbe wote  kwa ushirikiano uliouonysha lakini Leo mmeweza kupata viongozi wapya wa TWFA kamati ipo itadumu kwa miaka minne kama mutakuwa na tatizo lolote  kamati imefungua milango njooni mtuone"

Monday, September 9, 2024

DKT. BITEKO ASHIRIKI DUA YA MZEE MAJID NSEKELA

 




Na Alodia Dominick, Kyerwa.


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati,  Dkt. Doto Biteko ameiasa jamii kuwa na utaratibu wa  kuwatunza na kuwajali  wazazi wao, amesisitiza upendo miongoni mwa jamii na kuendelea kuwaombea ambao hawapo hai.


Dkt. Biteko ameyasema hayo Septenba 7, 2024 akiwa Nyakatuntu, wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera wakati aliposhiriki katika dua ya kuwaombea baba mzazi na ndugu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Mussa Nsekela



“ Tuendelee kuwakumbuka na kuwaombea ndugu na wazazi waliotangulia mbele za haki ni jambo zuri na wajibu wetu tuliobaki, Sheikh wetu katika mawaidha yake ameliongelea kwa uzuri sana. Tulitilie maanani na sote tuendelelee kufanya hivi, na kama huwa hatuwafanyii hivi ndugu zetu, hatuna budi tuanze kwa moyo wote.” Amesema Dkt. Biteko.

 


“Ndugu zangu tusisahau mapito yetu, Katika mapito huwa kuna watu, Katika watu hawa, kuna wazazi wetu, Kama wazazi wako wapo hai, mmoja au wote au wale waliokulea, jua nawe una wajibu wa kuwalea na kuwatunza, siyo kifedha tu bali pia kwa mahusiano mema hasa ya kihisia kwa kuwa hivyo ndivyo impendezavyo Mungu.”ameongeza Dkt Biteko 


Ametolea mfano wa  Rais wa awamu ya pili, Marehemu Ally Hassan Mwinyi, Mzee Rukhsa kuwa aliiasa jamii kuwa maisha hapa duniani si kitu ila ni hadithi tu na kuwa wayafanye maisha yao yawe hadithi nzuri. 


"Kwa dua hii, kwa umati huu, kwa wanafamilia hawa wa Nsekela inadhihirisha bayana kabisa kuwa maisha ya Mzee wetu, Alhaji Tibihika Mussa Nsekela, na wengine tuliowaombea dua leo hapa yameacha hadithi nzuri kwa sisi tuliobaki hili ni jambo zuri la kujifunza.”

 

Aidha, Dkt. Biteko ameendelea kuiasa jamii kushiriki katika shughuli za maendeleo katika maeneo yao wanapotoka, kuendelea kuishi kwa upendo sambamba na kuishukuru familia hiyo kwa kumualika kushiriki katika dua hiyo.

 

Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko amesema kuwa Serikali  imeendelea na jitihada zake mbalimbali za kuwaletea maendeleo wananchi wa Nyakatuntu kwa kutekeleza miradi mbalimbali katika Wilaya ya Kyerwa  na tayari imetenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa mradi wa barabara.


Kwa upande wake, Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zuber amempongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Majid Nsekela kwa kuandaa dua hiyo kwa ajili ya baba yake na kusema kwa kufanya hivyo inaonesha anaipenda familia yake na dini yake ya kiislamu.


Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Majid Nsekela amesema kuwa tukio hilo kwao ni la kihistoria na wanamshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema hiyo.


“Kwa dua hii ya leo tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko pamoja na kuwa na kazi nyingi amejumuika nasi hapa na wote mliopo nasi leo kwa upendo wenu na familia yote imefurahi na inawashukuru,” amesema  Nsekela.


Aidha, Majid amewakumbusha na kuwatakia heri wananchi wa Nyakatuntu kushiriki katika uchaguzi wa Serikali za 

Mitaa unaotarajiwa kufanyika Novemba mwaka huu kwa kuchagua viongozi wanaofaa.

Monday, August 26, 2024

MTAALAMU BINGWA WA NYONGA NA MAGOTI ATUA DAR.

 



Ashirikiana na wataalamu wazawa upasuaji Mloganzila


Na Mwandishi Wetu


MTAALAMU bingwa wa ubadilishaji wa nyonga na magoti  kutoka hospitali kubwa nchini India ya Yashoda, Dk. Ram Mohan Reddy amewasili jijini Dar es Salaam kwaajili ya kambi ya matibabu hayo kwa watanzania.


Daktari huyo kwa kushirikiana na wataalamu wa ndani atafanya upasuaji huo kwenye kambi ya siku tano itakayofanyika katika hospitali ya Muhimbili Mloganzila  kuanzia leo Jumatatu hadi tarehe 30.


Aliwasili jana usiku katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere ambapo alipokelewa na wafanyakazi wa Global Medicare ambao wameratibu kambi hiyo kwa kushirikiana na Muhimbili Mloganzila.


 Akizungumza kwenye mapokezi hayo, Meneja Mkuu wa Global Medicare, Daniel Lazaro,  alisema wamefurahi kuona amefika salama nchini Tanzania na kwamba ujio wake utakuwa wa manufaa makubwa kwa watanzania wenye matatizo ya nyonga na magoti.


“Tunajua ni mara yako ya kwanza kuja kufanyakazi na madaktari wa hapa Tanzania  kwenye upasuaji wa aina hii lakini tunatarajia watanzania wengi watanufaika na ujio wako kwenye kambi hii ya siku tano itakayoanza katika hospitali ya Muhimbili Mloganzila,” alisema


Naye Dk. Reddy aliishukuru serikali ya Tanzania na taasisi ya Global Medicare kwa kuratibu vyema safari yake ya kuja nchini Tanzania na aliahidi kutoa huduma bora kwa wagonjwa watakaojitokeza kwenye kambi hiyo.


“Natarajia tunashirikiana vizuri sana na wataalamu wenzangu wa hapa nchini kwenye kambi hii ya siku tano na kwa huduma hii natarajia tutaongeza chachu ya ushirikiano baina ya Tanzania na India na tutabadilishana uzoefu wa kufanya upasuaji wa aina hii kwa wataalamu na watu wa hapa nchini watakaokuja kusoma India,” alisema


Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Upasuaji wa hospitali ya Mloganzila, Goodlove   Mfuko, alisema hivi karibuni kuwa maandalizi yote yamekamilika na kwamba kwenye kambi hiyo watashirikiana na mtaalamu huyo Dk. Ram Mohan Reddy.


 


“Mtaalamu huyu atashirikiana na madaktari bingwa ambao ni wataalamu wa mifupa na ajali hapa Mloganzila, hii itakuwa mara ya pili kutoa huduma  kama hii kwani mara ya kwanza tuliwafanyia upasuaji wa kubadilisha nyonga na magoti wagonjwa 170 kwa mafanikio makubwa,” alisema


“Kwa hiyo kwenye kambi hii ambayo ni ya pili  tutashirikiana na daktari huyu mbobezi kutoka India kupata uzoefu ili tuweze kubadilishana naye uzoefu ili tuboreshe zaidi huduma zetu,” alisema


“Kwa hiyo watu wenye matatizo ya nyonga na magoti wafike Mloganzila mapema ili wafanyiwe uchunguzi wa mapema kwaajili ya kupewa hiyo huduma ya kubadilisha nyonga na magoti,” alisisitiza Dk. Mfuko.


 

WANAFUNZI WATAKAOFANYA VIZURI SHULE BRLILLIAN KUPELEKWA SERENGETI

 






Picha mbalimbali mahafali ya 14 ya kidato cha nne shule ya sekondari ya  Brilliant ya Kimara Mbezi kwa Msuguri jijini Dar es Salaam yaliyofanyika jana Jumamosi

...............................................

Na  Mwandishi Wetu

Mbunge wa Bukoba Vijijini (CCM), Dk. Jasson Rweikzia, ametangaza kwamba kwenye mtandao wa shule za St Anne Marie Academy unaominilikia pia shule ya Brilliant ya Kimara Mbezi kwa Msuguri jijini Dar es Salaam, hakuna mwanafunzi atakayefukuzwa shule baada ya wazazi wake kufariki na kushindwa kulipa ada ya kuendelea na masomo.


 


Alitangaza uamuzi huo mwishoni mwa wiki wakati wa mahafali ya  14 ya kidato cha nne ya shule ya Brilliant iliyoko Kimara Mbezi jijini Dar es Salaam.


 


Mtandao huo unamiliki shule za St Anne Marie Academy, Brilliant, Rweikiza Nursery and Primary na Sunshine ya Kibaha Mkoa wa Pwani.


 


Dk Rweikiza alisema shule hizo ziliwahi kupoteza wazazi 93 kwasababu mbalimbali na kusababisha baadhi ya wanafunzi kuacha masomo kwa kukosa ada hali ambayo alisema imeilazimu shule hiyo kuwapa msamaha wa ada wanaofiwa.


 


 " Tumekuwa tukipoteza wazazi wengi na mwezi huu pekee tumepoteza wazazi watatu na hali hii imekuwa ikiathiri sana wanafunzi kitaaluma na wengine kuacha shule kwa kushindwa kulipa ada lakini kuanzia sasa hakuna atakayefukuzwa shule kwa kukosa ada baada ya mzazi wake kufariki," alisema


 


 " Kama yuko darasa la kwanza na amefiwa na mzazi wake ataendelea kusoma mpaka darasa la saba na kama ni sekondari ataendelea mpaka kidato cha nne," alisema Dk. Rweikiza


 


Dk. Rweikiza alisema katika mpango wa kuinua taaluma shuleni hapo wameaandaa zawadi mbalimbali zikiwemo fedha taslimu kwa awatakaofanya vizuri kwenye masomo yao na ziara za kimasomo kwenye mbuga mbalimbali za wanyama.


 


Alisema mwanafunzi atakayepata daraja la kwanza atapata sh 600,000 na atakayepata daraja la II atapata Sh 200,000 na kwamba lengo ni kuhakikisha hakuna daraja la nne wala daraja la tatu shuleni hapo.


 


Mkuu wa shule ya Brilliant, Edrick Phillemon alisema wahitimu hao wa kidato cha nne wameandaliwa vizuri kitaaluma na wanatarajiwa kufanya vizuri kwenye mitihani yao na kwamba ana uhakika wa kupata daraja la kwanza na la pili.


 


“Tuna uhakika wa kufanya vizuri kwani ukiangalia historia ya shule ya Brilliant huwa haipati daraja la nne wa daraja 0, mara nyingi tunafaulisha kwa daraja la kwanza na la pili,” alisema


 


 Alisema wanafunzi hao wamewezeshwa kufikia hapo na walimu wenye taaluma na uzoefu wa kutosha huku akimshukuru Mkurugenzi wa shule hizo, Dk. Rweikiza kwa kuendelea kufanya maboresho ya miundombinu ya shule hiyo.