Saturday, September 16, 2023

MAKAMU WA RAIS AWAPONGEZA WATANZANIA WAISHIO NCHINI HUNGARY.

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ameipongeza Jumuiya ya Watanzania waishio nchini Hungary pamoja na Ubalozi wa Tanzania unaowakilisha nchini humo kwa msaada waliotoa wakati wa kuwaondoa watanzania waliokuwa wakiishi na kusoma nchini Ukraine mara baada ya kuanza kwa vita.
 
Makamu wa Rais ametoa pongezi hizo wakati alipokutana na kuzungumza na Jumuiya ya Watanzania wanaoishi na wale wanaopata elimu ya ngazi mbalimbali nchini Hungary, mazungumzo yaliofanyika Jijini Budapest nchini Hungary. Amewataka kuendelea kushikamana na kushirikiana wakati wote na kuwa na moyo wa huruma na upendo kama baadhi yao walivyojitolea hali na mali kusaidia watanzania waliokuwa wakiondoka eneo la vita.
 
Makamu wa Rais amewasihi watanzania waishio nchini Hungary kuhakikisha wanaishi kwa kufuata sheria katika nchi hizo na kujiepusha na vitendo vya kihalifu vitakavyoharibu taswira ya Tanzania. Aidha amewaasa kuendelea kuitangaza vema Tanzania, kuvutia wawekezaji pamoja na wao kuchangamkia fursa za uwekezaji katika sekta mbalimbali nchini. Pia amewasihi kuendelea kusaidia kwa karibu ndugu na jamaa wenye uhitaji katika familia zao nchini Tanzania kwa kutumia mifumo rasmi ya utumaji fedha.
 
 
Halikadhalika Makamu wa Rais amesema kutokana na lugha ya Kiswahili kuanza kutumika katika Jumuiya mbalimbali kama lugha rasmi, Diaspora wanapaswa kuendeleza lugha hiyo kwa kuitangaza na kuanzisha vituo vya kujifunzia lugha ya Kiswahili katika maeneo waliopo. Aidha amewataka watanzania waishio nje ya Tanzania kutambua jukumu la kwanza la ujenzi wa Tanzania litafanywa na watanzania wenyewe hivyo wanapaswa kutoa mchango wa kila hali katika kuliletea taifa maendeleo.
 
Amewasisitiza wanafunzi kutumia fursa waliopata vema kwa kuvuna maarifa na kutengeneza mahusiano mazuri na mataifa mengine ili kuweza kuijenga Tanzania.
 
Makamu wa Rais amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuleta mabadiliko yenye tija kwa watanzania wote na kueleza kwamba serikali imefanya jitihada katika kuboresha sekta mbalimbali ikiwemo afya, sekta ya elimu, kuimarisha sekta ya nishati, ujenzi wa mindombinu kama vile barabara, reli viwanja vya ndege na barabara. Pia amesema serikali inaendelea na jitihada za kuimarisha demokrasia, sekta ya madini, maji na sekta ya kilimo kwa kuanzisha programu za kuvutia vijana katika kilimo cha biashara.
 
Pia Makamu wa Rais amesema Serikali kwa kutambua ongezeko la watu nchini imedhamiria kuwekeza katika kuimarisha rasilimali watu ili iweze kutumika vema katika kuleta maendeleo. Makamu wa Rais amesema kwa kuzingatia hali hiyo huduma za afya na elimu zimeboreshwa kwa kuongeza vifaa tiba na miundombinu ya afya, kutoa fursa kwa madkatari kupata elimu zaidi pamoja na ujenzi wa vyuo vya ufundi.
 
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mbarouk Mbarouk amesema pamoja na kazi ya kukuza na kudumisha mahusiano ya kirafiki na kidiplomasia kati ya Tanzania na mataifa mengine pia serikali imeendelea kutekeleza kikamilifu kazi ya uratibu wa masuala ya diaspora. Amesema kuanzishwa kwa mfumo wa kuwasajili diaspora kidijitali (Diaspora Digital Hub) umesaidia katika kurahisisha kutambua takwimu za watanzania waishio nje ya Tanzania.
 
Balozi Mbarouk amesema takwimu zitakazopatikiana katika mfumo huo zitawezesha serikali kupanga na kuandaa kwa usahihi mahitaji yanayohitajika ili kuwapa diaspora huduma wanazohitaji kama vile huduma za kibenki, hati za kusafiria, vitambulisho vya taifa na vitambulisho rasmi vya utambuzi wa diaspora wakati wa utekelezaji wa hadhi maalum. 
 
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanafunzi Watanzania wanaopata Elimu nchini Hungary Michael Matonya ameishukuru serikali kwa ufadhili wa wanafunzi wanaosoma nchini humo na kuomba kuongezwa kwa idadi ya wanafunzi wanaosoma nchini humo hasa katika fani za kimkakati za sayansi na teknolojia.
 
Pia ametoa wito kwa serikali kuwekeza zaidi katika kushirikiana na nchi ya Hungary katika sekta ambazo nchi hiyo imepiga hatua kama vile utaalamu katika sayansi ya kompyuta, tehama, uhandisi, urubani, afya, elimu ya mimea na wanyama
 
Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
16 Septemba 2023
Budapest Hungary. 




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akizungumza na Jumuiya ya Watanzania wanaoishi na wale wanaopata elimu ya ngazi mbalimbali nchini Hungary, mazungumzo yaliofanyika Jijini Budapest nchini Hungary.

UAMUZI WA RAIS SAMIA WAWAKOSHA WAKAZI WA NANYAMBA.


 Na Immaculate Makilika - MAELEZO



Wakazi wa Halmashauri ya Mji Nanyamba Wilaya Mtwara Vijijini wamefurahishwa na uamuzi wa Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan wakuitaka Bandari ya Mtwara kuanza kusafirisha korosho.


Akizungumza leo wilayani humo katika mahojiano maalum na Afisa wa Idara ya Habari -MAELEZO, Mkazi wa Nanyamba na Mkulima wa korosho, Bw. Burhan Mwema anaeleza kuwa uamuzi huo wa Rais Samia utawanufaisha zaidi wakulima kwa kuwa awali iliwapa ugumu kusafirisha korosho kwa kutumia Bandari ya Dar es salaam.


" Napongeza sana Mhe. Rais kwa hili, itatusaidia sisi hata kujua kinachoendelea kuhusu korosho zetu, kwa kuwa tutaona kila kitu kuliko ilivyokuwa inaenda huko mbali".


Mkulima wa korosho, Ahmed Mchila anasema "Kwanza nimefurahishwa na uamuzi huu wa kutumia Bandari ya Mtwara kusafirisha korosho, hii bandari ipo karibu nasi hapa tutaweza kufuatilia kwa karibu zaidi kila kinachoendelea. Pia, kusafirisha kwa bandari yetu itasaidia hata uzito kutopungua tofauti na tukipeleka mbali muda unavyotumika zaidi katika kusafirisha na korosho zetu zinapungua uzito na bei pia inapungua". Amebainisha Mchila.


Naye, Mbaraka Said anasema " Kusafirisha korosho kupitia bandari yetu hapa itasaidia kuchochea uchumi wa Mtwara kwa kuwa hata wanunuzi kutoka mbali watafika na wakiwa hapa watafanya shughuli mbalimbali zitakazochochea uchumi wetu"


Aidha, Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan jana akizungumza na wananchi wa Mtwara katika Uwanja wa Nangwanda Sijaona ameeleza "Nimeona eneo jipya la bandari ambalo limejengwa na Serikali. Bandari ile haijajengwa kupamba Mji wa Mtwara. Bandari ile imejengwa kutoa huduma za usafiri na usafirishaji wa watu na bidhaa, kutoka Mtwara na kuingia Mtwara".



"Kilio chenu wananchi ni suala la korosho, kwamba korosho sasa isafirishwe kutokea Bandari ya Mtwara. Mimi sielewi ni nini kinawazuia Mtwara kutosafirisha pale Korosho". Amebainisha Mhe Rais Samia.



Amesisitiza "Niwaombe sana Wanamtwara hasa viongozi, yale ambayo yalikuwa yanazuia Korosho kusafirishwa kupitia bandarini kaeni mkubaliane. Najua kuna wafanyabiashara wenye malori ambayo ndio wanapakia korosho kupeleka Mjini au Dar es Salaam. Lakini kuna wenye vituo vya mafuta, korosho ikisafirishwa kwa meli hawatapata fursa ya magari kujaza mafuta".


Mhe. Rais Samia ameendelea na ziara yake mkoani Mtwara, ambapo mapema leo amezungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara eneo la Nangururuwe na Nanyamba na kisha kuelekea Uwanja wa Majaliwa Tandahimba kwa ajili ya kuzungumza na wanachi wa eneo hilo.







Friday, September 15, 2023

TUMIENI MITANDAO YA KIJAMII KUELIMISHA KUHUSU MAGONJWA YASIYOAMBUKIZA- MSIGWA

 


Na Athumani Shomari.

Msemaji Mkuu wa serikali, Gerson Msigwa, amewataka wadau mbalimbali wanaopambana na magonjwa yasiyoambukiza kutumia mitandao ya kijamii katika kutoa elimu kuhusu magonjwa hayo.


Msigwa ambae alikuwa mgeni rasmi katika Mkutano wa kuwajengea uelewa Wahariri wa vyombo vya habari kuhusu magonjwa yasiyoambukiza uliofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es salaam, amesema kwa sasa watu wengi wanatumia mitandao ya kijamii kwaajili ya kupata habari, kujiburudisha na mawasiliano hivyo ni vyema elimu ya magonjwa yasiyoambukiza ikatolewa pia kupitia mitandao hiyo.


Alisema zamani mitandao ya kijamii haikupewa kipaumbele lakini kwa sasa ni sehemu ya vyombo vya habari na taarifa zinawafikia wengi zaidi kwakuwa mitandao hiyo hupatikana kupitia simu janja ambazo watu wengi wanazo.


Aliongeza kwa kusema kuwa watu wengi kwa sasa wamekuwa wavivu wa kununua na kusoma magazeti lakini simu wanazo na wanazitumia kupata taarifa mbalimbali.


Aliwakumbusha wadau hao kuwa, wanapofikiria kutumia Tv, Radio na Magazeti wasisahau pia kutumia mitandao ya kijamii kufikisha elimu hiyo kama vile Blogs, Facebook, twitter na instagram ambayo inawatumiaji wengi kwa sasa.


Akizungumzia hali ya magonjwa yasioambukiza hapa nchini kwa sasa, Msigwa alisema Mtanzania 1 kati ya 3 ameathiriwa na magonjwa hayo na kupelekea asilimia 40 ya fedha za mfuko wa taifa wa bima ya afya kutumika kuhudumia walioathirika na magonjwa yasiyoambukiza.


Mkutano huo wa kuwajengea uelewa wahariri wa vyombo vya habari umeandaliwa na wadau mbalimbali wakiwemo Serikali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania, PharmAccese, Norad, Shirikisho la vyama vya magonjwa yasiyoambukiza Tanzania (TANCDA), Shirika la kisukari Duniani (WDF) Chama cha ugonjwa wa kisukari Tanzania (TDA) lengo ni kuleta mtazamo mpya juu ya mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.











MAGAZETI YA LEO TAREHE 15 SEPTEMBA 2023.

 
























Thursday, September 14, 2023

LUDEWA YAPOKEA ZAIDI YA BILIONI 1.5 KUKAMILISHA MIUNDOMBINU YA AFYA NA VIFAA TIBA.

 

Wilaya ya Ludewa mkoani Njombe imepokea zaidi ya Shilingi Bilioni 1.5 kwa ajili ya ukamilishaji na uboreshaji wa miundombinu ya Afya na Vifaa tiba.


Mkuu wa Wilaya ya Ludewa, Victoria Mwanziva ameyasema hayo mara baada ya ufunguzi wa Zahanati ya Chimbo katika Kijiji cha Amani ambayo inatarajiwa kuhudumia wananchi zaidi ya 5,000 waliokuwa wakisafiri umbali wa zaidi ya kilomita Saba kufuata huduma katika makao makuu ya kijiji. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutubeba kwa Milioni 50 kwa ajili ya ujenzi wa Zahanati hii ambayo itakuwa mkombozi kwa wananchi hawa. 


Mganga Mkuu wa Wilaya ya Ludewa, Dkt. Stanley Mlayi amesema kuanzia mwaka 2020 hadi mwaka huu zahanati 13 zimezinduliwa pamoja na vituo vya Afya vitano katika Wilaya hiyo.


Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa, Sunday Deogratias amesema vifaa tiba vilivyokabidhiwa katika kituo cha afya cha Mundindi vimegharimu Shilingi Milioni 150, na Serikali imekwishatenga Milioni 150 nyingine kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vya kuongezea kwa ajili ya Kituo cha Afya Cha Mundindi ambacho kinaenda kutoa huduma mtambuka kama Upasuaji, Afya ya Mama na Mtoto, Vipimo na huduma mbalimbali.


Kituo cha Afya Mundindi kimegharimu Milioni 500 mpaka kukamilika kwake na ni maendeleo makubwa kwa Kata ya Mundindi, Tarafa ya Liganga- Wilaya ya Ludewa. 

Diwani wa Kata ya Mundindi ambaye ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa; Wise Mgina ameshukuru kwa maendeleo haya thabiti kwa ajili ya utoaji wa huduma bora kwa wananchi. 

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi- Wilaya ya Ludewa Ndugu Gervas Ndaki naye ameshukuru utekelezaji wa Ilani unaoendelea Wilayani Ludewa; kwa maslahi ya kusogeza huduma bora kwa wananchi.